Vijana Wauliza . . .
Kwa Nini Niepuke Mafumbo ya Kiuchawi?
“NILIKARIBIANA sana na babu yangu,” akasema msichana huyo mchanga, “naye alipokufa, nilihuzunika sana sana. Nilitaka kujua kama ingewezekana kupashana habari naye tena.” Kwa hiyo msichana mchanga huyo akaanza kucheza na mafumbo ya kiuchawi.
Ripoti moja ya karibuni ilidai kwamba “angalau watoto na vijana 200,000 katika Jamhuri ya Muungano ya Ujerumani wamejihusisha na namna mbalimbali za mafumbo ya kiuchawi.” Japan ina wingi wa wawasiliani-roho wasiolipwa shuleni, baadhi yao wakiwa na utaalamu wa kupashana habari kwa njia ya mawazo ya akili ya mmoja na mwingine, wengine wao wakiwa na ule wa kuduwaza watu, na bado wengine ule wa kupunga pepo. Katika Nigeria si jambo lisilo la kawaida siku hizi kusikia juu ya watoto wa shule za msingi wakizoea uchawi. Na, yasikitisha kusema, hata baadhi ya vijana waliolelewa na wazazi Wakristo wamechezea, labda bila kujua, mambo yazidiyo uwezo wa kibinadamu.
Ni kwa nini mafumbo ya kiuchawi yanasisimua vijana hivyo? Na kwa nini kujihusisha nayo ni hatari sana?
Sababu Wanajihusisha
Kufuatia mafumbo ya kiuchawi huhusisha mambo yazidiyo uwezo wa kibinadamu, kupeleleza ulimwengu wa roho kupitia unajimu, ubashiri, uchawi, uganga, na kadhalika. Na ni kwa nini vijana wengi hivyo hutaka sana kuchungulia mambo hayo? Dirk alikuwa na tamaa kubwa ya kuwasiliana na baba yake aliyekufa. Akiwa amesadikishwa kwamba angeweza kufanya hivyo kama angesitawisha nguvu zake za akili, alianza utafakari wa kawaida ambao kwao alijaribu kufanya vitu visonge bila ya yeye kuvigusa. Utafakari huo, akasema Dirk, ulimfikisha kwenye mlango wa ulimwengu wa roho!
Vijana wengine huhofu wakati ujao. Wanataka ushauri kuhusiana na maksi zao au mataraja ya ndoa na hudhani kwamba ulimwengu wa roho waweza kuwasaidia. Lenye kuhangaisha zaidi ni ibada ya Shetani mwenyewe! Ni nini kinachovutia kwenye dini hiyo ya kutisha sana? “Mimi nimejiingiza kwa ajili ya uwezo,” akaeleza kijana mmoja Mkanada ambaye huzoea ibada ya Kishetani. “Jambo hilo hunipa uwezo wa kuumiza watu.”
Hata hivyo, wapelelezi walio wengi huamini kwamba sababu kuu inayofanya vijana wajihusishe kufuatia mafumbo ya kiuchawi ni udadisi tu. “Nilikuwa mdadisi sana,” akakiri msichana mmoja aliyekuja kuhusika katika mafumbo ya kiuchawi. Msichana mwingine alisema hilo hivi: “Hapo kwanza nilitia shaka sana, lakini nikafikiri, ‘Angalau utajua jambo hilo lilivyo kikweli.’” Kwa hiyo akakubali mwaliko wa rafiki ajiunge katika kipindi cha mafumbo ya kiuchawi.
Kwa kusukumwa na udadisi, vijana fulani hujaribu kupiga bao (ubao wa Ouija) au kuwazia hilo kwa kuchunguza miendo ya gilasi iliyosimamishwa. Kuanzia hapo kuna hatua ndogo tu ya kujihusisha zaidi na zaidi katika uwasiliani-roho kwa kutumia mawe ya kiuchawi yaliyo mfano wa chupa, karata za taroti, vitu vya kuning’inizwa, majani-chai, na vitabu vya unajimu. Wengine hata huanza kuulizia wabashiri au waganga wa kulipwa. Hata hivyo, wengi walio wa kulipwa ni walaghai tu. Kwa kielelezo, ili kufanya maksi zake ziwe nzuri, Alexander alimwendea mganga. Si kwamba tu alishindwa kufanya maksi zake kuwa bora zaidi bali alipata hasara ya kifedha. Mganga huyo bandia na mwenye kuitwa rafiki aliyempendekeza waligawana pesa zake.
Hata hivyo, kwa vijana wengi, kuingilia uwasiliani-roho hutokeza jambo lenye kudhuru zaidi ya hasara ya kifedha.
‘Mateso Yasiyowazika’
“Laiti ningalijua” ni usemi unaosikiwa kwa kawaida miongoni mwa wale waliokuja kusikitika kwa ajili ya kucheza na yazidiyo uwezo wa kibinadamu. Ndivyo lilivyoonelea Personality, gazeti moja la Afrika Kusini. Kilio hiki ni cha kawaida: “Laiti nisingalikuwa mpumbavu hivyo. . . . Nimepatwa na mateso yasiyowazika, sauti, majinamizi, vitisho, na nimeteswa kiakili na kimwili na wafuasi wengine wa waabudu wa kishetani nilipojaribu kujiondoa.”
Kwa ukamili asilimia 24 ya walimu waliofanyiwa utafiti katika Ujerumani waliona uvutano wenye kusumbua wa kufuatia mafumbo ya kiuchawi kwenye wanafunzi. Wanafunzi fulani walikuwa wamejinyamazia, walikuwa na matatizo ya kujifunza, waliishi katika hofu, walipatwa na mshuko wa moyo, na wakawa na mwelekeo wa kutoa umizo kwao wenyewe au kwa wengine. Mara nyingi Dirk hakuweza kulala usiku. Yeye akumbuka hivi: “Nikiwa na hofu ya kupagawa na roho waovu, sikuthubutu kufumba macho yangu. Nilijikunyata niliposikia kila sauti.” Vivyo hivyo, kijana mmoja aitwaye Michael “alikosa usingizi wakati wa usiku akisumbuliwa na roho waovu” baada ya kumeza vitu alivyoagizwa. Ripoti nyingine hueleza mabadiliko mabaya sana ya utu katika watu wanaoshiriki katika mazoea ya mafumbo ya kiuchawi. Msichana moja alimshtua mama yake kwa kumpa habari kwamba wakati ujao yeye angevaa nguo nyeusi (rangi ambayo alitaka pia kupaka chumba chake) na kulala ndani ya jeneza lisilofunikwa!
Wakaaji Halisi wa Ulimwengu wa Roho
Maandiko huonyesha wazi kwamba “wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Kwa hiyo ulimwengu wa roho haukaliwi na nafsi za wapendwa waliokufa. Basi, ni nini sababu ya mambo hayo yenye kuogopesha? Roho waovu! Kulingana na Biblia, wao ni malaika walioasi, wafuasi wa Shetani Ibilisi. (1 Petro 3:19, 20; Ufunuo 12:9) Wao wana historia ya kuendeleza vitendo vya ujanja na vya kudhuru mwili miongoni mwa binadamu.
Kwa kielelezo, Luka 9:42 hutuambia juu ya mwanamume aliyepagawa na roho mwovu ambaye ‘alibwagwa chini na pepo huyo na akamtia kifafa.’ Hilo ni jambo lenye jeuri kama nini! Vivyo hivyo Matendo 19:1 hueleza jinsi mwanamume mmoja aliyepagawa na roho mwovu alivyoshambulia kijeuri watu saba waliotaka kupunga pepo huyo. Mambo ya ki-siku-hizi yaliyotukia huthibitisha waziwazi kwamba roho waovu hawajabadili hata kidogo njia zao za kikatili.
Kijana anayeanza kucheza na ESP, unajimu, karata za taroti, au namna yoyote ya mafumbo ya kiuchawi huenda kwa njia hiyo akawa anafungulia mlango mambo hayo yenye kutisha sana. Gazeti Personality lilisema hivi: “Jambo lenye kufanana linaloonekana katika habari za wale wote tulionena nao [waliokuwa wamejihusisha katika mafumbo ya kiuchawi] lilikuwa ni kwamba wao walikuwa wamefyonzwa ndani zaidi na zaidi katika mfyonzo wa kishetani kwa njia ambazo kijuujuu zilionekana zenye staha.” Ndiyo, mafumbo ya kiuchawi ni jiwe la kukanyagia tu ili kuingia kwenye uwasiliano na Shetani na roho waovu!
‘Asali Kwenye Kisu Chenye Makali’
Kwa hiyo, sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilikataza namna yoyote ya uwasiliani-roho, ikisema hivi: “Asionekane kwako mtu . . . atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu.”—Kumbukumbu la Torati 18:10, 11.
Wakristo katika karne ya kwanza walijisafisha na ukamatano wowote wa uwasiliani-roho, wakaharibu vinyago vyote vya ibada ya kishetani. (Matendo 19:19) Vivyo hivyo, leo vijana wanaotamani urafiki wa Yehova watajiepusha kabisa na chochote kinachoshirikiana na mafumbo ya kiuchawi. Hiyo ingetia ndani sinema, vitabu, vitabu vya ucheshi, na karatasi za kubandikwa ukutani zenye namna-namna za uwasiliani-roho. Hata uchaguzi wa mtu wa muziki wapaswa kuchunguzwa sana. Kwa kielelezo, muziki wenye vyombo vyenye kudundwa kwa sauti kubwa umehusianishwa mara nyingi na ibada ya Shetani.
Watibeti wana usemi: ‘Fikiria mara mbili kabla ya kukubali asali unayopewa kwenye kisu chenye makali.’ Katika kujaribu kuramba asali kutoka kwenye kisu hicho, huenda ukapoteza ulimi wako! Vivyo hivyo, hata kama mambo yazidiyo uwezo wa kibinadamu yawe yanavutia udadisi wako namna gani, yanaweza kuua. Kwa hiyo kataa mwaliko wowote wa kushiriki au hata kutazama kipindi cha mafumbo ya kiuchawi. Jambo linaloonekana kuwa lisilo na dhara kama mchezo wa kusogeza gilasi laweza kuongoza kwenye uhusikaji wenye hatari katika ibada ya kishetani. Ni kweli, yaweza ikawa unadadisi. Lakini je! wewe waweza kula nyama iliyooza ili upate tu kujua inavyokuwa mtu anapotiwa sumu mwilini na chakula?
Dirk (aliyetajwa mapema) aliweza kujiweka huru na mafumbo ya kiuchawi. Kwa kujifunza Biblia kwa msaada wa vichapo vya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, alikuja kuelewa ukweli juu ya babae mfu, naye akajifunza juu ya tumaini la ufufuo. (Zaburi 146:4; Yohana 5:28, 29) Kweli hiyo ilimweka huru na tamaa yoyote ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho. (Linganisha Yohana 8:32.) Sasa Dirk yuko wapi? Yeye amejiunga na hesabu za Mashahidi wa Yehova na hufanya kazi kwenye mojawapo wa vifaa vya uchapaji vya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi akiwa mhudumu wa wakati wote.
Ndiyo, Biblia hutosheleza ‘mahitaji yetu ya kiroho.’ (Mathayo 5:3, NW) Na baada ya wakati mrefu, hilo ni lenye kunufaisha zaidi kuliko mtu kutosheleza udadisi wake wenye madhara makubwa kupitia mafumbo ya kiuchawi yaliyo hatari, yanayoleta kifo.
[Picha katika ukurasa wa 12]
Kujihusisha katika mafumbo ya kichawi kwaweza kuanza kwa mchezo unaoonekana kuwa usio na madhara, kama vile ubao huu wa Ouija au matumizi ya gilasi iliyosimamishwa