Karibuni—Wakati Bora Zaidi!
KULINGANA na Biblia, Mungu alinuia kwamba jamii ya kibinadamu iishi milele katika paradiso iliyoenea duniani kote. (Mwanzo 1:28; 2:8, 9) Kwa wazi, tumegeukia mbali kutoka kwenye kusudi la Mungu la awali. Ni nini kilitukia?
Wenzi wawili wa kwanza walikosa kutii Mungu, ikitokeza kutokamilika na kifo kwao wenyewe na wazao wao wote. (Mwanzo 2:16, 17; 3:6, 7, 17-19; Warumi 6:23) Biblia yaeleza hivi: “Dhambi ilikuja ulimwenguni kupitia mtu mmoja, na dhambi yake ilileta kifo pamoja nayo. Kama tokeo, kifo kimeenea kwa jamii yote ya kibinadamu kwa kuwa kila mtu ametenda dhambi.”—Warumi 5:12, TEV
Ijapokuwa hali hii, kusudi la Mungu labaki bila kubadilika. “Neno langu ni kama theluji na mvua ishukayo kutoka mbinguni ili kumwagilia maji dunia. Hizo hufanya mimea ikue na kuandaa mbegu kwa ajili ya kupanda na chakula kwa ajili ya kula. Ndivyo pia litakuwa neno langu nisemalo. . . Litafanya kila kitu nilicholituma kufanya.” (Isaya 55:10, 11, TEV) Mungu aahidi kutufanyia nini?
BARAKA CHINI YA UFALME WA MUNGU
Uhai wa milele
“Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.
“Wala mauti haitakuwapo tena, wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.—Ufunuo 21:4.
Usalama
“Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo.”—Zaburi 37:10.
Kazi yenye kuridhisha
“Watu watajenga nyumba na kupata kuishi ndani yazo—hazitatumiwa na mtu mwengineo. Watapanda mizabibu na kufurahia divai—haitanywewa na wengine. Kama miti, watu wangu wataishi maisha marefu. Watafurahia kikamili vitu ambavyo wamevifanyia kazi.”—Isaya 65:21, 22, TEV.
Afya
“Hapana mwenyeji atakayesema ‘Mimi mgonjwa.’ watu wakaao humo watasamehewa uovu wao.”—Isaya 33:24.
Hakuna ulemavu
“Macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6.
Wingi wa chakula
“Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zaburi 72:16.
Amani
“Njoni myatazame matendo ya BWANA, jinsi alivyofanya ukiwa nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia.”—Zaburi 46:8, 9.
KILE UNACHOHITAJIKA KUFANYA
Ni lazima ufanye nini ili ufurahie baraka hizi ambazo Mungu ameahidi? Biblia hujibu kwenye Yohana 17:3: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” Ndiyo, kwa kujifunza juu ya Mungu—jina lake, kusudi lake, na sheria zake—twapata maana ya mwelekezo. Isitoshe, kwa kujifunza juu ya Yesu—maisha yake duniani, dhabihu yake ya fidia kwa ajili ya dhambi zetu, cheo chake akiwa Mtawala wa Ufalme wa Mungu—twaweza kuwa na uhakika kwamba kusudi la Mungu litatimizwa.
Ustahimilivu wa Mungu kwa uovu umetumika kuonyesha bila tashwishi lolote kuachwa kwamba mwanadamu, kama msafiri katika eneo asilolifahamu, hawezi kuelekeza hatua zake mwenyewe. (Yeremia 10:23) Kwa hakika, ingawa serikali nyingi mno—kuanzia na udikteta hadi demokrasia—mwanadamu amejaribu kila njia inayowazika. Na bado, mafanikio yake yamekuwa haba chini ya hali zifaazo.
Jinsi tuwezavyo kuwa na shukrani kwamba Ufalme wa Mungu utajibu sala zisemwazo na mamilioni: “Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:10) Baraka za Ufalme wa Mungu zitafurahiwa duniani wakati hivi karibuni utakapochukua mahali pa serikali zote za kibinadamu. Biblia yaahidi: “Na katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Utakuwa wakati mtukufu ulioje! Kwa hakika ujuzi wa Biblia waweza kututia tumaini. Ndiyo, hizi ni nyakati zenye taabu—na zazidi kuwa mbaya zaidi. Lakini hilo lathibitisha tu kwamba twaishi katika siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo. Karibuni mahali pa nyakati mbaya zaidi patachukuliwa na nyakati bora zaidi chini ya Ufalme wa Mungu!