Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 5/22 kur. 21-23
  • “Afukuzacho Kuku Kwenye Mvua. . . ”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Afukuzacho Kuku Kwenye Mvua. . . ”
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tatizo Kubwa
  • Wasikilizaji Wenye Kuthamini
  • Mtumbwi—Usafiri Unaofaa Zaidi Nchini Kanada
    Amkeni!—2010
  • Nilifurahia Kufanya Mengi Zaidi
    Amkeni!—2005
  • ‘Ripoti Njema Kutoka Mabara ya Mbali’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kutumia Trakti Ili Kuwa na Matokeo Yenye Manufaa
    Huduma Yetu ya Ufalme—1992
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 5/22 kur. 21-23

“Afukuzacho Kuku Kwenye Mvua. . . ”

Na mleta-habari wa Amkeni! katika Nigeria

KUTANIKO letu dogo katika sehemu ya kusini mwa Nigeria lilipopokea ugavi wa trakti Habari za Ufalme Na. 34, ambayo ilitolewa ulimwenguni pote, tulikuwa na hamu ya kuzipeleka katika sehemu zote za eneo letu. Hiyo haikuwa kazi rahisi. Katika eneo letu mna vijiji, ambavyo hukuza mihogo, viazi vikuu, na vyakula vingine. Vijiji hivyo viko ndani sana katika msitu wa mvua wa kitropiki. Ni vigumu kuvifikia lakini si kwamba havifikiki. Kwani, ni mapenzi ya Mungu kwamba habari njema zifikie watu wa namna zote, hata wakulima walio katika misitu.—1 Timotheo 2:3, 4.

Kwa hiyo, mnamo Oktoba 16, 1995, watu 18 kati yetu tuliondoka saa 1:30 ya asubuhi ili kwenda kijiji fulani kilichoitwa Abomgbada, umbali wa karibu kilometa 3.5. Njiani, tulilazimika kuvuka kwa miguu kijito fulani. Maji yalitufikia viunoni.

Ili kufikia kijiji kingine siku iyo hiyo, ilitubidi tuvuke kijito kingine kikubwa zaidi. Pindi hii, ni ndugu wanne tu na dada mmoja waliokivuka kijito hicho. Wengine wote walibaki.

Wengi walitusikiliza siku hiyo. Jambo lililoongeza shangwe yetu ni lile tuliloliita ugavi wa msituni. Tulipokuwa tukienda, tulikuwa tukichuma na kula matunda ambayo yalikuwa yamekua yenyewe tu. Tulikutana na wakulima wenye ukaribishaji-wageni ambao walithamini sana jitihada zetu za kuwafikia; wao walitupatia machungwa ya kuzima kiu yetu. Tulizungumza na watu 250 hivi, tukiwatolea trakti zote tulizobeba.

Tatizo Kubwa

Tatizo kubwa likaja siku mbili baadaye. Kulikuwa na kijiji kiitwacho Ose Anasi kilichokuwa umbali wa kilometa 12, kijiji ambacho labda hakikupata kufikiwa kamwe kwa mahubiri yaliyopangwa rasmi. Wengine walisita kwenda huko. Ilikuwa hatari kuvuka Mto Urasi, na wengi wetu hatukujua kuogelea. Ingekuwa hatari kuuvuka kwa kutembea kwa sababu ya mashina makali ya miti. Sehemu zenye matope zingekuwa zenye utelezi, na kuanguka kungesababisha majeraha. Baadhi ya madaraja yaliyotengenezwa kwa mikono hayakuwa imara. Kulikuwa na nyoka, mamba, na vijito vilivyojaa ruba.

Watu 16 kati yetu tukaamua kwenda. Tulitembea kwa karibu kilometa 1.5 kabla ya kupanda mtumbwi ili kuvuka Mto Urasi wenye kwenda kwa kasi na ulio hatari. Ili kuufikia mtumbwi, tulilazimika kuteremka kwenye mlima ulioinama sana. Huo ulikuwa msimu wa mvua, na huo mto ulikuwa umefurika. Eneo hilo lote lina udongo wa mfinyanzi; na katika msimu wa mvua, lina utelezi sana. Tuliposhuka kwenye mtumbwi, tulipata kwamba kile kijia kilikuwa kimekuwa kijito chenye kina cha meta moja katika sehemu fulani. Huo ndio wakati matatizo yetu yalipoanza.

Tulitembea kwa karibu dakika 30 kwenye kijia hicho ambacho kilikuwa kimekuwa kijito. Ardhi ilikuwa yenye utelezi sana hivi kwamba wengi wetu tulianguka kwenye maji yenye matope, tukilowesha Biblia, magazeti, na trakti zetu. Tulikuwa na furaha, kwa hiyo mtu yeyote alipoanguka, sote tulicheka sana, kutia ndani yule aliyeanguka.

Tulipokuwa tunavuka kijito fulani kidogo, ruba walikwamia miguu yetu. Dada mmoja mchanga ambaye ruba alimkwamia alipiga yowe la kufa na kupona. Alikuwa angali akipiga kelele baada ya ruba kuondolewa. Tulicheka hilo pia tukiliona kuwa sehemu ya safari, tukaendelea na safari.

Kwenye kuvuka kijito kingine, ndugu mmoja aliamua kwamba hatavuka kwa miguu kama wengine bali yeye ataruka. Alifaulu kuruka maji lakini hakufaulu na matope. Aliteleza na kuanguka pu kwenye matope. Aliamka, akajichunguza, hakuona jeraha lolote, kisha akasema: “Hakuna tatizo; hiyo ni sehemu ya safari.” Tukakumbuka kwamba mtume Paulo pia alikabili “hatari kutokana na mito,” labda iliyo mikubwa zaidi ya ile tuliyokabili.—2 Wakorintho 11:26.

Tulivuka daraja lililotengenezwa kwa mikono, ambalo lilionekana kuwa hatari, lakini sote tukafaulu kuvuka. Baadaye eneo hilo likawa lenye utelezi zaidi, hivi kwamba wengi zaidi walikuwa wakianguka.

Ndugu mmoja mwenye umri wa karibu miaka 70 ambaye ni painia wa kawaida alikuwa pamoja nasi. Asubuhi hiyo alikuwa amekuja kututakia safari njema. Lakini baada ya sisi kusali ili tupate baraka za Yehova, aliuliza: “Nawezaje kubaki hali nyinyi mnakwenda kuhubiri?” Akasisitiza kwamba hata yeye yuaja na hakuna mtu kati yetu aliyeweza kumsadikisha abaki. Alisema Yehova angekuwa pamoja naye. Basi akaja.

Alipoanguka chali kwenye ardhi yenye utelezi, hakuna mtu alicheka. Tukiwa na hangaiko tulimwuliza ikiwa alikuwa ameumia. Alijibu: “La. Nilianguka polepole ili nisiumize ardhi.” Tulicheka kwa utulizo na kukumbuka Isaya 40:31, lisemalo kwamba “wamngojeao BWANA watapata nguvu mpya.”

Wasikilizaji Wenye Kuthamini

Hatimaye tulifika tulikokuwa tukienda. Itikio la watu lilitia moyo sana. Mtu mmoja aliogopa alipotuona tukienda kwenye nyumba yake, lakini alipojua sisi ni akina nani, yeye alisema: “Naona vigumu kuamini kwamba mmefunga safari hiyo ngumu ili tu kutuhubiria. Tunathamini.” Tukajibu kwa mithali ya huko: “Afukuzacho kuku kwenye mvua ni muhimu kwake.” Mtu huyo alielewa.

Mkulima mwingine alisema: “Ikiwa mahubiri yamefika huku, hiyo yamaanisha kwamba wokovu umetufikia.” Wengi walikuwa na maswali, ambayo tuliyajibu. Walituomba turudi, nasi takaahidi kurudi.

Katika Ose Anasi tuliangusha trakti 112 hivi—zote tulizokuwa nazo. Kwa ujumla tulihubiria watu wapatao 220.

Tukiwa njiani kurudi, tulipotea. Kurudi nyuma tena kijijini kungechukua muda wa saa moja na nusu, na usiku ulikuwa ukikaribia upesi. Tulimtolea Yehova sala za ukimya na kuamua kuendelea tu mbele, ingawa kufanya hivyo kulimaanisha kuvuka kwa kutembea kijito chenye kutisha ambacho kilifikia nyonga zetu.

Baada ya kuvuka, tuligundua njia na kupata kwa mshangao kwamba tulikuwa tumekaribia nyumbani zaidi. Kumbe kupotea kwetu kukawa njia ya mkato ambayo ilipunguza safari yetu kwa angalau muda wa saa moja! Bila shaka, sisi sote tulifurahi na kumshukuru Yehova. Jua lilipokuwa likitua, tulifika nyumbani—tukiwa tumechoka na wenye njaa lakini wenye furaha sana.

Baadaye, tulipokuwa tukisimuliana mambo tuliyojionea siku hiyo, dada mmoja alisema: “Nilikuwa nimesikia habari za sehemu tuliyoenda, basi nilijua nitaanguka. Kama si kwa ajili ya habari njema, singalienda huko, singalienda hata kama ningepewa pesa zote ulimwenguni!” Ndugu mmoja akapaaza sauti: “Hatimaye habari njema zimefikia Ose Anasi!”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kuvuka daraja la huku

Tulivuka vijito vingi vilivyojaa ruba

Chini ya njia hii hatari, tulipanda mtumbwi ili kuvuka Mto Urasi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki