Sanduku la Swali
◼ Kutaniko linapoombwa kusaidia katika kupanga maziko, huenda maswali yafuatayo yakazuka:
Ni nani anayepaswa kutoa hotuba ya maziko? Huu ni uamuzi wa washiriki wa familia. Wanaweza kuchagua ndugu yeyote aliyebatizwa mwenye msimamo mzuri. Baraza la wazee likiombwa litoe msemaji, kwa kawaida watachagua mzee anayestahili atoe hotuba inayotegemea muhtasari wa Sosaiti. Ijapokuwa hatutapita mpaka kwa kusifu-sifu aliyekufa, ingefaa kukazia sifa zenye kupendeza alizoonyesha.
Je, Jumba la Ufalme laweza kutumiwa? Laweza kutumiwa ikiwa ruhusa imetolewa na baraza la wazee na kama mipango hiyo haivurugi mikutano ya kawaida. Jumba laweza kutumiwa ikiwa aliyekufa alikuwa na sifa nzuri, naye alikuwa mshiriki wa kutaniko au mtoto mchanga wa mshiriki wa kutaniko. Ikiwa mtu huyo alikuwa na sifa mbaya kwa sababu ya mwenendo usio wa Kikristo, au ikiwa kuna mambo mengine ambayo huenda yasiletee kutaniko sifa nzuri, wazee wanaweza kuamua jumba lisitumiwe.—Ona kitabu Huduma Yetu, ukurasa wa 62-63.
Kwa kawaida, Majumba ya Ufalme hayatumiwi kwa maziko ya watu wasio Mashahidi. Mpango wa pekee unaweza kufanywa iwapo watu wa familia yake ni wahubiri waliobatizwa wanaoshirikiana na kutaniko kwa ukawaida. Na pia kama aliyekufa alikuwa anajulikana na watu kadhaa katika kutaniko kwamba alikuwa na mtazamo mzuri kuelekea kweli na alijulikana na watu wengine kuwa mtu mwenye sifa nzuri na mwenendo mnyofu. Na vilevile kama desturi za kilimwengu hazichanganywi na programu hiyo, Jumba la Ufalme laweza kutumiwa.
Ruhusa ya kutumia Jumba la Ufalme inapotolewa, wazee watachunguza kuona kama ni jambo la kawaida jeneza liwepo wakati wa hotuba ya maziko. Ikiwa inatazamiwa hivyo, wanaweza kuruhusu lipelekwe kwenye jumba.
Vipi maziko ya watu wa ulimwengu? Ikiwa aliyekufa alikuwa na sifa nzuri katika jumuiya, ndugu anaweza kutoa hotuba ya Biblia yenye kufariji kwenye chumba cha kuhifadhia maiti au kando ya kaburi. Kutaniko halitakubali kushughulikia maziko ya mtu aliyejulikana kuwa asiye na adili, mwenye mwenendo usiofaa au ambaye mtindo wake wa maisha ulipingana sana na kanuni za Biblia. Bila shaka ndugu hatashiriki pamoja na kasisi katika kufanya programu yenye mchangamano wa dini wala hatashiriki katika maziko yoyote yanayofanywa katika kanisa la Babiloni Mkubwa.
Vipi ikiwa aliyekufa alikuwa ametengwa na ushirika? Kwa ujumla kutaniko halitahusishwa. Jumba la Ufalme halitatumiwa. Ikiwa mtu huyo alikuwa ameonyesha uthibitisho wa toba na alionyesha tamaa ya kurudishwa, huenda dhamiri ya ndugu ikamruhusu kutoa hotuba ya Biblia kwenye chumba cha kuhifadhia maiti au kando ya kaburi, ili kuwatolea wasioamini ushahidi na kuifariji jamaa. Hata hivyo, kabla ya kufanya uamuzi huo, lingekuwa jambo la hekima ndugu huyo kuwasiliana na baraza la wazee na afikirie yale ambayo huenda wakapendekeza. Katika hali ambazo haingekuwa vizuri ndugu huyo ahusike, huenda ikafaa ndugu ambaye ni mshiriki wa familia ya mtu aliyekufa kutoa hotuba kuiliwaza jamaa ile.
Maelezo zaidi yanaweza kupatikana katika matoleo ya Mnara wa Mlinzi ya Oktoba 15, 1990, ukurasa wa 30-31; Januari 1, 1982, ukurasa wa 23; Novemba 15, 1980, ukurasa wa 5-7; Juni 1, 1978, ukurasa wa 5-8 (la Kiingereza); Novemba 1, 1977, ukurasa wa 495-496; Machi 15, 1970, ukurasa wa 191-192 (la Kiingereza); na Amkeni! la Mei 8, 1991, ukurasa wa 22-23 na Januari 8, 1979, ukurasa wa 9-13.