Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 6/22 kur. 11-13
  • Kwa Nini Siwezi Kujifunza?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Siwezi Kujifunza?
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ugumu wa Kukabiliana Nalo
  • Jifunze Kukaza Fikira
  • Kupunguza Hali ya Kutotulia
  • Dumisha Kujistahi Kwako
  • Jitihada za Kutafuta Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2020
  • Kuwasaidia Watoto Wenye Matatizo ya Kujifunza
    Amkeni!—2009
  • Nifanyeje Nisipofanikiwa?
    Amkeni!—2004
  • Kuna ubaya gani kuwa na uhusiano wa siri?
    Amkeni!—2007
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 6/22 kur. 11-13

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Siwezi Kujifunza?

“Sikutaka kurudi nyumbani,” akumbuka Jessica, “na kukabili wazazi wangu. Kwa mara nyingine tena nilikuwa nimeanguka kozi kadhaa.”a Akiwa na umri wa miaka 15, Jessica ni mwerevu na mrembo. Lakini sawa na vijana wengi, ana tatizo sana kupita kozi ya shule.

KUTOFANYA vema shuleni mara nyingi ni matokeo ya mtazamo mbaya kuelekea elimu au kumwelekea mwalimu wa mtu. Lakini sivyo ilivyo na Jessica. Yeye huona ikiwa vigumu sana kushika mambo ya kuwaziwa. Kwa kawaida, hili lilifanya iwe vigumu kwa Jessica kufanikiwa katika somo la hisabati. Na ugumu katika kusoma ulifanya iwe vigumu kwake kufanya vema katika masomo yake mengine.

Maria kwa upande ule mwingine, hawezi kuendeleza herufi kwa usahihi. Sikuzote yeye huficha maandishi ambayo yeye huandika katika mikutano ya Kikristo kwa sababu anaonea aibu makosa yake ya mwendelezo wa herufi. Hata hivyo, wala Jessica wala Maria si wajinga. Jessica ni mwenye ustadi katika kushughulika na watu hivi kwamba yeye hutumikia akiwa mpatanishi aliyewekwa rasmi na shule, au mtatuzi wa matatizo, taabu inapozuka kati ya wanashule wenzake. Na kimasomo Maria yuko katika asilimia 10 ya wanafunzi wenye gredi bora zaidi katika darasa lake.

Tatizo: Jessica na Maria wana matatizo ya kujifunza. Wataalamu huamini kwamba asilimia zipatazo 3 hadi 10 za watoto wote huenda zikawa na matatizo kama hayo katika kujifunza. Tania, ambaye sasa yuko katika umri wa miaka ya 20, anatatizika kwa kile kiitwacho Tatizo la Upungufu wa Makini Kutokana na Utendaji wa Kupita Kiasi (ADHD).b Yeye asema: “Nina tatizo kubwa na mikutano ya Kikristo, funzo la kibinafsi, na sala kwa sababu ya ukosefu wangu wa uwezo wa kukaza uangalifu au hata kuketi tuli. Huduma yangu inaathiriwa kwa sababu mimi huruka kutoka kichwa hiki hadi kingine haraka sana hivi kwamba hakuna mtu awezaye kufuatana nami.”

Wakati ambapo halifuatiwi na utendaji wa kupita kiasi, tatizo hilo huitwa Kasoro ya Upungufu wa Makini (ADD). Watu wenye tatizo hili mara nyingi hufafanuliwa kuwa waota-ndoto za mchana. Kuhusu wale wenye ADD, mtaalamu wa mfumo wa neva Dakt. Bruce Roseman alisema: “Wao huketi mbele ya kitabu kwa dakika 45, na hawajifunzi chochote.” Kwa sababu fulani-fulani ni vigumu kwao kukaza fikira.

Watafiti wa kitiba huamini kwamba hivi majuzi wameanza kufahamu kile kinachosababisha matatizo haya. Hata hivyo, mambo mengi bado hayajulikani. Na mipaka kati ya matatizo tofauti-tofauti na upungufu ambao huzuia kujifunza haiko wazi sikuzote. Licha ya kisababishi hususa au jina linalopewa tatizo hususa—iwe ni tatizo kuhusiana na kusoma, kukumbuka, kukaza uangalifu, au kuwa mtendaji kupita kiasi—tatizo hilo laweza kuvuruga elimu ya mtu na kusababisha kuteseka sana. Ikiwa una tatizo la kujifunza, waweza kukabilianaje nalo?

Ugumu wa Kukabiliana Nalo

Fikiria Jessica, aliyetajwa katika utangulizi. Akiwa ameazimia kushinda tatizo lake la kusoma, aliendelea kujaribu kusoma vitabu tofauti. Badiliko kubwa lilikuja wakati alipopata kitabu cha mashairi kilichovuta uangalifu wake. Alipata kitabu kama hicho, ambacho alifurahia kukisoma pia. Baadaye akaja kupendezwa na vitabu fulani vya hadithi, na hatua kwa hatua kusoma kukaja kuwa tatizo lisilo zito sana. Somo la kujifunza hapo ni kwamba udumifu huleta matokeo mazuri. Wewe pia waweza kushinda tatizo la kujifunza au waweza angalau kufanya maendeleo makubwa upande huo kwa kutoacha.—Linganisha Wagalatia 6:9.

Namna gani kushughulika na tatizo la kumbukumbu la muda mfupi? Ufunguo wa maana wa kutatua tatizo hili uko katika msemo wa kale: “Kurudia-rudia ndiko chanzo cha kudumisha habari.” Nicky alipata kwamba kujirudia-rudia kwa sauti alichosikia na kusoma kulimsaidia kukumbuka mambo. Jaribu hilo. Huenda kukakusaidia pia. Kwa kupendeza, katika nyakati za Biblia watu walizoea kutamka maneno, hata walipokuwa wakijisomea. Hivyo, Yehova alimwamuru mwandikaji wa Biblia Yoshua: “Ni lazima usome kwa sauti ya chini [Sheria ya Mungu] mchana na usiku.” (Yoshua 1:8, NW; Zaburi 1:2) Kwa nini kutamka maneno kulikuwa kwa maana sana? Kwa sababu kufanya hivyo kulihusisha hisi mbili—ya kusikia na ya kuona—nako kulisaidia kuacha mkazo wa kina akilini mwa msomaji.

Kwa Jessica, kujifunza hisabati kulikuwa kazi kubwa mno pia. Hata hivyo, alijaribu kujifunza sheria za hisabati kwa kuzirudia-rudia—nyakati fulani akitumia wakati mwingi mno kama nusu saa kwa sheria moja. Jitihada zake hatimaye zilileta matokeo mazuri. Kwa hiyo rudia, rudia, rudia! Zoea la hekima ni kuwa na karatasi na kalamu karibu nawe unaposikiliza darasani au kusoma ili uandike maandishi.

Ni jambo la muhimu kwamba ujitoe kikamili ili ujifunze. Fanya liwe zoea kubaki baada ya shule na kuzungumza na walimu wako. Wajue. Waeleze kwamba una tatizo la kujifunza lakini kwamba unaazimia kulishinda. Walimu wengi watakuwa na hamu ya kusaidia. Kwa hiyo pata msaada wao. Jessica alifanya hivyo na kupata utegemezo uliohitajiwa sana kutoka kwa mwalimu mwenye hisia-mwenzi.

Jifunze Kukaza Fikira

Husaidia pia kuwa na mpango wa kujiwekea mradi na wa kujithawabisha. Kuweka mradi hususa—kama vile kumaliza sehemu ya mgawo wa masomo ya nyumbani—kabla ya kujithawabisha kwa kuwasha televisheni au muziki uupendao sana kwaweza kukuhamasisha kukaza fikira. Hakikisha kwamba miradi unayoweka ni ya kiasi.—Linganisha Wafilipi 4:5.

Nyakati fulani kufanya mabadiliko yenye kuchochea maendeleo katika mazingira yako kwaweza kusaidia. Nicky alipanga kuketi mbele darasani karibu na mwalimu ili akaze fikira vema zaidi. Jessica alipata ikinufaisha kufanya mgawo wa masomo ya nyumbani pamoja na rafiki mwenye bidii ya kujifunza. Huenda ukapata ikisaidia kufanya tu chumba chako kiwe chenye kustarehesha.

Kupunguza Hali ya Kutotulia

Ikiwa waelekea kuwa mwenye utendaji wa kupita kiasi, kujifunza kwaweza kuwa pitio lenye maumivu sana. Hata hivyo, wataalamu fulani husema kwamba utendaji wa kupita kiasi waweza kuelekezwa katika mazoezi ya kimwili. “Uthibitisho waongezeka,” lataja U.S.News & World Report, “kwamba uwezo wa kila mtu kushika habari mpya na kukumbuka ya kale unaboreshwa na mabadiliko ya kibiolojia katika ubongo yanayotokezwa na mazoezi ya mwili.” Hivyo, viwango vya kiasi vya mazoezi—kuogelea, kukimbia, kucheza mpira, kuendesha baiskeli, kuteleza barafuni, na kadhalika—vyaweza kuwa na matokeo mazuri kwa mwili na akili.—1 Timotheo 4:8.

Kwa kawaida wale wenye matatizo ya kujifunza hupewa dawa. Yadaiwa kwamba asilimia 70 hivi ya vijana wenye ADHD ambao wamepewa dawa-chochezi wameitikia. Iwe utakubali tiba ya dawa ni jambo la wewe na wazazi wako kuamua baada ya kufikiria uzito wa tatizo, athari mbaya ziwezazo kutokea, na mambo mengineyo.

Dumisha Kujistahi Kwako

Ingawa ugumu katika kujifunza hauonwi kuwa tatizo la kihisia-moyo, waweza kuwa na matokeo ya kihisia-moyo. Mchanganyiko wa kukataliwa na kudhihakiwa kwa daima na wazazi na walimu, matokeo mabaya au ya chini ya shuleni, na ukosefu wa marafiki waweza kwa urahisi kushusha kujistahi. Vijana fulani huficha hisia hizi kwa kuenenda kwa njia ya hasira na ya kutisha.

Lakini si lazima upoteze kujistahi kwa sababu ya matatizo ya kujifunza.c “Lengo langu,” asema mtaalamu mmoja ashughulikaye na watoto wenye matatizo ya kujifunza, “ni kubadili mtazamo wao kuelekea maisha—kutoka ‘mimi ni mjinga, na siwezi kufanya chochote vizuri’ . . . hadi ‘ninashinda tatizo, nami naweza kufanya mengi zaidi kuliko nilivyopata kufikiri ningeweza.’”

Ingawa huwezi kufanya mengi kuhusu mtazamo wa wengine, unaweza kuathiri mtazamo wako mwenyewe. Jessica alifanya hivyo. Yeye asema: “Nilipojihukumu kwa kutegemea kile walichosema watoto shuleni na kuniita-ita majina nilitaka kutoroka shule. Lakini sasa najaribu kupuuza wanachosema na kufuliza kufanya niwezalo. Ni vigumu, nami ni lazima niendelee kujikumbusha, lakini ni suluhisho lenye mafanikio.”

Jessica alilazimika kushindana na uhalisi mwingine. Ndugu yake mkubwa alikuwa mwanafunzi bora zaidi akiwa na gredi za A. “Hili lilikuwa likiharibu kujistahi kwangu,” asema Jessica, “hadi nilipoacha kujilinganisha naye.” Kwa hiyo usijilinganishe na ndugu zako.—Linganisa Wagalatia 6:4.

Kuzungumza na rafiki mwenye kutumainiwa kutakusaidia pia kuona mambo kwa maoni yafaayo. Rafiki wa kweli atashikamana nawe kwa uaminifu-mshikamanifu huku ukijaribu kujiboresha. (Mithali 17:17) Rafiki asiye wa kweli, kwa upande ule mwingine, ama atakurarua au kukupa maoni yaliyokwezwa isivyofaa kukuhusu. Kwa hivyo chagua marafiki wako kwa uangalifu.

Ikiwa una tatizo la kujifunza, yaelekea utapata kusahihishwa zaidi kuliko vijana wengine. Lakini usiruhusu hilo likupe maoni hasi kukuhusu. Tazama nidhamu kwa njia ya kimungu, kama kitu chenye thamani kubwa. Kumbuka nidhamu inayotolewa na wazazi wako ni uthibitisho kwamba wanakupenda na kwamba wanakutakia mema.—Mithali 1:8, 9; 3:11, 12; Waebrania 12:5-9.

La, si lazima matatizo yako ya kujifunza yakuvunje moyo. Unaweza kufanya jambo fulani kuyahusu na kuishi maisha yenye matokeo. Lakini kuna sababu kubwa hata zaidi ya kuwa na tumaini. Mungu ameahidi kuleta ulimwengu mpya wa uadilifu ambao katika huo ujuzi utajaa na katika huo kila tatizo la akili na mwili litarekebishwa. (Isaya 11:9; Ufunuo 21:1-4) Kwa hiyo azimia kujifunza mengi zaidi juu ya Yehova Mungu na makusudi yake, na utende kwa kupatana na ujuzi huo.—Yohana 17:3.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Tafadhali ona mfululizo “Kuwaelewa Watoto Wagumu” katika toleo la Amkeni! la Novemba 22, 1994, na makala “Je, Mtoto Wako Ana Matatizo ya Kujifunza?” katika toleo la Mei 8, 1983, la Kiingereza.

c Ona makala “Vijana Huuliza . . . Naweza Kusitawishaje Hali ya Kujiheshimu Mwenyewe?” katika toleo la Amkeni! la Septemba 1984.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Jitoe kikamili ili ujifunze

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki