Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 6/8 kur. 18-20
  • Kwa Nini Udhibiti Hasira Yako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Udhibiti Hasira Yako?
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wanadamu Wasio Wakamilifu Wapatwapo na Hasira
  • Wakristo Ni Wenye Kutoa Hesabu
  • Biblia Inasema Nini Kuhusu Hasira?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Hasira
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Je! Ni Vibaya Nyakati Zote Kuwa na Hasira?
    Amkeni!—1994
  • Kuweza Hasira Yako na ya Wengine
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 6/8 kur. 18-20

Maoni ya Biblia

Kwa Nini Udhibiti Hasira Yako?

ULIKUWA mwanzo wenye kuogofya. “Kwa sababu sasa mimi ni kichwa cha nyumba hii, hutaendelea kunisumbua kwa kuchelewa,” John alimpigia kelele Ginger,a bibi-arusi wake mpya. Kwa zaidi ya dakika 45, John aliendelea kumpigia kelele Ginger huku akidai kwamba aendelee kukaa katika kochi. Usemi wenye kuudhi ulikuwa jambo la kawaida katika ndoa yao. Kwa kusikitisha, tabia ya hasira ya John iliendelea kuongezeka. Angebamiza milango, angepigapiga meza ya jikoni, angeendesha gari kama kichaa huku akigongagonga usukani, hivyo akihatarisha maisha ya wengine.

Kwa ubaya, kama ambavyo bila shaka wajua, matukio kama hayo hutukia kwa ukawaida. Je, hasira ya mtu huyu ilikuwa halali, au alikuwa anapoteza udhibiti? Je, hasira zote ni mbaya? Ni wakati gani hasira ifikiriwapo kuwa yakosa kudhibitiwa? Ni wakati gani ivukapo mpaka?

Hasira iliyodhibitiwa yaweza kuwa sawa. Mathalani, hasira ya Mungu iliwaka dhidi ya miji ya kale isiyo ya adili ya Sodoma na Gomora. (Mwanzo 19:24) Kwa nini? Kwa sababu wakazi wa miji hiyo walijihusisha na jeuri na mazoea ya ngono zilizopotoka, kama ilivyojulikana katika eneo lote. Mathalani, wajumbe wa kimalaika walipomtembelea Loti mwadilifu, kikundi cha wafanya-ghasia cha vijana pamoja na wazee kilijaribu kuwabaka kwa pamoja wageni wa Loti. Kwa halali Yehova Mungu alichukizwa na ukosefu wao mbaya sana wa adili.—Mwanzo 18:20; 19:4, 5, 9.

Kama Baba yake, mwanadamu mkamilifu Yesu Kristo alilazimika katika nyakati fulani kuwa mwenye hasira. Hekalu katika Yerusalemu lilipaswa kuwa kitovu cha ibada kwa wachaguliwa wa Mungu. Lilipaswa kuwa “nyumba ya sala,” ambapo watu mmoja-mmoja wangeweza kutoa dhabihu za kibinafsi na kumtolea Mungu matoleo na ambapo wangeweza kufundishwa katika njia zake na dhambi zao kusamehewa. Katika hekalu wangeweza, kwa kitamathali, kuzungumza na Yehova. Badala ya hivyo, viongozi wa kidini katika siku za Yesu walibadilisha hekalu kuwa “nyumba ya bidhaa za biashara” na “pango la wapokonyaji.” (Mathayo 21:12, 13; Yohana 2:14-17) Walifaidika kibinafsi kutokana na mauzo ya wanyama waliopaswa kutumika katika dhabihu. Katika maana halisi, walikuwa wanalilaghai kundi. Hivyo, ilikuwa halali kabisa wakati Mwana wa Mungu alipowafukuza wapokonyaji kutoka katika nyumba ya Baba yake. Kwa kueleweka Yesu alikuwa na sababu ya kuwa mwenye hasira!

Wanadamu Wasio Wakamilifu Wapatwapo na Hasira

Wanadamu wasio wakamilifu nyakati fulani waweza kwa haki kukasirishwa. Fikiria kile kilichotokea kwa Musa. Taifa la Israeli lilikuwa limetoka tu kukombolewa kimuujiza kutoka Misri. Yehova alikuwa ameonyesha kwa njia yenye kutazamisha nguvu zake juu ya miungu isiyo ya kweli ya Misri kwa kuwapiga Wamisri kwa mapigo kumi. Kisha alifungua njia kwa Waisraeli kuponyoka, kwa kutenganisha Bahari Nyekundu. Baadaye, waliongozwa hadi chini ya Mlima Sinai, ambapo walifanywa kuwa taifa. Akitenda akiwa mpatanishi, Musa alipanda juu mlimani ili kupokea Sheria za Mungu. Pamoja na sheria nyingine zote, Yehova alimpa Musa Amri Kumi, zilizoandikwa kwa “chanda cha Mungu” juu ya mabamba ya mawe ambayo Mungu mwenyewe aliyachonga kutoka katika mlima. Lakini, Musa aliposhuka, aliona nini? Watu walikuwa wamegeukia kuabudu mfano wa ndama wa dhahabu! Walisahau haraka namna gani! Wiki chache tu zilikuwa zimepita. Kwa haki, “hasira ya Musa ikawaka.” Aliyavunja yale mabamba ya mawe na aliendelea kuharibu kabisa mfano wa ndama.—Kutoka 31:18; 32:16, 19, 20.

Pindi fulani baadaye, Musa alishikwa na hamaki wakati watu walipolalamikia upungufu wa maji. Akiwa ameghadhibika, kwa muda mfupi tu alipoteza sifa yake maarufu ya unyenyekevu, au ya upole wa tabia. Hili liliongoza kwenye kosa zito. Badala ya kumtukuza Yehova kuwa ndiye Mwandaaji wa Israeli, Musa aliongea kwa ukali na watu na alielekeza uangalifu kwa ndugu yake Haruni na kwake mwenyewe. Hivyo, Mungu aliona inafaa kumtia Musa nidhamu. Asingeruhusiwa kuingia katika bara lililoahidiwa. Baada ya tukio hili katika Meriba, hakuna mtajo wowote zaidi wa Musa kushikwa na hamaki. Kwa wazi, alijifunza somo.—Hesabu 20:1-12; Kumbukumbu la Torati 34:4; Zaburi 106:32, 33.

Hivyo, kuna tofauti kati ya Mungu na mwanadamu. Yehova aweza ‘kuiacha hasira yake’ na kwa haki afafanuliwa kuwa “si mwepesi wa hasira” kwa sababu upendo ndio sifa yake kuu, wala si hasira. Sikuzote hasira yake ni ya uadilifu, sikuzote ni halali, sikuzote imedhibitiwa. (Kutoka 34:6, NW; Isaya 48:9; 1 Yohana 4:8) Sikuzote mwanadamu mkamilifu Yesu Kristo aliweza kudhibiti wonyesho wa hasira yake; alifafanuliwa kuwa “mwenye tabia-pole.” (Mathayo 11:29) Kwa upande mwingine, wanadamu wasio wakamilifu, hata wanaume wa imani kama vile Musa, wamepata ugumu kudhibiti hasira zao.

Pia, kwa ujumla wanadamu hushindwa kufikiria vizuri matokeo ya baadaye ya hasira zao zisizodhibitiwa. Kunaweza kuwa na matokeo mabaya mtu akishindwa kudhibiti hasira yake. Mathalani, ni matokeo gani ya wazi yawezayo kutokea ikiwa mume ashikwa na hamaki kuelekea mke wake kufikia hatua ya kutoboa ukuta kwa ngumi? Mali inaharibika. Mkono wake waweza kuumia. Lakini zaidi ya hilo, hamaki yake itaathirije upendo na staha ya mke wake kwake? Ukuta waweza kurekebishwa katika muda wa siku chache, na mkono wake waweza kupona katika majuma machache; lakini ni muda gani utakaomchukua kupata tena itibari na staha ya mke wake?

Kwa kweli, Biblia imejaa mifano ya wanaume ambao walishindwa kudhibiti hasira zao na ambao waliteseka kutokana na matokeo yaliyofuata. Fikiria mifano michache. Kaini alifukuzwa baada ya kumwua kikatili ndugu yake Abeli. Simeoni na Lawi walilaaniwa na baba yao kwa sababu ya kuua wanaume wa Shekemu. Yehova alimpiga Uzia kwa ukoma baada ya Uzia kuwa na hasira na makuhani ambao walikuwa wanajaribu kumrekebisha. Yona ‘alipokasirika’ Yehova alimkaripia. Wote hao walitozwa hesabu kwa sababu ya hasira zao.—Mwanzo 4:5, 8-16; 34:25-30; 49:5-7; 2 Mambo ya Nyakati 26:19; Yona 4:1-11.

Wakristo Ni Wenye Kutoa Hesabu

Vivyo hivyo, leo Wakristo lazima watoe hesabu kwa sababu ya matendo yao kwa Mungu, na kwa kiasi fulani, kwa waamini wenzao. Hili laweza kuonekana wazi kutokana na matumizi ya Biblia ya maneno ya Kigiriki yamaanishayo hasira. Moja kati ya maneno mawili yatumiwayo sana ni or·geʹ. Kwa ujumla hutafsiriwa “hasira ya kisasi” na hutia ndani wazo fulani la ufahamu na hata umakusudi, mara nyingi kukiwa na maoni ya kulipiza kisasi. Hivyo, Paulo aliwasihi sana Wakristo Waroma: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi hasira ya kisasi [or·geʹ]; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa, asema Yehova.’” Badala ya kuwawekea kinyongo ndugu zao, walitiwa moyo “kushinda lililo ovu kwa lililo jema.”—Waroma 12:19, 21.

Neno jingine litumiwalo mara nyingi kumaanisha hasira ni thy·mosʹ. Neno la msingi “humaanisha kiasili mwendo wenye nguvu nyingi wa hewa, maji, ardhi, wanyama, au wanadamu.” Hivyo, neno hilo hufafanuliwa katika njia tofauti-tofauti kuwa “mlipuko wa hisia kali yenye uhasama,” “mfoko wa hamaki,” au “hisia kali isiyodhibitika, isumbuayo upatano wa akili, na kutokeza usumbufu wenye kelele wa nyumbani na jamii na pia wasiwasi.” Kama volkano iwezayo kulipuka bila ya onyo na kutapika majivu yenye moto, miamba na lava, ambayo yaweza kujeruhi, kulemaza, na kuua, ndivyo ilivyo mwanamume au mwanamke ambaye hawezi kudhibiti hamaki zake. Wingi wa neno thy·mosʹ linatumiwa katika Wagalatia 5:20, ambapo Paulo aorodhesha “hasira za ghafula” pamoja na “kazi za mwili” (mstari wa 19), kama vile uasherati, mwenendo mlegevu, na vipindi vya kulewa. Kwa hakika, tabia ya John—iliyoelezwa mwanzoni —yaeleza vizuri “hasira za ghafula.”

Kwa hiyo, kutaniko la Kikristo linapaswa liwaoneje watu mmoja-mmoja wanaoshirikiana nalo ambao wanashiriki katika matendo ya kurudia ya jeuri dhidi ya mtu au mali za mwingine? Hasira isiyodhibitiwa ni yenye kusababisha uharibifu na kwa urahisi huongoza kwenye jeuri. Akiwa na sababu nzuri, Yesu alisema: “Mimi nawaambia nyinyi kwamba kila mtu aendeleaye kuwa na hasira ya kisasi na ndugu yake atapaswa kutoa hesabu kwa mahakama ya kuamulia haki.” (Mathayo 5:21, 22) Waume wanashauriwa: “Fulizeni kuwapenda wake zenu na msiwakasirikie kwa uchungu.” Mtu ambaye ana “elekeo la kuwa na hasira ya kisasi” hastahili kuwa mwangalizi katika kutaniko. Kwa sababu hiyo, watu ambao hawawezi kudhibiti hasira zao hawapasi kufikiriwa kuwa vielelezo katika kutaniko. (Wakolosai 3:19; Tito 1:7; 1 Timotheo 2:8) Kwa hakika, baada ya kufikiria mtazamo wa mtu kama huyo, kiolezo cha tabia, na kiasi cha maumivu ambacho ametia katika maisha za wengine, mtu ambaye hushindwa na hasira za ghafula zisizodhibitiwa aweza kufukuzwa kutoka katika kutaniko—kwa kweli, tokeo baya kama nini.

Je, John aliyetajwa mwanzoni, aliweza kudhibiti hisia-moyo zake? Je, aliweza kuacha mwendo wake uliomwelekeza kwenye msiba? Kwa kusikitisha, kelele ziliendelea hadi hatua ya kusukuma na kupiga kikumbo. Mashutumu ya kunyoosha kidole cha shahada yaliongoza kwenye midukuo halisi, ya kutia alama na yenye kuumiza. John alikuwa mwangalifu sana kuepuka kukwaruza sehemu za mwili wa Ginger ambazo zilionekana kwa urahisi na alijitahidi kuficha mwenendo wake. Hata hivyo, hatimaye, alianza kupiga mateke, ngumi, kuvuta nywele, na mambo mengine mabaya zaidi. Ginger sasa ametengana na John.

Hili halikupaswa kutokea. Wengi katika hali kama hiyo wameweza kudhibiti hasira zao. Kwa hiyo, ni muhimu kadiri gani kuiga kielelezo kikamilifu cha Yesu Kristo. Hakuwa kamwe na hatia ya hata tendo moja la hasira kali isiyodhibitiwa. Sikuzote hasira yake ilikuwa ya uadilifu; hakupoteza kamwe udhibiti wa hasira yake. Kwa hekima, Paulo alitushauri sisi sote: “Iweni na hasira ya kisasi, na bado msifanye dhambi; msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Hivyo, tukitambua kwa unyenyekevu kwamba tuna udhaifu tukiwa wanadamu na kwamba tutavuna kile tukipandacho, tuna sababu nzuri ya kupunguza hasira.

[Maelezo ya Chini]

a Majina yamebadilishwa.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]

Sauli Ajaribu Kumwua Daudi/The Doré Bible Illustrations/Dover Publications, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki