Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 1/8 kur. 26-27
  • Je! Ubatizwe Mara ya Pili?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Ubatizwe Mara ya Pili?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Fanyeni Wanafunzi, Mkiwabatiza
  • Simulizi la Kimaandiko la Kubatizwa Tena
  • Jinsi ya Kustahili Ili Kubatizwa
  • Ubatizo Ni Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Kwa Nini Ubatizwe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Ubatizo
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Maana ya Ubatizo Wako
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 1/8 kur. 26-27

Maoni ya Biblia

Je! Ubatizwe Mara ya Pili?

LUCILA alisumbuka. Ingawa alilelewa akiwa Mkatoliki, alikuwa ameanza funzo la bidii la Biblia hivi karibuni kwa msaada wa rafiki asiye Mkatoliki. Yeye angeweza kuona kwamba Biblia ilifafanua ubatizo kuwa jambo tofauti na ile sherehe aliyokuwa amepata utotoni. “Je! hilo lamaanisha itabidi nibatizwe mara ya pili?” yeye akauliza kwa unyoofu. “Nahofu kwamba kufanya hivyo ningemkosea Mungu.”

Mamia ya mamilioni ya watu, Wakatoliki na pia Waprotestanti, wamenyunyiziwa au kumwagiliwa maji wakiwa vitoto vichanga katika sherehe ya ubatizo. Mamilioni ya watu wengineo walibatizwa kwa aina fulani ya kuzamishwa kabisa majini walipokuwa wakubwa zaidi. Hilo latokeza swali, Ubatizo wa Kikristo ni nini hasa? Je! kuna hali fulani ambazo zingehitaji kuwe na ubatizo wa mara ya pili?

Kamusi ya Pocket Catholic Dictionary yafasili ubatizo kuwa “sakramenti ambayo, kwa maji na neno la Mungu, mtu huoshwa dhambi zote na kuzaliwa tena na kutakaswa katika Kristo kwenye uhai wa milele.” Kuhusu kubatizwa tena, chanzo iki hiki chasema kwamba “ubatizo hutia alama isiyofutika juu ya nafsi, jambo linalomaanisha kwamba [ubatizo] hauwezi kurudiwa, kwa sababu hauhitaji kurudiwa.” Je! hivyo ndivyo Biblia husema?

Fanyeni Wanafunzi, Mkiwabatiza

Kwenye Mathayo 28:19, 20, twasoma amri juu ya ubatizo ambayo Kristo aliyefufuliwa aliwapa wanafunzi wake, kabla ya kupaa kwenda mbinguni. “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu [Roho Takatifu, NW]; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” Kwa wazi, ubatizo watakwa kwa wanafunzi wa Kikristo—wale waliofunzwa kushika amri za Kristo—si vitoto vichanga.a Hilo lapatana na uhakika wa kwamba mabatizo yote yanayoelezwa katika Maandiko yalihusu wanafunzi ambao yaonekana walizamishwa kabisa majini. Kwa wazi hilo lilikuwa hivyo Kristo Yesu mwenyewe alipobatizwa na Yohana Mbatizaji. Simulizi la Biblia husema kwamba baada ya kubatizwa, Yesu ‘alipanda kutoka majini’ mwa Mto Yordani. (Mathayo 3:16) Kwa kweli, Maandiko yaonyesha kwamba Yohana alichagua kwa uangalifu mahali pa kubatizia ili pawe penye maji mengi.—Yohana 3:23.

Baadaye, katika kueleza juu ya ubatizo wa towashi Mwethiopia, Biblia hutuambia kwamba ‘walitelemka wote wawili majini, Filipo na yule towashi, naye akambatiza,’ baada ya hapo ‘wakapanda kutoka majini.’ (Matendo 8:38, 39) Mabatizo hayo kwa kuzamishwa yanapatana na maana ya ujumla ya neno la Kigiriki ba·ptiʹzo, “kubatiza,” kutoka baʹpto, kumaanisha “kuchovya ndani au chini,” ambalo ni shina la neno la Kiswahili “ubatizo.”

Simulizi la Kimaandiko la Kubatizwa Tena

Lakini vipi juu ya mamilioni mengi ya watu waliobatizwa wakiwa vitoto vichanga au ambao hawakuzamishwa kabisa? Je! kungefaa kwa vyovyote kuwabatiza mara ya pili? Tukio linalosimuliwa katika Matendo 19:1-7 hutusaidia kujibu maswali hayo. Yaelekea ilikuwa wakati wa kipupwe cha mwaka 52/53 W.K. kwamba mtume Paulo alizuru jiji la Efeso lenye utajiri la Asia Ndogo. Huko alipata baadhi ya wanafunzi waliohitaji kubatizwa mara ya pili. Baada ya kujifunza kwamba wanaume hao walikuwa wamebatizwa kwa ubatizo wa Yohana, Paulo aliwabatiza mara ya pili “katika jina la Bwana Yesu.” Hakuhisi kwamba kufanya hivyo kungemkosea Mungu. Kwa wazi, Mungu alikubali kusababu kwa Paulo, na badala ya kukasirika kwa sababu ya ubatizo huo wa mara ya pili, Mungu aliuidhinisha kwa zawadi ya roho takatifu.

Kama wale wanaume 12 wangekataa mafundisho ya Paulo juu ya aina ya ubatizo na umaana wa Mesiya, Kristo Yesu, hakuna shaka Paulo angezuia ubatizo. Kwanza, wanaume hao walipaswa wastahili ubatizo. Ndipo tu wangeweza kubatizwa mara ya pili kwa kibali cha Mungu.

Jinsi ya Kustahili Ili Kubatizwa

Sisi hustahilije kubatizwa? Fikiria umati wa watu waliobatizwa siku ya Pentekoste 33 W.K. Wao walistahilije? Kwanza, wakiwa Wayahudi na waongofu wa Kiyahudi, walianza kwa kuwa na ujuzi mwingi wa msingi juu ya Yehova Mungu, shughuli zake na watu wake, na unabii mbalimbali wa Biblia juu ya Mesiya wake aliyeahidiwa. Pili, walipata ujuzi sahihi zaidi wakati ushahidi uliopuliziwa ulitolewa na mtume Petro siku hiyo. Kukiwa na tokeo gani?

“Walipoyasikia haya, wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu? Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].” (Matendo 2:37, 38) Ona kwamba ushahidi wa Petro haukuwa wa kijuujuu. “Alisema nao kwa muda mrefu akitumia hoja nyingi.” Walisadikishwa na kusababu kwake, na walikubali yale aliyosema na wakabatizwa. “Siku ile wakaongezeka watu wapata elfu tatu.”—Matendo 2:40, 41.

Mambo yaleyale yatakwa kwa ajili ya mabatizo yanayokubaliwa leo Kimaandiko: (1) ujuzi sahihi, (2) kutubu kwa unyoofu, na (3) kuongoka, au kugeuka kuelekea Mungu na kutoka kwa “kizazi hiki chenye ukaidi.” Zaidi ya hayo, mabatizo yanayokubaliwa Kimaandiko lazima yawe “katika jina la Yesu Kristo,” yaani, yakitegemea kukubali dhabihu ya fidia kwa ajili ya msamaha wa dhambi na kujitiisha kwake akiwa mfalme mwekwa wa Mungu.—Matendo 2:40; Warumi 5:12-19; 7:14-25.

Watu wanyoofu ambao wamestahili Kimaandiko kwa ajili ya ubatizo hawahitaji kuhofu kwamba kwa kubatizwa mara ya pili hawatampendeza Mungu. Kinyume cha hilo, ubatizo unaofaa Kimaandiko wa watu waliostahili humletea Mungu shangwe.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa habari zaidi, ona makala “Ubatizo—Je! Ni wa Vitoto Vichanga?” katika toleo la Amkeni! la Septemba 8, 1987.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki