Kitu Bora Kuliko Kuwa Mashuhuri Ulimwenguni
Miaka mingi baada ya kuwa mchongaji mashuhuri katika Ulaya, msanii mwenzangu aliniambia hivi akinilaumu: “Umeharibu kipawa chako cha sanaa!” Kabla ya kueleza sababu iliyofanya anilaumu hivyo, ebu nieleze jinsi nilivyopata kuwa mchongaji.
KATIKA kijiji cha Aurisina, nilikozaliwa, wengi wa wanaume walifanya kazi katika machimbo fulani ya kale ya mawe. Aurisina kipo kaskazini mwa Italia karibu na Trieste na karibu na ile iliyokuwa Yugoslavia. Nilipokuwa na umri wa miaka 15, mimi pia nilianza kufanya kazi katika machimbo ya mawe ya kijiji. Huo ulikuwa mwaka wa 1939, mwaka ambao Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipoanza. Kufanya kazi ihusuyo mawe kulinifanya niwe na tamaa ya kuwa mchongaji mashuhuri. Pia sikutaka kufa kamwe. Ilionekana kama singeweza kutimiza tamaa hizo mbili.
Vita ilipokwisha mnamo 1945, nilihamia Roma ili niishi na dada yangu. Nilitumaini kujiunga na shule ya sanaa huko. Nilisisimuka kama nini nilipotimiza ndoto yangu na kukubaliwa kusoma kwa miaka mitatu! Masomo yangu yaligharimiwa na mashirika kadhaa ya kutoa msaada.
Njaa ya Kiroho
Pia nilijaribu kuridhisha tamaa yangu ya kiroho kwa kuhudhuria ibada za kidini, kutia ndani zile za Jeshi la Wokovu na za Wawaldo. Hata nilipata masomo katika chuo kikuu fulani cha Wajesuti, na pindi moja nilihudhuria semina ya siku tatu iliyofundishwa na askofu fulani. Katika mtaala huu hatukukubaliwa kuzungumza kati yetu, bali tulijitoa kwa sala, kutafakari, ungamo, na hotuba za askofu.
Baadaye, nilitambua kwamba imani yangu haikuwa imeimarishwa. “Kwa nini,” nilimwuliza huyo askofu, “sijasitawisha imani thabiti?”
“Imani ni zawadi ya Mungu,” askofu huyo akajibu, “naye humpa yeyote ambaye yeye ataka.” Jibu lake lilinivunja moyo sana hivi kwamba nikaacha kumtafuta Mungu na kuanza kujitoa kabisa kwa masomo yangu ya sanaa.
Napata Umashuhuri wa Kimataifa
Baada ya kumaliza shule kule Roma mnamo 1948, nilipokea msaada wa kusoma kwa mwaka mmoja katika shule ya sanaa kule Vienna, Austria. Nilihitimu mwaka uliofuata nami nikakubali msaada wa mwaka mmoja wa kusoma kule Ljubljana, Slovenia (ambayo zamani ilikuwa sehemu ya Yugoslavia). Wakati huo mradi wangu ulikuwa kuhamia Paris, Ufaransa, kitovu cha sanaa.
Hata hivyo, mwaka wa 1951, nilipewa fursa ya kufanya kazi Stockholm, Sweden. Nilihamia huko nikikusudia kuweka akiba pesa za kuniwezesha kufuatia kazi-maisha ya sanaa Paris. Lakini nikakutana na Micky, nasi tukafunga ndoa mwaka wa 1952 na kukaa Stockholm. Nilipata kazi katika karakana ndogo ambako nilichonga vitu vya mawe, marumaru, na itale. Baadhi ya hizo zimewekwa maonyeshoni katika Millesgarden, ambayo ni bustani iliyo pia jumba la makumbusho katika mji wa Lidingö, karibu na Stockholm.
Nilikuwa nimejifunza njia ya kale ya kukalibu shaba nyeusi kule Roma—ule mtindo wa kale wa kukalibu kwa nta—nami nilifundisha kukalibu shaba nyeusi katika Shule ya Ufundi wa Sanaa na katika Shule ya Sanaa ya Stockholm. Baadaye, niliweza kutumia mahali pa kukalibu shaba nyeusi katika makumbusho ya wazi ya Skansen katika Stockholm. Huko, mara nyingi mbele ya watazamaji, nilikuwa nikifanyiza michongo ya shaba nyeusi au ya risasi. Pia nilikodiwa kurekebisha michongo ya kale ya aliyekuwa wakati huo mfalme wa Sweden, Gustav wa Sita. Hiyo imewekwa maonyeshoni katika Royal Palace na vilevile katika makao ya Drottningholm kule Stockholm.
Kati ya miaka ya 1954 na 1960, kazi yangu ilisifiwa sana na vyombo vya habari na vilevile na wahakiki wa sanaa. Michongo yangu mingi imewekwa maonyeshoni katika majiji ya Ulaya, kutia ndani Stockholm, Roma, Ljubljana, Vienna, Zagreb, na Belgrade. Katika jiji la Belgrade, Marshal Tito alinunua baadhi ya michongo yangu iwe maridadi yake binafsi. Nimewakilishwa katika Modern Gallery jijini Roma na mchongo mkubwa wa itale wa kiwiliwili cha mwanamke, na sanaa yangu imewekwa maonyeshoni katika Jumba la Makumbusho la Albertina jijini Vienna. Lile Modern Museum jijini Stockholm lina mojawapo ya michongo yangu ya shaba nyeusi na risasi, na Modern Gallery katika Ljubljana ina mchongo wa shaba nyeusi.
Napendezwa Tena na Dini
Baada ya kufunga ndoa kwa miaka michache, Micky alitambua upendezi wangu uliokuwa ukiamka tena katika dini. Nilikuwa nikijiuliza daima, ‘Ipo wapi imani ambayo Wakristo wa kwanza walikuwa tayari kuifia?’ Tena nikaanza kuhudhuria ibada za kidini, kama zile za Kipentekoste na za Wasabato. Hata nilichunguza Uislamu na Ubuddha.
Mwaka wa 1959, kabla ya kuhudhuria wonyesho wa sanaa Milan, Italia, nilizuru kijiji chetu cha Aurisina kwa siku chache. Wanakijiji wakaniambia kuhusu mtu fulani ambaye wao walisema alijua Biblia sana. Alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilipopata fursa ya kuzungumza naye, alinionyesha mambo katika Biblia ambayo sikuwa nimepata kuyaona kamwe. Nilijifunza kwamba mwanadamu ni nafsi—hana nafsi iliyo tofauti na mwili wake—na kwamba nafsi ya kibinadamu inaweza kufa, si isiyoweza kufa kama zifundishavyo dini nyinginezo.—Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4.
Isitoshe, mtu huyo alinionyesha kwamba kusudi la Mungu alipowaumba Adamu na Hawa halikuwa kwamba wafe, bali lilikuwa waishi milele kwa furaha duniani. Hao wenzi wa kwanza wa kibinadamu walikufa kwa sababu hawakutii. (Mwanzo 1:28; 2:15-17) Nilijifunza kwamba kwa kumtoa Mwanaye kuwa fidia, Mungu aliwafanyia wanadamu uandalizi wa kuwa na taraja la uhai udumuo milele, ambalo lilikuwa limepotezwa na kutotii kwa Adamu. (Yohana 3:16) Nilifurahi sana kujifunza mambo haya.—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.
Nafanya Mabadiliko
Muda mfupi baadaye, nilirudi Sweden, na mimi na Micky tukajaribu kutafuta Mashahidi wa Yehova. Lakini tulishindwa kupata anwani zao. Lakini siku chache baadaye, kengele ya mlango wetu ililia, na ni hao walikuwa mlangoni petu! Nikaanza kusoma fasihi waliyoniachia, na upesi nikasadiki kwamba ilikuwa na kweli. Lakini, nilitaka kuthibitisha kauli yangu kwa kuzungumza na rafiki yangu wa zamani, askofu-mkuu wa Katoliki, ambaye nilifahamiana naye wakati nilipokuwa nikijifunza sanaa huko Roma mwishoni-mwishoni mwa miaka ya 1940. Basi, Januari 1961, nikaenda kumwona.
Wakati huo rafiki yangu alikuwa akisimamia utendaji wote wa kimishonari wa Katoliki ulimwenguni pote. Nilingojewa na mshangao ulioje! Nilishangaa kugundua kwamba askofu-mkuu huyo hata hakujua mambo ya msingi ya Biblia. Tulipozungumza kuhusu kinachotendeka mtu akifa, alisema: “Kile tuaminicho sasa chaweza kugeuka kuwa kinyume kabisa.” Na tulipozungumza juu ya rejezeo la mtume Petro kwa ahadi ya Biblia ya “mbingu mpya na dunia mpya,” yeye hakuwa na uhakika wa lililomaanishwa na ahadi hiyo.—2 Petro 3:13; Isaya 65:17-25.
Niliporudi Stockholm, nilianza kujifunza Biblia kwa ukawaida na mmoja wa Mashahidi ambaye mimi na mke wangu tulikuwa tumefahamiana naye. Nilifurahi kuona upendezi wa Micky ukizidi kuongezeka juu ya funzo. Hatimaye, Februari 26, 1961, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji, naye Micky akabatizwa mwaka uliofuata.
Nafanya Marekebisho ya Kazi ya Kuajiriwa
Tulipata mtoto msichana mwaka wa 1956 na kivulana mwaka wa 1961. Kwa kuwa sasa tulikuwa na familia ya kutegemeza, nilihitaji kazi ya kudumu. Nilifurahi kupokea mwaliko wa kujenga nguzo kubwa katika kijiji nilikozaliwa. Ingekuwa nguzo ya kukumbuka wanamgambo waliokufa katika Vita ya Ulimwengu ya Pili. Kujenga nguzo hiyo ingenipa faida kubwa sana. Lakini baada ya kufikiria mambo kadhaa—kutia ndani jambo la kwamba ningekuwa mbali na familia kwa miezi mingi na mbali na kutaniko la Kikristo na kwamba ningekaa katika nchi ambako Ukomunisti ulikuwa ukisitawi na ambako haingekuwa rahisi kufuatia mambo ya kiroho—nikakataa toleo hilo.
Kazi nyingine iliniletea tatizo la kusumbuliwa na dhamiri. Niliombwa nitengeneze pambo kubwa kwa ajili ya makaburi mapya nchini Sweden. Nilipoimaliza, nilialikwa nihudhurie kuzinduliwa kwake. Lakini baada ya kujua kwamba askofu wa Stockholm ndiye angezindua kazi yangu, nikaamua nisishiriki sherehe na watu ambao mafundisho yao na desturi zao zinapingana kabisa na Neno la Mungu.—2 Wakorintho 6:14-18.
Kwa sababu nilikosa kazi ya kudumu nikiwa mchongaji, nilianza kupata tatizo la kuandalia ifaavyo familia yangu mahitaji ya kimwili. (1 Timotheo 5:8) Nikafikiria kwa sala jambo ambalo ningeweza kufanya ili kujiruzuku. Baadaye, msanifuujenzi mmoja alinijia na kiolezo cha jengo alichokuwa amebuni. Aliniomba nikipige picha. Kwa kuwa nilijua kupiga picha sana kwa sababu ya uzoefu wangu wa kupiga picha michongo yangu, nilifurahi kukubali kazi hiyo. Katika miaka hiyo kazi nyingi za ujenzi zilikuwa zikiendelea Sweden, na kulikuwa na uhitaji wa wapiga-picha wa violezo. Basi, nikapata kazi nyingi kutoka kwa wasanifuujenzi wengi nami niliweza kuruzuku familia yangu ifaavyo.
Ni wakati huu ndipo nilipozuru Taasisi ya Kitamaduni ya Italia jijini Stockholm ili kushiriki nao habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Nilimjua mkurugenzi wa taasisi hiyo na niliweza kupanga kuzungumza naye. Ni baada ya yeye kutambua nilikuwa nimeacha kazi ya kuchonga ndipo alipopaaza sauti: “Umeharibu kipawa chako cha sanaa!” Nikamweleza kwamba nilikuwa na wajibu wa kwanza kwa Mungu na familia yangu.
Ni lazima nikiri kwamba kwa muda fulani sanaa ilikuwa ndiyo jambo kuu maishani mwangu. Hata hivyo, nikatambua kwamba kuendelea kufuatia kazi-maisha yangu kungekuwa kama kujaribu kutumikia mabwana-wakubwa wawili. (Mathayo 6:24) Nilisadiki kwamba jambo la maana zaidi ambalo ningeweza kufanya lilikuwa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Basi nikafanya uamuzi wa kibinafsi wa kuacha kazi yangu ya uchongaji, na Yehova Mungu ameubariki sana uamuzi wangu.—Malaki 3:10.
Mapendeleo ya Utumishi wa Kikristo
Katika miaka ya mapema ya 1970, wahamiaji wengi wa Sweden kutoka kusini na mashariki mwa Ulaya walianza kuonyesha upendezi katika kweli ya Biblia. Basi, kuanzia 1973, nilipata pendeleo la kujifunza Biblia na wahamiaji waliojua lugha za Kiitalia, Kihispania, na Kiserbia-Kikroatia, nami niliweza kusaidia kuanzisha makutaniko mapya na vikundi vya mafunzo kwa ajili ya watu wa lugha hizo. Niliwekwa rasmi kupanga mikusanyiko ya Kikristo ya lugha ya Kiitalia na kuongoza drama za Biblia katika mikusanyiko hiyo. Pindi kwa pindi, nilikuwa na pendeleo la kutumikia makutaniko nchini Sweden nikiwa mwangalizi asafiriye.
Kwa sababu ya kusaidia kupanga mikusanyiko ya Kiitalia nchini Sweden, nilikuwa nikiwasiliana na ofisi ya tawi ya Watch Tower Society jijini Roma. Hao ndugu wa Italia waliniambia kwamba kuna uhaba wa wazee wa kutaniko Italia kwa sababu ya ukuzi wa haraka sana wa kazi ya kuhubiri huko. Basi, mnamo 1987, mimi na Micky tukahamia Liguria, karibu na Genoa, Italia. Kufikia wakati huo watoto wetu walikuwa watu wazima na walikuwa wakijisimamia. Tulikaa Italia kwa miaka miwili yenye kupendeza nasi tukashiriki kuanzisha kutaniko jipya katika Liguria. Tuliona kikamili ukweli wa Mithali 10:22: “Baraka ya BWANA hutajirisha.”
Nyakati nyingine mimi na Micky hujumlisha baraka zetu kutoka kwa Yehova, na orodha hiyo huwa ndefu. Mbali na kushiriki katika kufanyiza makutaniko mapya, tumeweza kuwasaidia watu kadhaa, kutia ndani watoto wetu, kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa na kisha kuwa Wakristo wakomavu. Sijutii uamuzi wangu wa kuacha maisha yangu nikiwa mchongaji mashuhuri, kwa kuwa nimechagua kazi-maisha ambayo inathawabisha sana ya kumtumikia Mungu wetu mwenye upendo, Yehova. Familia yangu na mimi tumepokea tumaini thabiti la uhai wa milele, kwa sababu ya Yehova.—Kama ilivyosimuliwa na Celo Pertot.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Nikifanya kazi ya uchongaji mwaka wa 1955
[Picha katika ukurasa wa 15]
Nikiwa na mke wangu