Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g91 6/8 kur. 26-28
  • Je! Mimi Niko Tayari Kubatizwa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Mimi Niko Tayari Kubatizwa?
  • Amkeni!—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Je! Nina Umri wa Kutosha?’
  • ‘Je! Mimi Nimetwaa Maarifa ya Kutosha?’
  • “Watendaji wa Neno”
  • ‘Nimemfanya Mungu Kuwa Rafiki Yangu’
  • Ubatizo na Uhusiano Wako Pamoja na Mungu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Vijana Je, Mko Tayari Kubatizwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Je, Uko Tayari Kubatizwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Kufanye Kumtumikia Mungu Milele Kuwe Lengo Lako
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1991
g91 6/8 kur. 26-28

Vijana Wauliza . . .

Je! Mimi Niko Tayari Kubatizwa?

Wapendwa Watchtower Society:

Jina langu ni Sharon na nina miaka 13. Nimekuwa nikitaka kujua kama niko tayari kwa ubatizo. Nafikiri niko, lakini ningali sina uhakika. Nina hakika hilo pia liko kwenye akili za Wakristo wengine wachanga. Je! tafadhali mnaweza kuandika makala moja ya kunisaidia nielewe vizuri?

SHARON asema kweli. Kwa kweli ubatizo uko kwenye akili za vijana wengi wanaohofu Mungu. Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, vijana hutambua ni lazima wafanye uamuzi wao wenyewe wa kutumikia Mungu, kwamba wazazi wao hawawezi kuwafanyia uamuzi. Wao pia huthamini kwamba Yesu Kristo aliamuru wafuasi wake wafananishe wakfu wao kwa Mungu kwa njia ya maji ya ubatizo.—Mathayo 28:19, 20.

Kufanya julisho la peupe kuwa mtumishi wa Mungu aliye wakfu ni daraka kubwa. Kwa kweli hungependa kufanya mbiombio ili tu upendeze marafiki au wazazi wako. Kuongezea hayo, hakuna yeyote anayepaswa kukulazimisha ubatizwe. (Zaburi 110:3) Hata hivyo, Yesu alishauri wote ‘wahesabu gharama’ ya kuwa mwanafunzi wake. (Luka 14:28) Hiyo haimaanishi kwamba unapaswa kupima kama unataka kuwa mwanafunzi wa Kristo au la. Kwa wazi, hilo ndilo jambo linalofaa kufanya. Hata hivyo, unapaswa kujua kikamili yanayohusika katika kuwa Shahidi wa Yehova.a Kisha, unapaswa kuamua kama uko tayari kweli kweli kuchukua daraka hilo.—Linganisha Mithali 20:25.

‘Je! Nina Umri wa Kutosha?’

Vijana wanapokuwa na umri mkubwa zaidi, mara nyingi wao huona wana haki ya kufurahia mapendeleo na madaraka fulani. Wao hufanya haraka kusisitiza juu ya kuendesha motokaa ya familia, kuomba ruhusa ya kufanya kazi ya baada ya shule, kutaka kuwa na fedha zao wenyewe za matumizi. Lakini inapokuwa ni ubatizo, vijana wengi hujitolea udhuru kuwa ni wachanga mno au hawako tayari kwa ajili ya daraka hilo. Kijana mmoja aitwaye Andre aonelea hivi: “Vijana wengi husubiri mpaka wawe miaka 17 au 18 ndipo wabatizwe, umri ambao ni mkubwa mno.” Kwa nini? “Kwa sababu muda mrefu kabla ya hapo wao ni wenye umri wa kutosha kujifanyia maamuzi mengine.”

Ndiyo, ule uhakika tu wa kwamba wewe ni kijana si udhuru wa ‘kusita-sita katikati ya mawazo mawili,’ wala si sababu kamili ya kujiepusha kuchukua msimamo ukiwa Mkristo. (1 Wafalme 18:21) “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako,” yahimiza Biblia. (Mhubiri 12:1) Nabii Samweli alikuwa mmoja aliyeanza kutumikia Yehova akiwa na umri mdogo sana. (1 Samweli 3:1-18; 12:2) Mtunga zaburi Daudi angeweza pia kusema hivi: “Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU [Yehova, NW], tumaini langu tokea ujana wangu.”—Zaburi 71:5.

Vivyo hivyo, maelfu ya vijana Wakristo leo—kutia ndani wengine ambao hawajafika miaka 13—wamejithibitisha ni wenye kuchukua daraka vya kutosha kuweza kujiweka wakfu watumikie Mungu. Lakini, vijana fulani wanakosa uzito wa mambo na hawachukui daraka ifaavyo wala hawajakomaa katika maono ya moyoni kuweza kufanya uamuzi mkubwa kama ubatizo. (Mithali 22:15) Lakini je! ndivyo ilivyo katika kisa chako? (Bila shaka wazazi wako wana mengi ya kusema juu ya hilo.) Mungu hatazamii kamwe kijana awe na ukomavu wa mtu wa miaka 40. Yeye ajua vizuri kwamba wewe unapatwa na “tamaa za ujanani.” (2 Timotheo 2:22) Lakini ikiwa una umri wa kutosha kuweza kuchukua mambo kwa uzito na kuchukua daraka ifaavyo vya kutosha, basi yaelekea una umri wa kutosha kuweza kufikiria kujiweka wakfu. Hata hivyo, kuna maswali mengine unayopaswa kujiuliza.

‘Je! Mimi Nimetwaa Maarifa ya Kutosha?’

Kitabu The Adolescent, cha F. Philip Rice, chaonelea kwamba “wazo la kijuu-juu, la kutokuwa na habari ya dini mara nyingi halitasimama chini ya shambulio na jaribu.” Hata hivyo, Bw. Rice asema hivi: “Kuna dalili fulani kwamba vijana wa leo wamekosa habari mno. Uchunguzi wa maarifa ya Kibiblia kwa wanafunzi Waprotestanti na Wayahudi wa mwaka wa pili wa chuo kikuu ulifunua ukosefu halisi wa maarifa ya Agano la Kale na Jipya.”

Hilo halipaswi kuwa hivyo kwa yule anayebatizwa. Ni lazima kwanza mtu ‘atwae maarifa’ ili kuwa mwanafunzi, au aliyefundishwa. (Yohana 17:3, NW; Mathayo 28:19) Kwa hiyo je! halingekuwa jambo la akili kwamba kabla ya kubatizwa uyajue angalau “mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu”? (Waebrania 5:12) Hiyo ingetia ndani kujua ambayo Biblia hufundisha juu ya mambo kama nafsi, hali ya wafu, kutakaswa kwa jina la Mungu, Ufalme, na ukombozi.

Ni kweli, hutakosa kujua jambo fulani juu ya Biblia kwa sababu tu ya kufuatana na wazazi wako katika mikutano ya Kikristo. Lakini maarifa yanayopatikana katika njia hiyo huenda yakawa ya kijuu-juu na yasielekee ‘kusimama chini ya shambulio na jaribu.’ Unapaswa kuweza kuwatolea wengine ‘sababu ya tumaini lililomo ndani yako.’—1 Petro 3:15, NW.

Terry asema aliamini kweli za Biblia. Hata hivyo, anakiri hivi: “Sikuwa nimepata kujitosheleza kamwe kwa kujiuliza maswali yangu mwenyewe na kisha kuyajibu. Hivi karibuni nilianza kufanya hivyo.” Tokeo la programu hiyo ya funzo la Biblia likawa nini? “Imani yangu inaongezeka, na sasa naona ninaweza kuongea na watu nikiwa na usadikisho halisi. Nawaambia vijana wote Mashahidi wasiogope kujiuliza wenyewe kama hii ndiyo kweli. Chunguza! Fanya utafiti, jifunze. ‘Jaribu yote.’ Halafu utaweza kufanya wakfu wa moyo wote kwa Yehova.—1 Wathesalonike 5:21.

“Watendaji wa Neno”

Hata hivyo, ni lazima tuwe “watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu.” (Yakobo 1:22) Huwezi kujitolea ubatizwe na uwe mtu ‘anayeficha alivyo’ kwa kufunika makosa mazito. (Zaburi 26:4) Makosa hayo yangetia ndani ukosefu wa adili za ngono, ulevi, kutumia vibaya dawa za kulevya, au yoyote ya dhambi zinazotajwa kwenye 1 Wakorintho 6:9, 10. Kama umekuwa na matatizo katika mambo hayo, kwa nini usipange na wazazi wako ili kuzungumza na wazee Wakristo? Sadikishwa kwamba utapewa msaada wa fadhili.—Yakobo 5:14, 15.

Pia yawezekana kwamba mabadiliko fulani yanahitajiwa katika njia ambayo unawatenda wazazi wako au jinsi unavyoona shauri kutoka kwa wazee Wakristo, hata katika njia unayochagua marafiki. (Mithali 6:20; 13:20; 1 Wakorintho 15:33; Waebrania 13:17) Huenda isiwe rahisi kufanya mabadiliko hayo, lakini Mithali 11:19, NW, yatukumbusha hivi: “Mtu ateteaye uadilifu angojea uhai, lakini yule afuatiaye lililo baya angojea kifo chake mwenyewe.”

Je! Yehova anatazamia kwamba uwe mkamilifu? Sivyo kamwe. “Nani awezaye kusema, Nimesafisha moyo wangu; nimetakasika dhambi yangu?” yauliza Mithali 20:9. Tukiwa wasiokamilika, bado tuna mwelekeo wa kufanya makosa. Lakini kwa sababu ya ukombozi wa Kristo, twaweza kubaki tukiwa na msimamo mzuri pamoja na Mungu. (1 Yohana 2:1, 2) Kwa kielelezo, kijana anayepigana vikali na tabia mbaya, kama vile zoea chafu la kupiga punyeto, hapaswi kujiona hastahili ubatizo.b Kwa kweli, kwa kupinga kwa bidii uovu mtu aweza kuufurahisha moyo wa Yehova!—Mithali 27:11.

‘Nimemfanya Mungu Kuwa Rafiki Yangu’

Ingawa hivyo, labda swali la maana zaidi lahusisha uhusiano wako na Mungu. Kumbuka: Unajiweka wakfu, si kwa kazi wala kwa sababu fulani, au hata kwa tengenezo fulani, bali kwa Mungu. Je! yaonekana Mungu ni sifa fulani tu, asiyefikika? Au umepata kumjua na kumpenda kama Mtu? (Kutoka 34:6, 7) Ikiwa ndivyo utajikuta ukiongea naye mara nyingi, si kidesturi tu bali kutoka moyoni.—Zaburi 62:8.

Pia utajikuta ni kama unalazimika kuongea na wengine juu ya Mungu. (Linganisha 2 Wakorintho 5:14.) Mithali 15:7 yasema hivi: “Midomo ya mwenye haki hueneza maarifa.” Je! unafanya hivyo kwa kuwahubiri wengine kwa ukawaida? Au unaruhusu burudani, tafrija, au hata uvivu ukuzuie kuwasaidia wengine kuja kumjua Mungu?—Mithali 19:24.

Ndiyo, ili ubatizo uwe na maana, lazima Mungu awe rafiki yako wa karibu zaidi. (Linganisha Yakobo 2:23.) Ikiwa sivyo ilivyo sasa, lawama si la Mungu kwa kuwa yeye huwakaribisha wote wamtafute. (Matendo 17:27) Na kwa kuendelea na funzo la kibinafsi, sala, na kushirikiana na watu wake, baada ya muda fulani utajiona umekaribia Mungu zaidi. (Warumi 12:12; 1 Timotheo 4:15; Waebrania 10:24, 25) Ubatizo utakuwa tokeo la asili la ‘kukaribia Mungu.’—Yakobo 4:8.

Fikiria kwa kielelezo, msichana mchanga aitwaye Cindy. Aandika hivi: “Nilibatizwa nikiwa na miaka 14. Najua anavyoona mtu asipotaka kufanya hivyo. Lakini nataka kusema kwamba ndilo lililo jambo zuri zaidi kufanya. Wazia, kujua una kibali cha Yehova na kwamba ‘hatakupungukia wewe kamwe wala kukuacha’! (Waebrania 13:5) Kama yeyote angeniuliza mimi, ikiwa apaswa ajitoe wakfu kwa Yehova, ningemwambia ndiyo! Lakini usifanye hivyo ili umpendeze mtu mwingine. Fanya hivyo kwa sababu unataka.”

[Maelezo ya Chini]

a Ona “Je! Mimi Napaswa Kubatizwa?” katika Amkeni! ya Aprili 8, 1991.

b Ona sura 25, 26 za kitabu Young People Ask—Answers That Work, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Vijana wengi wastahili ubatizo. Vipi wewe?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki