Kutazama Juu, Si Chini, kwa Majibu
MAGEUZI hufundisha kwamba mfululizo wa mabadiliko ulitubadilisha polepole kuwa wanyama wa hali ya juu. Kwa upande mwingine, Biblia husema kwamba tuliumbwa tukiwa wakamilifu, kwa mfano wa Mungu, lakini kwamba muda mfupi baadaye, tuliingizwa kwenye kutokamilika na mwanadamu akaanza kudhoofika.
Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walianzisha hali hii mbaya walipojitafutia uhuru wa adili na kuharibu dhamiri zao kwa kutomtii Mungu kimakusudi. Ilikuwa kana kwamba waliendesha gari na wakavunja kimakusudi kingo za sheria ya Mungu na kutumbukia mahali tulipo sasa, tukiteseka kwa ugonjwa, uzee, na kifo, kwa kuongezea ubaguzi wa rangi, chuki za kidini, na vita vyenye kuogofya.—Mwanzo 2:17; 3:6, 7.
Je, Ni Jeni za Wanyama au Ni Jeni Zenye Dosari?
Bila shaka, Biblia haifafanui kwa njia ya kisayansi kilichopata miili mikamilifu ya Adamu na Hawa walipofanya dhambi. Biblia si kitabu cha sayansi, kama vile kijitabu cha maagizo cha mwenye kumiliki gari kisivyo kitabu cha mafundisho juu ya injini ya gari. Lakini kama vile kijitabu cha maagizo cha mwenye kuimiliki, Biblia ni sahihi; si ngano.
Adamu na Hawa walipovunja kingo za sheria ya Mungu, viungo vyao viliharibiwa. Baada ya hapo, walianza kudhoofika polepole wakielekea kifo. Kupitia sheria za urithi, watoto wao, familia ya binadamu, walirithi kutokamilika. Hivyo, wao pia hufa.—Ayubu 14:4; Zaburi 51:5; Waroma 5:12.
Kwa kusikitisha, urithi wetu watia ndani mwelekeo wa kufanya dhambi, ambao hujitokeza kwa njia ya ubinafsi na ukosefu wa adili. Bila shaka ngono inafaa inapowekwa mahali pake. Mungu aliwaamuru hivi wenzi wa kwanza wa kibinadamu: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi.” (Mwanzo 1:28) Na akiwa Muumba mwenye upendo, alifanya kutimiza sheria hii kuwe jambo liletalo raha kwa mume na mke. (Mithali 5:18) Lakini kutokamilika kwa binadamu kumeongoza kwenye matumizi mabaya ya ngono. Kwa kweli, kutokamilika huathiri kila upande wa maisha zetu, kutia ndani utendaji wa akili na mwili wetu, kama tujuavyo sote.
Lakini kutokamilika hakujaondoa hisi yetu ya adili. Kwa kweli tukitaka, twaweza kuelekeza mwendo wetu na kuepuka mitego ya maisha kwa kupinga mwelekeo wa kukengeuka ndani ya dhambi. Bila shaka, hakuna binadamu asiyekamilika awezaye kupigana na dhambi kwa mafanikio kamili, na kwa rehema Mungu hujua jambo hili.”—Zaburi 103:14; Waroma 7:21-23.
Sababu ya Kutotaka Kufa
Biblia pia hueleza juu ya fumbo jingine ambalo mageuzi hayaelezi kwa njia yenye kuridhisha: ile kawaida ya binadamu ya kutokubali kifo, hata ingawa kifo chaweza kuonekana kuwa kitu cha kawaida kisichoepukika.
Kama ifunuavyo Biblia, kifo kilisababishwa na dhambi, kwa kutomtii Mungu. Kama wazazi wetu wa kwanza wangebaki watiifu, wangeishi milele, pamoja na watoto wao. Kwa kweli, Mungu alibuni akili ya kibinadamu ikiwa na tamaa ya kuishi milele. “Pia ameweka umilele ndani ya mioyo ya wanadamu,” yasema Mhubiri 3:11, kulingana na New International Version. Kwa hiyo, kuhukumiwa kwao kifo kulizusha pambano la kindani katika wanadamu, pambano la daima.
Ili kupatanisha pambano hili la kindani na kutuliza tamaa ya asili ya kutaka kuendelea kuishi, wanadamu wamebuni itikadi za namna zote, kuanzia lile fundisho la kutokufa kwa nafsi hadi itikadi ya kuzaliwa upya katika umbo jingine. Wanasayansi wanachunguza fumbo la kuzeeka kwa kuwa wao pia wanataka kuepa kifo au angalau kukiahirisha. Wanamageuzi waatheisti hupuuza tamaa ya uhai udumuo milele kuwa udanganyifu wa mageuzi, kwa kuwa huo hupingana na maoni yao ya kwamba wanadamu ni wanyama tu wa hali ya juu. Kwa upande mwingine, taarifa ya Biblia kwamba kifo ni adui hupatana na tamaa yetu ya asili ya kutaka kuishi.—1 Wakorintho 15:26.
Basi, je, miili yetu huonyesha kwa njia yoyote kwamba tulikusudiwa tuishi milele? Jibu ni ndiyo! Ubongo wa binadamu pekee una uthibitisho wa kushangaza wa kwamba tuliumbwa tuishi kwa muda mrefu zaidi ya tuishivyo.
Tuliumbwa Tuishi Milele
Ubongo una uzito wa kilogramu 1.4, na una nyuroni kati ya bilioni 10 hadi bilioni 100, na yasemekana kwamba hakuna nyuroni ambazo hufanana kabisa. Kila nyuroni yaweza kuwasiliana na nyuroni nyingine 200,000, zikifanya njia katika ubongo ziwe nyingi sana. Zaidi ya hayo, “kila nyuroni ni kompyuta ya hali ya juu sana,” lasema gazeti Scientific American.
Ubongo hutumia kemikali nyingi ambazo huathiri namna nyuroni zinavyotenda. Na ubongo ni tata zaidi hata kuliko kompyuta yenye nguvu nyingi zaidi. “Ndani ya kila kichwa,” waandika Tony Buzan na Terence Dixon, “kuna kiungo chenye nguvu nyingi za kutisha, chenye kushikamana ambacho uwezo wake huonekana kana kwamba hauna kikomo kadiri tujifunzavyo mengi zaidi juu yake.” Wakimnukuu Profesa Pyotr Anokhin, waongezea hivi: “Bado hakuna mtu aliye hai awezaye kutumia uwezo wote wa akili yake. Ndiyo sababu hatukubali makadirio yoyote yasiyofaa juu ya mipaka ya ubongo wa binadamu. Hauna mipaka.”
Mambo haya ya kushangaza hupingana moja kwa moja na nadharia ya mageuzi. Kwa nini mageuzi ‘yangewabunia’ watu wa hali ya chini wenye kukaa mapangoni, au hata kuwabunia watu wa kisasa walioelimika sana, kiungo kilicho na uwezo wa kutumika kwa muda wa maisha uzidio milioni mara kadhaa au hata mabilioni kadhaa? Kwa kweli, ni uhai udumuo milele tu ulio na maana! Lakini namna gani mwili wetu?
Kitabu Repair and Renewal—Journey Through the Mind and Body chataarifu hivi: “Namna ambavyo mifupa iliyovunjika, tishu, na viungo hujiponesha kwa kweli ni muujiza. Kama tungechukua muda kufikiri juu ya jambo hili, tungetambua kwamba ile hali ya ngozi na nywele na makucha kujifanyiza upya—na vilevile sehemu nyingine za mwili—kuwa yenye kushangaza sana: Hiyo huendelea saa 24 kwa siku, mfululizo, ikitufanyiza upya kihalisi, mara nyingi katika muda wote wa maisha zetu.”
Katika wakati wa Mungu uliowekwa, halitakuwa tatizo kwake kuendeleza kwa wakati usio dhahiri utaratibu huu wa kimuujiza wa kujifanyiza upya. Ndipo, hatimaye, “kifo kitafanywa kuwa si kitu.” (1 Wakorintho 15:26) Lakini ili tuwe wenye furaha kikweli, twahitaji zaidi ya uhai udumuo milele. Twahitaji amani—amani pamoja na Mungu na wanadamu wenzetu. Amani hiyo yaweza kupatikana tu ikiwa watu wanapendana kwa kweli.
Ulimwengu Mpya Unaotegemea Upendo
“Mungu ni upendo,” lasema 1 Yohana 4:8. Upendo ni wenye nguvu sana—hasa upendo wa Yehova Mungu—hivi kwamba ndiyo sababu ya msingi ambayo huweza kutufanya tutumaini kuishi milele. “Mungu aliupenda ulimwengu sana,” lasema Yohana 3:16, “hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.”
Uhai udumuo milele! Ni tazamio la kustaajabisha kama nini! Lakini kwa kuwa tumerithi dhambi, hatuna haki ya kupata uhai. “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” Biblia husema. (Waroma 6:23) Ingawa hivyo, kwa kupendeza, upendo ulimsukuma Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, afe kwa niaba yetu. Mtume Yohana aliandika hivi kuhusu Yesu: “Huyo alitoa nafsi yake kwa ajili yetu.” (1 Yohana 3:16) Ndiyo, alitoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kuwa “fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi” ili kwamba sisi ambao hudhihirisha imani katika yeye tufutiwe dhambi na kufurahia uhai udumuo milele. (Mathayo 20:28) Biblia hueleza hivi: “Mungu alituma Mwana wake mzaliwa-pekee kuingia katika ulimwengu ili tuweze kupata uhai kupitia kwake.”—1 Yohana 4:9.
Ni jinsi gani, basi, tupaswavyo kuitikia upendo ambao Mungu na Mwana wake wametuonyesha? Biblia yaendelea kusema hivi: “Wapendwa, ikiwa hivi ndivyo Mungu alivyotupenda, basi sisi wenyewe tuko chini ya wajibu kupendana.” (1 Yohana 4:11) Lazima tujifunze kupendana, kwa kuwa sifa hiyo itakuwa msingi wa ulimwengu mpya wa Mungu. Leo wengi wamethamini umuhimu wa upendo, kama vile unavyosisitizwa na Yehova Mungu katika Neno lake, Biblia.
Kitabu Love and Its Place in Nature kilisema kwamba bila upendo “watoto huelekea kufa.” Na bado, uhitaji huo wa upendo hauishi watu wazeekapo. Mtaalamu mmoja mashuhuri wa elimu ya binadamu hata alisema kwamba upendo “huwa jambo kuu zaidi katika mahitaji yote ya kibinadamu kama vile jua lilivyo la maana zaidi katika mfumo wetu wa jua . . . Mtoto ambaye ameonyeshwa upendo huwa tofauti sana na mtoto ambaye hakuonyeshwa upendo kimwili, kifiziolojia, na kisaikolojia. Watoto wasioonyeshwa upendo hata hukua kwa njia tofauti na wale walioonyeshwa upendo.”
Je, waweza kuwazia jinsi maisha yatakavyokuwa wakati watu wote duniani watakapopendana kikweli? Kwani, hakutakuwa na mtu yeyote kamwe atakayekuwa na ubaguzi eti kwa sababu mtu ni wa taifa tofauti, ni wa jamii tofauti, au ana rangi ya ngozi iliyo tofauti na yake! Chini ya usimamizi wa Mfalme wa Mungu aliyewekwa rasmi, Yesu Kristo, dunia itajawa na amani na upendo, katika utimizo wa Biblia wa zaburi hii iliyopuliziwa:
“Ee Mungu, mpe mfalme hukumu zako . . . Atawahukumu walioonewa wa watu, atawaokoa wahitaji, atamseta mwenye kuonea. . . . Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma. Na awe na enzi toka bahari hata bahari, toka Mto hata miisho ya dunia. Kwa maana atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.”—Zaburi 72:1, 4, 7, 8, 12, 13.
Waovu hawataruhusiwa kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu, kama vile inavyoahidiwa na zaburi nyingine ya Biblia: “Watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi. Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:9-11.
Ndipo, akili na miili ya wanadamu wote watiifu, kutia ndani wale watakaoinuliwa kutoka makaburini kupitia ufufuo wa wafu, itakuwa imeponywa. Hatimaye, kila mtu atakayekuwa hai atadhihirisha kikamili mfano wa Mungu. Hatimaye lile shindano kubwa la kufanya lililo sawa litakuwa limeisha. Lile pigano kati ya kutamani kuishi na hali mbaya zilizo halisi za kisasa za kifo zitakuwa zimeisha pia! Ndiyo, hii ndiyo ahadi hakika ya Mungu wetu mwenye upendo: “Kifo hakitakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4; Matendo 24:15.
Kwa hiyo, usizimie kamwe katika pigano la kufanya lililo sawa. Sikiza onyo hili la upole la kimungu: “Pigana pigano bora la imani, pata mshiko imara juu ya uhai udumuo milele.” Uhai huo katika ulimwengu mpya wa Mungu ndio Biblia huuita “uhai ulio halisi.”—1 Timotheo 6:12, 19.
Na uthamini ukweli huu unaoelezwa katika Biblia: “BWANA ndiye Mungu; Ndiye aliyetuumba.” Kuthamini ukweli huo ni hatua muhimu kuelekea kustahili uhai katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye upendo na uadilifu.—Zaburi 100:3; 2 Petro 3:13.
[Blabu katika ukurasa wa 11]
Uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu ndio uitwao na Biblia kuwa “uhai ulio halisi.”—1 Timotheo 6:19
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wanadamu wamevunja kingo za sheria za Mungu, kwa matokeo yenye msiba
[Picha katika ukurasa wa 10]
Chini ya utawala wa Mungu, wanadamu watafurahia ulimwengu mpya wenye amani