Vijana Wauliza . . .
Je! Nibatizwe?
SUSANA mwenye miaka 13 alikuwa katika hatua za mwisho za kansa alipohudhuria mkusanyiko wake wa mwisho wa Mashahidi wa Yehova. Yeye hakujua kwamba angekufa katika muda wa siku kumi tu. Hata hivyo, hata kansa haingeweza kumzuia asitimize tamaa yake aliyoithamini sana: kubatizwa kuwa Shahidi aliye wakfu wa Yehova na mwanafunzi wa Yesu Kristo.
Susana alikuwa mmoja tu kati ya maelfu ya vijana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ambao katika miaka ya karibuni wamelithamini sana pendeleo la kubatizwa. Lakini labda wewe waliona taraja la kuchukua msimamo huo wa ujasiri kuwa lenye kuogofya kidogo. Si kwamba huamini kweli zenye msingi wa Biblia ulizofundishwa. Huenda ukawa unahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na huenda ukashiriki kweli za Biblia na wengine kwa ukawaida. Hata hivyo, inapokuwa ni kuweka wakfu maisha yako kwa Mungu, huenda ukasita. Kwa hiyo, ubatizo ni wenye maana jinsi gani? Na ni kwa nini vijana wengi sana hujiepusha nao?
Dini Bila Wakfu
Mara nyingi vijana hujibiwa swali la ubatizo na wazazi wao katika Jumuiya ya Wakristo. Madhehebu fulani hutia moyo wazazi walete watoto wao wabatizwe wakiwa watoto wachanga. Na hata wakati sherehe ya ubatizo inapofanywa mtu akiwa mzima, kwa kawaida vijana hutazamiwa wafuate dini ya wazazi wao kwa sababu ndivyo wanavyopaswa kufanya, hawana uchaguzi.
Hata hivyo, kwa kupendeza, uchunguzi wa kutafuta maoni wa Gallup katika United States ulifunua kwamba ingawa “karibu matineja wote (asilimia 96) huamini kuna Mungu,” ni asilimia 39 peke yake waliosali mara nyingi. Na ni asilimia 52 peke yake waliokuwa na uhakika katika matengenezo ya kidini. Diane kijana anaonyesha hali hiyo ilivyo anaposema: “Mimi naamini Mungu na kadhalika, lakini naamini afadhali zaidi kujaribu kuwa mtu mwema kuliko kusoma kila mstari wa Biblia.”
Ndiyo, dini yaweza kuwa isiyo na nguvu, hasa, wakati imelazimishwa kwa kijana na wazazi wake. Uchunguzi mmoja uliofanywa kwa kikundi cha watoto wahalifu Wakatoliki unaendelea kuonyesha hilo. Nusu yao walihudhuria kanisa. Walio wengi walijua mafundisho ya msingi ya imani yao. Na karibu asilimia 90 yao walipinga wizi. Hata hivyo, zaidi ya theluthi mbili walikuwa ni wezi! Kikaonelea hivi kitabu The Adolescent: “Sababu moja yaweza kuwa kwamba kujitoa kidini kwa wavulana hao kulikuwa ni kidogo. Wote walizaliwa Wakatoliki; kujitoa kwao kwa kwanza kulifanywa kwa ajili yao na wazazi wao. Dini yao haikuwa yao wenyewe.”
Ubatizo—Sababu Ni Takwa la Kikristo
Basi, kwa sababu nzuri, Biblia yakutaka wewe—wala si wazazi wako—ufanye wakfu wa kibinafsi kwa Mungu.a ‘Sawa kabisa,’ huenda ukasema, ‘lakini ikiwa wakfu ni jambo la kibinafsi, jambo kati ya Mungu na mimi, sababu gani nibatizwe?’
Kwa sababu ubatizo wahusisha ‘wokovu wa nafsi yako.’ (1 Petro 1:9, NW) Mungu anafikiria kulipiza “kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu; watakaoadhibiwa kwa maangamizi ya milele, kutengwa na uso wa Bwana na utukufu wa nguvu zake.” (2 Wathesalonike 1:8, 9) Vionyesho vyote ni kwamba uharibifu huo utakuja katika siku yetu.b
Hata hivyo, mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wote waokolewe.” (1 Timotheo 2:4) Anataka wewe uponyoke mwisho wa huu mfumo wa mambo na kuishi milele katika Paradiso juu ya dunia! (Ufunuo 21:3, 4) Lakini wewe unaweza kujitambulishaje kuwa mmoja anayetii habari njema? Haitoshi tu kuamini kweli za Biblia ambazo umefundishwa, wala haitoshi tu kuandamana na wazazi wako kwenye mikutano ya Kikristo. (Linganisha Yakobo 2:19.) Wale wanaotamani wokovu ni lazima wajiweke wakfu kwa Mungu na kufanya mapenzi yake. Asema hivi mtume Paulo kwenye Warumi 12:1, NW: “Kwa hiyo mimi nawasihi nyinyi kwa huruma za Mungu, ndugu, mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, [“wakfu,” The New English Bible] yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.”
Lakini wakfu hauwezi kubaki kabisa ukiwa jambo la kisiri. Ingawaje, kwa kweli mwanafunzi wa siri angewezaje kuwa mwenye kujitoa, aliye wakfu? (Linganisha Yohana 19:38.) Je! wewe ungetegemea rafiki ambaye anataka kuendeleza urafiki wenu ukiwa siri? Basi, ni jambo la hekima kwamba Mungu ataka wote ‘wafanye julisho rasmi la peupe.’ (Warumi 10:10, NW) Jambo hilo huanzia kwenye ubatizo. Wakati huo, mtu hutoa julisho rasmi la imani yake. Kisha, ubatizo katika maji hufuata. (Mathayo 28:19, 20) Hata hivyo, kungekuwa faida gani kutumbukizwa ndani ya maji?
Ubatizo si tendo la kuoga tu; ni kuzikwa kimfano. Unapozama kwenye maji ya ubatizo, unakaziwa kwamba umekufa kwa habari ya mwendo wako wa kale wa maisha. Hapo awali, matakwa yako ya kibinafsi, miradi, na tamaa zilichukua mahali pa kwanza maishani mwako. Lakini Yesu alisema kwamba wanafunzi wake ‘wangejikana.’ (Marko 8:34) Kwa hiyo unapoinuliwa, unakumbushwa kwamba sasa uko hai ili kufanya mapenzi ya Mungu. Kitendo hiki cha ujasiri, cha peupe, ni sehemu ya muhimu ya kutiwa alama kunakokutambulisha kwa ajili ya wokovu!—Ezekieli 9:4-6; linganisha 1 Petro 3:21.
‘Naogopa Nitatengwa na Ushirika’
Basi, ikiwa ubatizo ni wa maana hivyo, ni kwa nini vijana fulani hujiepusha nao? Amkeni! liliuliza vijana kadhaa Wakristo swali lilo hilo. Msichana mmoja alijibu hivi: “Wengi huona kwamba watakuwa na uhuru zaidi wasipobatizwa. Wanaona kwamba wakiingia taabani, hawatalaumiwa.” Kijana mmoja aitwaye Robert alirudia maelezo hayo kwa kusema hivi: “Nafikiri vijana wengi husita kubatizwa kwa sababu wanahofu huo ni hatua ya mwisho ambayo hawawezi kujiondoa wakiisha ingia. Wao huona kwamba kama wakifanya jambo baya, watafukuzwa kundini.”
Ni kweli kwamba mtu hawezi kujiondoa kwenye wakfu kwa Mungu akiisha ufanya. (Linganisha Mhubiri 5:4.) Mtu anayejiweka wakfu kwa Mungu hujichukulia daraka zito. Yeye ana wajibu wa ‘kuenenda kama ulivyo wajibu wake kwa Yehova, akimpendeza kabisa.’ (Wakolosai 1:10) Mtu anayeshiriki katika utendaji wa makosa mazito hata hujitia katika mashaka ya kufukuzwa kutoka kundi la Kikristo.—1 Wakorintho 5:11-13.
Hata hivyo, mtu hawezi kufikiri kwamba maadamu hajabatizwa, lolote ni sawa tu. Kwa maana “yeye ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi”—awe amebatizwa au hajabatizwa! (Yakobo 4:17) Huenda mtu akaepuka kufukuzwa kirasmi kundini, lakini mtu hawezi kuponyoka hukumu ya Yehova. “Msikosee,” aonya Paulo, “hakuna cha kufyotolea Mungu; kwa maana mtu atavuna kile kile apandacho.”—Wagalatia 6:7, Byington.
Mara nyingi hofu ya kutengwa na ushirika hufunika tamaa ya siri ya kuzoea kufanya makosa. Mwanamke mmoja kijana aitwaye Natalie alionelea hivi kwa unyofu: “Mimi nililelewa katika ulimwengu wa Shetani na najua jinsi ulivyo. Lakini vijana wengi wanataka kutoka nje na kujionea kulivyo kule nje.” Badala ya kuruhusu tamaa mbaya zikuzuie usibatizwe—au kuziruhusu zisitawi kuwa vitendo vyenye kosa—kwa nini usitafute msaada, labda uzungumze na mzazi au Mkristo aliyekomaa?—Yakobo 1:14, 15.
Kweli kweli, uhuru ambao ulimwengu wa Shetani hutoa ni udanganyifu mtupu. Ni kama mtume Petro alivyosema juu ya wengine waliodanganyika katika siku yake: “Wakiwaahidia uhuru, nao wenyewe ni watumwa wa uharibifu, maana mtu akishindwa na mtu huwa mtumwa wa mtu yule.” (2 Petro 2:19) Je! kweli ni uhuru kuacha kufikiri kwako, mwenendo wako, na adili zako zidhibitiwe na wengine? Je! kweli ni huru kushiriki katika vitendo vinavyoongoza kwenye maradhi, kuvunjiwa heshima, na, hatimaye, kwenye kifo?—Mithali 5:8-14.
Kijana mmoja Mjapan aitwaye Hitoshi alikabili maswali ayo hayo. Alikuwa amelelewa na wazazi Wakristo naye akumbuka hivi: “Wengine walipokuwa wakicheza, mimi nilipaswa kwenda kwenye mikutano. Nilitaka uhuru zaidi. Nilifikiri nilikuwa nakosa jambo fulani.” Ndiyo, kama vile mtunga zaburi Asafu, yeye ‘alionea wivu’ wakosaji. (Zaburi 73:2, 3) Lakini baada ya kufikiria kwa utimamu jambo hilo, maoni ya Hitoshi yalibadilika. Yeye asema hivi: “Nilitambua jinsi maisha yangu yangekuwa bila kweli—ningeweza kujiona nikiishi miaka 70 au 80 halafu kufa. Lakini Yehova anatoa uhai wa milele!” Hivyo, Hitoshi alijiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa.—Linganisha Zaburi 73:19-28.
Je! wewe unachochewa ufanye ilo hilo? Kijana mmoja aitwaye David alichochewa kufanya hilo. Yeye akumbuka hivi: “Kubatizwa nikiwa kijana kulikuwa ni ulinzi kwangu. . . . Matineja fulani wasiobatizwa kundini walijiona wako huru na mamlaka ya wazee na kwa hiyo wakapotoka wakaingia katika mwenendo mbaya. Lakini sikuzote mimi nilikumbuka kwamba nilikuwa nimeweka maisha yangu wakfu kwa Mungu.” Lakini, labda huna hakika kama uko tayari kuchukua hatua hiyo. Habari ya kukusaidia itatolewa katika makala ya wakati ujao.
[Maelezo ya Chini]
a Upumbavu wa kubatiza watoto wachanga umezungumzwa katika makala “Je! Watoto Wachanga Wabatizwe” katika Mnara wa Mlinzi wa Machi 1, 1986.
b Ona kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, (kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.), sura 18.
[Picha katika ukurasa wa 29]
Ule uamuzi mmoja wa kutumikia Mungu ni wewe tu unayeweza kuufanya. Ubatizo hutambulisha mtu kuwa mwanafunzi aliye wakfu wa Kristo Yesu