Ripoti ya Ulimwenguni Pote
◼ ASIA NA MASHARIKI YA KATI
Idadi ya nchi: 47
Idadi ya watu: 3,896,182,946
Idadi ya wahubiri: 582,360
Idadi ya mafunzo ya Biblia: 453,069
Kyrgyzstan: Svetlana, ambaye ni painia msaidizi, hakuweza kumpata mtu yeyote katika nyumba fulani kwenye eneo lake. Siku moja alipokuwa kwenye eno hilo, aliamua tena kubisha mlango wa nyumba hiyo ingawa hakudhani angempata yeyote. Alishangaa na kufurahi alipomkuta mwanamke fulani kijana. Mwanamke huyo alifurahi sana kutembelewa na Shahidi wa Yehova naye akasema kwamba alikuwa akijifunza Biblia hapo awali, lakini hakujua jinsi ambavyo angeweza kuwapata tena akina ndugu. Svetlana alimuuliza kama angependa kupata magazeti kwa ukawaida. Mwanamke huyo alijibu kwamba anataka magazeti na pia funzo la Biblia. Funzo lilianzishwa mara moja, na sasa mwanamke huyo huhudhuria mikutano ya Kikristo.
Japani: Dada wawili waliokuwa wakihubiri kwenye eneo la biashara waliingia ofisini mwa wakili anayejulikana kwa kuwasaidia maskini. Walimkuta mwanamke fulani aliyekataa kuwasikiliza na kusema kwamba ana shughuli nyingi, lakini akakubali kuchukua magazeti. Mwanamke huyo alikuwa peke yake dada hao walipofaulu kumpata tena. Hata kabla hawajamsalimu, aliwauliza hivi kwa hasira: “Kwa nini watoto wasio na hatia huuawa? Kwa nini ulimwengu uko hivi? Ninataka majibu yenye kusadikisha! Mkiwa nayo, niambieni!” Walizungumzia suala la enzi kuu ya ulimwengu kwa muda wa saa moja, na polepole mtazamo wa mwanamke huyo ukabadilika. Aliwashukuru dada hao kwa kutumia Biblia kujibu maswali yake ambayo alidhani hayawezi kujibiwa. Dada hao walipoondoka, mwanamke huyo aliwapa namba yake ya simu na akawaeleza mahali anapoishi, kisha akasema: “Kwa kawaida ni marafiki wangu wa karibu tu ninaowapa namba yangu ya simu na kuwaeleza mahali ninapoishi, lakini ninyi ni tofauti. Ninataka kuongea nanyi tena. Mambo ambayo tumezungumzia ni muhimu sana.” Funzo la Biblia likaanzishwa.
Nepal: Mwanamke fulani alienda kanisani miaka nenda miaka rudi, lakini fitina na pupa za wafuasi wa kanisa hilo zilimuudhi. Ijapokuwa mume wake alikuwa kasisi, alifukuzwa kanisani wakati mzozo ulipotokea kuhusu michango. Alianza kunywa kupindukia na akaacha kuiruzuku familia yake. Mwanamke huyo alianza kutafuta kweli kwa bidii na alisali kila siku. Ili kutegemeza familia yake, alianza kufanya kazi mahali ambapo watu hupeleka vitabu na karatasi zisizo na kazi. Siku moja alipata kitabu Wenye Umoja Katika Ibada ya Mungu wa Pekee wa Kweli miongoni mwa magazeti na vitabu alivyokuwa akipanga. Alikificha katika mavazi yake na kwenda nacho nyumbani. Alikisoma kila siku na akaendelea kusali. Siku moja painia wa pekee anayeitwa Bishnu alibisha hodi nyumbani kwa mwanamke huyo. Alipenda yale ambayo Bishnu alimwambia naye akamkaribisha. Mwanamke huyo alitambua pole kwa pole kwamba mambo ambayo Bishnu alikuwa akimwambia yalifanana na yale aliyokuwa amesoma katika kile kitabu alichokuwa amepata. Hatimaye alimwonyesha Bishnu kitabu hicho. Mwanamke huyo alifurahi sana kujua kwamba ni kimojawapo cha vitabu vyetu. Sasa yeye hujifunza Biblia kwa ukawaida na yeye na watoto wake huhudhuria mikutano yote.
Sri Lanka: Kabla ya kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, Punchibanda aliamua kuhubiri ujumbe wa Ufalme kila alipopata nafasi. Aliongea na ombaomba fulani aliyemwambia kwamba binti yake mkubwa alipatwa na ugonjwa fulani na akafa. Awali walihudhuria ibada katika kanisa fulani (Assemblies of God) wakitumaini kwamba angeponywa kimuujiza, lakini wapi! Punchibanda alieleza kwamba Mungu hawaponyi watu kimuujiza siku hizi bali wagonjwa wote wataponywa wakati Ufalme wa Mungu utakapotawala. Alimpa ombaomba huyo magazeti yanayozungumzia habari hiyo, kisha akamwalika kwenye Jumba la Ufalme. Ombaomba huyo alienda nyumbani na akawaambia watu wa familia yake kuhusu mwaliko huo na kuwaonyesha yale magazeti. Mke wake alimwambia kwamba hata yeye alikuwa amepewa magazeti na kualikwa kwenye Jumba la Ufalme. Mwanamume huyo aliamua kwenda kwenye Jumba la Ufalme peke yake kwanza. Ndugu na dada walimkaribisha kwa shauku. Sasa yeye, mke wake, mwana wao, na binti zao wawili, huhudhuria mikutano yote na wanafurahia sana kushirikiana na watu wa Yehova.
Lebanoni: Dada painia wa pekee ambaye anatoka Filipino anasema hivi: “Nilikutana na mwanamke fulani Mfilipino nilipokuwa nikihubiri barabarani. Nilimtembelea kazini na nikaanza kujifunza Biblia naye. Alikuwa na maswali mengi. Nyakati nyingine hata sikuweza kumaliza kujibu swali moja kabla hajauliza lingine. Hatimaye marafiki wake wa karibu, waliokuwa wafuasi wenye bidii wa kanisa lao, walianza kumpinga. Ijapokuwa nilimtia moyo aendelee kujifunza Biblia, nilisikitika alipoacha kwa sababu ya upinzani huo. Hata hivyo, niliwaza, ‘Ikiwa yeye ni mnyenyekevu, siku moja ataanza kujifunza tena.’ Mwaka mmoja ulipita, na bado nilimkumbuka, kwa hiyo nilimwandikia na kumwambia kwamba ninamfikiria na ningefurahi kumwona tena. Alinipigia simu, nami nikamtembelea. Wakati huo nilitambua kwamba anapendezwa hata zaidi kuliko hapo awali. Bado alikumbuka mambo tuliyokuwa tumejifunza na aliyathamini kwa moyo wote. Aliniambia kwamba alikuwa amehudhuria ibada katika makanisa mengi lakini hakuna hata moja lililofundisha kweli. Kwa hiyo alianza tena kujifunza, akafanya maendeleo, na sasa amebatizwa. Mwana wake aliye na miaka 12 ni mhubiri ambaye hajabatizwa.”
India: Dada fulani anaandika hivi: “Tulipokuwa tukihubiri nyumba kwa nyumba tulimwona msichana mdogo ambaye aliingia nyumbani mwao alipotuona. Punde si punde, tulikutana na mtu aliyetuamuru twende zetu. Tulipokuwa tukiondoka tulimwona yule msichana akiongea na mtu huyo. Baadaye, tulipokuwa tukingojea basi, msichana huyo alitujia kwa baiskeli na kutuambia hivi: ‘Ninajua kwamba Yehova ni Mungu wa kweli. Tafadhali nifundisheni Biblia. Niliingia nyumbani ili niwakaribishe, lakini mwenye nyumba hakukubali.’ Tulimuuliza jinsi alivyopata kujua kwamba Yehova ni Mungu wa kweli. Alisema kwamba miaka miwili iliyopita alikuwa akisafiri kwa basi alipowaona watu wengi waliokuwa wamekusanyika. Alifikiri kwamba huo ni mkutano wa Kikristo. Mkutano huo ulikuwa kusanyiko letu la wilaya. Alishuka kutoka katika basi na akahudhuria kusanyiko hilo siku zote tatu. Tangu wakati huo alikuwa amewatarajia Mashahidi wa Yehova waje nyumbani kwao. Tulitambua kwamba anapendezwa na tukampeleka nyumbani kwa dada fulani na kuanzisha funzo la Biblia. Ameanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na anafanya maendeleo ya kiroho.”
◼ AFRIKA
Idadi ya nchi: 56
Idadi ya watu: 781,767,134
Idadi ya wahubiri: 1,015,718
Idadi ya mafunzo ya Biblia: 1,820,540
Uganda: Lucy ni Shahidi anayefanya kazi katika hospitali fulani. Yeye na baadhi ya wafanyakazi wenzake waliitwa kuapa kwamba si wao walioiba kiasi kikubwa cha pesa ambacho wakaguzi waligundua kimepotea. Badala ya kushika Biblia na kuapa kwamba hana hatia, Lucy alifungua andiko la Methali 15:3 na kulisoma kwa sauti: “Macho ya Yehova yako kila mahali, yakiwaangalia wabaya na wema.” Kimya kilitanda chumbani humo, na punde yule mwenye hatia akamwendea msimamizi na kukiri kwamba yeye ndiye aliyeiba pesa hizo. Msimamizi alipendekeza kwamba kuanzia wakati huo, wote wakumbuke “andiko la Lucy.” Baadaye, mshahara wa Lucy uliongezwa, naye akakabidhiwa funguo za hospitali hiyo.
Benin: Josué amekabili dhihaka nyingi shuleni. Alipotoa jibu lisilo sahihi darasani, baadhi ya wanadarasa walimdhihaki kwa kusema: “Wewe, kasisi wa Yehova, unawezaje kukosea?” Wengine waliwaunga mkono kwa kusema maneno kama vile, “Yeye huzurura na mkoba wake saa zote.”
Josué anakiri, “Niliogopa hasa kukutana na wanadarasa wenzangu nilipohubiri mwishoni mwa juma.” Alisali kuhusu jambo hilo na akamwomba mzee fulani mashauri. Mzee huyo alimhimiza Josué asirudi nyuma bali atumie wakati mwingi zaidi katika huduma na awatolee wanadarasa wenzake vitabu na magazeti. Josué amefanikiwa kwa njia tatu. Anasema hivi: “Sasa mimi hutumika kama painia msaidizi mara kwa mara. Ninajifunza Biblia pamoja na wanadarasa wawili waliokuwa wakinidhihaki. Pia, maksi zangu zimeboreka sana sasa.”
Ethiopia: Miaka miwili hivi iliyopita, mwanamke anayeitwa Elsa alipoteza leseni yake ya kuendesha gari. Asnakech aliipata na akapanga aende kumwona Elsa ili amrudishie leseni yake. Elsa alishangazwa na unyoofu wa Asnakech na akataka kumpa pesa. Asnakech alikataa pesa hizo na akamtolea Elsa broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Siku iliyofuata Elsa alianza kujifunza Biblia. Alimwambia Asnakech kwamba tayari analijua jina la Yehova kwa sababu baba yake ambaye ni kasisi alikuwa amemweleza kulihusu. Mume wa Elsa alianza pia kujifunza baada ya familia nzima kuhudhuria kusanyiko la wilaya. Hata hivyo, baba ya Elsa alipogundua jambo hilo akafoka kwa hasira na kusema kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wasiofaa kitu. Elsa aliazimia kuendelea kujifunza Biblia na akamwambia baba yake kwa upole kwamba maoni yake kuwahusu Mashahidi si sawa. Kasisi huyo aliudhika na akachukua broshua ya binti yake bila kumwambia. Aliisoma mara kadhaa na akavutiwa na yale aliyosoma. Baada ya kuisoma, hakuwabariki wapita-njia tena katika jina la Utatu kama alivyozoea kufanya. Muda si mrefu, watu walianza kumwita “mwasi-imani,” na baadhi yao wakataka kumpiga. Kwa hiyo, akahamia Addis Ababa na kuanza kujifunza Biblia. Elsa na watu saba wa jamaa yao sasa ni Mashahidi ambao wamebatizwa. Mume wake na mtoto wake wanafanya maendeleo.
Côte d’Ivoire: Anderson alimwachia mwenye duka fulani broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Mwenye duka huyo alikuwa akisoma Biblia kwa ukawaida. Muda si muda, funzo la Biblia likaanzishwa. Mtu huyo alipendezwa hasa na somo lenye kichwa, “Maisha ya Familia Yanayompendeza Mungu.” Alisema: “Sikujua kwamba kila mmoja katika ndoa ana wajibu. Hapo awali niliporudi nyumbani usiku sikutaka kusikiliza malalamiko ya mke wangu. Nilizoea kumwambia: ‘Mimi ni mume, na nina haki ya kuondoka nikitaka; wewe nawe ni mke, ni wajibu wako kutunza nyumba.’ Sasa mimi hurudi nyumbani mara moja baada ya kazi na kumsaidia mke wangu kufanya kazi za nyumbani.”
Kenya: Mwanafunzi wa darasa la pili mwenye miaka saba alisikia kuhusu ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Juma moja kabla ya ziara hiyo, alimwendea mwalimu mkuu na kumwomba ruhusa ya kuhudhuria mikutano ya Jumanne alasiri. Alipewa ruhusa. Lakini mvulana huyo alipofika shuleni siku iliyofuata, aliambiwa arudi nyumbani akawalete wazazi wake na yule mgeni. Kwa hiyo, mwangalizi wa mzunguko aliandamana na baba ya huyo mvulana kwenye shule hiyo. Yule mwalimu mkuu alishtuka kuona kwamba kwa kweli kulikuwa na mgeni, na kwamba alikuwa ametembea kwa muda wa saa moja akipanda milima yenye miteremko mikali ili aje kumwona. Alikubali kuchukua vitabu na magazeti na sasa yeye ni mwenye urafiki na yuko tayari kusaidia.
Malawi: Alipokuwa akihubiri, ndugu fulani alisumbuliwa mara nyingi na mtu fulani mwenye baiskeli. Kwa kawaida mtu huyo alipomwona ndugu akihubiri, alisimama na kuanza kubishana naye. Hata alijaribu kumnyang’anya ndugu Biblia yake. Siku moja huyo mtu alipita mahali ambapo ndugu alikuwa akiongoza funzo la Biblia. Alipojaribu kurekebisha kitu fulani kwenye baiskeli yake, aliingiza mkono kwenye gurudumu na kujeruhiwa vibaya. Ijapokuwa mtu huyo alikuwa na maumivu makali hakuna yeyote aliyemsaidia ila ndugu yetu, ambaye alifunga majeraha yake na kupanga apelekwe hospitalini. Baadaye ndugu yetu alimtembelea mtu huyo nyumbani kwake. Jamaa huyo aliaibika sana kwa sababu ya tabia yake, na akakiri kwamba alikuwa ameathiriwa na uvumi. Alisema hivi: “Ninyi mnamwabudu Mungu wa kweli. Sikuzote nilikunyanyasa. Sikufikiri kamwe ungenitendea kwa fadhili.”
Kamerun: Dada kijana alikuwa ameketi katika chumba cha kungojea cha hospitali wakati mgonjwa fulani mkongwe alipoingia. Mkongwe huyo alilazimika kusimama kwa sababu viti vyote vilikuwa vimekaliwa. Dada anasema: “Nilimhurumia na kumpa kiti changu. Watu wote waliokuwa chumbani humo walianza kunong’onezana kwa sababu nilimpa kiti changu na pia zamu yangu ya kumwona daktari. Punde mwanamke mmoja akanijia na kutaka kujua dini yangu. Nilimwambia kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova. Alinipongeza na kusema kwamba si vijana wengi ambao wangetenda kama nilivyotenda. Nilitumia nafasi hiyo kumhubiria yeye na wale wengine kwa kutumia trakti kadhaa nilizokuwa nazo. Nilijibu maswali yao mengi. Baadhi ya wale nilioongea nao walibadili maoni yao kuwahusu Mashahidi wa Yehova na wakasema kwamba wangependa Mashahidi wawatembelee nyumbani kwao.”
Togo: Ndugu kadhaa waliokuwa wakihubiri katika eneo la mbali, walimpata mwanamume kijana aliyefurahi sana kukutana nao. Aliwaonyesha vitabu viwili vya kuandikia. Katika vitabu hivyo alikuwa amenakili kwa mkono kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani na sehemu ya kitabu kingine cha kujifunzia Biblia (“Make Sure of All Things”). Alikuwa ameishi na kasisi fulani kwa muda na alikuwa ameviona vitabu hivyo viwili nyumbani kwake. Kasisi huyo alikuwa amepanga vitabu vyake kwenye sehemu mbili, sehemu moja yenye vitabu alivyovipenda sana, na nyingine yenye vitabu ambavyo aliviona kuwa si vya maana. Kijana huyo alipata vitabu vyetu katika ile sehemu yenye vitabu visivyo vya maana. Baada ya kusoma kurasa chache tu za kimojawapo cha vitabu hivyo, alivutiwa sana na ujumbe wake. Hakuweza kwenda nacho na hakujua mahali ambapo angeweza kupata kingine, kwa hiyo alikinakili. Alipoanza kuwaeleza wengine kuhusu yale aliyokuwa amesoma, mama yake na yule kasisi walimpinga. Ndugu walimpa vitabu vingine na wanamsaidia kufanya maendeleo ya kiroho.
Afrika Kusini: Thandi ambaye ni Shahidi, aliombwa na mwajiri wake aongee na mfanyakazi mwenzake, Bella, aliyekuwa na matatizo ya ndoa. Bella alikuwa ameamua kumtaliki mume wake ambaye ni polisi na ambaye alikuwa amempiga na kumuumiza kihisia. Thandi alimpa Bella nakala mbili za kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia na akamhimiza ampe mume wake nakala moja. Baada ya juma moja, Thandi aliongea na Bella aliyemwambia kwamba mume wake anasoma kitabu hicho na kwamba sasa kuna amani nyumbani mwao. Miezi mitatu baadaye, Bella alimwambia Thandi kwamba Mungu ameokoa ndoa yake kupitia sala na kitabu Furaha ya Familia. Mwajiri wa Bella aliposikia jambo hilo, alipendekeza kwamba wafanyakazi wote 2,000 wapewe nakala za kitabu hicho. Thandi amewapa wafanyakazi wenzake nakala 96 za kitabu Furaha ya Familia. Kampuni hiyo ilitoa mchango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova.
◼ AMERIKA
Idadi ya nchi: 56
Idadi ya watu: 879,073,403
Idadi ya wahubiri: 3,199,835
Idadi ya mafunzo ya Biblia: 3,022,276
Venezuela: Hivi majuzi namba ya simu ya familia fulani ya Mashahidi ilibadilishwa. Lakini, kwa sababu ya hitilafu fulani, watu waliotaka kuwasiliana na kituo kimoja cha televisheni ili waongee na mwanamke anayebashiri kwa kutazama nyota, walianza kupiga namba hiyo. Watu wa familia hiyo waliamua kutumia hali hiyo vizuri. Ili kuwasaidia watu hao waliopiga simu, familia hiyo ilitafuta habari na maandiko machache ya Biblia katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko. Graciela, mama yao, akawa stadi wa kuwahubiria watu hao. Mwanamke mmoja aliyepiga simu alisema: “Hujambo? Je, wewe ndiye yule mungu wa kike wa nyota?”
Graciela akajibu: “Sijambo. Jina langu ni Graciela, nawe unaitwa nani?”
“Naitwa Carmen.”
“Carmen, kwa nini unataka kuongea na mungu wa nyota? Je, unahitaji msaada au shauri?”
Carmen alimweleza dada yetu juu ya tatizo fulani alilokuwa nalo. Graciela alimweleza kwa urafiki kwamba tunaweza kupata mashauri bora katika Biblia na akamsomea Carmen maandiko kadhaa ya Biblia. Kisha akamuuliza: “Je, si heri tumwendee Muumba wetu tunapohitaji mwongozo unaotegemeka, sasa na wakati ujao?” Carmen alikiri kwamba alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova zamani. Kwa hiyo Graciela akafanya mpango ili aanze kujifunza tena. Tangu wakati huo, watu wa familia ya Graciela wameongea na wengine wengi waliokuwa wanatafuta msaada. Mara nyingi wamefaulu kuwahubiria, kuwahimiza wawasikilize Mashahidi wanapowatembelea, na kuwaelekeza kwenye Jumba la Ufalme.
Kolombia: Dada anayeishi mjini Cali aliibiwa gari mnamo Machi 2005. Lilipatikana siku chache baadaye. Yeye na mume wake asiye Shahidi waliwangojea polisi mahali ambapo gari hilo lilipatikana. Lakini polisi walipochelewa kufika, wakaamua kwenda nalo. Hata hivyo, kwa sababu lilikuwa limetumiwa katika kisa fulani cha uhalifu, dada huyo na mume wake walisimamishwa na polisi, wakakamatwa, na kufungwa gerezani. Dada huyo alianza kuhubiri mara alipoingia gerezani, na muda si muda akaanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia. Mmoja wa wanafunzi wake aliachiliwa na akamwomba dada huyo aendelee kujifunza naye wakati ambapo angeachiliwa. Mwanafunzi huyo alimwambia mwanamume aliyekuwa akiishi naye kwamba anataka kuhalalisha ndoa ili ampendeze Mungu.
Huyo dada alikuwa amemwomba Mungu apate wakati mwingi zaidi wa kuhubiri, lakini hakufikiri kamwe kwamba angepata nafasi akiwa gerezani! Aliambiwa angeweza kuachiliwa mapema, lakini akakataa kwa sababu alihisi kwamba Yehova alimlinda na alifurahi kuhubiri. Baada ya kifungo cha siku 45 yeye na mume wake wakaachiliwa. Dada huyo alisema kwamba imani yake imeimarika. Ndugu walimtembelea na kumsaidia mume wake alipokuwa gerezani. Kwa miaka 20, mume huyo alikuwa amepuuza kumtumikia Mungu, lakini sasa ameanza kuhudhuria mikutano na anataka kujifunza Biblia. Dada yetu huenda kwenye gereza hilo kwa ukawaida ili ajifunze Biblia pamoja na wanawake wafungwa. Kwa sasa anaongoza mafunzo manne humo. Anamshukuru Yehova kwa kujibu sala zake na kumbariki sana.
Brazili: Miaka miwili iliyopita Renildo alikuwa akiombaomba katika masoko ya mji wao na katika miji jirani. Licha ya kupata marupurupu kwa sababu ya ulemavu, Renildo aliombaomba ili kuongeza mapato hayo. Alichuma pesa nyingi sana kwa kuombaomba hivi kwamba alikuwa na gari na nyumba yenye vitu maridadi. Pia, aliweza kununua vyakula vingi ambavyo kwa kawaida watu wanaoishi katika eneo hilo maskini hawawezi kununua. Alipojifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova alianza kuzingatia mambo ya kiroho maishani, na akafanya uamuzi fulani mzito. Renildo alizungumza na mke wake na watoto wake watatu kuhusu jinsi ambavyo wangeweza kusaidiana kupunguza gharama, halafu akaacha kuombaomba. Muda si mrefu, yeye na watu wa familia yake walifanya maendeleo ya kiroho na wakabatizwa kwenye kusanyiko fulani la wilaya. Sasa Renildo hajulikani tena kama ombaomba, bali kama mhubiri mwenye bidii wa habari njema. Yeye hutumia muda wa saa 40 kwa wastani kila mwezi katika kazi ya kuhubiri.
Ekuado: Painia fulani alimpelekea mwenye mkahawa magazeti ya Kichina kwa ukawaida. Mtu huyo alitembelewa na rafiki ambaye pia ana mkahawa. Yule rafiki aliyaona magazeti hayo na akayasoma. Alipendezwa sana hivi kwamba aliandikia ofisi ya tawi huko Hong Kong, na kuomba magazeti, Biblia, na kitabu Mkaribie Yehova. Aliomba pia funzo la Biblia. Ndugu kwenye ofisi ya tawi ya Hong Kong waliandikia ofisi ya tawi nchini Ekuado, na muda mfupi baadaye, mapainia walimtembelea mtu huyo wakiwa na magazeti na vitabu alivyokuwa ameomba. Walirudi baada ya siku nne. Alikuwa amesoma magazeti na vitabu hivyo, naye alisema: “Nilianza kusoma kitabu cha Mwanzo na sasa nimefika Ezekieli, lakini nina maswali. Kwa nini Yehova anawatendea wanadamu kwa fadhili? Vitu vyote ni vyake, kwa nini basi anajitahidi sana kuwasaidia wanadamu? Anapata faida gani?” Funzo la Biblia lilianzishwa, na mtu huyo akaanza kuhudhuria mikutano mara moja. Aliacha kuvuta sigara na kucheza kamari. Hata yeye hufunga mkahawa wake ili ahudhurie mikutano. Sasa anatarajia kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, naye anawafundisha baadhi ya ndugu wenyeji Kichina. Ndugu hao wanataka kujua Kichina ili wawasaidie watu wengine nchini humo wanaoongea lugha hiyo.
Honduras: Mnamo Januari 2005 nchini Guatemala, dada anayeitwa Flor alimhubiria Sebastián, mvulana mwenye miaka 15. Mvulana huyo ni mchekeshaji katika kikundi fulani cha wanasarakasi. Alipendezwa lakini hakuwa na nafasi nyingi za kuongea. Siku moja alianguka kutoka kwenye kilele cha hema kubwa la sarakasi, na akafungwa plasta. Katika kipindi hicho alikuwa na wakati mwingi wa kufikiria mambo ya kiroho. Flor alimtembelea kila siku ili kujibu maswali yake mengi. Baada ya muda mfupi, Flor aliona kwamba Doris, mama ya Sebastián, anapendezwa pia na akaanza kujifunza Biblia naye. Doris hufurahisha watu kwa kutembea kwenye kamba. Dalila, anayewafurahisha watu kwa kubembea, na pia Sofía, mchezaji wa dansi aliyejifunza na Mashahidi hapo awali, walijiunga nao pamoja na mabinti wao. Flor alijifunza na watu hao wote mara tano au saba kila juma kwa miezi miwili.
Hatimaye wakati ukawadia kwa wanasarakasi kwenda Honduras. Flor aliwahimiza wanafunzi hao wawatafute Mashahidi katika miji ambayo wangeenda ili waendelee kujifunza na wahudhurie mikutano. Walipofika mjini Copán, mapainia wa pekee waliokuwa wametumwa kwenye eneo hilo walijifunza Biblia nao. Wanasarakasi walipowasili kwenye mji unaoitwa Gracias, painia mwingine wa pekee aliongoza funzo hilo. Wakati wa kwenda mjini Santa Rosa de Copán ulipowadia, ndugu mmishonari na mke wake walipigiwa simu na kuombwa waongoze funzo hilo kwa majuma matatu.
Funzo hilo ni la pekee kwa sababu watu saba hadi kumi hujifunza katika hema kubwa la sarakasi. Wao hujifunza mara mbili kwa juma na wote hujitayarisha vizuri kwa ajili ya funzo, hata yule mdogo kabisa, yaani, msichana mwenye miaka tisa anayeitwa Julietta. Yeye hufurahisha watu kwa kubembea. Mara nyingi inawabidi kuondoka haraka baada ya mikutano ili waende wakavalie mavazi yao ya sarakasi na kuwa tayari kwa ajili ya maonyesho. Lakini wanafanya hayo kwa furaha.
◼ OCEANIA
Idadi ya nchi: 30
Idadi ya watu: 35,237,787
Idadi ya wahubiri: 93,961
Idadi ya mafunzo ya Biblia: 47,864
New Zealand: Wakati wa mapumziko ya mchana, dada kijana anayeitwa Cecilia alikuwa akisoma broshua fulani inayozungumzia Biblia. Mfanyakazi mwenzake alimuuliza kuihusu. Cecilia alipokuwa akieleza kuhusu yaliyomo katika broshua hiyo, watu 15 walikusanyika ili kumsikiliza, akiwemo mkubwa wake aliyemwalika ofisini mwake baadaye. Alimwambia Cecilia kwamba alivutiwa na yale aliyokuwa amesikia. Pia aliwaeleza wafanyakazi kwamba chumba cha kulia chakula cha mchana kingetumiwa kwa ajili ya majadiliano ya Biblia. Vilevile alirefusha muda wa mapumziko wa Cecilia kwa dakika 30 ili awe na nafasi ya kula na pia ya kuzungumzia Biblia. Kwa majuma manne, watu 9 hadi 15 walijiunga na majadiliano hayo. Wanawake wawili hujifunza Biblia kwa ukawaida sasa, wanafanya maendeleo kwa haraka, na wanawahubiria watu wa familia zao na marafiki wao.
Tuvalu: Peteli, ambaye jina lake linamaanisha “Betheli,” ni msichana mwenye miaka 14 aliye na tatizo kubwa sana la kusikia. Baadhi ya watu wake wa ukoo ni Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, hapo awali alihudhuria mikutano kadhaa, lakini hakunufaika sana kwa sababu hakusikia yaliyozungumziwa wala hakujua kusoma. Peteli alijifunza kusoma midomo. Hivi majuzi, dada mmishonari anayeitwa Dale, alianza kujifunza naye kwa kutumia broshua Furahia Milele Maisha Duniani! Dale alitumia picha za broshua hiyo ili kumfundisha Peteli habari za Biblia. Pia alitumia maandishi yake ili kumfundisha kusoma. Jambo hilo lilikuwa gumu hasa kwa sababu Dale ni mmishonari mpya ambaye bado anajifunza lugha, Peteli naye alihitaji kuonyeshwa jinsi ya kutamka maneno ifaavyo. Peteli ana bidii na hamu ya kujifunza. Baada ya miezi mitatu tu alijua kusoma. Yeye na yule dada mmishonari hutayarisha pamoja maelezo kwa ajili ya mikutano. Peteli hufanya mazoezi kwa bidii kabla ya mikutano na hujivunia kutoa maelezo. Yeye huketi mbele katika Jumba la Ufalme ili aone vizuri midomo ya msemaji. Dale anaandika hivi: “Pole kwa pole Yehova amekuwa rafiki wa kweli wa Peteli, naye hutokwa na machozi mara kwa mara tunapoongea kuhusu wakati ambapo ‘masikio ya viziwi yatazibuliwa.’”—Isa. 35:5.
Samoa: Elena ambaye ni painia anajifunza Biblia pamoja na mwanamke Mmethodisti. Nyumba ya mwanamke huyo ilikuwa karibu na nyumba ya kasisi wa kanisa la eneo hilo. Walikuwa wakijifunzia kwenye sehemu ya nyumba yake ambayo haina ukuta. Kwa hiyo, kasisi huyo aliweza kuwaona. Siku moja walipokuwa wakijifunza, yule kasisi alikuja. Huyo mwanafunzi wa Biblia alimuuliza alichotaka. Kasisi huyo alimjibu: “Ninamtafuta nguruwe wangu mdogo. Sijamwona kwa karibu mwezi mzima.” Kisha akamgeukia Elena na kumuuliza, “Unajua ni kwa nini nguruwe wangu mdogo alitoroka?” Elena alifikiri anaongea kumhusu nguruwe halisi, kwa hiyo akasema kwamba huenda alitoroka kwa sababu alikuwa akimpa chakula kilekile kila siku. Alimpendekezea ampe chakula kingine. Elena alishangaa kasisi huyo alipomwelekezea kidole yule mwanafunzi wa Biblia na kusema, “Huyu ndiye nguruwe wangu mdogo!” Kisha akaongeza: “Wewe umemwiba. Ni lazima mkomeshe funzo hili mara moja na msithubutu kujifunza tena kamwe.” (Makasisi katika vijiji vya Samoa wana mamlaka kubwa.) Mwanamke huyo alilia. Elena alijitahidi kumtuliza na kumweleza kwamba kulingana na Biblia mambo kama hayo yangewapata wale wanaojifunza Biblia.
Elena alibadili siku, wakati, na mahali pa funzo. Yeye anasema: “Badala ya kujifunza katika sehemu ya nyumba isiyo na ukuta, tulifanyia funzo kwenye chumba kidogo nyuma ya nyumba ya mwanamke huyo. Kulikuwa na joto kali ndani ya chumba hicho lakini angalau tuliweza kuendelea kujifunza. Tulijifunza katika chumba hicho kwa miezi miwili. Halafu siku moja, baada ya sala ya kufungua, yule kasisi aliingia ghafula. Nilifikiri alikuja kusimamisha funzo, lakini mtazamo wake ulikuwa umebadilika.”
Alijiunga nasi katika funzo na hata akauliza maswali. Baada ya funzo alimgeukia huyo mwanamke na kusema: “Nataka kukuambia jambo fulani. Jana usiku tulienda mjini, lakini tulipokuwa njiani kurudi nyumbani, gari letu liliharibika karibu na kijiji jirani. Mume na mke vijana, na mwanamume mwingine kijana, walikuja kutusaidia kutengeneza gari. Lakini gari lilikataa kuwaka, kwa hiyo, nikaliacha nyumbani kwao nao wakajitolea kutupeleka kwetu. Nilipoingia katika gari lao, niliona magazeti ya Mnara wa Mlinzi na vitabu vingine. Nilifikiri huenda ikawa watu hao ni wafuasi wa kanisa lilelile la mwanamke huyu ambaye hukutembelea.”
Mwanafunzi wangu alimjibu hivi: “Ni kweli kabisa, wao ni watoto wa Elena.” Aliomba radhi, kisha akasema: “Endelea kujifunza. Sasa najua kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wema na wenye upendo sana. Nisamehe kwa mambo niliyosema hapo awali. Funzo kama hili lingewasaidia wafuasi wa kanisa langu kubadili mitazamo yao.” Kuanzia siku hiyo, badala ya kujifunza katika kile chumba kidogo chenye joto jingi kilicho nyuma ya nyumba hiyo, wamekuwa wakijifunza katika sehemu ya mbele ya nyumba hiyo. Sehemu hiyo ya mbele iliyo wazi haina joto kali. Tangu wakati huo, kasisi hajawasumbua ijapokuwa anaweza kuwaona vizuri wakijifunza.
Saipan: Kweli kuhusu Ufalme wa Mungu iligusa moyo wa mwanamke anayeitwa Helen ambaye anaishi kisiwani Saipan. Alikuwa akijifunza Biblia pamoja na mmishonari fulani na alitaka kuonyesha kwamba anathamini yale aliyokuwa akijifunza. Siku moja baada ya funzo, Helen alimpa yule mmishonari mfuko mdogo uliotengenezwa kwa kitambaa na kusema: “Sina mali nyingi, lakini ningependa kutoa mchango kwa ajili ya kazi ya kuhubiri.” Ndani ya mfuko huo mlikuwamo lulu bora kutoka kisiwa cha kwao kinachoitwa Pohnpei. Helen alipendekeza lulu hiyo iuzwe na pesa ambazo zingepatikana zitolewe kama mchango. Lulu hiyo ilikuwa bora, na mwenye duka fulani la vito aliinunua kwa dola 100 za Marekani. Helen alipewa pesa hizo ili aamue kiasi ambacho angetaka kuchanga. Lakini alikataa kuzichukua na kusema: “Ziweke zote katika sanduku la michango.” Ni nini kilichomsukuma atoe mchango huo? Kama yule mtu katika mfano wa Yesu, Helen alikuwa amepata lulu bora, yaani, tumaini la Ufalme.—Mt. 13:45, 46.
◼ ULAYA
Idadi ya nchi: 46
Idadi ya watu: 731,536,437
Idadi ya wahubiri: 1,498,142
Idadi ya mafunzo ya Biblia: 717,797
Belarus: Pavel na mke wake Mayya ambao ni mapainia wa pekee, walikuwa wanahudhuria shule ya mapainia. Jioni moja walienda matembezi, lakini hawakunuia kuhubiri. Hata hivyo, walibeba kijitabu chenye ujumbe wa Ufalme katika lugha mbalimbali (Good News for People of All the Nations). Walipowaona wageni wawili waliamua kuwahubiria. Wageni hao waliwaambia kwamba wanatoka Pakistan na lugha yao ni Kiurdu. Mapainia walikumbuka kwamba walikuwa na kile kijitabu, nao wakawapa wanaume hao ili wajisomee. Mmoja wao alipendezwa na akasema anataka kujifunza Biblia. Juma hilohilo alihudhuria mkutano wa kutaniko. Ametiwa moyo sana kwa kushirikiana na watu wa Yehova, naye amesukumwa kusema hivi: “Nimeishi jijini Minsk kwa miaka mitatu, lakini hii ni mara yangu ya kwanza kukutana na Wakristo wa kweli.” Mtu huyo anaendelea kujifunza Biblia.
Uingereza: Richard ni mzee wa kutaniko. Yeye ni kipofu na ana mbwa anayeitwa Irvin ambaye amezoezwa kuwaongoza vipofu. Lakini Irvin alipata matatizo Richard alipohubiri nyumba kwa nyumba, kwa kuwa alitazamiwa kukumbuka kila mahali ambapo Richard alienda. Richard alipowaeleza wale waliomzoeza mbwa huyo kuhusu huduma ya nyumba kwa nyumba, walimwambia kwamba Irvin hawezi kukumbuka kila nyumba ambayo Richard anatembelea anapohubiri. Watu hao walipendekeza Irvin aandamane na Richard anapohubiri kwenye eneo la biashara. Walisema kwamba mbwa huyo angeweza kukumbuka sehemu mbalimbali ambazo Richard angetembelea kwa ukawaida katika eneo hilo. Hapo awali, Richard aliogopa kuhubiri kwenye eneo la biashara, lakini punde si punde, kwa msaada wa Irvin akapata ustadi wa kuhubiri katika eneo hilo.
Hungaria: Mwangalizi fulani wa mzunguko anaandika hivi: “Mnamo Mei 2004, mimi na mhubiri mwingine tulikutana na mtu anayeitwa Csaba aliyekuwa akifanya kazi bustanini. Alisema kwamba yeye ni mwanachama wa baraza la kanisa fulani. Baada ya kuzungumza naye kifupi tuliondoka. Siku mbili baadaye tulirudi na tukaanza kujifunza Biblia naye kwa kutumia kitabu Ujuzi. Tulipotaka kuondoka alituambia kwamba jiko lake lilikuwa limeharibika. Nilimwambia kwamba ninamjua ndugu ambaye ni fundi stadi wa majiko na kwamba ningempa ndugu huyo namba ya simu ya Csaba. Akina ndugu walipomrudia ili waendelee kujifunza, Csaba aliwarudishia kitabu hicho na hakutaka kuendelea kujifunza. Lakini yule ndugu niliyependekeza amsaidie kutengeneza jiko alimpigia simu kuhusu kazi hiyo. Ndugu huyo alitumia siku tatu kutengeneza jiko la Csaba na alipofanya kazi hiyo alizungumza naye kuhusu kweli kwa muda wa saa nyingi. Csaba alianza kujifunza Biblia tena, na mke wake akajiunga naye. Mnamo Mei 2005, tayari alikuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Nilipotembelea kutaniko hilo niliandamana naye aliposhiriki katika huduma kwa mara ya kwanza. Alichochewa kufanya maendeleo ya kiroho hasa kwa sababu ya urafiki wa akina ndugu, utayari wao wa kumsaidia, na mwenendo wao ulio tofauti sana na mwenendo wa wafuasi wa kanisa lake.”
Ubelgiji: Ndugu fulani alikuwa akimrudia mwanamke anayeishi katika nyumba iliyo kwenye pembe ya barabara, na kila mara aliongea naye mlangoni. Siku moja, ndugu huyo alipokuwa akiondoka baada ya mazungumzo, mtu fulani alimkaribia na kusema: “Marafiki wangu waliniambia kwamba si vizuri kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Lakini niliwatetea na kuwaambia kwamba sivyo ilivyo. Ningependa kukueleza jambo fulani. Mara nyingi nilipokuwa nikimtembeza mbwa wangu, nilikuwa nikisikiliza mazungumzo yako na mwanamke anayeishi katika nyumba ile. Mara nyingi mliongea kuhusu ufufuo na Paradiso. Ningependa kujua mengi zaidi kuhusu mambo hayo. Mke wangu amelazwa hospitalini kwa sababu alishambuliwa na kuchomwa kwa kisu mara 17. Nimekata tamaa kabisa, nimeshindwa la kufanya.” Funzo la Biblia lilianzishwa.
Italia: Mapema alasiri moja ndugu fulani alikuwa anarudi nyumbani baada ya kazi. Alipokaribia nyumba yake, watu wawili waliokuwa kwenye pikipiki walimpita. Yule aliyeketi nyuma ya mwendesha-pikipiki alichomoa bastola mfukoni na akampungia mkono ndugu asimamishe gari lake, na ndugu akafanya hivyo. Halafu yule mwenye bastola akafungua mlango wa gari na kumwambia ndugu atoke na ampe pesa zote alizokuwa nazo mifukoni. Ndugu akatii. Kisha yule mwenye bastola akaingia garini. Alipotaka tu kuondoka aliona Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova humo garini na kuuliza, “Je, wewe ni Shahidi wa Yehova?”
Ndugu akamjibu, “Ndiyo, mbona unaniuliza hivyo?” Hakumjibu, bali alitoka garini, akamwomba msamaha, na kumwambia ndugu arudi garini mwake. Yule jambazi mwingine alimwambia mwenzake amrudishie ndugu pesa zake.
Yule mtu mwenye bastola alifunga mlango wa gari na kusema: “Tunaomba msamaha tena.” Watu hao hawakumwambia ndugu kilichowafanya wabadili nia yao, lakini yaelekea wanawaheshimu Mashahidi.
Sweden: Mnamo Aprili 2003, mhubiri fulani alikutana na mtu aliyekubali kuchukua kitabu Ujuzi. Mtu huyo alikuwa na miaka 90. Miaka iliyopita alikuwa amesafiri kotekote nchini na kupiga picha za makanisa mengi. Kwa sababu hiyo alikuwa amefanywa kuwa mwanachama mheshimiwa katika kikundi fulani cha Kanisa la Sweden. Mhubiri huyo alimuuliza yule mtu kama ameliona jina la Mungu katika makanisa yoyote, kisha akamwonyesha picha ya jina la Mungu katika kanisa moja nchini Sweden. Jambo hilo lilimvutia yule mzee. Alikubali funzo la Biblia na akalifurahia sana. Alisema: “Nimesoma Biblia tangu utotoni, na nilifikiri niliielewa vizuri. Lakini sikuelewa chochote wakati huo ikilinganishwa na yale ninayojua sasa.” Punde alianza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Mnamo Juni 2005, alipokuwa na miaka 91, alikuwa na mgawo wake wa kwanza wa kusoma Biblia katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Sasa yeye ni mhubiri ambaye hajabatizwa na anafanya maendeleo ili astahili kubatizwa. Aliwasikiliza Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 2003 kwa sababu kipindi fulani cha televisheni kilikuwa kimetuchambua. Alitaka kujua kweli kutuhusu, na sasa anaijua.
[Picha katika ukurasa wa 43]
Svetlana, Kyrgyzstan
[Picha katika ukurasa wa 47]
Lucy, Uganda
[Picha katika ukurasa wa 52]
Graciela, Venezuela
[Picha katika ukurasa wa 55]
Renildo pamoja na familia yake, Brazili
[Picha katika ukurasa wa 57]
Dale na Peteli, Tuvalu
[Picha katika ukurasa wa 57]
Cecilia, New Zealand
[Picha katika ukurasa wa 58]
Elena, Samoa
[Picha katika ukurasa wa 61]
Pavel na Mayya, Belarus
[Picha katika ukurasa wa 61]
Richard na mbwa wake, Irvin, Uingereza