Kuwa na Adabu Nzuri Ni Sifa ya Watu wa Mungu
1 Leo si rahisi kuona adabu nzuri. Kwa nini? Watu wana haraka sana hivi kwamba mara nyingi hawafikirii matendo ya kawaida ya kiungwana kama vile kusema “Tafadhali,” “Asante,” au “Kunradhi.” Neno la Mungu lilitabiri kwamba siku za mwisho adabu zingeendelea kuharibika. Neno lake lilisema kwamba watu wangekuwa ‘wenye kujipenda wenyewe, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wasio na shukrani, wasio na shauku ya kiasili, wasio na hali ya kujidhibiti, wasio na upendo wa wema, na wenye vichwa vigumu.’ (2 Tim. 3:1-4) Sifa zote hizo ni ukosefu wa adabu. Wakiwa watu wa Mungu, lazima Wakristo wajihadhari ili wasiwe kama ulimwengu huu usiowaheshimu wengine.
2 Adabu Ni Nini? Adabu nzuri yaweza kufafanuliwa kuwa kutambua sana hisia za wengine, uwezo wa kuishi na wengine kwa amani. Sifa za adabu nzuri ni ufikirio, uungwana, fadhili, upole, busara na kujali. Sifa hizo zinatokana na upendo wa mtu kwa Mungu na kwa jirani yake. (Luka 10:27) Sifa hizo hazigharimu chochote, lakini zina thamani sana katika kuboresha uhusiano wetu na wengine.
3 Yesu Kristo aliweka kielelezo bora kabisa. Sikuzote alidhihirisha ile Kanuni Bora: “Kama vile mtakavyo watu wawafanyie nyinyi, wafanyieni wao kwa njia hiyohiyo.” (Luka 6:31) Je, sisi hatustaajabu jinsi Yesu alivyowajali na kuwapenda wanafunzi wake? (Mt. 11:28-30) Adabu yake njema haikutokana na sheria zilizoandikwa kwenye vitabu vya adabu nzuri. Zilitokana na moyo mnyoofu na mkarimu. Lazima tujaribu kumwiga.
4 Ni wakati gani ambapo Wakristo wanahitaji kuwa na adabu nzuri? Je, ni wakati wa vipindi vya pekee tu, wakati wanataka kujionyesha kuwa eti ni wazuri? Je, ni wakati tu wa kujaribu kuwavuta wengine? La! Twahitaji kuwa na adabu nzuri nyakati zote. Ni katika njia zipi tunazopaswa kuangalia jambo hili tunaposhirikiana na wengine kutanikoni?
5 Kwenye Jumba la Ufalme: Jumba la Ufalme ni mahali petu pa ibada. Sisi huenda hapo kwa kuwa tumealikwa na Yehova Mungu. Kwa njia hiyo, sisi ni wageni. (Zab. 15:1) Je, sisi ni wageni walio mfano mzuri tunapokwenda kwenye Jumba la Ufalme? Je, sisi huangalia sana jinsi tunavyovalia na kujipamba? Kwa kweli tungependa kuepuka mapambo tunayovaa mapumzikoni au yenye kupita kiasi. Iwe twahudhuria mikusanyiko au mikutano yetu ya Kutaniko ya kila juma, tukiwa watu wa Yehova twatambuliwa kwa sura yetu inayoonyesha adabu nzuri inayofaa kudhihirishwa na wale wanaodai kumhofu Mungu. (1 Tim. 2:9, 10) Kwa kufanya hivyo tunaonyesha ufikirio na staha kwa Mkaribishaji wetu wa kimbingu na kwa wageni wengine ambao wamealikwa.
6 Njia nyingine ambayo tunaonyesha adabu nzuri kuhusiana na mikutano yetu ni kwa kufika mapema. Ni kweli kwamba, jambo hilo si rahisi sikuzote. Huenda wengine wakawa wanaishi mbali sana au huenda wakawa na familia kubwa zinazochukua muda kujitayarisha. Hata hivyo, katika makutaniko fulani, imeonekana kwamba asilimia 25 ya wahubiri huwa na zoea la kufika baada ya wimbo na sala ya kufungua. Hilo ni jambo la kufikiriwa kwa uzito. Twapaswa kukumbuka kwamba adabu nzuri zatia ndani kutambua hisia za wengine. Yehova, ambaye ni Mkaribishaji wetu mwenye neema, ametuandalia karamu za kiroho kwa manufaa yetu. Twaonyesha tunathamini na kujali hisia zake kwa kufika mapema. Kwa kuongezea, kuchelewa mikutanoni kunakengeusha fikira na huonyesha ukosefu wa staha kwa akina ndugu na dada ambao tayari wameketi.
7 Tunapokutanika, je, sisi hutambua wapya waliohudhuria? Njia moja ya kuonyesha adabu nzuri ni kuwakaribisha. (Mt. 5:47; Rom. 15:7) Salamu changamfu, tabasamu ya kirafiki—ni mambo madogo, lakini huchangia kututambulisha kuwa Wakristo wa kweli. (Yn. 13:35) Baada ya kufika kwenye Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza, mwanamume mmoja alisema hivi: “Kwa siku moja tu nilikutana na watu nisiowajua kabisa wenye upendo wa kweli kuliko watu wa kanisa ambalo nilikulia. Ni wazi kwamba nilikuwa nimeipata kweli.” Kwa sababu hiyo, alibadili maisha yake, na baada ya miezi saba akabatizwa. Naam, adabu nzuri zaweza kuwa na matokeo makubwa!
8 Ikiwa tuna adabu nzuri kuelekea watu tusiowajua tunaokutana nao, je, hatupaswi kuwa hivyo hata zaidi “hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu”? (Gal. 6:10) Kanuni hii yafaa: “Heshimuni uso wa mtu mzee.” (Law. 19:32) Watu kama hao wasipuuzwe kamwe katika mikutano yetu.
9 Kusikiliza kwa Makini: Wakati wa mikutano ya kutaniko, wahudumu Wakristo wa Mungu hutoa hotuba ili kutupa zawadi ya kiroho na kutujenga. (Rom. 1:11) Kwa kweli ungekuwa ukosefu wa adabu kusinzia, kutafuna chingamu kwa sauti, kunong’ona mara kwa mara na mtu anayeketi karibu nawe, kwenda msalani isivyo lazima, kusoma vitabu visivyohusiana na mkutano huo, au kushughulika na mambo mengine wakati wa mkutano. Wazee wanapaswa kuonyesha mfano bora kwa upande huu. Adabu nzuri za Kikristo zitatuchochea tuonyeshe heshima kwa msemaji na ujumbe wake unaohusu Biblia kwa kumsikiliza kwa makini.
10 Kwa kuongezea, ili tusikengeushe fikira za msemaji na wasikilizaji, twapaswa kuzima bipa na simu za mkononi tukiwa mkutanoni.
11 Adabu Kuhusiana na Watoto: Sikuzote wazazi wanapaswa kuwa macho kuona mwenendo wa watoto wao. Mtoto akianza kulia au kusumbua wakati wa mkutano na kusumbua wengine, inafaa kumpeleka mtoto nje mara moja iwezekanavyo ili kumnyamazisha. Nyakati nyingine hilo si rahisi, lakini kumbuka kwamba hiyo yaonyesha uko macho kufikiria hisia za wengine. Wazazi walio na watoto wadogo ambao huenda wakasumbua, mara nyingi huketi nyuma ili wasisumbue watu wengi endapo watalazimika kwenda nje wakati wa mkutano. Bila shaka, wahudhuriaji wengine wanaweza kuonyesha wanazifikiria familia hizo kwa kuziachia viti vya nyuma.
12 Pia wazazi wanapaswa kuangalia jinsi watoto wao wanavyojiendesha kabla na baada ya mikutano. Watoto hawapaswi kukimbia-kimbia ndani ya jengo, kwa kuwa wanaweza kuumia. Pia kukimbia-kimbia nje ya Jumba la Ufalme kwaweza kuwa hatari, hasa jioni wakati mtu haoni vizuri. Kuongea kwa sauti ya juu kwaweza kusumbua majirani na hiyo haitaleta sifa nzuri kwa ibada yetu. Wazazi ambao hufanya jitihada nyingi kusimamia watoto wao ndani na nje ya Jumba la Ufalme wanapasa kupongezwa kwa kuwa kufanya hivyo kutafanya kuishi kwetu kwa umoja kupendeze zaidi.—Zab. 133:1.
13 Kwenye Funzo la Kitabu: Twathamini ukarimu wa ndugu zetu ambao hukubali nyumba zao zitumiwe kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. Tunapohudhuria funzo, twahitaji kuheshimu mali yao. Twapaswa kupangusa viatu vyetu vizuri kabla ya kuingia ili twepuke kuchafua sakafu au zulia. Wazazi wanapaswa kusimamia watoto wao, wakihakikisha kwamba wanaketi katika sehemu iliyotengwa kwa ajili ya funzo la kitabu pekee. Ingawa kikundi chaweza kuwa kidogo na hali iwe ya kistarehe, hatupaswi kujifanya wenyeji kwenye nyumba za wengine. Mzazi anapaswa kumpeleka mtoto wake mchanga msalani. Kwa kuongezea, kwa kuwa funzo la kitabu ni mkutano wa kutaniko, twapaswa kuvalia jinsi tunavyovalia tunapoenda kwenye Jumba la Ufalme.
14 Adabu Nzuri Ni Muhimu: Kujizoeza tabia za Kikristo hakuletei sifa huduma yetu tu, bali pia huendeleza uhusiano mzuri pamoja na wengine. (2 Kor. 6:3, 4, 6) Tukiwa waabudu wa Mungu mwenye furaha, yapaswa iwe rahisi kwetu kutabasamu, tuwe na utu wenye kupendeza na hata kufanya mambo madogo-madogo yenye fadhili ambayo huwaletea wengine shangwe. Sifa hizo zitapamba maisha yetu tukiwa watu wa Mungu.