Vijana Wanauliza...
Nifanye Nini Kuhusu Kazi Nyingi ya Shule ya Kufanyia Nyumbani?
“Kazi nyingi sana ya shule” imetajwa kuwa mojawapo visababishi vya kawaida sana vya mkazo miongoni mwa vijana
“Ikiwa huna mpango mzuri, unapoteza wakati mwingi sana ukiamua kile utakachofuata kufanya”
‘SISI hatuna wakati wa kutosha!’ Ndivyo kikundi kimoja cha wanafunzi wa shule ya upili walivyoteta. Sababu ya tatizo hilo? Matakwa ya shule na kazi ya shule ya kufanyia nyumbani. “Ninaanza shule saa 2:00 asubuhi na kumaliza saa 11:30,” asema kijana Véronique. “Ninapofika nyumbani, ni saa 12:30. Inachosha. Wazazi hufikiri kwamba kuwa shuleni ni maisha mazuri ajabu. Hawaelewi kwamba shule huchosha na hukaza akili, na kisha tunapofika nyumbani, kuna kazi ya shule ya kufanyia nyumbani.” Sandrine mwenye umri wa miaka kumi na saba aongeza hivi: “Mimi hutumia saa mbili hadi tatu usiku nikifanya kazi ya shule nyumbani, kutia na miisho-juma.”
Véronique na Sandrine huishi Ufaransa, ambako wanafunzi wana mojawapo siku ndefu zaidi za shule katika Ulaya. Wanafunzi katika nchi nyinginezo nyingi huhisi wamekazwa, wamefadhaishwa, na wamelemewa vilevile na matakwa yote ya wakati wao. “Kazi nyingi sana ya shule” imetajwa kuwa mojawapo visababishi vya kawaida sana vya mkazo miongoni mwa vijana.
Kwa kuwa ni vigumu kupata kazi katika sehemu nyingi za ulimwengu kuliko wakati mwingine wowote, vijana wengi huona kupata elimu bora kuwa jambo la maana kwa ajili ya wakati wao ujao wa kufanya kazi. Kama vile Violaine, mwanafunzi wa shule ya upili, asema: “Nafasi za kupata kazi nzuri zimekuwa haba sana hivi kwamba vijana leo wanang’amua kuna jambo moja tu la kufanya—KUJIFUNZA!”
Wakati Hautoshi?
Hata hivyo, wale wanaofanikiwa shuleni wanajua kwamba hilo huhitaji wakati na nishati nyingi. Ikiwa wewe ni kijana Mkristo, una mambo ya ziada yanayodai wakati wako: kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kujifunza Biblia, na kushiriki imani yako na wengine. (Yohana 17:3, Warumi 10:10; Waebrania 10:24, 25) Biblia inaendelea kusema kwamba kuna “wakati wa kucheka” na kufurahi. (Mhubiri 3:1, 4; 11:9) Kama vijana wengi, labda unataka angalau uwe na wakati fulani wa tafrija na starehe. Lakini huenda kazi ya shule ikakuacha na wakati mchache wa kufanya mambo unayohitaji kutimiza—na hata wakati mchache zaidi wa kufanya mambo ambayo ungependa kufanya.
Hata hivyo, mara nyingi tatizo si kukosa wakati tu. Uchunguzi wa hivi karibuni ulifunua kwamba sababu mbili kati ya zile kubwa kwa nini wanafunzi wa shule ya upili walikuwa na matatizo ya masomo zilikuwa ni “utumizi mbaya wa wakati” na “kukosa mpango.” Kama vile kijana aitwaye Olivier alivyogundua, mpango usiofaa wa kibinafsi waweza kuathiri zaidi ya maksi zako. Yeye asema: “Ikiwa huna mpango mzuri, unapoteza wakati mwingi sana ukiamua kile utakachofuata kufanya” Basi unaweza kupangaje mambo yako?
Maoni Yaliyosawazika ya Kazi ya Shule
Kwanza kabisa, ni lazima uweke kazi yako ya shule mahali panapofaa. Biblia hutuambia ‘tuhakikishe mambo ya maana zaidi.’ (Wafilipi 1:10, NW) Na unapotua na kufikiri, kwa kweli ni nini kinachopaswa kuwa cha maana zaidi maishani mwako? Je! si wajibu wako wa kiroho? Kwa vyovyote, Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake.” (Mathayo 6:33) Hiyo yamaanisha kutanguliza mikutano ya Kikristo, sala, funzo, na kazi ya kuhubiria wengine.
Je! hilo linamaanisha kwamba kazi ya shule si ya maana? Sivyo hata kidogo. Lakini ukiwa Mkristo, lengo lako katika kufuatia elimu fulani halipaswi kuwa kujielimisha kwa ajili ya kazi-maisha ya kilimwengu. Badala yake, lapaswa kuwa ni kujifunza stadi zitakazokusaidia katika kazi-maisha yako ukiwa mhudumu wa Mungu. Wakati uo huo, unajitayarisha mwenyewe ili udumishe kazi na ujitegemeze mwenyewe, na labda familia siku moja. (1 Wathesalonike 4:11, 12; 1 Timotheo 5:8) Kujua hivyo kwapaswa kukusaidie ujitahidi kufanya yote uwezayo shuleni. Wakati uo huo, unahitaji kutia bidii kwa kufaa ili uendelee kuwa mwenye nguvu kiroho.
‘Kununua wakati’ kwa ajili ya wajibu wa kiroho, kazi za nyumbani, tafrija, na kazi za shuleni, kwaweza kuwa tatizo kwelikweli, lakini kunawezekana.—Waefeso 5:15, 16.
Thamani ya Kuwa na Ratiba
Njia moja ya kununua wakati ni kuwa mwenye matokeo zaidi kwa namna unavyojifunza. Sura ya 18 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi chatoa madokezo kadhaa yenye kusaidia.a Kwa mfano, je, umejaribu kutengeneza ratiba au kuweka mpango kwa ajili ya kazi yako ya shule?—Linganisha Wafilipi 3:16.
“Bila shaka tatizo la kawaida sana katika kujifunza,” aandika Harry Maddox katika kitabu chake How to Study, “ni kushindwa tu kuanza kazi ya kawaida yenye kukaziwa fikira.” Namna gani wewe? Je! unaweka kazi ya shule kando hadi unapojihisi uko tayari kuifanya—au hadi wakati unapoifaa zaidi? Mhubiri 11:4 huonya: “Mwenye kuuangalia upepo hatapanda; naye ayatazamaye mawingu hatavuna.”
Harry Maddox aonelea zaidi hivi: “Ni rahisi sana kupoteza wakati hatua kwa hatua. Ikiwa hujiwekei ratiba inaelekea sana kwamba labda utatumia wakati ambao ungekuwa unajifunza, kutazama T.V., kusoma gazeti, . . . au katika kufanya yoyote kati ya mambo mengi ambayo wanafunzi wasio stadi wako tayari kufanya badala ya kufanya kazi. Ikiwa una ratiba na unaazimia kuifuata, hiyo ina uwezo wote wa sheria ambayo ni lazima itiiwe, na baadaye, kushikamana nayo huwa rahisi sana, na unaanza kuiona kuwa sehemu ya kawaida ya maisha yako.”
Ukishughulikia kazi yako ya shule kwa njia iliyopangwa vizuri na yenye nidhamu, itaelekea kwamba utakuwa na wakati mwingi zaidi unaopatikana. Mpango mzuri kwa upande wako waweza pia kukusaidia kuzuia kuhitilafiana kati ya kumaliza migawo yako ya shule na kutimiza wajibu wako wa Kikristo, kama vile kuhudhuria mikutano ya kundi.
Panga Wakati Wako!
Namna gani yale mambo mengine unayotaka na unayohitaji kutimiza, kama vile kazi za nyumbani? Hapo vilevile, kupanga vizuri kunahitajiwa. Jaribu kutumia madokezo yafuatayo:
Weka orodha ya mambo ya kufanya. Mshauri wa usimamizi wa wakati Stephanie Winston apendekeza kuchukua kijitabu kidogo cha kuandikia ukikichukua wakati wote. Kitumie kuandika “kila wazo, mgawo, simu, mradi, kazi, au utume—kubwa au dogo, la maana ndogo au kubwa—kadiri linavyotokea.” Kwa mtazamo wa kwanza, orodha yako huenda ikaonekana kuwa ndefu sana, lakini kwa kutumia madokezo yafuatayo, unaweza kuipunguza hadi kuwa ya kiasi unachoweza.
Panga mambo ya maana zaidi kwanza. Hiyo yaweza kukusaidia kukazia fikira mambo ambayo yanahitaji kufanywa kwelikweli. Wakati uo huo, unaweza kuondoa mambo yanayoweza kusubiri au ambayo huna wakati wa kuyafanya.
Tayarisha ratiba. Ndiyo, badili orodha yako kuwa mpango wa utendaji—ratiba iliyoandikwa. Kalenda ndogo ya mfukoni, au kijitabu cha mambo ya kila siku, yaweza kukusaidia sana katika jambo hilo. Badala ya kupunguza uhuru wako, ratiba yenye usawaziko mzuri itakuwezesha udhibiti wakati vizuri zaidi.
Chukua mambo kihalisi. Kwa njia ya kujaribu na kukosea, fahamu ni wakati upi wa kufanya mambo fulani. Kwa mfano, huenda ukaona kuwa inanufaisha kupanga vipindi vyako vya kufanya kazi ya shule mapema iwezekanavyo katika siku, wakati ambapo bado uko macho kiakili.
Hata hivyo, ng’amua kwamba si lazima upangie kila dakika ya maisha yako. Weka ratiba yako ikiwa yenye kubadilikana, ukiacha nafasi kwa ajili ya mambo yasiyotazamiwa na yanayotokea ghafula. Fanya marekebisho kadiri yanavyohitajiwa, lakini shikamana na ratiba yako kadiri iwezekanavyo. Angalia: Mara nyingi inafaa zaidi kukadiria wakati unaopita ule unaohitaji kumaliza kazi fulani. Sikuzote unaweza kubadilisha ukimaliza mapema.
Weka siku yako ya mwisho. Hilo hukusaidia uepuke mwelekeo wa kungoja hadi dakika ya mwisho ili ufanye jambo. Ikiwa una kazi ya shule, jaribu kuweka tarehe ya kuimaliza ambayo ni ya mapema zaidi ya ile tarehe ambayo inatakiwa ipelekwe.
Jitie nidhamu kushikamana na ratiba yako. Unaweza kushawishwa kwenda nyumbani kwa rafiki yako wakati ambapo unahitaji kubaki nyumbani ujifunze kwa ajili ya mitihani ya mwisho. Lakini ukipanda kwa uhaba kuhusiana na mafunzo yako, huenda ukavuna maksi mbaya baadaye. (Linganisha 2 Wakorintho 9:6.) Isitoshe, mara nyingi utafurahia zaidi wakati wako wa kupumzika ikiwa umekamilisha kazi yako. Kanuni yenye msaada ni, Mambo ya maana kwanza, mambo ya kufurahia baadaye.
Kupanga ratiba na mambo yako kutachukua wakati, subira, na kujitia nidhamu kwingi, lakini Wakristo wanaambiwa wajizoeze kujiweza katika mambo yote. (1 Wakorintho 9:25) Kujifunza kushikamana na ratiba ni zoezi zuri katika kutumia kanuni hiyo. Matokeo yaweza kuwa kupata uradhi kwa mambo uliyotimiza, kudhibiti zaidi maisha yako, na wakati zaidi wa kufanya mambo unayotaka na unayohitaji kufanya.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Panga ratiba ya kujifunza na ushikamane nayo