Kuzorota kwa Adabu
Mamilioni bado wana adabu nzuri. Mamilioni wengine huzipuuza.
MWANZONI mwa karne hii, uungwana ulipata mwanzo mbaya, kulingana na The New Encyclopædia Britannica: “Mwishoni mwa karne ya 19 na mwanzoni mwa ile ya 20 watu wa ngazi za juu katika jamii waliona kule kuwa waungwana katika mambo ya kawaida kuwa jambo lisilo la maana ingawa lenye umaana kwa wanawake. Desturi nyingi zaidi na zaidi zenye madoido zilikusudiwa kuwafanya washiriki wapya wa ngazi za juu wajione kuwa tofauti na kufanya wale wa ngazi za chini wasizifahamu, wakiwa kando kabisa.”[1]
Hiyo ni tofauti kabisa na jinsi adabu nzuri zipasavyo kuwa. Amy Vanderbilt aonwa kuwa mstadi katika mambo ya adabu, naye aandika hivi katika kitabu chake New Complete Book of Etiquette: “Kanuni zilizo bora zaidi za adabu zapatikana katika Sura ya 13 ya Wakorintho wa Kwanza, ule ufafanuzi mzuri wa Mt. Paulo juu ya upendo. Kanuni hizo hazihusiani hata kidogo na mambo madogomadogo ya mitindo wala yale ya tabia duni. Hizo zahusu hisia na mitazamo, kuwa mfadhili, na kuwafikiria wengine.”[2]
Maneno aliyorejezea Amy Vanderbilt ni yale ya Biblia kwenye 1 Wakorintho 13:4-8, (New World Translation) linalosema: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti masilahi yao wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na ile kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi wakati wowote.”
Ingekuwa nadra kama nini kuona upendo wa aina hiyo ukionyeshwa leo! Kila mahali, adabu zisingekuwa na dosari! Nyumba ya Kikristo ndipo mahali pa kuanzia kufundisha na kujifunza adabu hizo. Familia ni kama mashine inayotaka uangalifu ambayo sehemu zayo zakaribiana karibukaribu. Ni kwa kuilainisha kwa ustadi tu ndipo inapoweza kufanya kazi vizuri. Kujua jinsi ya kusaidia, kuwa muungwana, kupendeza, na kuwa mpole ni mambo ya maana katika kufanya nyumba iwe na furaha. Kujifunza jinsi ya kusema maneno ya kawaida yanayokubaliwa ya uungwana na kufikiria wengine—kama vile “Asante,” “Tafadhali,” “Nisamehe,” “Kunradhi”—kutasaidia sana kumaliza kutosikizana katika ushirika wetu mbalimbali. Hayo ni maneno madogo yenye maana kubwa. Kila mtu aweza kuyasema vizuri. Hayatugharimu chochote, lakini kwayo twapata marafiki. Tukiwa na adabu nzuri kila siku nyumbani mwetu, hatutazisahau tunapoacha washiriki wa familia na kutangamana na umma.
Adabu nzuri huhusisha kuonyesha ufikirio kwa hisia za wengine, kuwaonyesha staha, kuwatendea vile ambavyo tungependa watutendee. Hata hivyo, wengi wameona kwamba adabu zimezorota. Mwandikaji mmoja alisema: “Twakosa uungwana kwa sababu u-mimi umepata maana zaidi.”[3] Mwanafalsafa Arthur Schopenhauer aliandika hivi: “Ubinafsi ni jambo baya sana hivi kwamba tulibuni upole ili kuuficha.”[4] Leo wengi huamini kwamba “upole” humaanisha “udhaifu” na kwamba kutanguliza wengine ni unyonge. Je! si ni ule mwongo wa miaka ya 1970 wa U-Mimi ulioanzisha mtindo wa maisha wa sasa wa mimi-kwanza? Gazeti moja la habari la jiji kubwa lilisema hivi: “Tatizo limekua kufikia mahali ambapo uungwana wa kawaida hauwezi kusemwa kuwa wa kawaida kwa watu.”[5]
Gazeti Daily Mail la London laripoti kwamba watoto wa umri mdogo kama miaka mitano wanazidi kuwa wafanya-vita, bila staha kwa mali ya watoto wengine, wakikosa kuwastahi watu wazima, na wakitumia usemi mchafu. Walimu wengi waliochunguzwa wahisi kwamba wazazi wanawaharibu watoto wao na kwamba hiyo ndiyo sababu kuu ya ongezeko la utovu wa tabia. Kati ya walimu waliohojiwa katika uchunguzi mmoja, asilimia 86 walaumu “ukosefu wa kanuni na matarajio ya waziwazi nyumbani.” Asilimia 82 walilaumu ukosefu wa kielelezo chema cha wazazi. Familia zilizovunjika, talaka, uhusiano wa njoo-tukae, kutazama televisheni kupita kiasi, ukosefu wa nidhamu, ukosefu wa sheria imara—tokeo ni kuharibika kwa familia.[6]
Mkuu mmoja wa shule ya msingi alisema hivi: “Nasikitishwa na ukosefu wa staha miongoni mwa watoto leo. Ni kana kwamba hawajali wakiaibisha marika zao au wakikosea watu wazima. . . . Wao huonyesha ukosefu wao wa staha katika njia nyingi—ishara zenye kuudhi, machukizo, kukataa kutii sheria rahisi . . . , nia ya kudhibiti mpira kila wakati michezoni . . . [Kwa upande mwingine,] watoto kutoka nyumba fulani huwastahi wengine. Si kwamba wao ni vipenzi kwa walimu . . . , lakini wao huwastahi wengine. Wao hungojea zamu yao wengine wanapojiingiza mbele kwenye mstari . . . Ni dhahiri kama [watoto hao] wamejifunza staha au la.”[7]
Mkuu mwingine wa shule ya msingi, aliye na ujuzi wa miaka mingi, atoa habari zaidi: “Kuna uchoyo mwingi sana. Kwenye uwanja ni kama watoto hawachezi vile walivyocheza zamani; wao huzurura katika magenge. Ni wenye haraka kutambua wale walio dhaifu, watoto wasiomo katika kikundi chao, watoto wasiovaa viatu vizito vya mpira vinavyofaa au suruali-jini. Wao huwaonea watoto hao, kuwachokoza; na kuna ukatili fulani ulioko. Tumejaribu kuukomesha, lakini hatujafanikiwa sana.”[8]
“Watu wengi wanaendesha magari kwa ufidhuli sana,” asema Profesa Jonathan Freedman wa Chuo Kikuu cha Columbia. “Ni karibu kuwa kama uwanja wa vita kwenye barabara kuu.” Gazeti Monthly Letter la Benki ya Royal ya Kanada lasema juu ya “vifo vya barabarani vinavyoongezeka” na kumalizia kwamba “kiini cha tatizo ni kukosa hisani. Uungwana, kufikiria wengine, saburi, uvumilivu na staha kwa haki za kibinadamu zinazofanyiza ustaarabu zakosekana sana.”[9]
Gazeti The New York Times lilieleza hivi juu ya barabara za Jiji la New York: “Ni Waendesha-Magari Dhidi ya Ambulensi.” Waendesha-magari zaidi katika jiji hilo wanakataa kuyapa njia magari ya hali ya dharura, kama vile ambulensi na magari ya wazima-moto—hilo likiongeza hatari kwamba mtu fulani aliye mgonjwa mahututi au aliyeumia atakufa kwa sababu hawezi kufikiwa au kusafirishwa hadi kwenye hospitali upesi iwezekanavyo. Kapteni Ellen Scibelli wa Huduma za Dharura za Kitiba alimwambia mtu aliyekuwa akiendesha gari katika barabara ya Pelham Parkway katika Bronx aliyekataa kupisha ambulensi iliyokuwa ikienda kuchukua mgonjwa aliyeugua moyo. “Yeye alijaribu kuwa mkaidi sana na hakukubali kuondoka njiani, lakini alipowasili nyumbani mwake, aling’amua jinsi alivyofanya upumbavu. Mama yake alikuwa na ugonjwa wa moyo na ile ambulensi ilikuwa ikijaribu kumfikia.”[10]
Gazeti The New York Times International lilisema juu ya shirika la Uingereza liitwalo Jamii Yenye Upole lililofanyizwa kwa sababu “watu wamekuwa wafidhuli kabisakabisa wao kwa wao, na lazima jambo fulani lifanywe.” Katika safu moja katika The Evening Standard, mwanajarida wa utangazaji alilazimika kulalamika hivi: “Taifa ambalo hapo awali lilikuwa mashuhuri kwa sababu ya hisani zalo linakuwa nchi ya wafidhuli.” Kampuni moja ya bima ya Scotland “ilitoa mkataa kwamba asilimia 47 ya aksidenti zote za barabarani husababishwa na tendo la kukosa uungwana.”[11]
Televisheni ni kisababishi kikuu cha ukosefu wa adabu, hasa kuhusu watoto na matineja. Namna watu wanavyovalia, namna wanavyosema, namna watu wanavyoshughulika na mahusiano ya kibinadamu, namna watu wanavyotatua matatizo kijeuri tena na tena—televisheni ni mwalimu. Ikiwa sisi na watoto wetu twatazama kwa ukawaida programu za riwaya zisizo na maana, mwishowe adabu zetu zitakuwa na mitazamo ya kukosa kiasi, isiyo na staha, na ya ucheshi. Mara nyingi wazazi huonwa kuwa wapumbavu na watoto kuwa werevu.
Ulimwengu hupenda kusema kwa sauti kubwa, yenye kuamuru—ukikatiza maneno, wenye kiburi cha kutaka kutawala, wenye kujivuna, wenye kujitutumua, wenye uchokozi, wenye kutoa mwito wa ushindani. Zamani ilikuwa kwamba adabu mbaya ingechukiza jamii kwa ujumla, na mtovu wa adabu angetengwa. Katika jamii ya kisasa, tendo la ufidhuli laweza kufanywa bila mkosaji kuonwa vibaya. Na ikiwa mtu ajaribu kuteta, yeye aweza kutukanwa au kupigwa! Vijana fulani wanaosafiri katika vikundi vyenye makelele huwa na usemi mchafu, ishara zenye kinyaa, wakiudhi watazamaji kwa mwenendo wao mpotovu, uliokusudiwa kuvuta uangalifu kwenye uasi wao wa kivita na kushtua watu wazima kwa wonyesho wao wa ufidhuli wenye makelele. Hata hivyo, imesemwa kwamba, “ufidhuli ni mwigo wa nguvu wa mtu dhaifu.”[12]
Sheria ambazo watu wamefanyiza ili kuongoza mwenendo wa wanadamu ni nyingi sana, lakini hazijatokeza mwongozo wa mahitaji ya wanadamu. Je! twahitaji sheria zaidi? Au labda chache zaidi? Imesemwa kwamba kadiri jamii ilivyo bora zaidi, ndivyo inavyohitaji sheria chache zaidi. Vipi kukiwa sheria moja tu? Hii, kwa kielelezo: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii.”—Mathayo 7:12.
Kutii sheria hiyo kungeondoa matatizo mengi ya sasa, lakini, ili kukamilisha mahitaji ya jamii, sheria ya maana zaidi lazima iongezwe: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote.”—Marko 12:30.
Jamii ya kisasa hupuuza matakwa hayo mawili ya Biblia, kutia na miongozo mingineyo iliyo katika Biblia. Biblia husema hivi juu ya watu kama hao kwenye Yeremia 8:9: “Wenye hekima wametahayari. . . . wamelikataa neno la BWANA; wana akili gani ndani yao?” Wao pia hawaoni uhitaji wa kuwa na makubaliano ya pamoja juu ya kanuni zifaazo ambazo tangu jadi zimeonwa kuwa muhimu kwa ajili ya mwongozo wetu. Adili yao mpya ni njia pana inayoruhusu mitindo-maisha mingineyo ambayo watu waweza kuchagua—ile njia pana iliyotambulishwa na Yesu kuwa barabara inayoongoza kwenye uharibifu—na wengi wanaiendea njia hiyo.—Mathayo 7:13, 14.
Kielelezo Bora Kabisa
Yesu Kristo, yule “aliye katika mahali pa kifua pamoja na Baba,” ni kielelezo chenye kutokeza anayestahili kuigwa. (Yohana 1:18, NW) Aliposhughulika na watu, alikuwa mwororo na mwenye huruma kwa upande mmoja, mwenye nguvu na imara kwa upande mwingine; lakini yeye kamwe hakuwa mfidhuli au asiye na fadhili. Kikieleza juu ya “sifa yake isiyo ya kawaida ya kustarehe na watu wa aina zote,” kitabu The Man From Nazareth chasema hivi juu ya Yesu: “Hadharani na pia faraghani alishirikiana na wanaume na wanawake bila upendeleo. Alistarehe na watoto wachanga katika unyoofu wao na kwa ajabu akastarehe na wadanganyi wenye kuumizwa na dhamiri kama Zakayo. Wanawake watunza-nyumba wenye kuheshimika, kama Mariamu na Martha wangeweza kusema naye kwa uwazi wa kawaida, lakini malaya pia walimtafuta kana kwamba walikuwa na hakika kwamba angewaelewa na kuwa mwenye urafiki . . . Kwa njia isiyo na kifani, kutofikiria kwake mipaka iliyozuia watu wa kawaida ni mojawapo sifa zake kuu.”[13]
Sikuzote Yehova Mungu ni mwenye adabu anaposhughulika na wale wa cheo cha chini kuliko yeye, mara nyingi akiongeza “tafadhali” kwa maombi yake. Alipokuwa akimpa baraka Abrahamu rafiki yake, yeye alisema: “Inua macho yako, tafadhali, na utazame kutoka mahali ulipo.” Na tena: “Tazama juu, tafadhali, kwenye mbingu na uhesabu nyota.” (Mwanzo 13:14; 15:5, NW) Alipokuwa akimpa Musa ishara ya uwezo Wake, Mungu alisema: “Tia mkono wako, tafadhali, ndani ya kunjo la juu la vazi lako.” (Kutoka 4:6, NW) Miaka mingi baadaye, kupitia kwa nabii wake Mika, Yehova alisema hata kwa watu wake wasiotawalika: “Sikieni, tafadhali, nyinyi wakuu wa Yakobo na nyinyi maamiri wa nyumba ya Israeli. . . . Sikieni, tafadhali, jambo hili, nyinyi mlio wakuu.” (Mika 3:1, 9, NW) Katika jambo hilo, je! sisi ‘tumekuwa waigaji wa Mungu’ katika kusema tafadhali tunaposhughulika na wengine?—Waefeso 5:1, NW.[14]
Kwa hiyo, ni miongozo ipi au kanuni zipi ambazo wale walio na hekima ya kilimwengu watoa kuwa badala ya ile ya Biblia wanayokatalia mbali? Makala ifuatayo yazungumzia hayo.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Uungwana wa kawaida hauwezi kusemwa kuwa wa kawaida kwa watu
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Ile ambulensi ilikuwa ikijaribu kumfikia mama yake
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Ufidhuli ni mwigo wa nguvu wa mtu dhaifu”
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Kushoto: Life; Kulia: Grandville