“Endeleeni Kufanya Hivi kwa Kunikumbuka Mimi” Ukumbusho wa Kifo cha Yesu Utakuwa Aprili 2
1 Mnamo Aprili 2, 2007, mamilioni ya watu ulimwenguni pote watakusanyika kukumbuka kifo cha Yesu cha kidhabihu. Yesu alikufa kwa sababu alitetea enzi kuu ya Baba yake wa mbinguni, na hivyo akathibitisha kwamba Shetani Ibilisi alisema uwongo alipodai kwamba wanadamu wanamtumikia Mungu kwa kuchochewa tu na ubinafsi. (Ayu. 2:1-5) Mlo wa Jioni wa Bwana hutukumbusha pia kwamba kupitia kifo chake akiwa mwanadamu mkamilifu asiye na dhambi, Yesu ‘alitoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mt. 20:28) Kwa hiyo, Yesu aliwaamuru wanafunzi wake hivi: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Je, uthamini wako kwa zawadi hiyo yenye thamani kutoka kwa Mungu umekuchochea uanze kujitayarisha ili kukumbuka tendo hilo kubwa zaidi la upendo?—Yoh. 3:16.
2 Tayarisha Moyo Wako: Kufikiria mambo yaliyotukia katika kila mojawapo ya siku za mwisho za maisha ya Yesu akiwa mwanadamu, kutatuwezesha kutayarisha moyo wetu kwa ajili ya Ukumbusho. (Ezra 7:10) Ili kutusaidia kufanya hivyo, kuna ratiba ya usomaji wa Biblia wa pekee katika kijitabu Kuyachunguza Maandiko—2007 na Kalenda ya Mwaka wa 2007. Ratiba hiyo ya usomaji imepangwa kupatana na siku ambazo matukio yanayohusiana na kifo cha Yesu yalitukia kulingana na kalenda tunayotumia leo. Siku na tarehe zinazotajwa katika masimulizi hayo ya Biblia zinategemea kalenda ya Kiyahudi. Katika kalenda hiyo siku huhesabiwa kuanzia kushuka kwa jua mpaka kushuka kwa jua. Tofauti hiyo ya kuhesabu siku imezingatiwa katika ratiba ya usomaji wa Biblia wa Ukumbusho. Kusoma habari hiyo tena na kutafakari kwa sala kuhusu upendo mwingi wa Mungu, kutatusaidia kufaidika kikamili na Ukumbusho.
3 Waalike Wengine Wahudhurie: Nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari ilitangaza kampeni ya pekee ya kuwaalika watu kwenye tukio hilo muhimu. Je, umefanya mipango ili ushiriki kikamili katika kampeni hiyo? Je, umetayarisha orodha ya watu unaowafahamu ambao utawaalika, na umeanza kuwasiliana nao? Panga kufika mapema jioni hiyo ya Ukumbusho ili uwakaribishe wale ambao uliwaalika na wengine wanaopendezwa. Itafaa uketi nao na kuhakikisha wana Biblia na kitabu cha wimbo. Wajulishe kwa wengine kutanikoni. Baki baada ya programu ili kujibu maswali yao. Waalike kwenye hotuba ya pekee ya watu wote itakayotolewa Aprili 15. Wazee hasa wahakikishe kwamba washiriki wa kutaniko ambao si watendaji wamealikwa kuhudhuria Ukumbusho na hotuba ya pekee.
4 Wasaidie Wahubiri Wasiotenda na Wale Ambao Wameanza Kupendezwa Karibuni Wafanye Maendeleo: Msemaji wa hotuba ya Ukumbusho ataeleza kwa ufupi mpango wetu wa kujifunza Biblia na kuwatia moyo wale wanaopendezwa waendelee kujifunza kumhusu Yehova. Kupatana na maelezo yake, unaweza kuwaeleza wale ambao umewaalika kwamba ungependa kuwasaidia kumjua Yehova. Ikiwa hawajaanza kujifunza Biblia, watembelee haraka baada ya Ukumbusho na uwaonyeshe jinsi funzo la Biblia linavyofanywa bila malipo. Ili wafanye maendeleo ya kiroho, watahitaji pia kuhudhuria mikutano ya kutaniko. (Ebr. 10:24, 25) Watie moyo waanze kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Wazee wanapaswa kuwatembelea Wakristo wasiotenda ambao walihudhuria Ukumbusho na kuwatia moyo watafakari mambo yaliyosemwa katika hotuba. Huenda hilo likawachochea kuwa watendaji tena kutanikoni.
5 Ukumbusho unaandaa fursa ya kutafakari kwa uzito mambo ambayo Yehova na Yesu wametufanyia. Kutafakari mambo hayo hutufanya tuwapende zaidi na kujiendesha ifaavyo. (2 Kor. 5:14, 15; 1 Yoh. 4:11) Sasa ndio wakati wa kuanza kujitayarisha na kuwatayarisha wanaopendezwa kwa ajili ya tukio hilo muhimu ambapo ‘tunakitangaza kifo cha Bwana.’—1 Kor. 11:26.
[Maswali ya Funzo]
1. Kwa nini Aprili 2, 2007, ni tarehe muhimu?
2. Tunaweza kutayarishaje moyo wetu kwa ajili ya Ukumbusho?
3. Tunaweza kuwasaidiaje watu wanaopendezwa na wasiotenda wafaidike na Ukumbusho?
4. Tunaweza kuwasaidiaje watu waendelee kufanya maendeleo ya kiroho baada ya Ukumbusho?
5. Tunaweza kufaidikaje kwa kuhudhuria Ukumbusho?