Linda Dhidi ya Kutopenda Kusoma
AINA mpya ya tatizo la kusoma inaathiri ulimwengu wetu kwa kadiri kubwa. Hilo ni kutopenda kusoma. Hilo hufafanuliwa kuwa “ubora au hali ya kujua kusoma lakini kutopendezwa kufanya hivyo.” (Merriam-Webster’s Collegiate Dictionary, Tenth Edition) Ndiyo, kusoma—ambako wakati mmoja watu walijihusisha nako kukiwa jambo la kufurahisha—sasa mara nyingi husukumiwa mbali kama kwamba ni kazi. “Ni lazima ujikakamue ili uweze kusoma,” akalalamika msichana mmoja mwenye umri wa miaka 12, “na hilo halifurahishi.”
Watu wazima wengi ni wenye kutopenda kusoma pia. Kwa kielelezo, Marekani hudai kwa majivuno kwamba ina kiwango cha kujua kusoma na kuandika cha asilimia 97; hata hivyo, nusu hivi ya watu wazima wa Marekani husoma vitabu au magazeti mara chache! Kwa wazi, uwezo wa kusoma sikuzote haulinganishwi na tamaa ya kusoma. Hili ni kweli hata miongoni mwa watu wenye elimu ya juu. “Ninapokuja nyumbani nikiwa nimechoka kutokana na siku yenye kazi ngumu,” asema mhitimu fulani wa Chuo Kikuu cha Harvard, “mimi huwasha televisheni badala ya kuchukua kitabu. Hilo ni rahisi zaidi.”
Ni nini kimepata usomaji? Katika miongo ya majuzi umashuhuri wao umeshindwa na vyombo vya habari vyenye kuvuta uangalifu. “Kwa kuwa sasa tuna MTV (idara ichezayo muziki saa 24 kwa siku)—mashine za vidio na Nintendo (michezo ya vidio) na Walkman—taraja la kusoma vitabu kwa jasho halionekani kuwa rahisi kama lilivyokuwa katika nyakati ambako hakukuwa na maendeleo sana,” aandika Stratford P. Sherman katika gazeti Fortune. Labda mshindani wa kusoma mwenye kutumia wakati mno ni televisheni. Kwa hakika, kufikia umri wa miaka 65 Mmarekani wa wastani atakuwa ametumia miaka tisa ya maisha yake akitazama televisheni!
Kwa kuwa thawabu za kusoma hudhabihiwa mara nyingi kwa televisheni, lingekuwa jambo zuri kufikiria yafuatayo.
Manufaa za Kusoma
Kusoma huchochea kuwazia. Televisheni hufikiri kwa niaba yako. Kila kitu kinawekwa wazi: ishara za uso, badiliko la sauti, na mandhari.
Hata hivyo, kwa kusoma, unachagua kikundi cha waigizaji, unatayarisha jukwaa, na kuelekeza mchezo. “Una uhuru mwingi mno,” asema mvulana mwenye umri wa miaka 10. “Unaweza kufanya kila mhusika aonekane barabara vile utakavyo aonekane. Una udhibiti zaidi wa mambo unaposoma kitabu kuliko unapoona kitu kwenye televisheni.” Kama Dakt. Bruno Bettelheim alivyoonelea, “televisheni huteka uwazio lakini haiuwachi huru. Kitabu kizuri mara moja huchochea na kuacha huru akili.”
Kusoma hukuza stadi za usemi. “Hakuna mtoto au mtu mzima huwa mtazamaji bora zaidi wa televisheni kwa kuitazama zaidi na zaidi,” aonelea Reginald Damerall wa Chuo Kikuu cha Massachusetts. “Stadi zinazohitajiwa kutazama televisheni ni za kawaida mno hivi kwamba hatujapata kusikia juu ya tatizo la kutoweza kutazama televisheni.”
Kwa kutofautisha, kusoma huhitaji na hukuza stadi za usemi; huo hushikamanishwa kabisa na usemi na kuandika. Asema mwalimu mmoja wa somo la Kingereza wa shule ya sekondari: “Ni jambo la hakika kwamba kufanikiwa kwako ukiwa mwanafunzi hutegemea kwa sehemu kubwa msamiati wako, katika kile unachoweza kufahamu unaposoma na katika jinsi unavyosababu unapoandika, na hakuna namna unavyoweza kujenga msamiati mzuri isipokuwa kwa kusoma—hakuna kabisa.”
Kusoma hukuza subira. Zaidi ya picha elfu moja zaweza kumweka kwenye kiwambo cha televisheni kwa saa moja tu, ikimwachia mtazamaji wakati mchache wa kuwazia kile anachoona. “Ufundi huu kihalisi hufanyiza kipindi kifupi cha uwezo wa mtu wa kukaza fikira,” asema Dakt. Matthew Dumont. Haishangazi, chunguzi fulani huhusianisha kutazama televisheni kupita kiasi na kufanya maamuzi kwa ghafula na kukosa utulivu—katika watoto na watu wazima.
Kusoma huhitaji subira. “Sentensi, mafungu, na kurasa hufunuka polepole, kwa mfuatano, na kulingana na akili ambayo kwa hakika si hali ya ghafula tu bila kufikiri,” aandika mtaalamu wa mawasiliano Neil Postman. Kwa mwendo wake mwenyewe, msomaji lazima afasiri, achanganue, na kuwaza juu ya kile kilichoko ukurasani. Kusoma ni utaratibu tata wa kufasiri mambo yaliyofichika ambao hudai—na hukuza—subira.
Maoni Yaliyosawazika
Licha ya manufaa za kusoma, ni lazima ikubaliwe kwamba televisheni ina faida zayo pia. Inaweza kupita kusoma katika kuwasilisha namna fulani za habari.a Utoaji wenye kuvutia wa televisheni waweza kuchochea upendezi katika kusoma. “Inaripotiwa kwamba programu za televisheni ziigizazo fasihi ya watoto na sayansi huchochea watoto watafute vitabu juu ya vichwa hivyo na vichwa vinavyohusiana,” yasema The Encyclopedia Americana.
Maoni yaliyosawazika ni ya muhimu. Vichapo na televisheni ni njia mbili tofauti za kupitisha uwasiliano. Kila moja ina nguvu za kawaida na mapungukio. Kila moja yaweza kutumiwa vizuri—au kutumiwa vibaya. Ndiyo, kusoma kupita kiasi kufikia kiwango cha kujitenga kwaweza kuwa kwenye uharibifu kama kutazama televisheni kupita kiasi.—Mithali 18:1; Mhubiri 12:12.
Hata hivyo, mara nyingi kusoma hupuuzwa huku kipitisha wakati kinachotazamwa kikipendelewa zaidi. Mleta-habari mmoja Mjapani alalamika hivi: “Tunabadilika kutoka utamaduni wa wasomaji kuingia ule wa watazamaji.” Hili laonwa hasa miongoni mwa vijana. Likiwa tokeo, wengi wao hukua wakiwa wasiopenda kusoma na baadaye hupatwa na matokeo mabaya. Kwa hivyo, wazazi wanaweza kusaidiaje watoto wao wakuze tamaa ya kusoma?
Jinsi Wazazi Wawezavyo Kusaidia
Weka kielelezo. Makala moja ya Newsweek iliyokuwa na kichwa “Jinsi ya Kukuza Wasomaji Wazuri” hutoa onyo hili la moja kwa moja: “Ikiwa wewe ni mtu atumiaye wakati mwingi mno mbele ya televisheni, yaelekea mtoto wako atakuwa hivyo, pia. Kwa upande ule mwingine, ikiwa watoto wako wanakuona umejikunja kwa furaha ukiwa na kitabu kizuri, watapata wazo la kwamba hauhubiri tu manufaa za kusoma, bali unafanya hivyo vilevile.” Vyema hata zaidi, wazazi fulani husomea watoto wao vitabu kwa sauti kubwa. Kwa kufanya hilo, wao hukuza kifungo kichangamfu—kitu ambacho, kwa kuhuzunisha kinakosekana katika familia nyingi leo.
Anzisha maktaba. “Uwe na vitabu karibu—vitabu vingi mno,” apendekeza Dakt. Theodore Isaac Rubin. “Nakumbuka nikivisoma kwa sababu vilipatikana na kwa sababu kila mtu alikuwa akivisoma, pia.” Watoto watasoma ikiwa vitabu vyapatikana kwa urahisi. Kichocheo cha kusoma kitakuwa kikubwa hata zaidi ikiwa vitabu vinakuwa sehemu ya maktaba yao wenyewe ya kibinafsi.
Fanya kusoma kufurahishe. Imesemwa kwamba ikiwa mtoto apenda kusoma, umeshinda nusu ya pigano la kujifunza. Kwa hiyo fanya kusoma kuwe ono lenye kufurahisha kwa mtoto wako. Jinsi gani? Kwanza, weka mipaka kwa wakati wa televisheni; sikuzote itaelekea kushinda usomaji. Pili, fanyiza mazingira ambayo yanafaa kwa kusoma; nyakati na mahali patulivu, kama vile maktaba ya kibinafsi yenye nuru nzuri, hukaribisha kusoma. Tatu, usilazimishe kusoma. Fanya habari na fursa za kusoma zipatikane, kisha uache mtoto akuze tamaa.
Wazazi fulani huanza kuwasomea watoto wao vitabu katika umri mchanga. Hili laweza kuwa na manufaa. Wataalamu fulani husema kwamba kufikia umri wa miaka mitatu, mtoto hufahamu sehemu kubwa ya lugha atakayotumia katika mazungumzo ya kawaida ya watu wazima—hata ingawa hawezi bado kueleza maneno haya kwa ufasaha. “Watoto huanza kujifunza kufahamu lugha mapema zaidi na kwa kiwango cha haraka zaidi kuliko wajifunzavyo kuitumia kwa usemi,” chasema kitabu The First Three Years of Life. Biblia husema hivi kumhusu Timotheo: “Tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu.” (2 Timotheo 3:15) Neno kitoto hurudi nyuma hadi kwenye neno la Kilatini infans, ambalo kihalisi humaanisha “asiyeongea.” Ndiyo, Timotheo alisikiliza maneno ya kimaandiko muda mrefu kabla ya kuweza kuyaongea.
Biblia—Msaada Bora Zaidi
“Biblia ni mkusanyo mkubwa mno wa vitabu vya fasihi,” chasema kitabu The Bible in Its Literary Milieu. Kwa hakika, vitabu vyayo 66 vina namna za kishairi, nyimbo, na masimulizi ya kihistoria ambayo kutoka kwayo wachanga kwa wazee wanaweza kujifunza. (Warumi 15:4) Isitoshe, Biblia ni ‘yenye pumzi ya Mungu, yafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki.’—2 Timotheo 3:16.
Ndiyo, habari ya kusoma iliyo muhimu zaidi ipatikanayo ni Neno la Mungu, Biblia. Kukiwa na sababu nzuri kila mfalme wa Israeli alihitajiwa kuwa na nakala yake binafsi ya Maandiko na “asome humo siku zote atakazoishi.” (Kumbukumbu la Torati 17:18, 19) Na Yoshua aliamriwa asome maandiko “kwa sauti ya chini”—yaani, ajisomee, kwa sauti nyororo—“mchana na usiku.”—Yoshua 1:8, NW.
Inakubalika kwamba sehemu fulani za Biblia si rahisi kusoma. Huenda zikadai kukaza fikira. Kumbuka, Petro aliandika: “Kama watoto wachanga sana waliozaliwa karibuni, fanyizeni hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya lile neno.” (1 Petro 2:2, NW) Kwa mazoezi, mtazamo kuelekea “maziwa” ya Neno la Mungu waweza kuwa wa kawaida kama hamu ya kiasili ya kitoto kikitaka maziwa ya mama yacho. Uthamini wa kusoma Biblia waweza kusitawishwa.b Unastahili jitihada itakayofanywa. “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu,” akaandika mtunga-zaburi. (Zaburi 119:105) Je, sote hatuhitaji mwongozo huo katika nyakati zetu zenye taabu?
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kutambua hili, Watch Tower Society katika miaka ya majuzi imeongeza utokezaji wayo wa habari iliyochapishwa kwenye kaseti za vidio juu ya habari mbalimbali zinazohusiana na Biblia.
b Ili kusaidia watoto wafanyize hamu sana ya ujuzi wa Biblia, Watch Tower Society imetokeza misaada ya Biblia iliyorahisishwa, kama vile Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na Kumsikiliza Mwalimu Mkuu. Vitabu vyote viwili vyapatikana pia kwenye kaseti.