Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 12/8 kur. 14-15
  • Ujitiisho wa Mke—Wamaanisha Nini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ujitiisho wa Mke—Wamaanisha Nini?
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ufahamu Wahitajiwa
  • Mume Anapoepuka Daraka
  • “Ujitiisho Kuelekea Mmoja na Mwenzake”
  • Ujitiisho Katika Ndoa Humaanisha Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Alitenda kwa Busara
    Igeni Imani Yao
  • Alitenda kwa Busara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • “Kichwa cha Mwanamke Ni Mwanamume”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 12/8 kur. 14-15

Maoni ya Biblia

Ujitiisho wa Mke—Wamaanisha Nini?

NENO LA MUNGU, Biblia, hutaarifu hivi kwenye Waefeso 5:22: “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana.” Hili lamaanisha nini hasa? Je, ni lazima mke akubali kila kitu anachotaka mume, haidhuru ni nini? Je, hawezi kamwe kutumia busara yake mwenyewe au kuwa na maoni yaliyo tofauti na ya mume?

Fikiria simulizi la Biblia la Abigaili. Yeye alitenda kwa hekima lakini kinyume cha matakwa ya mume wake mwenye mali, Nabali. Licha ya fadhili aliyoonyeshwa Nabali na wafuasi wa Daudi, ambaye ndiye aliyekuwa chaguo la Mungu kuwa mfalme wa Israeli, Nabali alikuwa ‘amewatukana.’ Daudi, akiwa ameghadhabishwa na ukosefu wa shukrani wa Nabali alikuwa tayari kumwua Nabali. Abigaili alitambua kwamba nyumba yake yote ilikuwa hatarini. Akamfanya Daudi apoe hasira. Jinsi gani?—1 Samweli 25:2-35.

Abigaili alikiri kwa Daudi kwamba Nabali alikuwa “mtu asiyefaa” akampa Daudi maandalizi ambayo Nabali alikuwa ameyazuilia. Kwa kawaida, ni makosa kwa mume au mke kutangaza hadharani kasoro za mwenzi. Je, Abigaili alikuwa mwasi katika kusema na kutenda kwa njia hii? La. Alikuwa akijaribu kuokoa maisha ya Nabali na ya nyumba yake. Hakuna dokezo kwamba alifanya tendo la kukosa staha au la kujitegemea. Wala Nabali aliye mgumu kupendeza hakuwa ameonyesha kutoridhika na njia ambayo Abigaili alishughulikia shamba lake kubwa. Lakini katika hali hii yenye tatizo, hekima ilimwongoza Abigaili atumie busara yake mwenyewe. Isitoshe, Biblia husema kwa kuunga mkono kile alichofanya Abigaili.—1 Samweli 25:3, 25, 32, 33.

Muda mrefu kabla ya siku ya Abigaili, kulikuwa na nyakati ambapo wake wa wazee wa ukoo walidhihirisha maoni na kuchukua hatua tofauti na walizotaka waume zao. Hata hivyo, hawa “wanawake watakatifu waliomtumaini Mungu” wanaonwa kuwa violezo vya kufuatwa vya ujitiisho wa mke Mkristo. (1 Petro 3:1-6) Kwa kielelezo, wakati Sara alipohisi kwamba mwana wa Abrahamu Ishmaeli alikuwa amekuwa tisho kwa mwana wao, Isaka, aliamua kwamba Ishmaeli afukuzwe. Hili lilikuwa “baya sana machoni pa Ibrahimu.” Lakini Mungu alimwambia Abrahamu: “Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana . . . Kila akuambialo Sara sikiza sauti yake.”—Mwanzo 21:11, 12.

Ufahamu Wahitajiwa

Basi, halingekuwa jambo la hekima kwa mke kuhisi akiwa amesongwa kufanya kitu ambacho ajua hakina hekima kabisa au kinachopinga kanuni za kimungu, eti kwa sababu anajitiisha. Wala hapaswi kufanywa ahisi akiwa na hatia kwa kuchukua hatua ya busara katika jambo fulani muhimu, kama walivyofanya Abigaili na Sara.

Ujitiisho wa mke haumaanishi kwamba ni lazima mke sikuzote akubaliane na kila kitu anachotaka mume. Tofauti ni nini? Wakati kanuni zifaazo zinapokuwa hatarini, anaweza kulazimika kutoafikiana na mume wake. Hata hivyo, bado apaswa kudhihirisha roho ya jumla ya ujitiisho wa kimungu.

Bila shaka, mke apaswa kuwa mwangalifu asipuuze matakwa ya mume wake kwa sababu yeye anataka iwe hivyo, kwa chuki au nia nyinginezo mbaya. Apaswa kuwa mwenye ufahamu, “mwenye akili njema,” kama alivyokuwa Abigaili.—1 Samweli 25:3.

Mume Anapoepuka Daraka

Lengo kuu na msukumo wa ujitiisho wa kimungu wa mke ni kumpendeza Yehova kwa kushirikiana na mume wake na kuunga mkono maamuzi yake. Hili ni rahisi zaidi ikiwa mume ni mkomavu kiroho. Laweza kuwa gumu ikiwa sivyo alivyo.

Kwa habari hii, anaweza kukabilije hali? Anaweza kumsihi sana au kudokeza ni maamuzi gani yatanufaisha familia zaidi. Akimwacha ‘aongoze meli,’ huenda akapata ustadi zaidi wa kufanya hivyo. Kumnung’unikia mume daima hupinga roho ya ujitiisho ufaao. (Mithali 21:19) Hata hivyo, ikiwa hali-njema ya familia imo hatarini kabisa kulingana na sera ya mume, mke aweza kuchagua kupendekeza, kama alivyofanya Sara, mwendo ulio sahihi.

Ikiwa mume si mwamini, ugumu kwa mke ni mkubwa hata zaidi. Hata hivyo, apaswa kujitiisha mradi hamwambii avunje sheria za Biblia. Akifanya hivyo, itikio la mke Mkristo lapasa kuwa kama lile la wanafunzi wakati mahakama ilipowaagiza wavunje amri za Mungu: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

Hata hivyo, kwa sababu ya kukosa uzoefu na kuwa na hekima chache, hata waume na wake wenye nia njema wanaweza kukiuka mafungu yao. Mume huenda akakosa ufikirio; huenda mke akasisitiza mno mapendezi yake. Ni nini kitakachosaidia? Maoni yenye kiasi kujihusu ni ya maana kwa wote, kwa kuwa “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi.”—Yakobo 3:2.

Wanaume wengi watathamini hatua ya busara ya mke ikiwa aitumia kwa hekima. Na ushirikiano unaimarishwa ikiwa wote wanaomba radhi wanapofanya makosa. Kama vile Yehova atusamehevyo mapungukio yetu ya kila siku, basi twapaswa kusameheana. “BWANA, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha [“wa kweli,” NW].”—Zaburi 130:3, 4.

“Ujitiisho Kuelekea Mmoja na Mwenzake”

Basi kwa masilahi yetu bora kuelekea mmoja na mwenzake, Maandiko hushauri hivi: “Iweni katika ujitiisho kuelekea mmoja na mwenzake katika hofu ya Kristo.” Onyeshaneni staha yenye upendo; msizuiane wala kushindana. Andiko hilo laendelea: “Acheni wake wawe katika ujitiisho kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko.”—Waefeso 5:21-23, NW.

Neno la Kigiriki lililotumiwa na Paulo kwenye Waefeso 5:21, 22 humaanisha kujitiisha mwenyewe, si kulazimishwa kujitiisha. Na ujitiisho huo ni kwa ajili ya Bwana, si kwa ajili ya upatano wa ndoa tu. Kutaniko lililotiwa mafuta la Kristo hujitiisha lenyewe kwa Kristo kwa hiari, kwa shangwe. Mke afanyapo vivyo hivyo kwa mume wake, basi yaelekea sana ndoa itakuwa na furaha na kufanikiwa.

Maandiko pia husema: “Kila [mume] ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe,” bila unyimivu. (Waefeso 5:33; 1 Petro 3:7) Mume apaswa kukumbuka kwamba yeye pia apaswa kujitiisha kwa kichwa chake, kwa kuwa Biblia hutaarifu: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo.” Ndiyo, mwanamume apaswa kujitiisha kwa mafundisho ya Kristo. Vivyo hivyo, Kristo naye hujitiisha kwa kichwa chake: “Kichwa cha Kristo ni Mungu.” Hivyo, kila mtu ana kichwa isipokuwa Yehova. Na hata yeye hujifungamanisha na sheria zake mwenyewe.—1 Wakorintho 11:3; Tito 1:2; Waebrania 6:18.

Ujitiisho wa Kikristo umesawazika na unanufaisha jinsia zote mbili. Huo huletea ndoa upatano na uradhi ambao ni Muumba wetu mwenye upendo tu awezaye kuuandaa.—Wafilipi 4:7.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 14]

Leslie’s

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki