Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 7/22 kur. 7-11
  • Je! Adabu Zakataliwa na Ile “Adili Mpya”?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Adabu Zakataliwa na Ile “Adili Mpya”?
  • Amkeni!—1994
  • Habari Zinazolingana
  • Kusitawisha Adabu za Kikristo Katika Ulimwengu Usio na Adabu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • “Jiendesheni kwa Namna Inayozistahili Habari Njema”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kuwa na Adabu Nzuri Ni Sifa ya Watu wa Mungu
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • Je, Ni Muhimu Kuwatendea Wengine kwa Adabu?
    Vijana Huuliza
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 7/22 kur. 7-11

Je! Adabu Zakataliwa na Ile “Adili Mpya”?

‘Ole wale watiao uovu badala ya wema, giza badala ya nuru, uchungu badala ya utamu.’—Isaya 5:20.

KARNE ya 20 ilipata mabadiliko makubwa ya adabu na maadili. Katika miongo iliyofuata vile vita viwili vya ulimwengu, hatua kwa hatua ile mifumo ya kanuni ya zamani ikaja kuonwa kuwa ya kizamani. Hali zenye kubadilika na mawazo mapya katika nyanja za tabia na sayansi ya kibinadamu iliwasadikisha wengi kwamba zile kanuni za zamani hazikutumika tena. Adabu zilizoonwa hapo awali kuwa za maana sana ziliondolewa mbali kuwa mzigo usiotakwa. Miongozo ya Biblia iliyostahiwa zamani ilikataliwa kuwa ya kizamani. Ilikuwa yenye kuzuia mno kwa jamii isiyojali, iliyowekwa huru ya watu mmoja-mmoja walio wa kisasa sana wa karne ya 20.

Mwaka 1914 ndio uliokuwa wakati wa badiliko hilo kubwa katika historia ya kibinadamu. Maandishi ya wanahistoria kuhusu mwaka huo na Vita ya Ulimwengu 1 yamejaa maoneleo yao yanayojulisha 1914 kuwa mwaka wa mabadiliko ya maana, kitia-alama halisi kilichogawanya tarehe za maana katika historia ya kibinadamu. Ile Miaka Yenye Hekaheka ya Ishirini ilifuatia upesi ile vita na watu wakajaribu kupata raha waliyokosa wakati wa miaka hiyo ya vita. Kanuni za zamani na vizuizi vya adili visivyopendeza viliwekwa kando ili watu wajiingize katika raha bila kujizuia. Adili mpya, kufuatilia mambo ya kimwili bila kujizuia, ilianzishwa kwa njia isiyo rasmi—yaani mtu aweza kufanya atakacho. Sheria mpya ya adili ikaleta badiliko katika adabu bila kuzuilika.

Mwanahistoria Frederick Lewis Allen asema hivi juu ya hilo: “Tokeo lingine la mvuvumuko huo lilikuwa kwamba adabu hazikuwa tu tofauti, bali—kwa miaka michache—zikawa utovu-adabu. . . . Wakati wa mwongo huu wanawake wauzaji . . . walipata kwamba wateja wao hata hawakusumbuka kusema nao walipowasili au walipoondoka; kwamba ‘kuingia kwa kutumia kifua’ katika dansi kukawa zoea lililokubaliwa, watu wakawa wenye ‘mtindo wa kuchelewachelewa’ kwenye chakula cha jioni, wakatupa huku na kule sigareti zilizowashwa, wakatapakaza majivu ya sigara juu ya mazulia madogo, bila kuomba msamaha. Zile kanuni za zamani hazikutumika, hakuna mpya zilizokuwa zimefanyizwa, na wakati uo huo watu watovu wa adabu walikuwa huru kufanya watakacho. Labda siku moja, ile miaka kumi iliyofuatia vita huenda ikajulikana kwa kufaa kuwa mwongo wa Adabu Mbaya. . . . Ikiwa mwongo huo ulikuwa wenye adabu mbaya, ulikosa furaha pia. Utaratibu wa mambo wa zamani pamoja na fungu la kanuni ambazo zilikuwa zimefanya uhai uwe na maana na uwe bora, zilikuwa zimetoweka, na kanuni nyingine hazikuwa rahisi kupatikana.”[1]

Kanuni nyingine ambazo zingerudisha tena umaana na ubora wa uhai hazikupatikana. Hazikufuatiwa. Ule mtindo-maisha wenye kusisimua wa kufanya chochote utakacho wa ile Miaka Yenye Hekaheka ya Ishirini uliondolea watu vizuizi vya kiadili, jambo lililowafaa sana. Wao hawakuwa wanaondolea mbali adili; wao walikuwa wanairekebisha tu, kuilegeza kidogo. Baadaye wakaiita ile Adili Mpya. Kwa adili hiyo mtu afanya yale yanayofaa machoni pake. Ubinafsi wa mimi-kwanza hufuata. Yeye afanya kile atakacho. Afuata mwendo wa kujitegemea.

Au eti ndivyo anavyofikiri. Kwa kweli, miaka elfu tatu iliyopita, Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Jambo jipya hakuna chini ya jua.” (Mhubiri 1:9) Hata mapema zaidi, wakati wa Waamuzi, Waisraeli walikuwa na uhuru kadiri fulani juu ya kama wangetii Sheria ya Mungu au la: “Siku hizo hapakuwa na mfalme katika Israeli; kila mtu alifanya yaliyokuwa ni mema machoni pake mwenyewe.” (Waamuzi 21:25) Lakini walio wengi hawakutii ile Sheria. Kwa kupanda kwa njia hiyo, Waisraeli wakavuna mamia ya miaka ya misiba ya kitaifa. Vivyo hivyo, mataifa leo yamevuna karne nyingi za maumivu na kuteseka—na mabaya zaidi yangali mbele.

Kuna neno lingine linalotambulisha ile Adili Mpya kwa njia hususa zaidi, yaani, “ukadirifu.” Kamusi ya Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary hulifasiri hivi: “Maoni kwamba unyoofu wa kiadili hutegemea watu mmoja-mmoja na vikundi vinavyoushikilia.”[2] Kwa ufupi wafuasi wa ukadirifu hutoa hoja kwamba chochote kinachowafaa ni cha maadili kwao. Mwandikaji mmoja alifafanua juu ya ukadirifu aliposema hivi: “Ukadirifu, uliojificha kwa muda mrefu bila kutambuliwa, ulitokea ukiwa falsafa iliyoenea ya ‘mwongo wa u-mimi’ wa miaka ya sabini; bado huo waendelea katika upondaji-mali wa miaka ya themanini. Huenda bado tukasifu kwa mdomo maadili ya kale, lakini kihalisi, yaliyo mema ni yale yanayonifaa.”[3]

Na hilo latia ndani adabu—‘Ikiwa lanifaa, nitalifanya; ikiwa halinifai, sitalifanya. Lisingenifaa mimi, hata ikiwa lingekuwa jambo la adabu zaidi kwao. Lisingefaa hadhi zangu za kibinafsi, lingenifanya nionekane kuwa dhaifu, linifanye niwe hafifu.’ Yaonekana kwamba, kwa watu kama hao, ni hivyo si katika mambo ya ufidhuli tu bali pia kwa hisani rahisi za kila siku kama vile ‘Tafadhali, Nisamehe, Kunradhi, Asante, Ebu nikufungulie mlango, Keti kwenye kiti changu, Acha nikubebee furushi hilo.’ Maneno hayo na mengineyo ni kama mafuta mororo yanayolainisha na kufanya mahusiano yetu ya kibinadamu yawe mazuri. Hata hivyo mtu mwenye u-mimi-kwanza angepinga akisema: ‘Lakini kuwa mwenye adabu kwa wengine, kungeathiri vibaya hali yangu ya u-mimi-kwanza.’

Mwanasosholojia James Q. Wilson aonyesha sababu ya ongezeko la mikazo na mwenendo wa uhalifu kuwa kuporomoka kwa yale ambayo leo “yarejezewa kwa dharau kuwa ‘kanuni za watu wa ngazi za juu,’” na ripoti hiyo yaendelea kusema: “Kutoweka kwa kanuni hizo—na ongezeko la ukadirifu wa maadili—kwaonekana kukihusiana na kiasi cha juu zaidi cha uhalifu.”[4] Kwa kweli kwahusiana na mwendo wa kisasa wa kukataa vizuizi vyovyote vya kujitosheleza, hata iwe kujitosheleza huko kwakosa adabu jinsi gani au kwaudhi jinsi gani. Hayo ni kama vile mwanasosholojia mwingine, Jared Taylor, alivyosema: “Hatua kwa hatua jamii yetu imeacha kujidhibiti na badala ya hivyo ikafuatia kujitosheleza, na watu wengi hupuuza kanuni za zamani kuwa zuifu.”[5]

Kuzoea ukadirifu hufanya wewe uwe mwamuzi wa mwenendo wako wa kibinafsi, ukipuuza uamuzi wa mtu mwingine yeyote, kutia ule wa Mungu. Wajiamulia yale yakufaayo na yale yasiyokufaa, kama vile wale wanadamu wawili wa kwanza walivyofanya katika Edeni walipokataa amri ya Mungu na kujiamulia yaliyofaa na yasiyofaa. Yule Nyoka alimdanganya Hawa kufikiri kwamba ikiwa angekosa kumtii Mungu na kula baadhi ya tunda lililokatazwa, basi ingetokea kama vile alivyomwambia: “Mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” Kwa hiyo Hawa akatwaa baadhi ya tunda akala na kisha akampa Adamu baadhi yalo, naye akala. (Mwanzo 3:5, 6) Uamuzi wa Adamu na Hawa kula uliwaletea msiba na kuleta maafa kwa wazao wao.

Baada ya muhtasari mrefu juu ya ufisadi miongoni mwa wanasiasa, wafanyabiashara, wanariadha, wanasayansi, mshindi wa tuzo la Nobeli, na kasisi mmoja, mchunguza-mambo mmoja mlimwengu alisema hivi katika hotuba mbele ya Shule ya Biashara ya Harvard: “Naamini kwamba katika nchi yetu leo twapata kile ninachochagua kuita hatari ya utu, kupoteza vile ambavyo tangu zamani kupitia ustaarabu wa Magharibi, vilionwa kuwa vizuizi vya kindani na kanuni za kindani zinazotuzuia tusitosheleze mibetuko yetu isiyofaa.” Yeye alisema juu ya “maneno ambayo karibu yatasikika kuwa mageni yasemwapo katika hali hizo, maneno kama vile uhodari, heshima, jukumu, daraka, huruma, hisani—maneno ambayo karibu yamekoma kutumiwa.”[6]

Katika miaka ya 1960, katika vyuo vikuu, masuala fulani yalizuka. Wengi walidai kwamba ‘hakuna Mungu, Mungu amekufa, kuna utupu, hakuna kitu, hakuna kanuni inayopita zote, uhai hauna maana kabisa, waweza kushinda hali ya utupu ya uhai kwa ushujaa wa kibinafsi.’ Vijana wenye maadili ya kiajabu-ajabu wakapata ishara ya kusonga mbele na wakajaribu kuondolea mbali utupu wa uhai kwa ‘kuvuta kokeni kwa pua, kuvuta bangi, kufanya ngono za ovyo-ovyo, na kutafuta amani ya akilini ya mtu binafsi.’ Hawakuipata kamwe.

Halafu kulikuwa na maandamano ya miaka ya 1960. Yakiwa zaidi ya mitindo tu, yalikubaliwa na walio wengi katika utamaduni wa Marekani na kuongoza katika mwongo wa U-Mimi wa miaka ya 1970. Hivyo tukaingia katika mwongo ambao Tom Wolfe, mchambuzi wa jamii, aliita “mwongo wa U-Mimi.” Hiyo ilisonga mbele katika miaka ya 1980, iliyoitwa na wengine kwa dharau “enzi ya ufanisi yenye pupa.”[7]

Yote hayo yahusianaje na adabu? Yanahusu kujitanguliza, na ukijitanguliza, huwezi kuwapa wengine nafasi, huwezi kutanguliza wengine, huwezi kuwa na adabu nzuri kuelekea wengine. Kwa kweli, kwa kujitanguliza, huenda ukajiingiza katika namna ya kujiabudu, ibada ya U-Mimi. Biblia yasema mtu afanyaye hivyo ni nini? “Mtu mwenye pupa—maana yake kuwa mwabudu-sanamu,” kuwa mwenye “choyo, ambako ni ibada ya sanamu.” (Waefeso 5:5; Wakolosai 3:5, NW) Watu hao wanaabudu nani hasa? “Mungu wao ni tumbo.” (Wafilipi 3:19) Mitindo-maisha mingine michafu ambayo watu wengi wamechagua kuwa yafaa kiadili kwao na matokeo yenye msiba, na yenye kuleta kifo ya mitindo-maisha hiyo yathitibisha tu ukweli wa Yeremia 10:23: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”

Biblia ilitangulia kuona hayo yote na ikayatabiri kuwa onyo la “siku za mwisho,” kama zilivyorekodiwa kwenye 2 Timotheo 3:1-5, Biblia ya New English Bible yasema: “Ni lazima ukabili jambo hili hakika: enzi ya mwisho ya ulimwengu huu itakuwa wakati wa matatizo. Watu watapenda pesa na kujipenda sana; wenye kujitanguliza, wenye kiburi, watukanaji; wasiostahi wazazi, wasio na shukrani, wasiowaaminifu kwa wajibu, wasio na shauku ya asili; wasiotaka upatano katika chuki yao, wachongezi, wasiojizuia na wakali, wasio na wema wowote, wasaliti, wenye kujasiria, wenye kututumuka kwa ubinafsi. Watakuwa watu wanaotanguliza raha badala ya Mungu, watu wanaodumisha wonyesho wa nje wa dini, lakini hukana uhalisi wayo. Jiepushe na watu wa aina hiyo.”

Tumeelea mbali kutoka kwa ile hali tuliyoumbwa kuwa—katika mfano na ufanano wa Mungu. Uwezekano wa sifa za upendo, hekima, haki, na uwezo ungali ndani yetu lakini zimekosa usawaziko na zikapotoka. Hatua ya kwanza ya kurudia hali ya kwanza imefunuliwa katika ile sentensi ya mwisho ya andiko la Biblia lililonukuliwa juu: “Jiepushe na watu wa aina hiyo.” Tafuta mazingira mapya, yatakayobadili hata hisia zako za ndani. Maneno yenye hekima yanayofundisha ni yale yaliyoandikwa miaka mingi iliyopita katika kitabu The Ladies’ Home Journal cha Dorothy Thompson.[8] Nukuu lake laanza kwa julisho kwamba ili kushinda utovu wa adabu wa watoto, yabidi kuelimisha hisia-moyo za kijana badala ya akili yake:

“Vitendo na mitazamo yake akiwa mtoto huamua kwa kiasi kikubwa vitendo na mitazamo yake akiwa mtu mzima. Lakini hizo hazitokezwi na akili yake, bali na hisia zake. Yeye huja kuwa kile anachotiwa moyo na kuzoezwa kupenda, kuvutiwa, kuabudu, kuthamini, na kujidhabihu. . . . Adabu huwa na fungu la maana katika yote hayo, kwani adabu nzuri ni wonyesho wa ufikirio kwa wengine. . . . Hisia za kindani huonyeshwa katika tabia ya nje, lakini tabia ya nje pia hutia moyo usitawishaji wa hisia za ndani. Ni vigumu kuwa mfanya-vita na wakati huohuo kuwa mwenye kufikiria wengine. Mwanzoni adabu nzuri zaweza kuwa za kijuu-juu tu, lakini mara nyingi hazidumu kuwa hivyo.”[8a]

Yeye pia alionelea kwamba, isipokuwa katika hali chache, wema na ubaya “haziletwi na akili bali na hisia-moyo” na kwamba “wahalifu huwa wahalifu si kutokana na ugumu wa arteri bali kutokana na ugumu wa moyo.” Yeye alikazia kwamba mara nyingi hisia-moyo huongoza mwenendo wetu, zaidi ya vile akili inavyoweza kuuongoza na kwamba jinsi ambavyo tumezoezwa, jinsi tunavyotenda, hata ikiwa mwanzoni ni kwa kujilazimisha, huwa na uvutano juu ya hisia za ndani na kuubadili moyo.[8b]

Hata hivyo, ni Biblia ndio hufanikiwa kabisa katika kutoa njia iliyopuliziwa ya kubadilisha utu wa ndani wa moyo.

Kwanza, Waefeso 4:22-24: “Mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.”

Pili, Wakolosai 3:9, 10, 12-14, NW: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea ya huo, na mjivike wenyewe utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba. Basi, kama wachaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni wenyewe shauku zenye wororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuchukuliana nyinyi kwa nyinyi na kusameheana kabisa mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kabisa, fanyeni hivyo nyinyi pia. Lakini, zaidi ya mambo hayo yote, jivikeni wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”

Mwanahistoria Will Durant alisema: “Suala kuu zaidi katika wakati wetu si ukomunisti dhidi ya kujitegemea, si Ulaya dhidi ya Marekani, hata si Mashariki dhidi ya Magharibi; ni kama watu waweza kuishi bila Mungu.”[10]

Ili kuishi maisha yenye fanaka, ni lazima tutii shauri lake. “Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku, na miaka ya uzima, na amani. Rehema na kweli zisifarakane nawe; zifunge shingoni mwako; ziandike juu ya kibao cha moyo wako. Ndivyo utakavyopata kibali na akili nzuri, mbele za Mungu na mbele ya mwanadamu. Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe. Katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.”—Mithali 3:1-6.

Kumbe adabu nzuri zenye fadhili na kuwafikiria wengine ambazo wanadamu wamejifunza kwa karne nyingi za kuishi si mzigo usiotakwa, na miongozo ya Biblia kwa ajili ya kuishi si ya kizamani hata kidogo bali ni kwa ajili ya wokovu wa milele wa wanadamu. Bila Yehova, wao hawawezi kuendelea kuishi, kwani ‘kwa Yehova iko chemchemi ya uhai.’—Zaburi 36:9.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Jinsi tunavyotenda, hata ikiwa mwanzoni ni kwa kujilazimisha, huwa na uvutano juu ya hisia za ndani na kuubadili moyo

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

Adabu za Mezani Zisizo na Dosari Ambazo Watu Waweza Kuiga

Ndege-Mwerezi, wazuri, wenye adabu nzuri, wenye urafiki sana, wakila pamoja katika kichaka kikubwa chenye beri zilizoiva. Wakiwa wamepanga mstari juu ya tawi, wao hula matunda hayo. Lakini si kwa uchoyo hata kidogo. Wao hupitishiana beri kutoka mdomo mmoja hadi mwingine, hadi hatimaye mmoja wao anapoila kwa hisani. Wao hawasahau “watoto” wao kamwe, wakileta chakula bila kuchoka, beri baada ya beri, hadi midomo yote mitupu inapotosheka.

[Hisani]

H. Armstrong Roberts

[Picha katika ukurasa wa 8]

Wengine husema: ‘Tupilia mbali Biblia na kanuni za kiadili’

[Picha katika ukurasa wa 9]

“Mungu amekufa.”

“Uhai hauna maana!”

“Vuta bangi, vuta kokeni kwa pua”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]

Kushoto: Life; Kulia: Grandville

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki