Kuyaweza Maisha ya Jeuri
RAFIKI yangu nami tukakimbia upesi kadiri tulivyoweza, na tulipofikia mto ulio karibu na mji wa nyumbani kwetu, tulijichovya ndani. Tulipotokeza tena juu ya maji, tulianza kuogelea mbio sana kuelekea upande ule mwingine wa ukingo.
Je! huu ulikuwa tu mchezo wa ujana? La hata kidogo! Lilikuwa ni jambo la kufa na kupona. Nilipoangalia nyuma, niliona polisi na silaha zikielekezwa kwetu. Nilijiingiza chini ya maji ili kuepa risasi na nikaendelea kuogelea kuelekea upande ule mwingine wa ukingo. Hata nikiwa chini ya maji ningeweza kusikia sauti ya bunduki.
Tulipofika kwenye ukingo ule mwingine, tulikuwa tumefaulu kutoroka gerezani, ambapo tulikuwa tumefungwa kwa uvunjaji wa nyumba na kuiba na wizi wa magari.
Hii ilikuwa mojapo ya nyakati ambazo nilitafutwa au kukimbizwa na polisi kwa sababu ya matendo fulani ya uhalifu. Ingawa nilikuwa na umri wa miaka 17 wakati huo, nilikuwa nimeweka rekodi kubwa ya kutiwa nguvuni na wenye mamlaka. Mwishowe, rafiki yangu nami tulishikwa, na tena nilihukumiwa kufungwa gerezani, wakati huu kwa muda wa miaka miwili na nusu.
Hata katika gereza nilionyesha mwelekeo wa jeuri. Kwa sababu ya kupigana na wafungwa wengine kila mara, nilipewa nguo nyeupe. Hili lilifanya wafanya ghasia wengine na mimi tupewe uangalifu wa pekee na walinzi.
Mwenye Jeuri Sana Baada ya Kufunguliwa
Nilifunguliwa kutoka gerezani, lakini sikuwa nimebadilika kuwa mzuri. Hata hivyo, nilikuwa mwenye jeuri sana kuliko awali. Upesi nikawa kiongozi wa mitaa fulani fulani. Yeyote ambaye angenitisha haraka angepata mpinzani mwenye utayari.
Wakati mmoja kikundi cha vijana kilinichokoza. Niliwashambulia, nikawaumiza wengine kabla ya polisi kusimamisha ghasia hiyo, hata ingawa mkono wangu ulikuwa umevunjika kwa sababu ya vita wiki moja kabla ya hapo.
Wakati mwingine marafiki zangu wawili nami tulitisha kikundi cha watu waliotoka mji jirani. Kiongozi wao alinijia na chuma. Nikamnyang’anya, lakini akaponyoka mkononi mwangu na kukimbia. Njia pekee ya kumfanya aendelee kupigana ilikuwa ni kumrudishia chuma chake, jambo ambalo nilifanya. Alirudi, na nikamnyang’anya tena, wakati huu nikihakikisha kwamba hakuhepa kabla ya kumpiga.
Usiku mmoja, ili tu “kujifurahisha,” nilisimama katika pembe ya barabara katika Harlem, New York City, na kumtisha yeyote tupigane naye. Wengine waliitikia, na vita vikawa vingi. Kama tokeo, sifa yangu nikiwa mtu mwenye jeuri na hatari, ikakua. Katika vita hivi mbalimbali, nilipigwa kwa chupa, vyombo vya kurekebisha magurudumu, na rungu na visu na silaha nyingine. Lakini yote hayo hayakufanya lolote kugeuza njia zangu za jeuri.
Jeuri Yaongezeka
Upesi nikagundua kwamba pesa nyingi sana zingepatikana kupitia uuzaji wa dawa za kulevya. Nikiwa mtumiaji wa dawa za kulevya, nilifahamiana na jamii iliyohusika na dawa za kulevya. Hata kabla ya muda mrefu kupita nilipata watu wa kuniuzia dawa za kulevya, wakinifanya niwe mwenye jeuri hata zaidi.
Wakati mmoja tulimwingilia kwa ghafula mchuuzi wa dawa za kulevya, tukitumaini kuiba dawa zake za kulevya. Tukiwa na bastola na kisu, tukavunja nyumba yake na kuwashika mateka wanaume watatu na mwanamke mmoja huku tukipekuapekua nyumba yote, tukitafuta dawa za kulevya.
Wakati mwingine rafiki yangu nami, tukiwa na bastola, na tukiwa tumevalia vifuniko vya uso, tuliamua kumnyang’anya mtu tajiri ili tupate pesa za dawa za kulevya. Tukangojea nyumbani mwake, lakini hakuonekana, kwa hiyo tukaenda. Bila shaka, kama angalikuja, tungetimiza kusudi letu.
Hivyo, katika umri wa miaka 20 tu, nilijipata nimeingia sana katika jeuri, dawa za kulevya, na uhalifu mkubwa. Wakati wangu ujao, ungekuwa wa maisha katika gereza—na nilikuwa sina furaha.
Mara nyingi nilijiuliza ni nani anayepaswa kuamua ni lipi lililo sawa na lipi baya. Niliamua kwamba ni yeyote aliye na nguvu nyingi katika jamii. Pia nilifikiri kwamba kwa vile wanadamu walikuwa na haki ya kuamua jema na baya, na nilikuwa sina heshima yoyote kwa mamlaka yoyote ya kibinadamu, nilikuwa na haki ya kuamua swali kama hilo mimi mwenyewe kama yeyote. Lakini karibuni ningepata jibu linalofaa.
Njia Nzuri Zaidi
Dada yangu, ambaye aliolewa na mmoja wa marafiki zangu niliokuwa nimefungwa pamoja nao gerezani, alikua amekubali funzo la Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alishiriki mambo aliyokuwa akijifunza kutoka katika Biblia pamoja na kila mtu katika familia yetu—isipokuwa mimi. Familia yetu waliniambia nimwepuke dada yangu. Kwa nini? Walisema ni kwa sababu yote aliyokuwa akizungumza ni juu ya “dini hiyo yenye kichaa.”
Nilitaka kujua mengi zaidi. Ni nini alilosema ambalo lingewakasirisha watu sana hivyo? Nilitaka kujua, lakini dada yangu hakuongea nami kuhusu hilo. Kwa nini? Alifikiri nilikuwa mbaya sana nisiweze kusikiliza lolote kuhusu Biblia.
Lakini jioni moja nilijikaribisha nyumbani mwake kwa chakula cha jioni. Niliketi hapo nikila na dada yangu na mume wake, na nikasema: “Niambie kuhusu hii dini mpya.” Walifanya hivyo—kwa muda wa saa sita! Ilikuwa yenye umaana sana kwangu hata nikarudi jioni iliyofuata ili nisikie mengi.
Baada ya ziara hii ya pili, nilihakikishiwa kwamba nilikuwa nimepata jambo katika maisha, kusudi halisi maishani. Upesi, nikaanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova na pia kuongea na marafiki zangu juu ya mambo niliyokuwa nikijifunza.
Mtindo-maisha wangu ulibaki bila kubadilishwa kwa muda. Lakini niliendelea kujifunza na kujua lile Yehova Mungu alitazamia, na nikahakikisha kwamba sikukosa mikutano kwenye Jumba la Ufalme, ambapo Biblia ilizungumzwa. kupitia njia hii nilipata nguvu za kiroho za kubadilisha maisha yangu, jambo moja baada ya jingine.
Kwanza, niliacha kuuza dawa za kulevya. Hili liliwakasirisha wale niliokuwa nimejiunga nao, lakini bado nilikuwa na sifa yangu ya jeuri, ambayo iliniepusha na dhara. Halafu, nikaacha kutumia dawa za kulevya na pia nikaacha mtindo-maisha wangu wa ukosefu wa adili. Jambo la mwisho ambalo nilidhibiti ni tabia ya tumbako. Katika miezi minane nilikuwa nimefanya maendeleo kufikia kustahili ubatizo, na nikabatizwa katika 1970.
Hatimaye nilifikia utambuzi wa kujua ni nani aliyekuwa na haki ya kuamua ni nini lililo sawa na lililo baya. Jibu ni: Yehova, Mpaji Uhai wetu, mwenye haki hiyo, na pia mwenye haki ya kutazamia viumbe wake waishi kulingana na anayotaka.
Mara nyingi nimefikiria jinsi kiolezo katika andiko la Isaya 65:25 limetimizwa kwangu katika njia ya mfano. Unabii huo unazungumzia juu ya wakati utakaokuja ambapo hali jeuri ya simba itabadilishwa kuwa ya amani kufikia kula nyasi kama ng’ombe. Nilihisi kwamba katika njia hiyo hiyo, nilikuwa nimebadilika kutoka kuwa mtu mwenye jeuri sana mpaka kuwa mwenye hali ya amani na mtazamo wa amani maishani.
Bado, nilikuwa na sifa mbaya niliyohitaji kusahau kwa kutoirudia tena. Kama kielelezo, nilienda nyumba kwa nyumba kuzungumza na watu juu ya Biblia pamoja nao. Katika mlango mmoja, mwanamume mchanga aliyejibu alinitambua na akaogopa, akifikiri nimekuja kumdhuru. Kwa haraka nilimwelezea haraka haraka ujumbe wangu wa amani kutoka kwa Biblia, nikimwacha akiwa ameduwaa lakini akiwa amepumzishwa.
Haikuwa muda mrefu baada ya ubatizo wangu, nikaoa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Jambo lenye kusikitisha, katika 1974 mke wangu akaamua kwamba hataki kufanya mapenzi ya Mungu. Alinipa neno la mkataa: niachane na njia yangu ya ibada au sivyo angeniacha, akichukua watoto wetu wadogo wawili. Hiyo ilikuwa pindi yenye magumu sana maishani mwangu. Lakini singeweza kuacha njia yangu ya kumwabudu Mungu, na niliendelea kufanya mapenzi yake.
Njia Mpya ya Maisha
Hata hivyo, Yehova alinithawabisha kwa kuendelea kuwa mwaminifu kwake. Katika 1977, nilikutana na Shahidi mzuri sana, na tukaoana. Alikuwa na mvulana wa miaka mitano. Upesi mke wangu nami tukaingia katika utumishi wa wakati wote, tukijitolea kufundisha wengine juu ya Mungu na makusudi yake. Wakati mvulana wetu alipokuwa mkubwa, aliingia kwenye utumishi wa wakati wote pia. Sasa anasaidia katika shughuli mbalimbali katika kundi la kwetu.
Mke wangu nami tumekuwa na pendeleo la kusafiri katika sehemu nyingi za dunia, tukifanya kazi ya kujitolea ya kujenga. Hili latia ndani kujenga ofisi mpya za tawi katika nchi mbalimbali ili kutegemeza kazi ya uelimishaji ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova.
Tunapokuwa nyumbani, sisi huwa na shughuli katika sehemu za kwetu, tukisaidia wengine wajifunze juu ya Biblia na kusaidia kujenga Majumba mapya ya Ufalme. Mimi pia hutumikia katika Halmashauri ya Ujenzi wa Eneo katika sehemu ya kusini ya United States. Na aliyekuwa mfungwa mwenzangu—mume wa dada yangu—pamoja nami hutumikia tukiwa wazee katika kundi moja la Mashahidi wa Yehova.
Namshukuru Yehova kwa kunisaidia nidhibiti maisha yangu na kuyapa mwongozo mpya kabisa. Kadiri nikubalivyo anionyeshe lililo sawa na lililo baya, maisha yangu yanakuwa bora zaidi.—Imechangwa.