Vijana Huuliza. . .
Nifanye Nini Rafiki Akitumbukia Katika Matatizo?
Sherrie mwenye umri wa miaka 14 asema: “Rafiki yangu bora zaidi alipeperuka kutoka kuwa Mkristo. Hilo lanihuzunisha. Nimejaribu sana kumtia moyo!”a
JE, MTU fulani aliye na uhusiano wa karibu nawe ametumbukia katika matatizo au kuanza kufuata mtindo-maisha wenye kutilika shaka? “Nilikuwa na uhusiano wa karibu na Chris,” Johnny asema. “Tulikuwa marafiki bora sana. Siku moja alitoroka nyumbani. Hilo lilinishtua, nikahisi nikiwajibika kwenda kumtafuta. Niliendesha gari usiku kucha nikimtafuta.”
Biblia ilionya kwamba katika siku za mwisho, misongo mingi ingelemea watu, wachanga kwa wazee. (2 Timotheo 3:1-5) Kwa hiyo hatupaswi kushtuka wakati pindi kwa pindi Mkristo mchanga ajikwaa. Lakini inapotukia kwa mtu unayempenda, huenda ukapatwa na hisia nyingi zenye kufuatana, kuanzia huzuni na huruma nyororo hadi hasira. Unataka kumsaidia rafiki yako. Lakini waweza kufanyaje hivyo?
‘Naweza Kumwokoa’
Biblia husema hivi: “Yeye amrejezaye mwenye dhambi hata atoke katika njia ya upotevu, ataokoa roho [“nafsi,” New World Translation] [ya mtenda-dhambi] na mauti, na kufunika wingi wa dhambi.” (Yakobo 5:20) Lakini je, hili lamaanisha kwamba ni daraka lako kufanya hivyo? Si lazima iwe hivyo. Wazazi wa rafiki yako wana daraka la msingi juu yake. (Waefeso 6:4) Biblia huendelea kusema kwenye Wagalatia 6:1: “Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole.” Waangalizi wa kutaniko ndio hasa wanastahili kwa habari hii. Kwa hiyo wako katika hali nzuri zaidi ya kusaidia kuliko wewe.
Ni lazima utambue kwamba ukiwa kijana, huna uzoefu mwingi maishani. (Linganisha Waebrania 5:14.) Kwa hiyo kubali mapungukio yako kwa kiasi kuhusiana na jambo hili na uepuke kufanya mengi zaidi ya unayoweza kutimiza. (Mithali 11:2) Fikiria kijana aitwaye Rebekah. Yeye alijaribu kumsaidia rafiki wa kiume, mtu wa ukoo, ambaye alikuwa amejihusisha na dawa za kulevya. Yeye asimulia hivi: “Kilichonipa msongo ni kwamba yeye alinieleza yaliyokuwa moyoni mwake badala ya kueleza wazazi wake. Nilijaribu kumsaidia, lakini nilishindwa. Ilinisaidia wakati nilipogundua hatimaye singeweza kufanya lolote . . . singeweza kumwokoa.” Kisha Rebekah akamsihi atafute msaada kutoka kwa watu wazima wanaostahili.
Matthew mchanga alikuwa katika hali kama hiyo, lakini alitambua mapungukio yake mwanzoni. Yeye asema hivi kuhusu rafiki aliyekuwa katika matatizo: “Alikuwa akinijia na matatizo yake, lakini nilikuwa nikimwambia aende kwa wazazi wake. Sikutaka kuwa na daraka kwa matatizo yake.”
Jinsi Unavyoweza Kusaidia
Hilo halimaanishi kwamba huwezi kufanya lolote ili kusaidia. Mengi hutegemea hali. Labda rafiki yako ataka kukueleza yaliyo moyoni. Kwa kawaida, ungetaka kuwa mwenye kutegemeza na kusikiliza. (Mithali 18:24; 21:13) Au yaweza kuwa kwamba ameanza kufuata mtindo-maisha wenye kutilika shaka. Lingekuwa jambo lifaalo kuchukua hatua ya kwanza na kumweleza kwamba ingawa unamjali, huwezi kukubali kile anachofanya.
Hali nyingine huenda ikahusisha rafiki ambaye akiri kosa zito. Huenda hata akajaribu kukufanya uahidi kutoambia mtu yeyote. Lakini Biblia husema: “Usizishiriki dhambi za watu wengine. Ujilinde nafsi yako uwe safi.” (1 Timotheo 5:22) Ikiwa rafiki yako angekuwa mgonjwa mahututi na ahitaji msaada wa kitiba, je, hungesisitiza kumpeleka kwa daktari? Vivyohivyo, ikiwa ametumbukia katika kosa zito, yeye ahitaji msaada wa kiroho. Kuweka mambo siri kunaweza kumwua kiroho—na kuathiri kutaniko vibaya mno. Kwa hivyo una wajibu wa kuhakikisha kwamba wazee wa kutaniko wanajulishwa.—Linganisha Mambo ya Walawi 5:1.
Caroline mchanga alichukua msimamo wenye ujasiri kwa habari ya rafiki aliyepotoka ambaye alikuwa akidanganya wazazi wake. Yeye asema: “Nilimpatia majuma mawili kwenda kwa wazee. Ikiwa hangekwenda, nilimwambia ningewaendea. Hili halikuwa rahisi kwangu kufanya.” Johnny, aliyetajwa mwanzoni, alionyesha nguvu kama hiyo ya kiutu. Kuhusu rafiki yake, Johnny akumbuka hivi: “Nilishangaa kupata kwamba alikuwa akiishi na msichana. Kulikuwa na jamaa wengine hapo wakinywa na kuvuta sigareti.” Johnny alimwomba rafiki yake atoke nje kisha akadokeza kwa mkazo kwamba atafute msaada kutoka kwa wazee kutanikoni.
Huenda rafiki yako athamini au asithamini jitihada zako. Biblia yatueleza kwamba ndugu zake walipojihusisha katika kutenda makosa, kijana Yusufu “akamletea baba yao habari zao mbaya.” Hili kwa hakika halikufanya apendwe na ndugu zake. Kwa kweli, “wakamchukia.”—Mwanzo 37:2-4.
Kutenda Kana Kwamba Mambo Ni Sawa?
Ingawa hivyo ungekuwa ukiharibu jitihada zako za kusaidia, ikiwa ungeendelea kushirikiana na rafiki yako kana kwamba hakuna kitu kilikuwa kimetukia. Kwenye 1 Wakorintho 15:33, mtume Paulo alionya Wakristo dhidi ya kushirikiana na watenda makosa. Ushirika wa karibu na watu kama hao waweza tu kukuangusha!
Mollie mchanga alijifunza hili kwa njia ngumu wakati rafiki yake Sally alipoanza kupeana miadi ya kijinsia kisiri. Sally hakuwa tu mchanga mno kuolewa bali alikuwa akipeana miadi ya kijinsia na wavulana ambao hawakuwa Wakristo. Mollie alipuuza hali hiyo na kuendelea kushirikiana na rafiki yake. Tokeo lilikuwa nini? Mollie asema hivi: “Hatimaye, Sally alinipangia mvulana wa kilimwengu wa kufanya naye miadi, kisha tukaenda kwenye miadi.” Jambo zuri ni kwamba Mollie alipata msaada kutoka wazee wa kutaniko kabla ya hali kuwa mbaya zaidi.
Lynn vilevile aliridhiana kwa njia ya kuhatarisha ili kudumisha urafiki wake na msichana fulani aliyeitwa Beth. “Nilihisi kwamba ningeweza kumwokoa,” akumbuka Lynn, “lakini haikuwezekana. Nilikwenda kwenye vilabu vya usiku pamoja naye. Nilijua lilikuwa kosa, lakini sikutaka kumuumiza. Matatizo yake yakaanza kunilemea. Nilinyamaza kuhusu jambo hilo, nikifikiri kwamba hilo tatizo lingekwisha, lakini likazidi kuwa kubwa.” Msiba ulimshtua Lynn. Rafiki yake, Beth aliuawa na kijana aliyekuwa akipeana miadi ya kijinsia naye.
Kushikamana na rafiki huenda kukaonekana kuwa jambo bora. Lakini ikiwa rafiki yako angekuwa akizama kihalisi katika kizingia cha maji chenye nguvu, je, ungeruka ndani mwenyewe? Hilo lingefanya nyote wawili mfe maji. Jambo la akili kufanya lingekuwa kumrushia kiokoa uhai. Vivyohivyo, unahitaji kutoa msaada kwa umbali fulani.—Yuda 22, 23.
Kuwa mbali ni kwa lazima ikiwa rafiki yako anaondoshwa kutanikoni. Amri ya Biblia ni kwamba ‘usichangamane’ na huyo. (1 Wakorintho 5:11) Ingawa bado unamjali huyo, unaweza kumsaidia vyema kabisa, si kwa kumfuata katika kutenda kosa, bali kwa kuonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova. (Zaburi 18:25) Msimamo wako usioridhiana huenda ukawa tendo muhimu ambalo litamsukuma kufikiria tena matendo yake. La maana hata zaidi, uaminifu-mshikamanifu wako utamfurahisha Yehova.—Mithali 27:11.
Mzigo Wenye Kulemea
Ingawa hivyo, mara nyingi majaribio ya mtu ya kusaidia hukosa kufaulu. Rebekah akumbuka hivi kuhusu rafiki yake: “Nilijaribu kumsaidia. Hata nilimwandikia barua, lakini hakuijibu kamwe.” Caroline alipata kwamba baada ya miezi mingi ya kujaribu kumsaidia rafiki yake ambaye alikuwa akijihatarisha, yeye “alianza kuhisi mkazo.”
Ni jambo la maana kutambua kwamba “kila mtu miongoni mwetu atatoa habari zake mwenyewe mbele za Mungu.” (Warumi 14:12) Na ingawa inafaa kumsaidia mtu fulani kubeba mizigo yake, au matatizo ya kibinafsi, kwa kutoa msaada wa kihalisi, ni jambo ambalo haliwezekani kubeba “furushi” la mtu mwingine—yaani, daraka lake kumwelekea Mungu. “Kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe,” yasema Biblia. (Wagalatia 6:5) Wewe huna daraka juu ya machaguo anayofanya rafiki yako.
Hata hivyo, kumwona rafiki akiharibu maisha yake huleta maumivu. Kijana aitwaye Mike asema hivi kuhusu kumpoteza rafiki yake: “Lilinihuzunisha mno. Nilikuwa na uhusiano wa karibu sana na Mark na wazazi wake. Nilipatwa na mshuko-moyo.”
Ni jambo la kawaida kuhuzunikia potezo kama hilo. Hata hivyo, kuzungumza kuhusu hisia zako na mtu fulani unayemtumaini kwaweza kusaidia. (Mithali 12:25) “Kwa msaada wa wazazi wangu,” asema Rebekah, “niliweza kushinda hali hiyo.” Waweza pia kumwaga hisia zako kwa Yehova Mungu kupitia kwa sala. (Zaburi 62:8) Caroline ajumuisha hali vizuri kwa kusema hivi: “Kusali kwa Yehova na kuhubiria wengine kulinisaidia sana. Pia niliwakaribia wengine kutanikoni, hasa wanawake wazee-wazee. Nilitambua hatimaye kwamba watu wanatozwa hesabu kwa matendo yao wenyewe na kwamba nilihitaji kuendelea na maisha yangu.” Kwa kufanya yote hayo, kwa hakika utajisaidia. Na labda waweza kumsaidia rafiki yako aliyepotoka pia.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mtie moyo rafiki yako atafute msaada