Wafariji Waliovunjika Moyo
1 Katika historia ya wanadamu, hakujawa na wakati mwingine kama huu ambao wanadamu wanahitaji faraja. Kwa kufuata mfano wa Mfalme wetu, Kristo Yesu, sisi pia hujitahidi “kufunga majeraha ya waliovunjika moyo.”—Isa. 61:1.
2 Jinsi ya Kuwafikia: Ili kuwafariji watu, tunapaswa kuzungumzia mambo yenye usawaziko na yenye kutia moyo katika huduma yetu. Tunajitahidi kuzungumzia kidogo tu kuhusu matendo mabaya ya ulimwengu na mafundisho ya uwongo, lakini tunazungumzia hasa kweli za Maandiko na tumaini zuri la ahadi za Mungu zenye kufariji. Lakini hilo halimaanishi kwamba tusizungumze kuhusu Har–Magedoni. Utume wetu ni kutangaza “mwaka wa nia njema upande wa Yehova na siku ya kisasi upande wa Mungu wetu,” na vilevile “kumwonya mwovu aiache njia yake ya uovu.” Hata hivyo, maonyo kuhusu Har–Magedoni na ufafanuzi kuhusu uharibifu wake hayapaswi kuficha kichwa chetu kikuu, yaani, habari njema ya Ufalme wa Mungu.—Isa. 61:2; Eze. 3:18; Mt. 24:14.
3 Nyumba kwa Nyumba: Ni jambo la kawaida kuwakuta watu walioshuka moyo kwa sababu ya magonjwa, kufiwa na mpendwa, ukosefu wa haki, au matatizo ya kiuchumi. Tukiwa waigaji wa Kristo, ‘tunawasikitikia’ na kuwaonyesha huruma wale tunaokuta katika huduma. (Luka 7:13; Rom. 12:15) Ingawa tutasoma andiko moja au mawili yanayohusiana na tatizo hilo, tunapaswa kuwa ‘wepesi kuhusu kusikia,’ na hivyo kumruhusu mwenye nyumba aeleze hisia zake. (Yak. 1:19) Baada ya kusikiliza, tuna nafasi nzuri ya kutoa faraja.
4 Wakati unaofaa katika mazungumzo, tunaweza kusema, “Ningependa kukueleza maneno yenye kutia moyo kutoka katika Biblia.” Utambuzi unahitajika ili tusipinge maoni yote yenye kasoro ambayo mtu huyo anaweza kutoa. Badala ya hivyo, tunapaswa kukazia fikira jinsi ya kumtia moyo na kumfariji kwa kutumia Maandiko kuimarisha moyo wake. Kuhusu jambo hilo, huenda ukapenda kuchunguza kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko ukurasa wa 106-110 chini ya kichwa “Kitia-Moyo.” Au unaweza kumpa mwenye nyumba trakti yenye kichwa Faraja kwa Walioshuka Moyo na mpitie habari yenye kutia moyo inayopatikana humo.
5 Tafuta Nafasi za Kuwafariji Wengine: Je, unamfahamu jirani, mfanyakazi mwenzako, mwanafunzi mwenzako, au mshiriki wa familia ambaye anahitaji kutiwa moyo? Mbona usijitahidi kuwatembelea watu hao nyumbani kwao ukiwa na lengo la kuwafariji kwa kutumia Maandiko? Ukijua sababu inayowafanya wahitaji kufarijiwa, unaweza kutayarisha kwa ajili ya hali yao. Wengine wameandika barua au wakawapigia simu. Upendo wa kweli kuelekea jirani utatuchochea kuonyesha hisia-mwenzi na kutoa faraja inayohitajika kwa kutumia Maandiko.—Luka 10:25-37.
6 Naam, tumepewa utume wa kuwafariji wanaoomboleza, kuitia moyo mioyo iliyohuzunika, na kuwapa watu tumaini la wakati ujao mzuri. Hiyo ndiyo faraja ambayo watu ulimwenguni pote wanahitaji. Kuzungumza kwa shangwe kuhusu mambo mengi mazuri ambayo Mungu ameahidi kutawafariji na kuwatolea tumaini watu wenye mioyo minyoofu. Sikuzote na tukumbuke uhitaji wa kufunga majeraha ya waliovunjika moyo.