Vijana Wanauliza. . .
Naweza Kufanyaje Maendeleo ya Kiroho?
“Nilipoenda kanisani, nilitatanishwa kweli kweli. Sikuelewa walichokuwa wakijaribu kusema, basi nikaacha kwenda. Sidhani kama inakubidi kuwa sehemu ya dini fulani yoyote ili uwe na imani katika Mungu.”—Carrie mwenye umri wa miaka kumi na saba.
KWA nini Kanisa huwachukiza vijana wengi sana? Katika utafiti uliofanywa na mtafiti wa kura za maoni, George Gallup, vijana walitoa sababu zifuatazo: ‘Mahubiri ni yenye kuchosha.’ ‘Hawafundishi juu ya Mungu na Biblia.’ ‘Wao huomba pesa sikuzote.’ ‘Makanisa na wanaoenda kanisani hawaishi kulingana na yale wanayojidai kuwa.’ Ni wazi kwamba, makanisa yameshindwa kulisha hali ya kiroho ya vijana.
Lakini, je, wewe unataka ‘kuushika uzima ule wa milele’? (1 Timotheo 6:12) Je! wewe unataka kuheshimiwa ukiwa Mkristo mkomavu, anayeweza kukabidhiwa madaraka? Je! unataka pendeleo la kuwa mmoja wa “wafanya kazi pamoja na Mungu” katika kuwasaidia wengine kupata uhai wa milele? (1 Wakorintho 3:9) Basi ni lazima ufanye maendeleo ya kiroho! Kwa kushirikiana na Mashahidi wa Yehova unafurahia faida ambazo vijana wa Jumuiya ya Wakristo hawapati. Unahudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, ambapo mafunzo thabiti ya Biblia hutolewa. Unapokea uangalifu wa kibinafsi kutoka kwa wazazi wako kupitia funzo la Biblia la familia. Unashiriki kwa kawaida na watu wanaojitahidi kutumia Biblia katika maisha zao. Hata hivyo, ikiwa utafanya maendeleo ya kiroho, mengi zaidi yanatakiwa. Kama alivyoeleza mtume Petro, ni lazima ‘ujitahidi sana.’ (2 Petro 1:5) Ebu tuone yanayohusika katika kufanya hivyo.
Sitawisha Hamu ya Kiroho
Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3, NW) Katika Kigiriki cha awali, fungu hilo la maneno kwa uhalisi lilirejezea “wale walio fukara wa roho.” Kama fukara wa mwisho anayefahamu kwa uchungu uhitaji wake wa chakula cha kimwili, ni lazima uone uhitaji wako wa chakula cha kiroho. Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu. Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.
Vijana wengi hufanya kidogo ili wajaze mahitaji yao ya kiroho. Kitabu The Psychology of Adolescence kinasema hivi juu ya kijana wa kawaida: “Huenda ufahamu wake wa imani yake ya kidini ukawa wa chini, ingawa kufikiri kwake na kupendezwa kwake katika dini ni kwa juu kabisa.” Katika utafiti mmoja kikundi cha vijana waliulizwa maswali mia moja juu ya Biblia. Kijana wa kawaida aliweza kujibu 17 tu. Katika utafiti mwingine, matineja saba kati ya kumi hawakuweza kutaja Gospeli zote nne.
Vipi wewe? Umejibidiisha kwa kadiri gani katika funzo la uzito la Biblia? Je! unaweza kukanusha mafundisho ya uwongo kama vile Utatu na kutokufa kwa nafsi? Je! unaweza kuthibitisha Kimaandiko kwamba kuna tumaini la uhai wa milele mbinguni na duniani? Unaweza kuthibitisha kwamba tumekuwa tukiishi katika “siku za mwisho” tangu 1914? (2 Timotheo 3:1-5) Au ‘unahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu’?—Waebrania 5:12.
Ikiwa hivyo ndivyo ilivyo, unahitaji ‘kutamani maziwa ya akili yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo upate kuukulia wokovu.’ (1 Petro 2:2) Huenda ikahitaji jitihada kubwa mwanzoni lakini kadiri unavyotia bidii katika kusoma Neno la Mungu, ndivyo utakavyozidi kutamani mambo ya kiroho.
Shaka Zenye Kuendelea
Kevin mwenye umri wa miaka 19 asema hivi: “Kwa hakika sijui ninaposimamia kidini sasa. Kwa kweli ninatatanishwa na jambo hilo.” Vijana wengi katika Jumuiya ya Wakristo wanahisi hivyo. Lakini, je, inawezekana kwamba maendeleo yako ya kiroho yamezuiwa jinsi iyo hiyo kwa sababu ya shaka zenye kuendelea?
Kwa mfano, je, umesadikishwa kabisa kwamba kuishi kulingana na kanuni ya maadili ya Biblia ndiyo njia bora ya kuishi? Au, unajikuta ‘ukiwaonea wivu watu waovu’? (Zaburi 73:3, NW) Je! umekubali katika moyo wako kwamba tunaishi katika siku za mwisho? Au, unapanga kazi-maisha katika mfumo huu wa mambo kwa kutazamia sana? Je! unaamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa? Au, mara nyingine unashangaa endapo nadharia za kisayansi zinaikanusha? Ikiwa shaka zinakusumbua, kumbuka inavyosema Biblia katika Yakobo 1:6: “Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yo yote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku.” Shaka kuhusiana na imani ya mtu zinaweza pia kulinganishwa na jahazi ya meli inayovuja. Kadiri mashimo yalivyo makubwa, ndivyo ilivyo yamkini kwamba meli itazama.
Je! hilo lamaanisha kwamba imani yako iko karibu “kuzama” ikiwa muda kwa muda unakuwa na maswali yasiyotatulika? Sivyo kwa lazima. Lakini ukiwa na shaka zenye kuendelea, ni lazima ufanye juhudi kuzitatua. Kwa mfano, ikiwa ulikuwa na shaka juu ya kununua suruali ndefu mpya, je, usingechunguza vazi hilo kwa ukaribu ukiangalia ufundi, ubora wa kitambaa, na bei kabla ya kufanya uamuzi? Vivyo hivyo, shaka nyingi zilizo halali zaweza kutatuliwa kwa kuichunguza Biblia kwa ukaribu au kwa kuongea juu ya mambo hayo pamoja na Mkristo mkomavu, mwenye maarifa.a Mithali 15:14 husema hivi: “Moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa.”
Kujiwekea Miradi ya Kiroho
Mtume Paulo alimwambia kijana Timotheo hivi: “Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.” Ingawaje hivyo, ona kwamba Paulo hakumpa Timotheo mradi wa juu sana usio halisi, usioweza kufikiwa. Alimpa Timotheo miradi hususa, iliyoweza kufikiwa ili kufanyia kazi: “Uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”—1 Timotheo 4:12-14.
Kama Timotheo, unahitaji kujiwekea miradi ya kiroho ambayo ni halisi na inayoweza kufikiwa. Kwa mfano, wazia kwamba unaamua kujifunza upishi. Ingekuwa jambo la ubatili kama nini kujaribu kuwa mpishi mwenye ustadi kwa siku moja tu! Hata hivyo, unaweza kujifunza ustadi wa upishi hatua kwa hatua—labda kwa kujifunza kwanza kutayarisha mboga na kisha kuendelea na kupika nyama, mikate, vyakula vya mapishi ya kufunikizia joto, au vyakula vitamu vya kumalizia. Vivyo hivyo, unaweza kwa upesi zaidi kufikia mradi wako wa ukomavu wa kiroho wa kuchukua muda mrefu ukiukaribia kwa kupitia miradi au hatua za katikati. Hizo zaweza kutumika kuwa alama za kuonyesha maendeleo yako ya kiroho. Kila wakati unapokamilisha hatua moja, unajenga uhakika wako wa kibinafsi. Hilo laweza kukutia moyo ukabiliane na hatua ya pili.
Kuifikia Miradi Yako
Ebu tuangalie baadhi ya miradi unayoweza kujiwekea. Kwa mfano, Je, umepata kuisoma Biblia yote? Ndiyo, Biblia ni kitabu kikubwa, lakini kwa nini usigawanye usomaji wayo katika vipande vidogo vidogo? (Mtu wa kawaida katika United States hula zaidi ya kilo 640 za chakula kila mwaka. Lakini ni nani ambaye angeweza kula chakula hicho kwa safari moja?) Waberoya ‘waliokuwa waungwana waliyachunguza maandiko kila siku.’ (Matendo 17:11) Ukifuata ratiba ya usomaji wa kila siku wa dakika 15 tu—karibu wakati unaochukua kusikiza katika redio nyimbo tano zenye kupendwa sana—ungeweza kukamilisha usomaji wa Biblia kwa mwaka mmoja.
Unaweza kujiwekea mradi wa kusoma kila toleo la magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Habari nzuri unayopata ndani humo bila shaka itaharakisha maendeleo yako ya kiroho. Ikiwa wewe bado huwakilishi kundi ukiwa mhubiri asiyebatizwa, ungeweza pia kufanya hilo kuwa mradi wako. Hiyo ingehusisha kushiriki kwa kawaida katika kazi ya kuhubiri mlango kwa mlango na kuripoti utumishi kama huo kila mwezi. Unaweza kuzungumza jinsi ya kustahili kwa ajili ya pendeleo hilo pamoja na wazazi wako au wazee wa kundi la kwenu.
Ni ipi mingine inayoweza kuwa miradi ya kiroho? Kuwa mwenye busara na mkomavu katika kufikiri kwako. (Waebrania 5:14) Kusitawisha kila tunda la roho. (Wagalatia 5:22, 23) Kufanya maendeleo katika ubora wa sala zako. (Wafilipi 4:6) Kudhihirisha heshima zaidi kwa ukichwa wa wazazi wako. (Waefeso 6:1) Kuwa mstadi zaidi katika kuitetea imani yako. (1 Petro 3:15) Miradi hiyo ni ya akili na yaweza kufikiwa!
Hata hivyo, kumbuka haitoshi kujiwekea miradi tu. Ni lazima ushikamane nayo! Kama alivyosema Benjamin Disraeli aliyekuwa waziri mkuu wa Uingereza: “Siri ya kufaulu ni kuwa na uthabiti wa kusudi.” Ndiyo, sitawisha hamu ya kiroho. Jiwekee miradi ya kiroho ya akili. Onyesha uthabiti kwa kushikamana nayo. Kwa hakika tokeo litakuwa maendeleo ya kiroho.b
[Maelezo ya Chini]
a Vitabu The Bible—God’s Word or Man’s? na Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? (vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.) vyaweza kukusaidia utatue maswali ambayo huenda ukawa nayo juu ya kupuliziwa kwa roho kwa Biblia.
b Makala za wakati ujao zitaeleza sehemu nyinginezo za habari hiyo.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Kuratibu dakika chache za usomaji wa Biblia kila siku ni njia moja ya kukuza maendeleo yako ya kiroho