Sababu Gani Usimsalimu Mtu?
Katika 2 Wafalme 4:29 tunasoma kwamba nabii Elisha alipokuwa akimtuma mtumishi wake Gehazi katika utume wa haraka, alimwagiza asimsalimu mtu ye yote njiani wala kumjibu. Hata Yesu katika Luka 10:4 alitoa amri inayofanana na hiyo kwa wale 70 aliotuma kwenda kuhubiri. Lo! jinsi hilo lilivyo jambo geni kwa kuwa watumishi hao waaminifu wa Yehova walikuwa watu wenye fadhili na wenye urafiki! Ili kufahamu sababu zilikuwa nini juu ya amri hizo ni lazima tufikirie desturi za nchi hizo za wakati wa Biblia.
Salamu za watu wa Mashariki mara nyingi zinachukua wakati mwingi. Rafiki wawili wanapokutana kunakuwa na kuinama, kufanya ishara za mkono na kurudia kusema maneno yale yale juu ya hali njema ya mmoja na mwenzake. Desturi hizo za kusalimiana huenda zikachukua dakika fulani. Mara nyingi mazungumzo yanaendelea pamoja na habari nyingine za ziada na kupashana habari ndefu sana. Hilo laweza kuchukua muda wa kama nusu saa. Kwa hiyo watumishi wa Mungu katika nyakati hizo waliamriwa wasisimame na kusalimiana kirefu namna hiyo kwa sababu walikuwa wakitakiwa kufanya kazi ya haraka!