Maisha Ambayo Singependa Kubadili
WATU wengi husikitikia jinsi ambavyo wameishi maisha zao. Huenda wakasema: ‘Kama tu ningalianza maisha tena, ningalifanya mambo mengi sana kwa njia tofuati!’ Lakini ninapofikiria maisha yangu, ingawa hayajakuwa maisha rahisi, yamekuwa maisha ambayo nisingependa kubadili.
Nililelewa na wazazi wangu nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na sheria za Mungu zilikuwa zimekazwa kikiki moyoni mwangu tangu utoto. (2 Timotheo 3:15) Siwezi kukumbuka pindi ambazo sikuenda kwenye mikutano na mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Na nikiwa msichana mchanga, mimi pia niliandamana na Mashahidi wenye umri mkubwa katika kutembelea watu na kuwasaidia kujifunza juu ya tumaini la Biblia la uhai wa milele katika dunia paradiso chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Ningali naweza kukumbuka nikiwa na umri wa miaka mitano nikitolea wengine kile kijitabu The Kingdom, the Hope of the World (Ufalme, Tumaini la Ulimwengu).
Wazazi wangu walisikia kweli kuhusu Ufalme wa Mungu kwa mara ya kwanza mwaka wa 1917. Ingawa walikuwa wahudhuriaji kanisa, walitambua kweli iliyokuwa katika hotuba iliyotolewa mjini Bridgeton, New Jersey, U.S.A., na mwakilishi asafiriye wa Watchtower Society. Babu yangu alisikiliza hotuba iyo hiyo, naye pia alisadiki kwamba yale aliyosikia yalikuwa kweli. Kisha, nilipokuwa mwenye miaka 14, nilibatizwa katika mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova mjini Detroit, Michigan, ili kuonyesha kwamba nilikuwa nimeweka maisha yangu wakfu kwa Yehova.
Katika miaka hiyo mikutano yetu ya kila juma kwa ajili ya funzo la Biblia ilifanywa katika sebule yetu. Hatimaye duka fulani lilinunuliwa na kugeuzwa kuwa Jumba la Ufalme. Nyakati hizo kulikuwa na Majumba ya Ufalme machache. Lakini leo, makumi ya maelfu ya majumba kama hayo yanatumikia makutaniko zaidi ya 70,000 ya Mashahidi wa Yehova.
Kuanza Utumishi wa Wakati Wote
Mama yangu alianza kazi yake ya maisha akiwa mtumishi wa wakati wote mwaka wa 1939 na aliendelea hivyo mpaka kifo chake akiwa na miaka 85. Ndugu yangu, Dick, nami tulianza kazi zetu za maisha za utumishi wa wakati wote mnamo Aprili 1, 1941, wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilipokuwa ikiendelea katika Ulaya na uhasama dhidi ya Mashahidi wa Yehova ulipokuwa umeenea kwa sababu ya msimamo wetu wa kutokuwamo kisiasa.
Watatu kati ya Mashahidi vijana katika kutaniko letu walihukumiwa miaka mitano gerezani kwa sababu ya kutokuwamo kwao. Inatia moyo kama nini kuona wawili kati yao wangali wakitumikia wakiwa wazee katika kutaniko! Baadaye ndugu yangu alitumikia katika Betheli ya Brooklyn, ambayo ni makao makuu ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni, katika New York, na angali anatumikia akiwa mzee katika mji wa kwetu wa Millville, New Jersey.
Kama ilivyo na kwingineko, miaka hiyo ya vita ilikuwa migumu sana katika United States kwa Mashahidi wa Yehova. Vitendo vya umati wenye ghasia vilikuwa kawaida. Watoto walifukuzwa shuleni. (Ona Amkeni! la Julai 22, 1993, juu ya maisha ya Lillian Gobitas Klose.) Maelfu ya ndugu zetu wa kiroho walifungwa jela, kwa hiyo ikawa lazima sisi wanawake tufanye kazi mbalimbali za kutaniko. Hiyo ndiyo sababu, nikiwa ningali mchanga, nilikuwa mtumishi wa vitabu. Kwa msaada wa Yehova tuliokoka miaka hiyo migumu ya vita, na ndugu zetu waliporudi kutoka gerezani, kazi ilisonga mbele.
Ulikuwa wakati huo ambapo Lyman Swingle kutoka Betheli alizuru kutaniko letu. Alinitia moyo niende Brooklyn na kusaidia katika kazi ya kutoa msaada kwa Mashahidi wenzetu katika Ulaya baada ya Vita ya Ulimwengu 2. Basi nikaenda Brooklyn mnamo Machi 1948.
Miaka Yenye Furaha Katika Kutaniko Jipya
Nilipewa mgawo wa kwenda kutaniko jipya, lile la Brooklyn Center. Hilo lilikuwa kutaniko la kwanza kabisa lililofanyizwa katika Jiji la New York na viunga vyalo kabla ya Vita ya Ulimwengu 1, ingawa wakati huo likiitwa kwa jina tofauti. Wakati huo lilikuwa katika eneo la Brooklyn Heights. Lakini nilipokuja Brooklyn Center mnamo 1948, kutaniko hilo lilikuwa katika makutano ya barabara za 5th Avenue na 8th Street katika Brooklyn. Kwa karibu miaka 30, mahali hapo palipokodishwa palikuwa mahali pa mkutano, mpaka jumba jipya liliponunuliwa mwendo mfupi kutoka hapo.
Sitasahau kamwe siku yangu ya kwanza katika utumishi wa shambani katika Brooklyn—kwenye barabara ya Henry Street. Ilikuwa tofauti sana na kuhubiri katika mji mdogo. Lakini upesi nilikutana na mwanamke mchanga aliyekubali fasihi ya Biblia na kukubali funzo la Biblia nyumbani. Baada ya muda fulani akawa mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu, watoto wake wawili vilevile wakifanya hivyo. Kwa wakati huu, mwana wake Arthur Iannone, anatumika katika Betheli ya Brooklyn akiwa pamoja na mke wake, Linda, pamoja na mwana na binti-mkwe wao.
Eneo la kutaniko tulilohubiri lilikuwa kubwa na lenye mazao. Kwa msaada wa Yehova, niliweza kuona wengi wa wanafunzi wangu wa Biblia wakijifunza kweli na kubatizwa. Kufikia leo hii baadhi yao wanatumika katika utumishi wa wakati wote katika nchi hii ya United States. Wengine ni wamishonari katika nchi za mbali. Wengine walikuja kuwa wazee katika makutaniko. Na wengi wametumika katika hali nyinginezo wakiwa watangazaji waaminifu wa habari njema za Ufalme wa Mungu.
Ukuzi ulistaajabisha sana. Eneo ambalo hapo awali lilikuwa na kutaniko moja tu lililotumikia Jiji la New York na viunga vyalo, sasa lina makutaniko yapatayo 400 katika Jiji la New York. Hizo ni kumbukumbu nzuri kama nini za kushiriki katika baadhi ya upanuzi huo!
Upendezi wa Wasemaji wa Kifaransa Wasitawi
Katika miaka ya 1960, tulianza kupata watu wengi wanaosema Kifaransa katika eneo la kutaniko letu ambao walikuwa wametoka Haiti. Wengi wao walisema Kiingereza kidogo sana ama hawakukijua kabisa. Hapo palikuwa na tatizo. Tungeweza kuwasaidiaje wajifunze zaidi juu ya Biblia? Mimi sikuelewa Kifaransa, lakini nikiwa na nakala ya Kiingereza ya kitabu chetu cha msingi cha kufundisha Biblia wakati huo, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, kwa mkono mmoja na kitabu Kweli cha Kifaransa kwenye mkono mwingine, niliweza kuongoza mafunzo ya Biblia.
Hata hivyo, hakukuwa na mikutano katika Kifaransa ili kusaidia watu hao wakue kiroho. Hiyo ndiyo sababu Shahidi yeyote mishonari aliyezuru Brooklyn na ambaye alijua Kifaransa alikuwa akiombwa msaada mara hiyo. Mmoja wa hao waliokuwa wa kwanza kuja kutusaidia aliitwa Nicolas Brisart, ambaye ni mratibu wa Halmashauri ya Tawi katika Guadeloupe. Alitutolea hotuba ya kwanza ya watu wote katika Kifaransa katika nyumba ya Dada Bertha Luisdon, ambaye angali anamtumikia Yehova kwa uaminifu. Watu 27 walihudhuria.
Na kufikia wakati huo bado hakukuwa na makutaniko yoyote ya lugha za kigeni katika Jiji la New York ila tu ya Kihispania. Kwa hiyo ilikuwa vigumu hata kuwazia kuanzishwa kwa kutaniko lenye kusema Kifaransa. Mwangalizi mmoja asafiriye hata alifanya matazamio yetu yadidimie zaidi alipotuambia kwamba mwongozo wa wakati huo ulikuwa ni kutia moyo watu waliokuwa wakiishi katika nchi hiyo wajifunze Kiingereza.
Ndugu Fred W. Franz, ambaye baadaye alikuja kuwa msimamizi wa Watch Tower Society, alikuwa mwenye kitia-moyo sana. Yeye alisema hivi: “Mary, ikiwa ni mapenzi ya Yehova, kutakuwa na Kutaniko la Kifaransa.” Ndugu Harry Peloyan, ambaye alikuwa mwangalizi-msimamizi wa Kutaniko la Brooklyn Center, vilevile alikuwa mwenye kitia-moyo. Alisema kwamba katika jioni ambazo Jumba la Ufalme halitumiwi, tungeweza kupanga kuwe na Funzo la Kitabu la Kutaniko na hotuba za watu wote zisizo rasmi wakati wowote mgeni alipokuja aliyesema Kifaransa.
Kufikia wakati huu tulikuwa na idadi kadhaa ya ndugu waliobatizwa kutoka Haiti waliokuwa wamehamia huku, lakini bado hakukuwa na mtu mwenye ujuzi wa kutosha wa kuchukua uongozi wa kitengenezo katika lugha ya Kifaransa. Kisha, Ndugu Timothy Galfas, aliyesomea Paris na ambaye wakati huo alikuwa mshiriki wa familia ya Betheli ya Brooklyn akaja kujua juu ya hali yetu. Kila Jumamosi baada ya kazi ya Betheli, angekuja, nasi tungetafuta ndugu na dada kutoka Haiti waliokuwa wakiishi huku na ambao hawakujua mahali pa kushirikiana na akina ndugu.
Upesi tukawa na karibu watu 40 wakishirikiana nasi. Tulimwomba mwangalizi wetu wa mzunguko aandikie Sosaiti ili ituruhusu kuanzisha rasmi Funzo la Kitabu la Kutaniko katika Kifaransa. Tulifurahi kama nini tuliporuhusiwa! Baadaye tuliruhusiwa pia kuwa na hotuba za watu wote kwa ukawaida na Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma.
Kutaniko la Kwanza la Kifaransa
Mnamo Desemba 1, 1967, tulipokea kibali cha kuanzisha kutaniko la kusema Kifaransa, la kwanza katika United States. Lingetumia Jumba la Ufalme pamoja na makutaniko ya Brooklyn Center na Prospect. Tulichachawa sana! Tulijua kwamba watu wote wangefanya maendeleo ya kiroho katika lugha waliyoelewa. Tulithamini sana utegemezo tuliopokea katika nyakati hizo ngumu kutoka kwa ndugu kama Harry Peloyan, George Haddad, na Carlos Quiles waliokuwa katika halmashauri ya utumishi ya kutaniko la Brooklyn Center.
Tuliongezeka haraka. Upesi makutaniko ya Kifaransa yalifanyizwa katika Manhattan, Queens, na Nyack, katika New York. Jeff Keltz na Tom Cecil wa Betheli ya Brooklyn walisaidia katika upanuzi huo. Ndugu Keltz alikuwa mwangalizi wetu wa mzunguko, na Ndugu Cecil ametumika katika Halmashauri ya Mikusanyiko ya Wilaya. Wengine walisaidia, kama vile wamishonari kutoka nchi zilizokuwa zikisema Kifaransa na ambao walilazimika kurudi United States kwa sababu za kiafya. Msaada wao ulikuwa wenye thamani kama nini! Miongoni mwao ni Stanley Boggus, anayetumika akiwa mwangalizi-msimamizi na pia mwangalizi wa mzunguko wa badala.
Imekuwa ni pindi yenye kufurahisha kama nini kuona kikundi kile kidogo cha Kifaransa katika makutano ya barabara za 5th Avenue na 8th Street kikikua mpaka makumi ya makutaniko na mizunguko miwili! Kwa kweli, tulikuwa na kusanyiko letu la kwanza la mzunguko katika Kifaransa mnamo Aprili 1970. Ndugu Nathan H. Knorr, msimamizi wa wakati huo wa Watch Tower Society, alituhutubia usiku wa Ijumaa na kututakia mema. Tukawa pia na mkusanyiko wetu wa kwanza wa wilaya katika kiangazi cha wakati huo, katika sehemu fulani iliyotayarishwa tu kijuu-juu chini ya mbao katika Stediamu ya Roosevelt katika Jiji la Jersey, New Jersey. Kulikuwa na joto jingi na vumbi nyingi, lakini wale wahudhuriaji zaidi ya 200 walikuwa na furaha sana kuweza kusikia programu yote, kutia ndani na drama, katika Kifaransa.
Tulichachawa pia tuliporuhusiwa, katika 1986, kutumia Jumba la Makusanyiko la Jiji la Jersey la Mashahidi wa Yehova kwa ajili ya mkusanyiko wetu wa wilaya. Katika mkusanyiko mmoja wa Kifaransa uliofanywa huko mwaka uliopita, watu 4,506 walihudhuria, na 101 walibatizwa. Na wakati uo huo, mkusanyiko mwingine wa Kifaransa ulifanywa katika Florida.
Wenzi wa Chumba Waaminifu
Sehemu nyingine ya maisha yangu ambayo imekuwa yenye kufurahisha sana ni kushiriki chumba kimoja katika Brooklyn pamoja na dada wengine waliokuwa katika utumishi wa wakati wote. Dada wawili wa kwanza (Rose Lewis Peloyan na Madelyn Murdock Wildman) walienda Betheli. Baadaye dada wengine wawili (Lila Rogers Molohan na Margaret Stelmah) pia wakaja kuwa washiriki wa familia ya Betheli. Wengine wawili (Barbara Repasky Forbes na Virginia Burris Beltramelli) walihudhuria Watchtower Bible School of Gilead na wangali wanatumika katika Guatemala na Uruguay.
Nyakati zote sisi akina dada tulichukua wakati wa kuzungumza juu ya Andiko ili kuanza siku, kisha tulienda kwenye kazi zetu za kimwili na katika huduma. Tulikuwa tukirudi usiku tukiwa tumechoka na wenye njaa lakini wenye furaha! Tulikuwa tukisimuliana maono mengi yenye kujenga! Kwa kielelezo, katika pindi moja nilijifunza na mwanamke mmoja mchanga, Elisa Beumont Farina, aliyesisitiza kwamba nijifunze naye saa 4:00 za usiku. Alifanya maendeleo haraka. Mara ya kwanza nilipompeleka katika huduma, yeye alisema hivi: “Usifikirie kwamba nitafanya kazi hii nyakati zote!” Lakini alikuja kuwa mhudumu wa wakati wote na baadaye akahudhuria shule ya Gileadi, akitumika miaka mingi nchini Ekuado. Angali anatumika wakati wote katika Trenton, New Jersey.
Baadhi ya wale niliokaa nao katika chumba kimoja wamelea watoto ambao nao wamthamini na kumtumikia Yehova. Mwaka uliopita (Jodi Robertson Sakima) binti ya mmoja tuliyeshiriki naye chumba kimoja (Virginia Hendee Robertson) aliolewa na sasa yeye na mume wake wanatumika katika Betheli ya Brooklyn.
Kati ya wale wote ambao nilishiriki nao chumba kimoja, ambao ni zaidi ya 20, ninafurahi kusema kwamba wote walibaki waaminifu kwa Yehova, na wengi wao wangali katika utumishi wa wakati wote.
Kufurahia Familia Yetu ya Ulimwenguni Pote
Pia imekuwa shangwe kwangu kujuana na Mashahidi wengi kutoka nchi nyinginezo. Mathalani, kwa kuwa tuliishi karibu na makao makuu ya Sosaiti, tulikuwa na pendeleo la kushirikiana na wanafunzi wanaohudhuria shule ya mishonari ya Gileadi, wakati huo ikiwa Betheli ya Brooklyn.
Wanafunzi wawili, Guenter Buschbeck, ambaye wakati huu anatumika katika ofisi ya tawi nchini Austria, na Willi Konstanty, anayetumika katika ofisi ya tawi ya Ujerumani, walipewa mgawo wa kuhudhuria Kutaniko la Brooklyn Center walipokuwa kwenye shule ya Gileadi. Hao walikuwa kitia-moyo kama nini kwetu! Walikuwa na uvutano mzuri sana kwa wale tulioshiriki nao chumba hivi kwamba wao nao wakaanza kufikiria utumishi wa Gileadi.
Nyakati nyingine nimekuwa na pendeleo la kupanua urafiki wangu na familia yetu ya ulimwenguni pote kwa kusafiri nchi za nje. Nimepata kuhudhuria mikusanyiko ya kimataifa na tena nimewaona wahitimu wengi wa Gileadi niliokuwa nimejua zamani wakiwa kwenye migawo yao.
Maisha Yaliyojaa
Nikifikiria maisha yangu, naweza kusema kwamba yamekuwa mazuri ajabu—maisha yenye furaha yenye kujawa baraka. Ingawa nimepata matatizo mengi ya kawaida ambayo huja na mfumo huu wa mambo, hakuna chochote ambacho kimepata kunifanya nisikitike juu ya maisha yangu au kuacha pendeleo langu lenye thamani kubwa la utumishi wa wakati wote.
Nikiwa mchanga, mama yangu alinikazia maneno ya Zaburi 126:5, 6: “Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha. Ingawa mtu anakwenda zake akilia, azichukuapo mbegu za kupanda. Hakika atarudi kwa kelele za furaha, aichukuapo miganda yake.” Andiko hilo lingali kiongozi changu. Hata nilipopata matatizo ya aina gani, Yehova alinisaidia kupata njia ya kuyashinda na kudumisha shangwe hiyo.
Kwa kweli maisha yangu ni yale ambayo singependa kubadili. Sina masikitisho kwa kutoa miaka ipatayo 53 kwa Yehova katika huduma ya wakati wote. Natazamia kuendelea kumtumikia kwa umilele wote katika ulimwengu wake mpya.—Kama ilivyosimuliwa na Mary Kendall.
[Picha katika ukurasa wa 16]
Mary Kendall