Wasaidie Wengine Wapate Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele
1 Ingawa dini zote hudai kwamba zina mwongozo wenye kutegemeka kuhusu kumtumikia Mungu, mafundisho ya dini hizo hutofautiana. Yesu, “Yule Nabii,” hakufundisha kwamba dini zote ni barabara mbalimbali tu zinazoongoza kwenye wokovu. (Yoh. 7:40; Mt. 7:13, 14) Ingawa Yesu alijua kwamba watu fulani wangekuwa tu na “namna ya ujitoaji-kimungu,” alikuwa na uhakika kwamba wengine wangeipata na kuifuata dini ya kweli.—2 Tim. 3:5; Yoh. 4:23.
2 Wengine wanaweza kujuaje kweli kumhusu Mungu na wamwabudu kwa njia inayokubalika? Tofauti za kidini zaweza kutatuliwa kwa amani watu wanapokubali chanzo cha kweli kinachokubalika kumhusu Muumba wetu. Chanzo hicho ni Biblia. (Yoh. 17:17) Ingawa watu wengi hufuata dini ya wazazi wao au ya jamii yao, watu wanyenyekevu wanaweza tu ‘kumkaribia Mungu’ kikweli kwa kuchunguza Maandiko na kutumia yale wanayojifunza. Kwa kufanya hivyo, wanapata nguvu inayohitajiwa ya kuacha mazoea yote yasiyompendeza.—Yak. 4:8.
3 Broshua Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele? huchunguza kwa staha imani na desturi zinazofuatwa na watu wengi. Kwa kulinganisha imani na desturi hizo na Neno la Mungu, watu wanyoofu watapata ujasiri wa kuacha dini zote za uongo wajapopingwa na jamii na familia yao.—Mt. 10:36; 2 Kor. 6:17, 18.
4 Masomo mawili ya kwanza katika broshua hiyo yanaeleza sababu za kuitumaini Biblia na kuikubali kuwa msingi wa ibada ya kweli. Somo la 3, 4 na 5 lazungumzia mafundisho ya Maandiko kuhusu makao ya roho, wafu na kuwasiliana na roho waovu. Masomo yanayosalia yanawasaidia watu wenye kupendezwa watambue dini ya kweli na kuwachochea watumie yale wanayojifunza. Mifano rahisi inayotokana na mambo ya kawaida inakazia maana ya habari hiyo. Na mambo halisi ya wale walioacha mazoea yenye kudhuru yanathibitisha kwamba Yehova atawasaidia wale wanaotaka kufanya yaliyo sawa na kuepuka yasiyofaa.—Flp. 4:6; Yak. 4:7.
5 Watu wa mataifa yote wanakubali mwaliko wa ‘kuingia kupitia lango jembamba’ na kutembea katika barabara inayoongoza kwenye uhai wa milele. Tuna kila sababu ya kuendelea kuwa na maoni yanayofaa kuhusu huduma yetu na nguvu ya Neno la Mungu ya kuwafanya watu wabadilike. Na tuwaonyeshe wengine kwa usemi na mwenendo wetu hekima ya kufuata dini ya kweli ili wao pia waweze kufurahia baraka za Yehova milele!—Mt. 7:13, 14; 2 Kor. 10:4, 5; Zab. 37:29.