Ratiba ya Familia—Mikutano ya Kutaniko
1 Ikiwa wewe ni mzazi Mkristo, bila shaka unataka watoto wako wawe watu wazima wanaompenda Yehova na kumtumikia, na hatimaye wapate uzima wa milele katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. Unaweza kuwasaidiaje kutanguliza ibada ya Yehova maishani mwao? Njia moja muhimu ni kuwawekea mfano. (Met. 20:7) Akikumbuka mfano wa mama yake aliye Shahidi, dada mmoja alisema hivi: “Tulienda mikutanoni, tupende tusipende.” Hajasahau jambo hilo.
2 Je, familia yako inaelewa kusudi la mikutano? Mafundisho tunayopata katika mikutano hiyo hutuchochea kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu, na ushirika tunaofurahia pamoja na ndugu zetu hututia moyo sana. (Isa. 54:13; Rom. 1:11, 12) Hata hivyo, kusudi muhimu zaidi la mikutano yetu ni kumsifu Yehova “kati ya makundi yaliyokutanika.” (Zab. 26:12) Mikutano ya Kikristo hutupa nafasi ya kuonyesha upendo wetu kwa Yehova na kumwabudu.
3 “Endeleeni Kuangalia Sana”: Kuthamini kusudi takatifu la mikutano yetu kutatuchochea ‘kuendelea kuangalia sana’ ili pole kwa pole tusisitawishe desturi ya kukosa mikutano kwa sababu ya mambo yasiyo muhimu. (Efe. 5:15, 16; Ebr. 10:24, 25) Unapopanga ratiba ya familia, unaweza kuanza kwa kupangia wakati wa mikutano ya kutaniko. Kisha hakikisha kwamba huruhusu mambo mengine yavuruge ratiba hiyo ya mikutano. Hakikisha kwamba uhudhuriaji wa mikutano unatangulizwa katika familia yako.
4 Je, hatuchochewi tunaposoma jinsi ndugu zetu wanavyokabiliana na magumu ili wahudhurie mikutano na makusanyiko? Huenda hukabili hali ngumu sana, hata hivyo, yaelekea unakabili magumu fulani. Shetani hufanya iwe vigumu zaidi kwa watu wa Mungu kumwabudu Yehova. Lakini, uwe na hakika kwamba, bila shaka, watoto wako wataona jinsi familia yenu inavyojitahidi kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Kwa kweli, kwa kufanya hivyo unaweza kuwapa zawadi ya kiroho ambayo hawataisahau kamwe.