Vijana Huuliza...
“Kupita Kiasi” Kwafikia Wapi?
“Tafadhali, mwaweza kuonya watu juu ya hatari ya kupita kiasi? . . . ‘Migusano hiyo yote yahitaji kujadiliwa,’ kwa sababu inaongoza kwenye ngono. Swali langu ni, kikomo kiko wapi?”
Hilo ndilo swali ambalo msichana mmoja aliuliza gazeti moja la matineja. Lakini labda ni swali ambalo wewe mwenyewe umejiuliza.
Kama wewe ni Mkristo, unachukua kwa uzito maneno yapatikanayo katika 1 Wathesalonike 4:3-6: “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kutakaswa kwenu, mwepukane na uasherati; . . . Mtu asimpunje ndugu yake wala kumkosa katika jambo hili; kwa sababu Bwana [Yehova, NW] ndiye alipizaye kisasi cha haya yote.”
Kwa hiyo ingawa huenda umejua kwamba ngono kati ya Wakristo wasiooana ni mbaya, bado huenda ukajiuliza jinsi Mungu huona kupiga busu, kukumbatia, au kupapasa-papasa mtu wa jinsia tofauti.
Ni Sehemu ya Ukuzi?
Kwanza kabisa, ni vizuri kukumbuka kwamba Biblia haishutumu maonyesho safi ya shauku yasiyokuwa na madokezo ya kingono. Wakristo wa kale walikuwa wenye kuonyesha sana upendo wao kwa moja na mwenzake. Kwa kawaida ‘wangesalimiana kwa busu takatifu.’ (Warumi 16:16; 1 Wakorintho 16:20) Hata Wakristo wa jinsia moja walikuwa wakipigana busu na kukumbatiana.—Linganisha Matendo 20:37.
Katika tamaduni nyingi, kupiga busu na kukumbatia bado huonwa kuwa njia zifaazo za kuonyesha shauku kwa mtu mwingine. Hata hivyo, vijana wengi leo huonyesha shauku kwa njia zenye kupita kiwango kinachoonwa kuwa chafaa. Uchunguzi mmoja wa U.S. ulipata kwamba zaidi ya theluthi mbili za matineja walioombwa maoni walisema kwamba walikuwa wamejihusisha kwa namna fulani ya kugusana kimapenzi kunakotia ndani kupapasa-papasa sehemu za siri za mwili. Wengi walianza kufanya hivyo wakiwa na umri wa mapema kama miaka 14. Kama ilivyopatikana katika uchunguzi mwingine, asilimia 49 walikuwa wamejihusisha kwa kugusana kimapenzi kufikia mshindo (upeo) wa kingono.
Watu fulani hutetea majaribio hayo ya kingono kuwa tu sehemu ya ukuzi. Kulingana na kitabu The Family Handbook of Adolescence, “michezo na majaribio ya ngono ni ya kawaida miongoni mwa karibu vijana wote wa kawaida wanaobalehe.” Watu fulani hata hupendekeza kugusana kimapenzi. Kitabu Growing Into Love, cha Kathryn Burkhart, chadai hivi: “Kwa sababu [kugusana kimapenzi] hukaribia sana ngono, kugusana kwingi kwaweza kujaribiwa bila kuwa na wasiwasi na kutumike kuwa njia bora ajabu ya kuondoa hisia za kingono.”
Lakini, swali lauliza hivi, Mungu aonaje tabia ya namna hiyo?
Busu Yaweza Kutokeza Nini?
Wakati umo katika “uzuri wa ujana,” tamaa za kingono zaweza kuwa zenye nguvu sana. (1 Wakorintho 7:36) Kwa hiyo, ni kawaida tu kwa mtu kuwa mdadisi kwa kutaka kujua huwa inakuwaje kubusu au kugusa mtu wa jinsia tofauti. Lakini The Family Handbook of Adolescence chaeleza hivi: “Uwezo wa kingono hutangulia, nyakati nyingine kwa miaka mingi, ukomavu wa kihisia.” Kwa kweli vijana wengi hawajui kwa hakika kwamba busu au kupapasa-papasa kuna uwezo wa kuamsha hisia zenye nguvu za kimahaba au tamaa za kingono.
Basi, ni lazima ufikirie kwa hekima matokeo ya kujihusisha katika mwenendo wenye kuamsha hisia za kingono. Vipi kama wewe ni mdogo mno kufunga ndoa? Basi kwa nini ubusu au ufanye kitu chochote kwa njia iwezayo kukuamsha kingono? Mambo hayo yatakusababishia mfadhaiko tu. Hiyo ni kwa sababu haiwezekani kwako ukiwa Mkristo wa kweli kuendelea na hisia hizo za kimahaba hadi mwisho wazo wa kawaida—kufanya ngono. Biblia yasema wazi kwamba mahusiano kama hayo yafaa tu katika ndoa.—1 Wakorintho 6:18.
Fikiria pia yule mtu mwingine, ambaye anaweza kuamshwa kingono kutokana na utendaji wako wa kimahaba. Je! si tendo la ulaghai, na hata la ukatili, kubusu au kupapasa-papasa mtu ambaye huwezi kumwoa au hata hufikirii kwa uzito kama kuna uwezekano mkubwa awe mwenzi wa ndoa? (Linganisha Mithali 26:18, 19.) Biblia yaonya hivi: “Aliye mkali hujisumbua [huharibu, NW] mwili wake.”—Mithali 11:17.
Haipasi kuwa siri kwa mwanafunzi yeyote wa Biblia kwamba mguso au busu ya kimahaba yaweza kuamsha tamaa zenye nguvu za kufanya ngono. Biblia yasimulia kutongozwa kwa kijana na malaya mmoja. Yasema hivi: “Basi akamshika, akambusu.” (Mithali 7:13) Busu ama mguso kama huo waweza kuleta itikio kubwa la mwili. Mapenzi yanapoongezeka mvulana au msichana huendelea kuamshwa kingono. Bila kuficha, mwili unajitayarisha kwa ajili ya ngono.
Kama wenzi wameoana, wanaweza kuridhisha nyege zao kwa njia yenye kufurahisha na yenye kuheshimika. Lakini, wenzi wasiooana wanapojihusisha na michezo ya kingono yenye kuamsha nyege, kwa hakika matatizo yatatokea. Katika uchunguzi mmoja, mwandikaji Nancy Van Pelt aligundua kwamba vijana wengi waliojihusisha na kugusana kimapenzi walikiri waziwazi kwamba, kama walivyosema, “walishindwa kujidhibiti.” Mfano mmoja wa hali ya kawaida ni msichana mmoja mchanga aliyesongwa kufanya tendo lenye kupita kiasi cha alivyopata kufanya wakati mwingine wowote. Ingawa hakufanya ngono, aliruhusu mvulana huyo amshike-shike sehemu za siri. Yeye asema hivi: “Sasa najihisi vibaya sana.” Je! tendo aliloruhusu mvulana huyo kufanya lilikuwa baya kweli?
“Kupita Kiasi” ni Nini?
Vijana fulani huamini kwamba mradi tu hawajihusishi katika kufanya ngono, hawajapita kiasi, kwamba kwa kweli tendo wanalofanya si baya. Biblia yaonyesha kinyume cha wazo hilo. Katika Wagalatia 5:19-21, mtume Paulo alisema hivi: “Matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi [mwenendo mlegevu, NW], . . . watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”
Uasherati ni nini? Neno la awali la Kigiriki la uasherati ni por·neiʹa. Larejezea utendaji wa kingono unaohusu matumizi ya viungo vya uzazi ufanywao nje ya vifungo vya ndoa. Msichana mmoja aliyenukuliwa katika gazeti Seventeen aliruhusu rafiki yake mvulana amsonge mpaka akafanya ngono ya kimdomo. “Najihisi mjinga sana,” yeye akasema, “kwa sababu marafiki wangu wote husema kwamba wao hufanya hivyo na marafiki wao wavulana na angeniacha kama nisingefanya hivyo.” Utafiti waonyesha kwamba idadi kubwa ya vijana wamejihusisha katika namna hiyo ya ukosefu wa adili. Hata hivyo, matendo kama hayo hujumuika kuwa por·neiʹa na Mungu hakubali matendo hayo.
Mtume Paulo pia alilinganisha uasherati na “uchafu.” Neno la awali la Kigiriki, a·ka·thar·siʹa, hutia ndani uchafu wa namna yoyote ile, katika usemi au tendo. Kwa kweli ingekuwa uchafu kwa mtu kuruhusu mikono yake kukengeuka na kuingia ndani ya vazi la mtu, kutoa vazi la mtu, au kupapasa-papasa sehemu za siri za mtu mwingine, kama vile matiti. Kwani, katika Biblia kupapasa-papasa matiti kunashirikishwa na raha zinazohifadhiwa wenzi wa ndoa pekee.—Mithali 5:18, 19; linganisha Hosea 2:2.
Vijana wengine hupuuza waziwazi viwango hivyo vya kimungu. Wao hupita kiasi kimakusudi, au wao hutafuta kwa pupa wenzi wengi ambao wanaweza kushiriki nao uchafu wao wa kingono. Hivyo wanakuwa wenye hatia juu ya kile mtume Paulo alikiita “mwenendo mlegevu.”
Vichapo vingi vyenye mamlaka huonyesha kwamba neno la awali la Kigiriki kwa “mwenendo mlegevu” (a·selʹgei·a) humaanisha ‘matendo mabaya sana, kupita kiasi, ufidhuli, nyege isiyozuilika, na ubaya zaidi.’ Vijana wanaozoea mwenendo mlegevu ni kama wapagani ambao Paulo alirejezea. Kwa sababu ya “ubatili wa nia zao,” wapagani hao walikuja ‘kufa ganzi na kujitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani.’ (Waefeso 4:17-19) Kwa kweli ungetaka kuepuka kushutumiwa hivyo!
Basi, ng’amua kwamba si lazima mtu ajihusishe katika kufanya ngono ndipo ‘apitishe kiasi’ kwa maoni ya Yehova. Ukiwa mchanga mno kufunga ndoa, kugusana kimahaba na kubusu kwapaswa kuepukwa. Na ni lazima wale wanaochumbiana wawe waangalifu maonyesho yao ya shauku yasije yakawa machafu. Ni kweli kwamba si rahisi kushikamana na viwango vya kimungu. Lakini Mungu asema hivi katika Isaya 48:17: “Mimi ni BWANA [Yehova, NW] Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”—Ona pia Wagalatia 5:16.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Kama hujafunga ndoa, kujihusisha katika tabia inayoamsha nyege kwaweza kuleta mfadhaiko na hata matokeo mabaya zaidi