Sanduku la Swali
◼ Mtu ambaye amekuwa asiyetenda kwa muda mrefu anaweza kusaidiwaje astahili tena kuwa mhubiri wa habari njema?
Mtu asiyetenda anapotoa uthibitisho kwamba ana tamaa ya kutoka moyoni ya kumtumikia Yehova, hiyo huwa sababu ya kuleta shangwe. (Luka 15:4-6) Yaelekea kwamba mtu huyo aliruhusu upinzani au mikazo ya maisha imzuie kuwa na funzo lake la kibinafsi, kuhudhuria mikutano, na kushiriki huduma ya shambani. Anaweza kusaidiwaje ili afanye maendeleo ya kiroho?
Sisi sote twapaswa kuchukua hatua kumhakikishia upendo wetu wa Kikristo. Wazee wataangalia mahitaji yake hususa ya kiroho bila kukawia. (Yak. 5:14, 15) Ikiwa hali ya kutotenda ilikuwa ya muda mfupi, huenda usaidizi kutoka kwa mhubiri mwenye uzoefu ukawa ndio unaohitajika ili kumfanya awe mtendaji tena katika utumishi wa shambani. Hata hivyo, ikiwa asiyetenda amekuwa hahudhurii mikutano kwa muda mrefu, labda msaada zaidi utahitajiwa. Ili kujenga imani na uthamini wake, funzo la Biblia la kibinafsi kwa kichapo kinachofaa litahitajiwa. Ikiwa hivyo, mwangalizi wa utumishi atapanga mhubiri mwenye kustahili aongoze funzo hilo. (Ebr. 5:12-14; ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Novemba 1998, Sanduku la Swali.) Ikiwa wajua mtu anayehitaji msaada, ongea na mwangalizi wa utumishi katika kutaniko lenu.
Kabla ya kumwalika tena mtu ambaye amekuwa asiyetenda kwa muda mrefu kwenye huduma, inafaa wazee wawili wakutane naye waone kama anastahili kuwa mhubiri wa Ufalme. Watafuata utaratibu unaofanana na ule unaotumiwa wakati wa kukutana na wapya wanaotaka kustahili wawe wahubiri wa habari njema. (Ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 15, 1988, ukurasa wa 17.) Mtu asiyetenda apaswa kuwa na tamaa yenye unyoofu ya kushiriki habari njema na wengine. Pia anahitaji kutimiza matakwa yaliyo kwenye ukurasa wa 98-99 wa kitabu Huduma Yetu na ahudhurie mikutano kwa ukawaida.
Kuwa na utaratibu mzuri wa kiroho kutasaidia sana mtu anayerudi kuimarisha na kudumisha uhusiano wake wenye thamani na Yehova na kuendelea kutembea kwenye barabara ya uhai wa milele. (Mt. 7:14; Ebr. 10:23-25) Kutia kwake “jitihada yote yenye bidii” na kusitawisha sifa za Kikristo zinazodumu kutamzuia kuwa tena ‘asiyetenda ama asiyezaa matunda’ akiwa mwanafunzi Mkristo.—2 Pet. 1:5-8.