Barua Kutoka Kwa Baraza Linaloongoza
Tuna pendeleo kubwa sana. Tukiwa Mashahidi wa Yehova tuna pendeleo, si la kujua tu kwamba Yehova ni Mungu wa pekee wa kweli aliye hai, Muumba wa ulimwengu, bali pia kuitwa kwa jina lake na kumtumikia. Tuna baraka isiyo na kifani jinsi gani!—Isa. 43:12; Ebr. 8:11.
Tuna tumaini la wokovu na agizo la kuhubiri habari njema ya Ufalme ili wengine pia waweze kumwabudu Yehova na kushiriki tumaini letu. (Mt. 24:14; Rom. 10:13, 14; 1 The. 5:8) Pia tuna shangwe ya kuwa sehemu ya udugu wa ulimwenguni pote wa waabudu wenye upendo na wanaojitahidi kusaidiana. Mambo hayo yanathawabisha kama nini!
Kwa kufaa, Biblia inatupa mwaliko huu: “Mtumikieni BWANA kwa furaha . . . . Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru, nyuani mwake kwa kusifu. Mshukuruni, lihimidini jina lake; kwa kuwa BWANA ndiye mwema; rehema zake ni za milele; na uaminifu wake vizazi na vizazi.” (Zab. 100:2-5) Ili kumtumikia Yehova kwa shangwe ni lazima tuwe na uhusiano wa kibinafsi na wa karibu pamoja naye. Yeye hutusaidia kuwa na uhusiano wa aina hiyo, na tuna pendeleo la kuusitawisha. Tunapokuwa na uhusiano huo, tunajua kwamba Yehova yuko tayari wakati wowote kutusaidia na kutuimarisha tunapokuwa na taabu. Tunakuwa na hakika kwamba yeye atatuandalia nguvu na mwelekezo wa kiroho unaohitajiwa ili kukabiliana na magumu ya siku hizi za mwisho za mfumo huu wa mambo. Tujapokabiliana na mikazo, tuna shangwe katika utumishi wetu, na tunamshukuru Yehova kila siku kwa sababu Neno lake linatukumbusha kwamba ‘yeye hutujali sisi.’—1 Pet. 5:7.
Kwa kweli, Yehova alitubariki sana mwaka uliopita. Kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa “Watekelezaji wa Neno la Mungu,” tulisisimuka kuwa pamoja na maelfu ya watu wenye imani yenye thamani kama sisi, tukiimba na kulishwa pamoja katika meza ya kiroho ya Yehova. Kwenye Mafunzo yetu ya Kitabu ya Kutaniko, tulifurahia funzo lenye kuimarisha imani tuliposoma pamoja kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! Na zaidi ya hayo tulisisimuka kama nini tulipopokea Buku la Kwanza la kitabu kipya, Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote! ‘Kikombe chetu kimefurika.’—Zab. 23:5.
Ni shangwe iliyoje kujua kwamba tukiwa mamilioni, ndugu na dada wa kiroho, tunamtumikia Yehova kwa umoja! Jinsi inavyotia moyo kusoma kuhusu vilele vipya tulivyofikia katika utumishi wa shambani! Tunafurahi kwamba mamilioni walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Bwana wetu ijapokuwa hali ngumu za ulimwengu. Tutazamapo eneo la ulimwenguni pote, ni wazi kwamba “kwa kweli, mavuno ni mengi.” (Luka 10:2) Kwa wastani, wanafunzi wa Biblia 5,555 walifanya maendeleo kila juma kufikia wakfu na ubatizo mwaka uliopita. Ingawa mavuno ni mengi zaidi katika sehemu fulani za dunia kuliko sehemu nyinginezo, sote tunapendezwa sana na yale ambayo Yehova anatufanyia. Tunaona uthibitisho hakika wa baraka zake kwa jitihada za pamoja za watumishi wake.
Ujenzi wa Majumba ya Ufalme mapya umekuwa sababu nyingine ya kutuletea shangwe! Tunafurahi kuona jinsi kazi hii inavyoungwa mkono kwa moyo wote na ndugu na dada zetu katika nchi zinazositawi. Wafanyakazi wa kujenga Majumba ya Ufalme waliozoezwa ifaavyo tayari wamesaidia kujenga mamia ya Majumba ya Ufalme. Ndugu hawa hutembelea makutaniko mbalimbali katika nchi zao wenyewe kuongoza miradi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Kwa kuwa bado maelfu ya Majumba ya Ufalme yanahitaji kujengwa, kuna uhitaji wa wafanyakazi wa kujitolea katika nchi zinazositawi kusaidia katika kazi hii ya muhimu. Iwapo unaishi katika mojawapo ya nchi hizi, je unaweza kujitolea? Jinsi ndugu na dada zetu wanavyothamini sana kukutana kwa ajili ya ibada katika Jumba la Ufalme lao wenyewe! Nao ni wenye shukrani kama nini kwa msaada wa kifedha unaotolewa na udugu wa ulimwenguni pote kufanya jambo hilo liwezekane!
Tunafurahi sana tunapopata habari za ushindi wa kesi za kutetea ibada yetu. Hata hivyo, katika sehemu nyingi pia kuna watu mashuhuri ambao wangependa kukomesha ibada ya Yehova. Tunapokabiliana na hali hizi, tuna hakika kwamba hata wapinzani wetu wawe wengi kadiri gani na hata tuwe tunaonekana kuwa dhaifu namna gani, Yehova atatusaidia. (2 Nya. 14:11) Tunawapongeza nyinyi nyote ndugu na dada mnaoendelea kusimama imara katika ibada ya kweli.
Endeleeni kuimarisha imani yenu na kutegemea sana uongozi wa Yehova mnapotimiza kwa shangwe madaraka yenu ya Kikristo. (Mit. 3:5, 6) Tusivunjike moyo haidhuru mambo ambayo huenda adui akaruhusiwa kututendea. Kumbuka jinsi Elisha alivyomtia moyo mtumishi wake mwenye wasiwasi: “Usiogope; maana walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.” (2 Fal. 6:15-17) Leo, kama ilivyokuwa katika siku za Elisha, majeshi ya Yehova ya kimbingu yako tayari kulinda masilahi ya ibada safi. Tuna tumaini hakika la wakati ujao. Yehova anaongoza mambo. Mataifa hayawezi kumshinda. Yeye amemtawaza Mwana wake na kumpa mamlaka yote ya utawala. “Heri wote wanaomkimbilia.”—Zab. 2:1-6, 12.
Enyi ndugu na dada wapendwa, kumbukeni kwamba tunawafikiria sana kwa upendo wenye shauku nyingi siku zote. Sala yetu ya kutoka moyoni ni kwamba kila mmoja wenu ‘asimame akiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu.’—Kol. 4:12.
Ndugu zenu,
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova