Ahadi Ambayo Nimeazimia Kutimiza
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MARIAN TSIBOULSKI
MNAMO Februari 1945, nilikuwa mwanajeshi mwenye umri wa miaka 20 katika jeshi la Sovieti, ambalo lilikuwa limewarudisha nyuma Wajerumani mamia ya kilometa hadi nchi yao. Kila siku nilikuwa nikiona maogofyo ya vita, huku wenzangu wakifa kotekote. Tulikuwa tumekaribia Breslau, Ujerumani, ambao kwa wakati huu ni Wrocław, Poland. Jioni moja huko, nikiwa nimechoshwa na machinjo na kuteseka, nilimwahidi Mungu kwamba kama angeniwezesha nirudi nyumbani salama, ningetumia maisha yangu kufanya mapenzi yake.
Miezi mitatu baadaye, Ujerumani ilishindwa. Baada ya kutoka jeshini, Desemba 1945 niliingia Rogizno, kijiji kilichoko karibu na Lvov (sasa unaitwa Lviv), Ukrainia, nyumbani kwa babangu. Asubuhi iliyofuata nilikutana na mmoja wa Mashahidi wa Yehova naye alinihubiria kwelikweli kuhusu Ufalme wa Mungu. Ingawa tayari nilikuwa nimejua kidogo juu ya Biblia na hata nilikuwa nimesoma vichapo fulani vya Mashahidi, sasa moyo wangu uliguswa. Nikatambua kwamba ahadi yangu ilihusika na kukutana na huyo Shahidi.
Natimiza Ahadi Yangu
Upesi nilipata kazi ya kufundisha kwenye shule ya msingi. Lakini muda usiozidi miaka miwili baadaye, wakati ambapo mkuu wa elimu wilayani alipotoa amri ya kwamba ni lazima watoto wafundishwe kwamba hakuna Mungu, nilifutwa kazi. Karibu na wakati huo, Mei 1947, nilianza kushiriki katika huduma ya kuhubiri peupe na Mashahidi wa Yehova. Mashahidi walinitia moyo nihamie kusini kwenye mji wa Borislav, ambako upesi nilipata kazi ya fundi wa umeme.
Mjini Borislav, nilikutana na watu ambao walikuwa wamekuwa Mashahidi tangu miaka ya 1930. Walikuwa na vichapo vingi vya Biblia, ambavyo nilivisoma sana, kutia ndani mabuku ya Studies in the Scriptures, na vitabu vingi vilivyoandikwa na Joseph F. Rutherford, aliyekuwa msimamizi wa zamani wa Watch Tower Society. Pia nilisoma makala za zamani za Mnara wa Mlinzi na The Golden Age (sasa ni Amkeni!), ambayo baadhi ya Mashahidi walikuwa nayo. Lakini kilichonivutia zaidi ni mkusanyo wa barua zilizoandikwa na Mashahidi wa Ujerumani ambao walikuwa wamehukumiwa kifo chini ya utawala wa Hitler. Barua hizo zilikuwa zimetafsiriwa katika Kipoland, zikarudufishwa, na kutolewa kwa njia ya kijitabu. Baadaye, nilipata nguvu za kuvumilia majaribu nilipokumbuka uaminifu-maadili wa ndugu hao wa Ujerumani.
Hatimaye, nilibatizwa mwaka wa 1949 kwenye mojawapo ya maziwa ya Borislav, kwa njia hiyo nikitekeleza rasmi ahadi niliyotoa nikiwa vitani ya kumtumikia Mungu. Lakini sasa hiyo ilikuwa ahadi yenye kutegemea ujuzi sahihi.
Majaribu Yangu Yaanza
Punde si punde nilifutwa kazi. Basi mnamo Februari 1950, nikahamia jiji la Stry lililokuwa karibu, ambako nilipata tena kazi ya fundi wa umeme. Nilikaribishwa kwa uchangamfu na ndugu zangu Wakristo na hata wakanialika niongoze Ukumbusho wa kila mwaka wa kuadhimisha kifo cha Yesu Kristo ambao ungefanywa majuma machache baadaye.
Wakati huu, watu walizidi kuwachokoza na kuwatisha Mashahidi. Tulikuwa tukifuatwa-fuatwa na polisi wa KGB. Basi tulitahadhari tulipojitayarishia uwezekano wa kukamatwa na kuhojiwa. Kuimba nyimbo za Ufalme kwenye mikutano kulitusaidia tubaki tukiwa imara.
Mnamo Julai 3, 1950, niliombwa nitie sahihi ile hati ya Ombi la Stockholm, ambayo ilikuwa ombi la kupinga kutengenezwa kwa silaha za nyuklia na inaripotiwa kwamba ombi hilo lilitiwa sahihi na zaidi ya watu 273,000,000, hasa wakazi wa nchi za Kikomunisti. Nilipokataa kutia sahihi yangu, nikieleza kwamba sikuunga mkono upande wowote kisiasa, nilifutwa kazi tena. Kufuatia tukio hilo, nilikamatwa, nikafanyiwa kesi, nikahukumiwa kifungo cha miaka 25 katika kambi ya kazi ngumu.
Nahama Kambi Hadi Kambi
Mnamo Desemba 1950, wengi wetu tuliwekwa katika behewa la kubebea ng’ombe na kupelekwa umbali upatao kilometa 3,000 katika eneo lililo karibu na kaskazini mwa Milima ya Ural, ambalo hugawanya kidogo Urusi ya Asia na Urusi ya Ulaya. Hapo nilifungwa katika kambi nyingi tofauti-tofauti. Nilitendwa kwa njia ileile katika kila kambi—kazi ngumu na chakula haba. Miezi miwili au mitatu ilitosha kuwageuza wanaume wenye afya nzuri kuwa kama maiti tu. Wengi walikufa. Hatukuwazia kuokoka, hasa sisi ambao tulikuwa tumehukumiwa vifungo virefu.
Mwaka ambao sikuwa na kichapo cha Biblia wala kuwasiliana na Mashahidi wengine ulikuwa mgumu zaidi kwangu. Upweke huo ulinitesa kabisa. Lakini niliimarishwa kiroho wakati wafungwa fulani waliposikiliza nilipokuwa nikiongea nao juu ya Ufalme wa Mungu. Hatimaye, sala yangu ya kutoka moyoni ilijibiwa, nikahamishwa kilometa zipatazo 2,000 kusini-mashariki kwenye sehemu yenye kambi nyingi katika jiji jipya la Angarsk, mashariki mwa Siberia. Kiwanda kikubwa cha kemikali kilikuwa kinajengwa huko, na kazi nyingi zilikuwa zinafanywa na wafungwa.
Mimi nilikuwa katika Kambi ya 13, karibu na mahali pa kujengea kiwanda. Nikakutana mara moja na Mashahidi wengine huko, wakanipa makala za karibuni zaidi za Mnara wa Mlinzi na Informant, kama vile Huduma ya Ufalme Yetu ilivyokuwa ikiitwa. Nikawa na karamu kubwa ya kiroho! Lakini vichapo hivyo vyote vilitoka wapi?
Aprili 1951, maelfu ya Mashahidi katika Ukrainia walikuwa wamehamishwa hadi Siberia, wengi wao wakienda kwenye maeneo ambayo si mbali na Angarsk. Ndugu hao walipata na kufanyiza makala za Mnara wa Mlinzi na vichapo vinginevyo kwa siri, kisha waliviingiza kisiri katika kambi. Tuliweza kupata Biblia pia. Tuliigawanya katika sehemu mbalimbali, ambazo tuligawanyana miongoni mwetu. Basi, iwapo kuna msako ni sehemu moja tu ya Biblia ingepotea. Hata tuliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika kambi!
Mwishoni mwa 1952, nilihamishwa hadi Kambi ya 8. Machi uliofuata tulisherehekea Ukumbusho katika chumba kidogo ambamo wafungwa walikuwa wameweka vitu vyao vya kibinafsi. Kulikuwa na watu 12 tu—Mashahidi 3 na watu 9 wenye kupendezwa. Kwa njia fulani wenye mamlaka waligundua kwamba tulikuwa tumefanya mkutano, nikahamishwa hadi Kambi ya 12 kwa sababu waliniona kuwa “mchocheaji sugu.” Mashahidi wengine watano, ambao pia walikuwa wakiadhibiwa kwa ajili ya kuhubiri, tayari walikuwa katika kambi hiyo. Tulipokuwa huko, tulilazimika kuchimba msingi mkubwa kwa sururu na sepetu tu.
Wafungwa wengi waliokuwa katika Kambi ya 12 walikuwa wahalifu wabaya zaidi. Kwa wazi maofisa walifikiria kwamba tungevunjika moyo wakituweka pamoja nao. Lakini sisi tuliongea nao juu ya Ufalme wa Mungu, na katika makao yetu tuliimba nyimbo za Ufalme. Pindi moja, baada ya kumaliza kuimba, kiongozi wa ndani ya kambi aliguswa moyo akamfikia Shahidi mmoja na kusema: “Mtu yeyote athubutuye kukugusa, nitamwua!” Hata baadhi ya wahalifu hao walijifunza nyimbo zetu za Ufalme na kuimba nasi!
Katikati ya miaka ya 1953, Mashahidi wengi walihamishwa hadi Kambi ya 1 kutoka kambi nyinginezo. Mwanzoni, kulikuwa na Mashahidi 48 katika Kambi ya 1, lakini kwa kipindi kipunguacho miaka mitatu, tulikuwa tumeongezeka hadi 64. Kwa hakika, wakati huo watu 16 walichukua msimamo kwa ajili ya kweli ya Biblia na kubatizwa! Ingawa daima maofisa wa kambi walikuwa wakitafuta ushuhuda wa utendaji wa kidini, tuliweza kufanya mikutano yetu na ubatizo katika bafu ya kambi kwa sababu yule aliyeisimamia alikuwa Shahidi.
Uhuru, na Familia
Mwaka wa 1956 wengi wa Mashahidi waliokuwa katika kambi walifunguliwa, hivyo wajumbe wa habari njema wakatawanyika katika sehemu nyingi za eneo kubwa la Sovieti. Hukumu yangu ya kifungo cha miaka 25 ilikuwa imepunguzwa hadi miaka 10 na hatimaye ikapunguzwa hadi miaka 6 na miezi 6. Basi, nikafunguliwa pia Februari 1957.
Kwanza nilienda Biryusinsk, ambao ni mji ulio katika Siberia, kilometa zipatazo 600 kaskazini-magharibi ya Angarsk. Mashahidi wengi wa Ukrainia walikuwa wamehamishwa huko, nikafurahia kushiriki nao mambo yaliyoonwa na kujua juu ya Mashahidi wenzetu ambao tuliwafahamu. Kutoka hapo nikarudi Borislav, katika Ukrainia, ambako Shahidi mmoja wa Ukrainia aliyeitwa Eugenia Bachinskaja aliishi. Alikuwa amefunguliwa kutoka gerezani mwaka mmoja kabla yangu.
Eugenia alikuwa Shahidi thabiti ambaye alikuwa amehukumiwa kifo mnamo 1950 kwa sababu ya utendaji wake wa kuhubiri. Lakini, baada ya siku 18 akingojea kifo, hukumu yake ilipunguzwa kuwa miaka 25 katika kambi ya kipekee. Kuelekea mwishoni mwa 1957, niliporudi Ukrainia, tulifunga ndoa. Baada ya ndoa yetu, tulikusudia kuishi Borislav, ambako nilikuwa nimebatizwa miaka tisa awali. Badala yake, nilipewa muda wa saa 48 kuondoka Ukrainia!
Nikaenda Caucasus, kusini mwa Urusi, ambako Eugenia alinipata baadaye. Hata hivyo, baada ya kuishi hapo katika ghala moja kwa miezi sita hivi, tulienda Biryusinsk ili tujiunge na ndugu na dada zetu Wakristo waliokuwa uhamishoni. Kulikuwa na ndugu na dada wapatao 500 katika Biryusinsk na makutaniko matano, nikawekwa rasmi kuwa mwangalizi-msimamizi katika mojawapo ya makutaniko hayo. Mnamo 1959 binti yetu Oksana alizaliwa, na Marianna akafuata mwaka wa 1960. Tangu utotoni walihudhuria mikutano daima, nao wakakua katika utendaji wa kawaida wa kiroho katika Siberia.
Wenye mamlaka wa Siberia hawakuingilia sana utendaji wetu wa kutaniko, angalau kwa kulinganisha na vikwazo vikali vilivyokuwa vimewekwa juu ya kazi yetu katika Ukrainia. Lakini bado haikuwa rahisi kwa kutaniko letu lote kukutana pamoja. Mazishi yalitupa fursa za kukutana kwa wingi. Katika pindi hizi, ndugu kadhaa walikuwa wakitoa hotuba za Biblia zenye kufundisha. Lakini wenye mamlaka walipogundua yale yaliyokuwa yakitendeka, walichukua hatua. Kwa mfano, pindi moja msafara wa mazishi ulisimamishwa na jeneza likatwaliwa kwa nguvu hadi kwenye kaburi na kuzikwa.
Twarudi Ukrainia
Tulirudi Ukrainia mwaka wa 1965, tukakaa Kremenchug. Jiji hili, lililokuwa kilometa 800 hivi mashariki ya Borislav, lilikuwa na Mashahidi 12 pekee. Tuliishi hapo kwa miaka mitano hivi; wakati mwingi nikitumikia makutaniko nikiwa mwangalizi asafiriye. Mnamo 1969, binti zetu walipokuwa na umri wa miaka tisa na kumi, tuliombwa tuhamie kusini ili kusaidia ndugu katika mji mdogo wa Molochansk.
Huko Molochansk niliitwa na polisi wa KGB kwa mazungumzo yaliyochukua muda wa saa kadhaa. Kwa hakika niliitwa mara sita! Katika kila mojawapo ya mazungumzo hayo, niliahidiwa wakati ujao mzuri ikiwa ningekana uhusiano wangu na “Wayehova.” Hatimaye KGB ikakosa subira, na mimi na Shahidi mwingine tukafungwa gerezani kwa mwaka mmoja.
Baada ya kukamilisha kifungo hicho, katika 1973 nilihama na familia yangu tukaenda katika kijiji kidogo karibu na Kremenchug. Tulifanya mikutano yetu ya Kikristo kwa siri katika nyumba yetu, kutia ndani mwadhimisho wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo, mwaka wa 1974. Asubuhi iliyofuata nyumba yetu ilipekuliwa, nikakamatwa.
Kesi, Kambi ya Kazi Ngumu, na Uhamisho
Umma haukuruhusiwa kuhudhuria kesi yangu ila tu wale walioalikwa. Wale waliokuwapo walikuwa maofisa wa vyeo vya juu na viongozi wa jumuiya. Nilionelea nisiwakilishwe na wakili nikapewa dakika 45 za kujitetea. Siku moja kabla ya kesi, Eugenia na binti zetu walipiga magoti wakasali, wakiomba, si kwamba nisipewe adhabu kali au niachiliwe, bali kwamba nitoe ushahidi mzuri kuhusu Ufalme na jina takatifu la Yehova.
Kesi ilianza huku hakimu akisoma mafungu kadhaa katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Wasikilizaji waliitikia tofauti na alivyotarajia hakimu. Watu waliposikia kwamba ulimwengu huu mwovu ungeondolewa kwenye Har–Magedoni na kwamba Ufalme wa Mungu ungetawala dunia, walichanganyikiwa akili—wakishindwa waamini nini. Upesi hakimu akagundua kosa lake, na katika hoja zangu za kumalizia, alijaribu kujirudishia hadhi yake kwa kunikatiza-katiza. Lakini, kwa kusoma moja kwa moja vichapo vyetu, hakimu huyo alikuwa amesaidia kutoa ushahidi mzuri, moyo wangu ukajaa shukrani. Hata hivyo nikahukumiwa kifungo cha miaka mitano yenye kazi ngumu, ikifuatwa na miaka mitano uhamishoni.
Kwa miaka mitano iliyofuata nilikaa na wahalifu sugu kaskazini ya mbali katika kambi ya kazi ngumu ya Yodva katika Jamhuri Huru ya Komi ya Muungano wa Kisoshalisti wa Sovieti. Wakati huo nilikuwa na fursa ya kutoa ushahidi wa Ufalme kwa wafungwa wapatao 1,200 na vilevile kwa wasimamizi wa kambi. Baada ya kufunguliwa gerezani mnamo 1979, nilipelekwa uhamishoni katika Vorkuta, ndani ya Mzingo wa Aktiki. Punde si punde nikapata kazi na mahali pa kuishi katika Vorkuta, ambako familia yangu ilijiunga nami.
Imejulikana kwamba wafungwa wengi walikufa katika Vorkuta, kutia ndani Mashahidi wengi waliokuwa wafungwa katika miongo iliyokuwa imepita. Leo hilo ni jiji la kawaida, na kambi za kazi ngumu hazipo tena. Lakini chini ya barafu ya daima katika jiji hilo na vitongoji vyake kuna wengi sana waliofia imani kwa sababu ya kumsifu Yehova.
Shangwe ya Uhuru wa Kidini
Mnamo 1989 tulisafiri kutoka Vorkuta hadi Poland ili kuhudhuria mikusanyiko miwili ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova. Hatukuona haya kutoa machozi ya shangwe tulipotazama makumi ya maelfu ya ndugu na dada Wakristo jijini Warsaw na Katowice wakifurahia ushirika bila hofu ya kukamatwa. Ndoto yetu ilikuwa imetimia. Tulirudi Vorkuta tukiwa tumeazimia zaidi kutumikia masilahi ya Ufalme.
Lakini, tabia ya nchi ndani ya Mzingo Aktiki ni kali sana, na afya ya Eugenia ilikuwa imekuwa mbaya. Kwa hiyo baadaye mwaka huo tulihamia tena Kremenchug, ambako tunafurahia utumishi wetu kwa Yehova kwa uhuru mwingi zaidi ambao tunao sasa. Waume wa binti zetu wawili ni wazee katika kutaniko hapa Ukrainia. Na japo binti zetu wanalea watoto wanne, wao ni mapainia, kama waitwavyo watumishi wa wakati wote.
Pindi kwa pindi, bado mimi hukumbuka pale vitani mwaka wa 1945 na ahadi niliyoitoa zaidi ya nusu karne iliyopita. Ili niendelee kuitimiza, Yehova aliniandalia ujuzi sahihi, ujuzi uleule ambao umewezesha mamilioni ya wengine kufanya ahadi kama hiyo—ya kumtumikia Yehova milele.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 23]
URUSI
Vorkuta
Lviv
Borislav
UKRAINIA
Kremenchug
Molochansk
Caucasus
Biryusinsk
Angarsk
Tukiwa na binti zetu wawili, waume zao, na watoto wao wanne
[Hisani]
Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.