Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g91 6/8 kur. 6-7
  • Zawadi Nzuri Ajabu ya Hiari

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Zawadi Nzuri Ajabu ya Hiari
  • Amkeni!—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi Tulivyofanyizwa
  • Uhuru Wenye Mipaka
  • Sheria za Nani?
  • Ile Zawadi Nzuri Ajabu ya Hiari
    Je, Kweli Mungu Anatujali?
  • Usikose Kusudi la Uhuru wa Kupewa na Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Watu Huru Lakini Wanaotakwa Watoe Hesabu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Jinsi ya Kupata Uhuru wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1991
g91 6/8 kur. 6-7

Zawadi Nzuri Ajabu ya Hiari

JE! WEWE unathamini uhuru wa kuchagua jinsi utakavyopangia maisha yako, mambo utakayofanya na kusema? Au je! wewe ungetaka mtu mwingine akuamurie kila neno na tendo lako litakuwa nini, kila dakika ya kila siku, muda wote utakaokuwa hai?

Hakuna mtu wa kawaida anayependa kunyang’anywa uhai wake uongozwe kikamili hivyo na mtu mwingine. Mtu akilazimika kuishi hivyo lingekuwa jambo la uonevu na la kufadhaisha sana. Sisi twataka uhuru.

Lakini ni kwa nini sisi tuna tamaa hiyo ya uhuru? Ufunguo wa kuelewa jinsi uovu na taabu vingeweza kuanza ni kuelewa ni kwa nini sisi twathamini sana uhuru wa kuchagua. Pia kutatusaidia kuelewa ni kwa nini Mungu amesubiri mpaka sasa kabla ya kuchukua hatua ya kukomesha uovu na taabu.

Jinsi Tulivyofanyizwa

Mungu alipoumba wanadamu, miongoni mwa zawadi nyingi zilizo nzuri ajabu alizowapa ilikuwa ni hiari. Biblia hutuambia kwamba Mungu aliumba binadamu katika ‘mfano na sura’ yake, na mojawapo sifa alizo nazo Mungu ni uhuru wa uchaguzi. (Mwanzo 1:26; Kumbukumbu la Torati 7:6) Kwa hiyo, alipoumba binadamu, aliwapa sifa iyo hiyo iliyo nzuri ajabu—zawadi ya hiari.

Ndiyo sababu sisi hupendelea uhuru kuliko kutumikishwa na watawala waonevu. Ndiyo sababu chuki husitawi juu ya utawala mkali wenye vizuizi hivi kwamba mara nyingi watu huasi ili wapate uhuru.

Tamaa ya uhuru haikutukia tu. Biblia hueleza sababu ya msingi. Hiyo husema hivi: “Mahali palipo roho ya Yehova, pana uhuru.” (2 Wakorintho 3:17, NW) Kwa hiyo kutaka uhuru ni sehemu ya asili yetu kwa sababu Mungu alituumba hivyo. Ni jambo ambalo yeye ataka sisi tuwe nalo kwa sababu yeye mwenyewe ndiye Mungu wa uhuru.—2 Wakorintho 3:17.

Pia Mungu alitupa uwezo mbalimbali wa kiakili, kama vile nguvu za kufahamu, kufikiri, na kuamua, ambazo hufanya kazi kwa kupatana na hiari. Huo hutuwezesha tufikiri, tupime mambo, tufanye maamuzi, na kutofautisha mema na mabaya. (Waebrania 5:14) Sisi hatukuumbwa tuwe kama mashine zisizo na akili ambazo hazina hiari yazo; wala hatukuumbwa tutendeshwe hasa na hekima ya kisilika, kama vile wanyama.

Pamoja na hiari, wazazi wetu wa kwanza walipewa kila kitu ambacho mtu yeyote angetaka kwa kufaa: Walikuwa wamewekwa katika paradiso iliyo kama bustani; walikuwa na akili na miili mikamilifu ambayo haingezeeka au kuwa yenye ugonjwa na kufa; wangekuwa na watoto ambao pia wangekuwa na wakati ujao wenye furaha; na idadi ya watu yenye kuongezeka ingekuwa na kazi yenye kuridhisha ya kugeuza dunia yote kuwa paradiso.—Mwanzo 1:26-30; 2:15.

Kwa habari ya yale ambayo Mungu alikuwa ameanzisha, Biblia yasema hivi: “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Pia Biblia yasema juu ya Muumba: “Kazi yake ni kamilifu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Ndiyo, yeye aliipa familia ya kibinadamu mwanzo mkamilifu. Ulikuwa bora kabisa.

Uhuru Wenye Mipaka

Hata hivyo, je! zawadi nzuri ajabu ya hiari ingekuwa bila mipaka? Basi, je! wewe ungekubali kuendesha motokaa katikati ya magari mengi kama kusingekuwako sheria za barabarani, mahali ambapo ungekuwa na uhuru wa kuendesha popote, kuelekea upande wowote, kwa mwendo wowote? Bila shaka, matokeo ya uhuru huo usio na mipaka katikati ya magari yangekuwa yenye msiba.

Ndivyo ilivyo katika mahusiano ya kibinadamu. Uhuru usio na mipaka kwa wengine ungemaanisha ukosefu wa uhuru kwa wengine. Uhuru usio na mipaka waweza kutokeza mvurugo, ambao unadhuru uhuru wa kila mtu. Lazima kuwe mipaka. Kwa hiyo, zawadi ya Mungu ya uhuru haimaanishi kwamba yeye alikusudia wanadamu wajiendeshe katika njia yoyote bila kufikiria hali njema ya wengine.

Kuhusu jambo hilo Neno la Mungu lasema hivi: “Jiendesheni kama watu walio huru, na msitumie kamwe uhuru wenu kuwa udhuru kwa ajili ya uovu.” (1 Petro 2:16, The Jerusalem Bible) Kwa hiyo Mungu ataka hiari yetu iwekewe mipaka kwa ajili ya faida ya wote. Yeye hakukusudia wanadamu wawe na uhuru kamili, bali uhuru wa kadiri, wenye kutegemea sheria.

Sheria za Nani?

Tulibuniwa tutii sheria za nani? Ni sheria za nani zenye matokeo bora zaidi kwetu? Sehemu nyingine ya lile andiko katika 1 Petro 2:16 lililoonyeshwa juu yasema: “Nyinyi si watumwa wa yeyote isipokuwa Mungu.” Hilo halimaanishi utumwa bali, badala yake, kwamba tuliumbwa tuwe chini ya sheria za Mungu. Twawa wenye furaha zaidi tukijiweka chini yazo.

Sheria za Mungu, zaidi ya orodha yoyote ya sheria iwezayo kubuniwa na wanadamu, hutoa uongozi unaofaa zaidi kwa kila mtu. Ni kama Isaya 48:17 isemavyo: “Mimi ni BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.” Hata hivyo, wakati uo huo, sheria za Mungu huruhusu uhuru wenye mapana bila kupita mipaka yazo. Hilo huruhusu uchaguzi na utofautiano mwingi wa kibinafsi, hilo likifanya familia ya kibinadamu kuwa yenye kupendeza zaidi, kwa kweli, yenye kuvutia.

Pia wanadamu wako chini ya sheria za kiasili za Mungu. Kwa kielelezo, tukipuuza sheria ya nguvu za uvutano turuke kutoka mahali palipo juu, tutajeruhiwa au kufa. Tukikaa chini ya maji bila ya vyombo maalumu vya kupumulia, tutakufa baada ya dakika kadhaa. Na tukipuuza sheria zetu za ndani zilizo kwa ajili ya mwili na kuacha kula chakula au kunywa maji, tutakufa pia.

Kwa hiyo, wazazi wetu wa kwanza, na wote waliotokana nao, waliumbwa wakiwa na uhitaji wa kutii sheria za Mungu za adili au kijamii na pia sheria zake za asili. Na utii kwa sheria za Mungu haungekuwa mzigo. Badala yake, ungetokeza hali njema yao na ile ya familia nzima ya kibinadamu itakayokuwapo. Kama wazazi wetu wa kwanza wangalikaa ndani ya mipaka ya sheria za Mungu, mambo yote yangalikuwa mazuri.

Ni nini kilichotukia ili kuharibu mwanzo huo mzuri? Badala yake, ni kwa nini uovu na taabu vimesitawi sana? Ni kwa nini Mungu ameviruhusu kwa muda mrefu hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Zawadi nzuri ajabu ya hiari hututofautisha na mashine zisizo na akili na kutokana na wanyama ambao hutenda hasa kisilika.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki