Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 6/22 kur. 6-9
  • Je, Waweza Kutumaini Ahadi za Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Waweza Kutumaini Ahadi za Mungu?
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuzuka na Kuanguka kwa Serikali Kuu za Ulimwengu
  • Mesiya Aahidiwa
  • Hakuna Tarehe Ijulikanayo ya Mwisho
  • Rekebisho la Maoni Lahitajiwa
  • Neno la Yehova Ni Hakika!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Unabii Mwingi Uliotimizwa
    Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?
  • Kumtambua Masihi, Yule Mfalme
    “Ufalme Wako Uje”
  • Danieli Kitabu Kilichohakikishwa Kuwa cha Unabii
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 6/22 kur. 6-9

Je, Waweza Kutumaini Ahadi za Mungu?

YEHOVA MUNGU, Muumba wetu, sikuzote ametimiza neno lake. “Nimenena,” yeye alisema. “Nami nitafanya.” (Isaya 46:11) Baada ya kuongoza Waisraeli kuingia katika Bara Lililoahidiwa, mtumishi wa Mungu Yoshua aliandika hivi: “Hakuna ahadi iliyokosa kutimia kati ya ahadi yote njema ambayo Yehova alikuwa amefanya kwa nyumba ya Israeli; yote ilikuja kuwa kweli.”—Yoshua 21:45; 23:14, NW.

Tangu siku ya Yoshua hadi kuja kwa Mesiya, mamia ya unabii uliopuliziwa na Mungu ulitimia. Kielelezo kimoja ni wakati mjengaji-upya wa Yeriko alipopata adhabu iliyotabiriwa karne nyingi kimbele. (Yoshua 6:26; 1 Wafalme 16:34) Kingine tena ni ahadi, ionekanayo vigumu kutimiza, ambayo wakazi wenye njaa kali wa Samaria wangepata chakula kingi cha kula siku iliyofuata huo utabiri. Katika 2 Wafalme sura ya 7 waweza kusoma jinsi Mungu alivyotimiza ahadi hiyo.

Kuzuka na Kuanguka kwa Serikali Kuu za Ulimwengu

Mungu alipulizia waandikaji wa Biblia warekodi maelezo ya kindani kuhusu kuzuka na kuanguka kwa serikali kuu za ulimwengu. Kwa kielelezo, Mungu alimtumia nabii wake Isaya kutabiri kupinduliwa kwa Babiloni yenye nguvu karibu miaka 200 kabla ya hilo kutukia. Kwa hakika, Wamedi, walioungana na Waajemi, walitambulishwa katika Biblia kuwa washindi. (Isaya 13:17-19) Na bado lenye kutokeza zaidi, nabii wa Mungu alimtambulisha mfalme wa Uajemi Sairasi kuwa yule ambaye angechukua uongozi katika huo ushindi, hata ingawa Sairasi alikuwa hata hajazaliwa bado wakati huo unabii uliporekodiwa! (Isaya 45:1) Lakini kuna zaidi.

Nabii Isaya alitabiri pia jinsi kushindwa kwa Babiloni kungetimizwa. Aliandika kwamba maji ya jiji yenye kutoa ulinzi, mto Efrati, ‘lazima yakauke’ na kwamba “malango [ya Babiloni] hayatafungwa.” (Isaya 44:27–45:1) Maelezo haya hususa yalitimizwa, kama mwanahistoria Herodoto alivyoripoti.

Wakati Babiloni ilipokuwa ingali yenye ukuu kabisa, Mungu alimtumia pia nabii Danieli kueleza kuhusu serikali za ulimwengu ambazo zingeifuata. Danieli alipata njozi ya kondoo mume wa mfano mwenye pembe mbili aliyefanikiwa katika kushinda “mahayawani-mwitu” wengine wote. Pasipo kuacha shaka lolote kuhusu ni nani aliyewakilishwa na kondoo mume mwenye pembe mbili, Danieli aliandika kwamba “[husimamia] wafalme wa Umedi na Uajemi.” (Danieli 8:1-4, 20, NW) Kwa kweli, kama tu ilivyotabiriwa, Umedi-Uajemi ilikuja kuwa serikali ya ulimwengu iliyofuata wakati iliposhinda Babiloni katika 539 K.W.K.

Katika njozi hii kutoka kwa Mungu, Danieli aliona “beberu yule alikuwa na pembe mashuhuri kati ya macho yake.” Danieli aliendelea na ufafanuzi wake hivi: ‘Nikamwona akimkaribia kondoo mume, akampiga kondoo mume, akazivunja pembe zake mbili, wala hapakuwapo awezaye kumwokoa kondoo mume katika mkono wake. Na yule beberu akajitukuza sana; na alipokuwa na nguvu pembe ile kubwa ikavunjika, na badala yake zikazuka pembe nne.’—Danieli 8:5-8.

Neno la Mungu haliachi nafasi yoyote ya kuwa na shaka kuhusu kinachomaanishwa na yote haya. Ona lile elezo: “Yule beberu, mwenye manyoya mengi, ni mfalme wa Uyunani [“Ugiriki,” NW]; na ile pembe kubwa iliyo kati ya macho yake ni mfalme wa kwanza. Tena katika habari ya pembe ile iliyovunjika, ambayo badala yake zilisimama pembe nne, falme nne zitasimama kutoka katika taifa lile, lakini si kwa nguvu kama zake.”—Danieli 8:21, 22.

Historia inaonyesha kwamba huyu ‘mfalme wa Ugiriki’ alikuwa Aleksanda Mkubwa. Baada ya kifo chake katika 323 K.W.K., milki yake iligawanywa hatimaye kati ya majenerali wanne—Seleuko 1 Niketa, Kasanda, Ptolemy 1, na Lisimako. Sawa tu na ilivyotabiri Biblia, “badala yake zilisimama pembe nne.” Pia kama ilivyotabiriwa, hakuna mojapo ya hizi iliyokuwa na kiwango cha uwezo ambacho Aleksanda alikuwa nacho. Kwa kweli, huo utimizo umekuwa wenye kutokeza sana hivi kwamba unabii kama huo wa Biblia umekuwa ukiitwa “historia iliyoandikwa kimbele.”

Mesiya Aahidiwa

Mungu hakuahidi tu Mesiya ili kukomboa binadamu kutoka kwenye athari za dhambi na kifo bali pia aliandaa unabii mwingi wa kutambulisha Mwahidiwa huyo. Fikiria mchache wa huo, unabii ambao Yesu hangelikuwa amepanga ili kuutimiza.

Ilikuwa imetabiriwa mamia ya miaka kimbele kwamba yule Mwahidiwa angezaliwa katika Bethlehemu na kwamba angezaliwa na bikira. (Linganisha Mika 5:2 na Mathayo 2:3-9; Isaya 7:14 na Mathayo 1:22, 23.) Ilikuwa imetabiriwa kwamba atasalitiwa kwa vipande 30 vya fedha. (Zekaria 11:12, 13; Mathayo 27:3-5) Ilitabiriwa pia kwamba hakuna mfupa wake ambao ungevunjwa na kwamba mavazi yake yangepigiwa kura.—Linganisha Zaburi 34:20 na Yohana 19:36, Zaburi 22:18 na Mathayo 27:35.

Lenye umaana hasa ni uhakika wa kwamba Biblia ilitabiri ni lini Mesiya angekuja. Neno la Mungu lilitabiri hivi: ‘Tangu kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu hata zamani zake masihi aliye mkuu; kutakuwa na majuma saba, [“na pia majuma sitini na mawili,” NW].’ (Danieli 9:25) Kulingana na Biblia, amri ya kutengeneza na kujenga upya kuta za Yerusalemu ilitolewa katika mwaka wa 20 wa utawala wa Mfalme Atashasta, ambao historia ya kilimwengu inaonyesha ulikuwa katika mwaka wa 455 K.W.K. (Nehemia 2:1-8) Haya majuma 69 ya miaka yaliisha miaka 483 baadaye (7 x 69 = 483), katika mwaka 29 W.K. Huo ndio uliokuwa mwaka hasa ambao Yesu alibatizwa na kutiwa mafuta kwa roho takatifu akawa yule Mesiya, au Kristo!

Kwa kufaa, watu katika siku ya Yesu walikuwa wakitazamia Mesiya atokee wakati huo, kama mwanahistoria Mkristo Luka alivyotaja. (Luka 3:15) Wanahistoria Waroma Tasito na Suetonio, mwanahistoria Myahudi Yosefo, na mwanafalsafa Myahudi Filo Yudeo pia walitoa ushahidi wa hali hii ya kutazamia. Hata Abba Hillel Silver, katika kitabu chake A History of Messianic Speculation in Israel, hukubali kwamba “Mesiya alitazamiwa katika robo ya pili ya karne ya kwanza W.K.” Hilo, yeye alisema, lilikuwa kwa sababu ya “kronolojia maarufu ya wakati huo,” iliyotolewa kwa sehemu kutoka kitabu cha Danieli.

Kwa kufikiria habari hiyo, haipasi kushangaza kwamba Biblia ingeonyesha pia wakati Mesiya angerudi ili kuanza utawala wake wa kifalme. Uthibitisho wa kikronolojia unaopatikana katika unabii wa Danieli ulionyesha kikamili wakati hususa ambao “Aliye juu” angepatiana utawala wa dunia kwa “aliye mnyonge,” Yesu Kristo. (Danieli 4:17-25; Mathayo 11:29) Kipindi cha “nyakati saba,” au miaka saba ya kiunabii, kinatajwa, na kipindi hiki kilijumlishwa kuwa kiliisha katika mwaka wa 1914.a

Hakuna Tarehe Ijulikanayo ya Mwisho

Hata hivyo, mwaka wa 1914, ni tarehe tu ya mwanzo wa utawala wa Kristo ‘kati ya adui zake.’ (Zaburi 110:1, 2; Waebrania 10:12, 13) Kitabu cha Biblia cha Ufunuo chafunua kwamba katika wakati ambapo utawala wa Kristo katika mbingu ungeanza, angewavurumisha Shetani Ibilisi na malaika zake chini duniani. Kabla ya kuwaondolea mbali watu hawa wa kiroho waovu, Biblia yasema, wangesababisha taabu nyingi mno duniani kwa “wakati mchache.”—Ufunuo 12:7-12.

Kwa kufaa, Biblia haiandai tarehe ambayo huu “wakati mchache” utaisha na wakati ambapo Kristo atatenda akiwa Mfishaji wa adui za Mungu kwenye Har–Magedoni. (Ufunuo 16:16; 19:11-21) Kwa hakika, kama ilivyoonyeshwa katika makala iliyotangulia, Yesu alisema tuwe tayari kwa sababu hakuna binadamu ajuaye tarehe ya tukio hilo. (Marko 13:32, 33) Mtu aendapo ng’ambo ya alichosema Yesu, kama walivyofanya Wakristo wa mapema katika Thesalonike na wengine baada yao, kutakuwa na matabiri ya uwongo, au yasiyo sahihi.—2 Wathesalonike 2:1, 2.

Rekebisho la Maoni Lahitajiwa

Kabla ya sehemu ya mwisho ya mwaka wa 1914, Wakristo wengi walitazamia Kristo arudi wakati huo na kuwachukua hadi mbinguni. Hivyo, katika mhadhara uliotolewa Septemba 30, 1914, A. H. Macmillan Mwanafunzi fulani wa Biblia alitaarifu hivi: “Yaelekea huu ndio mhadhara wa mwisho nitakaotoa kwa sababu tutakwenda nyumbani [mbinguni] karibuni.” Kwa wazi, Macmillan alikuwa amekosea, lakini hilo halikuwa ndilo tarajio pekee lililokuwa halijatimizwa ambalo yeye au Wanafunzi wa Biblia wenzake walikuwa nalo.

Wanafunzi wa Biblia, walioitwa Mashahidi wa Yehova tangu 1931, walitazamia pia kwamba mwaka 1925 ungepata utimizo wa unabii wa Biblia wenye kupendeza. Waliamini bila misingi yenye nguvu kwamba katika wakati huo ufufuo wa kidunia ungeanza, ukitokeza wanaume waaminifu wa kale, kama vile Abrahamu, Daudi, na Danieli. Majuzi zaidi, Mashahidi wengi walifikia mkataa kwa kukisia kwamba matukio yaliyohusianishwa na mwanzo wa Utawala wa Mileani wa Kristo huenda yangeanza kutukia katika 1975. Tazamio lao lilikuwa na msingi wa uelewevu kwamba mileani ya saba ya historia ya binadamu ingeanza wakati huo.

Maoni haya yaliyo na kosa hayakumaanisha kwamba ahadi za Mungu zilikuwa na kosa, kwamba alikuwa amekosea. Sivyo hata kidogo! Makosa au kuelewa isivyofaa, kama katika kisa cha Wakristo wa karne ya kwanza, yalikuwa kwa sababu ya ukosefu wa kutii onyo la Yesu, ‘hamjui saa ile.’ Mikataa yenye makosa ilikuwa si kwa sababu ya uovu au kukosa uaminifu kwa Kristo, bali kwa sababu ya tamaa ya moyo wote ya kuona utimizo wa ahadi za Mungu katika wakati wao wenyewe.

Kama tokeo, A. H. Macmillan alieleza baadaye hivi: “Nilijifunza kwamba twapaswa kukubali makosa yetu na kuendelea kutafuta katika Neno la Mungu ili kupata mnurisho zaidi. Haidhuru ni marekebisho yapi tutapaswa kufanya wakati fulani-fulani katika maoni, hilo halitabadili uandalizi wenye fadhili wa fidia na ahadi ya Mungu ya uhai wa milele.”

Kwa kweli, ahadi za Mungu zaweza kutumainiwa! Ni wanadamu ambao huelekea kukosa. Kwa hiyo Wakristo wa kweli watadumisha mtazamo wa kungoja kwa kutii amri ya Yesu. Wao wanafuliza kuwa macho na tayari kwa ajili ya kuja kwa Kristo kusikojulikana akiwa Mfishaji wa Mungu. Hawataruhusu matabiri ya uwongo yafifishe akili zao na kuwasababisha wapuuze onyo la kweli la mwisho wa ulimwengu.

Namna gani basi, kuhusu ile itikadi ya kwamba ulimwengu huu utakwisha? Je, kuna uthibitisho kweli kwamba utatokea muda mfupi, katika muda wa maisha yako?

[Maelezo ya Chini]

a Ona kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kurasa 138-141, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Maelezo hususa yalitabiriwa kuhusu kuanguka kwa Babiloni

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yesu hangeliweza kupanga ili kutimiza mwingi wa unabii uliomhusu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki