Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 2/22 kur. 7-9
  • Kujua Kusoma na Kuandika Miongoni mwa Watu wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujua Kusoma na Kuandika Miongoni mwa Watu wa Mungu
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Watu wa Mungu Leo
  • Kujifunza Kusoma
  • Je, Nimpeleke Mtoto Wangu Shuleni?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kunufaika kwa Usomaji wa Biblia Kila Siku
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Jitahidi Uwe Msomaji Mzuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Elimu ya Biblia Husaidia Watu Kujua Kusoma na Kuandika
    Amkeni!—2015
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 2/22 kur. 7-9

Kujua Kusoma na Kuandika Miongoni mwa Watu wa Mungu

KATIKA nyakati za kale watu wa Mungu walijua sana kusoma na kuandika. Karibu miaka 3,500 iliyopita, Musa aliandika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. Mwandamizi wake, Yoshua, aliamriwa asome Maandiko “mchana na usiku” ili afanikiwe katika mgawo ambao Mungu alikuwa amempa. Na Mungu alikuwa ameagiza kwamba wafalme wa Israeli, wanapokuwa wafalme, wajiandikie nakala ya Torati na kuisoma kila siku.—Yoshua 1:8; Kumbukumbu la Torati 17:18, 19.

Si viongozi wa taifa hilo pekee waliojua kusoma na kuandika. Ingawa kwa wazi agizo la Mungu kwa Waisraeli la ‘kuandika’ amri za Mungu juu ya miimo ya nyumba yao lilikuwa mfano tu, amri hiyo ilionyesha kwamba watu walijua kusoma na kuandika. Amosi alikuwa mfugaji wa kondoo, na Mika alikuwa nabii kutoka kijiji cha mashambani; lakini wote wawili waliandika vitabu vya Biblia.—Kumbukumbu la Torati 6:8, 9; Amosi 1:1; Mika 1:1.[1]

Yesu angeweza kupata hati-kunjo zote zenye pumzi ya Mungu za Maandiko ya Kiebrania katika masinagogi, ambapo katika pindi moja, alisoma peupe na kutumia andiko alilosoma kwake mwenyewe. Mitume wake pia walijua kusoma na kuandika, wakinukuu na kurejezea kutoka Maandiko ya Kiebrania mara mia kadhaa katika maandishi yao.—Luka 4:16-21; Matendo 17:11.

Watu wa Mungu Leo

Yesu aliambia wafuasi wake ‘wafanye mataifa yote kuwa wanafunzi na kuwafundisha kuyashika yote aliyokuwa ameamuru.’ Pia alitabiri kwamba ‘habari njema ya ufalme ingehubiriwa katika ulimwengu wote.’—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

Kama ilivyo na Wakristo katika karne ya kwanza, leo Mashahidi wa Yehova wametekeleza agizo hilo kwa kufundisha na kuhubiri kwa bidii kupitia maneno ya midomo. Wao pia wameeneza habari njema ya Ufalme kupitia vichapo. Tangu 1920, Mashahidi wa Yehova wametokeza na kugawanya Biblia, vitabu, magazeti, na vijitabu zaidi ya bilioni tisa katika lugha zaidi ya 200.[2]

Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wameitikia ifaavyo, na kuwa wafuasi wa Kristo. Miongoni mwao mna wanaume na wanawake ambao hawajui kusoma wala kuandika. Si kwamba watu hao wasiojua kusoma na kuandika ni Wakristo wa hali ya chini zaidi—wengi wamemtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miongo mingi, wamevumilia mnyanyaso wa kidini, na wameonyesha upendo wao kwa Yehova kwa kutii amri zake.—1 Yohana 5:3.

Wengi wao wanatamani kujua kusoma na kuandika, waking’amua kwamba kujua kusoma na kuandika ndio ufunguo utakaofungua njia ya kushiriki zaidi katika ibada yao kwa Mungu. Wanataka kufuata usomaji wa Biblia na wa vichapo vya Kikristo kwenye mikutano, na wanataka kusoma maneno ya nyimbo ili waweze kuimba pamoja na ndugu na dada zao wa kiroho. Wakiwa nyumbani, wanatamani kujijenga na kujenga familia zao kupitia funzo la Biblia. Katika huduma, wanatamani kufundisha wengine kweli ya Neno la Mungu bila kutegemea mtu mwingine kuwasomea neno hilo.

Kujifunza Kusoma

Wakiitikia uhitaji huo, Mashahidi wa Yehova wamepanga kuendeleza kujua kusoma na kuandika kupitia makutaniko yao na kwa mtu mmoja-mmoja. Wamefundisha wanaume na wanawake wengi sana ulimwenguni pote. Nchini Naijeria pekee, Mashahidi wa Yehova wamefundisha watu zaidi ya 23,000 kujua kusoma na kuandika.[3] Mmoja wa watu hao alikuwa Effor. Yeye asimulia hivi:

“Nilianza kusoma na kuandika katika 1950 nilipokuwa na umri wa miaka 16. Masomo ya kujifunza kusoma na kuandika yalikuwa yakiendeshwa na Mashahidi wa Yehova. Tulitumia kitabu cha mafundisho kilichotangazwa na Watch Tower Society, na tulikuwa tukipewa migawo ya kusomea nyumbani.

“Nilihisi kwamba kutojua kwangu kusoma na kuandika kulikuwa ni kama ugonjwa. Nilitaka kufafanua Biblia kwa ndugu zangu na marafiki wangu, lakini kwa vile sikujua kusoma na kuandika, sikufanikiwa sana. Jambo lililonichochea nijifunze lilikuwa ni tamaa yangu ya kuhubiri na kuwafundisha wengine wawe wafuasi wa Kristo. Niliandika juu ya kila kitu ambacho ningepata, hata juu ya matawi ya mgomba. Nilikuwa na tamaa kubwa sana ya kutaka kujua kusoma na kuandika hivi kwamba nilikuwa nikiota kwamba ninafanya mazoezi ya kusoma na kuandika. Niliomba msaada wa wengine; kwani sikuwa na haya juu ya jambo hilo. Nakumbuka nilikuwa nikiandikia marafiki zangu barua na kuwapatia wale waliokuwa wakienda shuleni wazisahihishe.

“Nilichukua muda wa mwaka mmoja kujifunza katika darasa la kutaniko la kujifunza kusoma na kuandika. Baada ya hapo nilipewa mgawo wa kufundisha darasa la masomo. Hilo lilinipa fursa ya kusaidia watu wengine wengi.

“Shule hiyo ilinisaidia sana katika miaka ya baadaye hivi kwamba nilipata pendeleo la kutafsiri drama za Sosaiti kutoka Kiingereza hadi Kiisoko, ambayo ni lugha yangu. Mbali na hayo, nimetumikia nikiwa mwangalizi wa kutaniko tangu miaka ya 1960. Katika miaka ya 1980, nilitumikia nikiwa mwangalizi wa badala asafiriye wa Mashahidi wa Yehova. Pia nilikuwa na pendeleo la kuongoza Shule ya Utumishi wa Painia [shule ya wahudumu wa wakati wote] na mara mbili kuwa mfunzi katika Shule ya Huduma ya Ufalme [shule ya wazee wa Kikristo]. Najua kwamba kama ningalikuwa bado sijui kusoma na kuandika, nisingepata mapendeleo hayo yote.

“Ninathamini kama nini mpango huu wa kufundisha watu wanyenyekevu kujua kusoma na kuandika! Nyakati nyingine ninapojilaza usiku, mimi bado humshukuru Yehova kwamba mimi si mtu asiyejua kusoma na kuandika katika ulimwengu huu wa kisasa.”[4]

Muumba wetu, Yehova Mungu, amewapa jamii ya kibinadamu uwezo wa kusoma na kuandika. Lakini stadi hizo hazipatikani tu bila jitihada. Thawabu kuu zaidi ya kujifunza kusoma na kuandika ni kuweza kutwaa Neno la Mungu na kutii agizo hili la kimungu: ‘Ulisome kwa ukimya-kimya mchana na usiku.’—Yoshua 1:8, New World Translation.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Jinsi ya Kusaidia Watoto Wako Wasitawishe Upendezi wa Kusoma

● Weka kielelezo kwa kusoma kwa ukawaida wewe mwenyewe. Wazazi wanaosoma wanaelekea kuwa na watoto wanaosoma.[5]

● Sema na mtoto wako kutokea utoto wake. Kuzungumziwa lugha ifaayo huwawezesha watoto waelewe maneno na mawazo yatakayofanya kujifunza kusoma kuwe rahisi.[6]

● Somea watoto wako kwa ukawaida. Wanapobebwa pajani na kusomewa, watoto hutambua kwamba maneno na vitabu ni vizuri, hata kama hawajafikia umri wa kuelewa hadithi inayosomwa. Endelea kusomea watoto wako baada ya wao kujua kusoma wenyewe. Walimu wa shule husaidia watoto kujua jinsi ya kusoma, lakini wazazi wanaweza kufanya mengi zaidi katika kuwasaidia kufurahia kusoma. Watoto hufurahia kusikiliza mara kwa mara hadithi wazipendazo.[7]

● Uwape watoto vitabu vya kusoma nyumbani.[8]

● Tia moyo watoto wako waandike. Mara nyingi mtoto aandikaye huwa msomaji vilevile.[9]

● Weka vipindi hususa kila siku vya usomaji wa familia. Someni kwa zamu, na kisha mjadiliane habari hiyo pamoja. Nyakati hizo zapasa kuwa zenye furaha na zenye kujenga.[10]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Watu wenye kumhofu Mungu wa nyakati za kale walijua kusoma na kuandika

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki