Tumekabidhiwa Hazina
1 Mtume Paulo alithamini utume wa kuhubiri aliopewa na Mungu naye akaurejezea kuwa “hazina.” (2 Kor. 4:7) Alivumilia hali ngumu na mnyanyaso alipotimiza utume huo. Alimhubiria bila kuchoka mtu yeyote aliyekutana naye. Alifunga safari nyingi ngumu na zenye hatari kwenye nchi kavu na baharini. Tunaweza kumwigaje Paulo na kuonyesha kwamba tunathamini huduma yetu? (Rom. 11:13) Ni nini kinachofanya huduma yetu iwe hazina isiyo na kifani?
2 Hazina Yenye Thamani Zaidi: Mara nyingi hazina za kidunia humletea mtu maumivu ya moyo na manufaa ya muda tu. Kwa upande mwingine, huduma yetu hutuletea sisi na wengine manufaa ya kudumu. (1 Tim. 4:16) Huduma hiyo huwasaidia watu wanyoofu kumjua Yehova, kufanya mabadiliko yanayohitajika maishani, na kupata tumaini halisi la uzima wa milele. (Rom. 10:13-15) Tunapoona huduma yetu kuwa kitu chenye thamani, tunapata kusudi lenye kuridhisha maishani, hisia ya kudumu kwamba tumetimiza jambo muhimu, na tumaini lenye kutia-moyo kwa ajili ya wakati ujao.—1 Kor. 15:58.
3 Onyesha Kwamba Unathamini Hazina Yako: Mara nyingi tunapojidhabihu tunaonyesha tunakithamini kitu kwa kadiri gani. Ni pendeleo kama nini kutumia wakati na nguvu zetu kumsifu Yehova! (Efe. 5:16, 17) Njia ambayo sisi hutumia wakati wetu inapaswa kuonyesha kwamba tunathamini zaidi mambo ya kiroho badala ya mambo ya kimwili. Kwa kuwa tuna kitu chenye thamani sana cha kuwapa wengine, bila shaka tutahubiri kwa uchangamfu na kuwa chonjo kuhubiri habari njema kila tunapopata nafasi.
4 Kwa kawaida, sanaa zenye thamani hazifichwi, bali huwekwa wazi katika majumba ya maonyesho ili kila mtu afurahie kuziona. Tukiona huduma yetu kuwa yenye thamani, itakuwa jambo kuu maishani mwetu. (Mt. 5:14-16) Tukiwa na mioyo iliyojawa uthamini, sikuzote na tumwige mtume Paulo kwa kutumia kila nafasi kuonyesha tunathamini kikweli huduma yetu, na kuiona kuwa hazina.