Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 4/8 kur. 16-18
  • Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa Baada ya Ukosefu wa Uaminifu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa Baada ya Ukosefu wa Uaminifu?
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nyumba Yaharibiwa
  • Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa?
  • Kuondolea Mbali “Magofu”
  • Kujenga Upya
  • Udumishaji
  • Baada ya Siku ya Harusi
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Uzinzi
    Amkeni!—2015
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Wajibika Sikuzote Katika Ndoa Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 4/8 kur. 16-18

Maoni ya Biblia

Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa Baada ya Ukosefu wa Uaminifu?

“Nawaambia kwamba yeyote yule atalikiye mke wake, ila kwa sababu ya uasherati, na kuoa mwingine afanya uzinzi.”—MATHAYO 19:9.

KWA maneno hayo Yesu Kristo alitoa ruhusa kwa Mkristo kuchagua kutaliki mwenzi asiye mwaminifu.a Lakini, itakuwaje ikiwa mwenzi asiye na hatia achagua kuhifadhi ndoa na wenzi hao waazimia kuujenga upya uhusiano wao? Ni matatizo gani yako mbele kwa wenzi hao, na jinsi gani wao waweza kukabiliana na magumu hayo kwa mafanikio? Ebu tuone jinsi Biblia inavyosaidia kujibu maswali hayo.

Nyumba Yaharibiwa

Kwanza twapaswa kuelewa ukubwa wa madhara yasababishwayo na ukosefu wa uaminifu. Kama vile Yesu Kristo alivyoeleza, Mwanzilishi wa ndoa alikusudia kwamba mume na mke wawe “si wawili tena, bali mwili mmoja.” Aliongeza: “Kwa hiyo, kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.” Ndiyo, ndoa inakusudiwa kuwaunganisha wanadamu bila ya kuwatenganisha. Mtu avunjapo nadhiri ya ndoa kwa kufanya uzinzi, matokeo yenye kuumiza sana hufuata.—Mathayo 19:6; Wagalatia 6:7.

Kuthibitisha hili ni msononeko upatwao na mwenzi asiye na hatia. Matokeo ya uzinzi yaweza kulinganishwa na yale ya kimbunga ambacho huvunja-vunja nyumba. Dakt. Shirley P. Glass alisema: “Wenzi kadhaa wasio na hatia waliohitaji tiba ambao niliwatibu walinieleza kwamba ingekuwa rahisi kwao ikiwa wenzi wao wangekufa.” Kweli, baadhi ya watu ambao wamepoteza wenzi wao katika kifo huenda wasikubali. Lakini, ni wazi kwamba uzinzi husababisha maumivu makali sana. Baadhi ya watu hawaponi kabisa kutokana na usaliti huo.

Kwa kufikiria maumivu makali kama hayo, mtu aweza kuuliza, ‘Je, uzinzi lazima ukomeshe ndoa?’ Siyo lazima. Maneno ya Yesu kuhusu uzinzi yaonyesha kwamba mwenzi mwaminifu ana chaguo la Kimaandiko kutaliki lakini hawajibiki kufanya hivyo. Baadhi ya wenzi huamua kujenga upya na kuimarisha kile ambacho kiliharibiwa, kwa kufanya mabadiliko yahitajiwayo—ingawa uzinzi hauna udhuru.

Bila shaka, ni bora kufanya mabadiliko ya lazima katika uhusiano wa ndoa wakati wenzi wote wawili ni waaminifu kwa kila mmoja. Lakini, hata kama ukosefu wa uaminifu umetokea, baadhi ya wenzi wasio na hatia huchagua kuhifadhi ndoa. Badala ya kutegemeza uamuzi kwa kufikiria eti mambo yote yatakuwa sawa, mwenzi asiye na hatia apaswa kupima matokeo yatakayotokea. Bila shaka atafikiria mahitaji ya watoto wake na pia hali yake mwenyewe ya kiroho, kihisia-moyo, kimwili, na mahitaji ya kifedha.b Atakuwa mwenye hekima kufikiria pia ikiwa ndoa yake ina uwezekano wa kuokolewa.

Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa?

Kabla ya kujaribu kujenga upya nyumba iliyoharibiwa na kimbunga, mjenzi lazima apime ikiwa inaweza kujengwa upya. Hali kadhalika, kabla ya kujaribu kujenga upya uhusiano ambao umeharibiwa na ukosefu wa uaminifu, wenzi—hasa mwenzi asiye na hatia—atataka kuchanganua vizuri uwezekano wa kurudishwa kwa ukaribu na itibari katika ndoa.

Jambo la kufikiriwa ni ikiwa mwenzi mwenye kosa aonyesha toba ya moyo mweupe au badala ya hivyo, bado afanya uzinzi “moyoni wake.” (Mathayo 5:27, 28) Ingawa aahidi kubadilika, je, anasita kukomesha mara moja uhusiano wake usio wa adili? (Kutoka 20:14; Mambo ya Walawi 20:10; Kumbukumbu la Torati 5:18) Je, bado aendelea kuwaangalia wanawake wengine kwa kuwatamani? Je, amlaumu mke wake kwa sababu ya uzinzi wake? Ikiwa ndivyo, juhudi za kurudisha itibari kwa ndoa zaelekea hazitafanikiwa. Kwa upande mwingine, ikiwa akomesha uhusiano huo haramu, akubali daraka kwa kosa lake, na aonyesha kujitoa kabisa katika kuijenga upya ndoa, mke wake aweza kuona msingi wa kutumaini kwamba itibari ya kweli yaweza kurudishwa siku moja.—Mathayo 5:29.

Pia, je, mwenzi mwaminifu asamehe kwa kupenda kwake mwenyewe? Hii haina maana kwamba hapaswi kueleza hisia zake za kuumizwa sana kwa habari ya kile kilichotokea au kwamba ajifanye kama hakuna kitu chochote kimebadilika. Humaanisha kwamba katika wakati ufaao, atajitahidi kuondoa uchungu mkuu wa moyo. Msamaha kama huo huchukua wakati lakini waweza kusaidia kuanzisha msingi imara ambao juu yao ndoa yaweza kujengwa upya.

Kuondolea Mbali “Magofu”

Baada ya mwenzi mwaminifu kuamua kuokoa ndoa yao, ni hatua gani zipaswazo kuchukuliwa na wenzi? Kama vile magofu katika nyumba iliyoharibiwa vibaya na kimbunga lazima yaondolewe, ndivyo “magofu” katika ndoa lazima yaondolewe mbali. Hili laweza kutimizwa kwa kiasi kikubwa ikiwa wenzi hao wanaelezana hisia zao. Mithali 15:22 (NW) husema: “Pasipo mazungumzo ya siri, mipango inavunjika.” Neno la Kiebrania litafsiriwalo “mazungumzo ya siri” hudokeza usiri na hutafsiriwa “kikundi cha siri” katika Zaburi 89:7. Hivyo basi ingehusisha, si mazungumzo ya juu juu tu, bali uwasiliano wenye kufuatia haki na idili ambao wote wawili wafunua hisia zao za ndani kabisa.—Mithali 13:10.

Kwa mfano, katika matukio fulani mwenzi mwaminifu angekuwa na maswali zaidi ya kumwuliza mume wake. Jambo hilo lilianzaje? Liliendelea kwa muda gani? Nani mwingine ajua jambo hilo? Kwa kweli, litakuwa jambo lenye kuumiza kwa wenzi wa ndoa kuzungumza mambo hayo. Lakini, mwenzi mwaminifu aweza kupata kwamba ujuzi kama huu ni wa lazima ili kurudisha itibari. Ikiwa ndivyo, ni bora kwa mwenzi asiye mwaminifu kujibu kwa unyofu na kwa ufikirio. Apaswa kueleza mambo katika njia ya upendo na fadhili, akikumbuka kwamba kusudi la mazungumzo ni kuponyesha si kuumiza. (Mithali 12:18; Waefeso 4:25, 26) Wote wawili watahitaji kutumia busara, kujidhibiti, na kusikia kwa hisia mwenzi kadiri wajielezapo hisia zao kuhusu kile kilichotokea.c—Mithali 18:13; 1 Wakorintho 9:25; 2 Petro 1:6.

Wale ambao ni Mashahidi wa Yehova waweza kuomba msaada wa wazee wa kutaniko. Bila shaka, kwa Wakristo, dhambi nzito kama uzinzi lazima ziungamwe mara moja kwa wazee, ambao wahangaikia hali njema ya wenzi wa ndoa na kutaniko. Yaweza kuwa kwamba alipowaona wazee, mzinzi huyo alionyesha toba ya kweli na hivyo aliruhusiwa kubaki katika kutaniko. Katika hali kama hiyo, wazee waweza kutoa msaada wenye kuendelea kwa wenzi wote wawili.—Yakobo 5:14, 15.

Kujenga Upya

Baada ya wenzi hao kuimarisha hisia zao kwa kiasi kinachowezekana, wapo katika nafasi nzuri kujenga upya sehemu muhimu za ndoa yao. Uwasiliano wenye bidii waendelea kuhitajiwa. Udhaifu mbalimbali unapojulikana, mabadiliko yafaayo lazima yafanywe.

Uhitaji wa kufanya mabadiliko utakuwa hasa juu ya mwenzi mwenye hatia. Lakini, mwenzi asiye na hatia apaswa kufanya sehemu yake ili kuimarisha maeneo yenye udhaifu katika ndoa. Hii haina maana kwamba uzinzi ulikuwa kosa lake au kwamba unaweza kuhalalishwa—hakuna sababu halali ya kufanya uzinzi. (Linganisha Mwanzo 3:12; 1 Yohana 5:3.) Yamaanisha tu kwamba huenda kumekuwa na matatizo fulani katika ndoa ambayo yalihitaji kusuluhishwa. Kujenga upya ni mradi wa pamoja. Je, kuna uhitaji wa kuimarisha johari na miradi ya pamoja? Je, shughuli za kiroho zimepuuzwa? Utaratibu huu wa kugundua udhaifu mkubwa na kufanya mabadiliko yahitajiwayo ni muhimu katika kujenga upya ndoa iliyoharibiwa vibaya sana.

Udumishaji

Hata nyumba iliyojengwa vizuri huhitaji kudumishwa kwa ukawaida. Hivyo basi, ni jambo la maana kama nini kudumisha uhusiano uliojengwa upya. Wenzi hao hawapaswi kuruhusu kupita kwa wakati kumomonyoe azimio lao la kushikilia maazimio yao mapya. Badala ya kuvunjika moyo wapatwapo na matatizo madogo-madogo, kama vile kurudia mazoea yasiyo mazuri ya mawasiliano, wanapaswa kuchukua hatua za mara moja warudie mawasiliano mazuri na kuendelea kusonga mbele.—Mithali 24:16; Wagalatia 6:9.

Zaidi ya yote, mume na mke wapaswa kutanguliza kawaida yao ya kiroho au ndoa yao kuliko shughuli nyingine. Zaburi 127:1 husema: “BWANA asipojenga nyumba waijengao wafanya kazi bure.” Pia, Yesu alionya: “Kila mtu anayesikia semi zangu hizi na hazifanyi atafananishwa na mwanamume mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga. Na mvua ikamwagika na mafuriko yakaja na pepo zikavuma na kugonga dhidi ya nyumba hiyo nayo ikaporomoka, na anguko layo lilikuwa kubwa.”—Mathayo 7:24-27.

Ndiyo, ikiwa kanuni za Biblia zinapuuzwa kwa sababu ni ngumu kuzifuata, ndoa itaharibiwa kwa urahisi na mtihani mkali kama kimbunga wa uaminifu. Lakini, ikiwa mume na mke washikilia viwango vya Biblia katika mambo yote, ndoa yao itapata baraka ya kimungu. Pia watakuwa na kichocheo chenye nguvu zaidi katika uaminifu wa ndoa—tamaa ya kumpendeza Mwanzilishi wa ndoa, Yehova Mungu.—Mathayo 22:36-40; Mhubiri 4:12.

[Maelezo ya Chini]

a Kuna sababu za msingi zinazofanya mtu aweze kuchagua kutaliki mwenzi aliye mzinzi. Kwa mazungumzo zaidi juu ya jambo hili, ona “Maoni ya Biblia: Uzinzi—Kusamehe au Kutosamehe?” katika toleo la Amkeni! la Agosti 8, 1995.

b Twamrejezea mwenzi asiye mwaminifu kuwa mwanamume. Uchunguzi mmoja ulikadiria kwamba wanaume wana kiwango cha mara mbili cha ukosefu wa uaminifu kuliko wanawake. Lakini, kanuni zizungumzwazo zatumika sawa wakati mwenzi asiye na hatia ni mwanamume Mkristo.

c Kwa habari zaidi juu ya usikilizaji mzuri, ona Amkeni! la Januari 22, 1994, ukurasa wa 6-9, na Desemba 8, 1994, ukurasa wa 10-13.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki