Vijana Huuliza . . .
Ugoni-Jinsia-Moja—Je, Kweli Ni Mbaya Hivyo?
“Tangu nikiwa mtoto, nimekuwa na tamaa za ugoni-jinsia-moja. Kwa sababu sikuzielewa, sikuchukua tahadhari. Hili liliniongoza kufanya jambo baya sana na rafiki yangu mvulana. Nilipatwa na hisia nyingi za hatia, na nilifikiri Yehova hangenisamehe kamwe.”
“TELEVISHENI Yajaribu Kuwauza Watoto Wetu kwa Ugoni-Jinsia-Moja.” Hiki kilikuwa kichwa cha makala fulani kilichoandikwa na mwandikaji mmoja wa magazeti. Mwandikaji alionelea hivi: “Watazamaji wa televisheni huonyeshwa kwa wingi mno mtindo-maisha wa wagoni-jinsia-moja kuwa wafaa.” Hata hivyo, televisheni ni mojapo ya njia nyingi zinazotumiwa siku hizi ili kuendeleza ugoni-jinsia-moja miongoni mwa vijana. Maenezi ya ugoni-jinsia-moja pia yanaendelezwa na walimu, marika, sinema, vitabu, na magazeti.
Taaluma ya kitiba pia imefuata halaiki. Kidesturi, madaktari huuona ugoni-jinsia-moja kuwa ugonjwa fulani. Lakini katika 1973, shirika la American Psychiatric Association lilitangaza kwamba ugoni-jinsia-moja haungeonwa tena kuwa kasoro za kiakili. Tangu wakati huo, wengi walio katika taaluma ya kitiba wameonyesha ukubali wa mtindo-maisha wa ugoni-jinsia-moja. Kwa kielelezo, mwanatiba wa akili Albert Ellis, alitangaza kwamba mahusiano ya ugoni-jinsia-moja “hayana upotovu kamwe lakini huwa na tabia zifaazo za ngono. . . . Zifurahie ukizichagua, na usiruhusu yeyote akutolee maenezi ya kuwa ni ‘mbaya’ ama ni ‘usumbufu.’”
Maoni kama hayo ni upotovu hivi kwamba gazeti la Newsweek laripoti hivi: “Kwa kile kionyeshwacho na vyanzo vya habari na uvutano wa kuukubali, matineja wanaujaribu ugoni-jinsia-moja na ugoni-jinsia-tofauti bila kuficha.” Ingawa nyakati zilizopita matineja walikataa katakata mahusiano ya jinsia moja, si kutia chumvi kusema kwamba idadi inayoongezeka sasa ya vijana huuona kuwa “ufashoni.” Hata vijana ambao hawajiingizi katika matendo ya ugoni-jinsia-moja mara nyingi hawaoni ubaya kwa wale wanaoufanya. “Natumai ikiwa rafiki yangu angeniambia alikuwa mgoni-jinsia-moja, bado nitakuwa rafikiye,” akasema kijana aitwaye Darren. Kijana mmoja mwanakoleji hata alionyesha hangaiko kwamba huenda awe na kasoro kwani yeye “aliwapenda wasichana tu”!
Leo hali ya uhuru yaweza kuwa yenye kuvuruga kwa vijana Wakristo—hasa wale ambao kwa sababu fulani huhisi uvutio kwa watu wa jinsia-moja.a Wanajua kwamba ugoni-jinsia-moja haumpendezi Mungu, na kwa moyo mweupe wataka kuiepuka. Ingawa, nyakati nyingine ule mng’ang’ano wa kudhibiti hisia zao waweza kuchosha mno hivi kwamba huenda waanze kutilia mashaka kama msimamo wa Biblia ni mzuri ama wafaa. ‘Je, kwa kweli ugoni-jinsia-moja ni mbaya hivyo?’ huenda wajiulize.
Kile Neno la Mungu Husema
Katika kujibu, jisomee yale mtume Paulo alisema kwenye 1 Wakorintho 6:9, 10: “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji [“wanaume malaya,” New International Version; “wenye tabia ya kike,” King James Version], wala walawiti [“wasodomu,” Jerusalem Bible; “wapotovu wa ugoni-jinsia-moja,” Today’s English Version], wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi.” Ona kwamba Paulo hasa awataja wale wanaofanywa ngono na wale walichukualo fungu la “kiume” kwa dhati katika mahusiano yao yasiyo ya adili. Hivyo aliweka wazi kwamba Mungu hukataa matendo yote ya ugoni-jinsia-moja.
Hili pia ni wazi katika maneno ya Paulo kwenye Warumi 1:18-27: “Ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni juu ya uasi wote na uovu wa wanadamu waipingao kweli kwa uovu . . . Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate [u]chafu, hata wakavunjiana heshima miili yao . . . Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa [“yenye kukirihisha,” New World Translation].” Hapa Paulo kihususa alilaani aina zote mbili za ugoni-jinsia-moja wa kiume na kike. Alishutumu mazoea ya ugoni-jinsia-moja kuwa yasiyo ya asili na “yenye kukirihisha.”
Ugonjwa ama Afya?
Wengi huenda waitikie hili kwa kusema kwamba maoni ya Biblia ni ya kikale tu, yasiyotumika leo. Lakini ukifikiria kulihusu, je, ni nani ajuaye umbo letu la kimwili, kiakili, kihisia-moyo, na kiroho kuliko Muumba wetu? Mungu alimfanya mwanamume, na mwanamke na kuwaweka katika hali ya uvutano wa wao kwa wao. (Mwanzo 1:27, 28) Hakuwafanya wawe na uvutio kwa mtu wa jinsia moja. Zaidi, Mungu alikuwa ameamua kwamba mahusiano ya kingono kati ya mwanamume na mwanamke yapasa kufanywa katika mpango wa ndoa tu.—Waebrania 13:4.
Hili halitokezi magumu kwetu. Kwenye Isaya 48:17, Yehova Mungu husema kwamba ni yeye ‘akufundishaye ili upate faida.’ (Italiki ni zetu.) Naam, yeye ajua kinachotusaidia na kinachotudhuru. Ingawa kwa wengine mafundisho ya Biblia huenda yaonekane magumu kufuata, sikuzote ni ‘mafundisho yenye afya,’ yaani, yafaidi akili na mwili. (Tito 2:1) Ugoni-jinsia-moja, kwa upande ule mwingine, waweza tu kuwa na madhara ya hali njema ya kimwili, kihisia-moyo, na kiroho ya mtu.
Lile dhara la UKIMWI ni kielelezo cha jinsi mtindo-maisha wa ugoni-jinsia-moja usivyo wa afya. Katika Amerika Kaskazini, wanaume wagoni-jinsia-moja kwa kiasi kikubwa wana uelekeo wa kuambukizwa ugonjwa huo. Lakini UKIMWI ni mojapo tu ya unamna wa magonjwa—mchochota wa ini, maambukizo ya ini, kisonono, kaswende, na vimelea-utumbo mdogo—ambayo kwa kawaida huwafika wagoni-jinsia-moja. Ni nini huchochea usambaaji wa maradhi haya? Dakt. Joseph Nicolosi hueleza hivi: “Hali ya mtindo-maisha yenye uraibu wa kushurutisha ya wagoni-jinsia-moja imedhihirishwa na waandikaji wengi.” Uchunguzi mmoja mpana ulifunua kwamba “asilimia 28 ya wanaume wagoni-jinsia-moja [wamepata] kufanya ngono na wenzi elfu moja ama zaidi. . . . Karibu nusu ya wanaume wagoni-jinsia-moja weupe . . . walisemwa kuwa walikuwa na wenzi tofauti-tofauti zaidi ya 500.”
Kitabu Homosexual Behavior hueleza kwamba miongoni mwa wagoni-jinsia-moja wengi “kuna hofu kuingia katika mikataba ihitajiyo ushikamanifu, uhusiano wa ndani, ama daraka . . . Ule msukumo wa kutofanya ngono na mmoja tu nyakati nyingine hushurutisha sana. Baadhi ya watu hawa huenda wakajihusisha na makumi au zaidi ya mikataba ya kingono katika kipindi cha siku moja au jioni.” Je, ingeliwezekana tabia kama hizo zisizodhibitiwa kuwa zenye afya? Je, badala yake, si ugonjwa na upotovu? Kwa wazi wale ambao hujiingiza katika upotovu kama huo wanakuwa “watumwa wa uharibifu.”—2 Petro 2:19.
Hata zaidi, ngono ya ujinsia-moja yakirihisha, yajeruhi, na kwa kweli ni ya kikatili. Mtume Paulo alisema hivi: “Yanayotendeka kwao kwa siri, ni aibu hata kuyanena.” (Waefeso 5:12) Jeuri kama hizo huonyesha hasira na maumivu yanayoukumba eti mtindo-maisha wa “wagoni-jinsia-moja.” Kweli, baadhi ya wagoni-jinsia-moja hudai kwamba hawafanyi ngono ovyoovyo. Lakini wagoni-jinsia-moja walio na “mwenzi mmoja” ni wachache mno—na kwa kulinganishwa mahusiano yao huwa ya muda mfupi tu. Hata maungano ya jinsia-moja yadumupo, hayawezi kuwa ni tokeo la upendo uliofafanuliwa katika Biblia. Upendo kama huo “haukosi kuwa na adabu.”—1 Wakorintho 13:4, 5.
Matokeo
Paulo asema kwenye Warumi 1:27: “Wanaume kwa wanaume walitenda misiba hii yenye aibu, bila shaka, wakipata kwenye nyutu zao matokeo ya upotovu wa kingono.” (The New Testament in Modern English, na J. B. Phillips) Katika njia zipi? Kuhusu mojapo ya matokeo kitabu Homosexual Behavior huripoti hivi: “Wanawake wagoni-jinsia-moja hupatwa sana na utumizi mwingi na mbaya wa alkoholi kuliko wanawake wagoni-jinsia-tofauti.” Baadhi ya watafiti pia wadai kwamba majaribio ya kujiua ni ya kawaida mno miongoni mwa wanaume wagoni-jinsia-moja.
Yadhuruyo zaidi ya yote ni matokeo kwa hali ya kiroho ya mmoja. Wagoni-jinsia-moja hujipata kuwa “akili zao zimetiwa giza, nao wamefarakishwa na uzima wa Mungu.” (Waefeso 4:18) Lakini namna gani kuhusu vijana wahofu-Mungu ambao, wajapokuwa na ujuzi wa kanuni za Mungu, hujipata wakivutiwa na watu wa jinsia-moja? Kwa wazi, wana vita vyenyewe. Bila shaka, kujua maoni ya Mungu yalivyo kuhusu ugoni-jinsia-moja kwawasaidia hao ‘walichukie lililo ovu.’ (Warumi 12:9) Kunazo pia idadi za hatua zenye kutumika wawezazo kuchukua ili kuziepuka tamaa mbaya. Hii itakuwa mada ya makala ya wakati ujao.
[Maelezo ya Chini]
a Ona “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Nina Hisia Hizi?” katika toleo letu lililotangulia.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Mtindo-maisha wa ugoni-jinsia-moja una uovyo ovyo, mikazo ya kihisia-moyo, na maradhi