Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 7/8 kur. 20-22
  • Kuna Ubaya Gani wa Kuchezeana Kimapenzi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuna Ubaya Gani wa Kuchezeana Kimapenzi?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ikiwa Mtu Amefunga Ndoa
  • Mahusiano ya Kihisia-Moyo
  • Vipi Kuhusu Watu Ambao Hawajafunga Ndoa?
  • Je, Kuwachezea Wengine Kimapenzi Kuna Madhara?
    Vijana Huuliza
  • 1 Hutusaidia Kuepuka Matatizo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2018
  • Dumisha Usafi wa Kiadili kwa Kuulinda Moyo Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Suala Linalokuhusu Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 7/8 kur. 20-22

Maoni ya Biblia

Kuna Ubaya Gani wa Kuchezeana Kimapenzi?

“Kwa nini twafikiri kwamba ni vibaya kuchezea wengine kimapenzi? Si vibaya! Ni mchezo tu! Na ni mchezo ambao huwanufaisha wote wawili kwa sababu unamfanya yule mtu mwingine ahisi vizuri.”—Susan Rabin, mkurugenzi wa Shule ya Kuchezeana Kimapenzi, New York City.

WATU wengi huona kuchezeana kimapenzi kuwa jambo la kawaida na lisilodhuru, na hata kuwa muhimu katika kufanyiza na kudumisha mahusiano na watu. Katika nchi za Magharibi, hivi majuzi kumekuwa na ongezeko kubwa la vitabu, makala za magazeti, na mitaala ya kipekee ambayo hufundisha ishara za mwili, vikao na mitazamo ambazo ni muhimu katika “ustadi wa mchezo wa kimapenzi.”

Mchezo wa kimapenzi ni nini? Kuna ufafanuzi na maelezo mbalimbali. Kamusi moja inaufafanua kuwa “tabia ya kuonyesha ashiki kidogo au ya kushawishi kingono.” Kamusi nyingine yaufafanua kuwa tabia ya kuwa tu “mwenye ashiki bila makusudi mengine.” Kwa hiyo inaonekana kwamba kwa ujumla inakubalika kwamba mtu mwenye mchezo wa kimapenzi ni yule aonyeshaye ishara za kupendezwa kimapenzi lakini bila kusudi la kufunga ndoa. Je, kuchezeana kimapenzi kuonwe kuwa hakudhuru? Biblia ina maoni gani juu ya kuchezeana kimapenzi?a

Ingawa kuchezeana kimapenzi hakutajwi moja kwa moja katika Maandiko, tunaweza kujua maoni ya Mungu. Kwa njia gani? Kwa kuchunguza kanuni za Biblia zinazohusika na suala hili. Kwa hiyo twasitawisha ‘nguvu za ufahamu ili kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa.’ (Waebrania 5:14) Kwanza, ebu tuone kama kuchezeana kimapenzi ni tabia inayowafaa watu waliofunga ndoa.

Ikiwa Mtu Amefunga Ndoa

Ni jambo la kawaida kwa wenzi waliooana kuchezeana kimapenzi wakiwa faraghani. (Linganisha Mwanzo 26:8.) Lakini, kuchezeana kimapenzi na watu walio nje ya ndoa kunapinga kanuni za Mungu. Yehova alikusudia kwamba wenzi waliooana wafurahie uhusiano wa karibu na wenye kutumainika. (Mwanzo 2:24; Waefeso 5:21-33) Yeye aona ndoa kuwa takatifu na muungano wenye kudumu. Malaki 2:16 lasema hivi kuhusu Mungu: “Ninachukia talaka.”b—Biblia Habari Njema.

Je, mchezo wa kimapenzi unaofanywa na mtu aliyefunga ndoa unapatana na maoni ya Mungu juu ya ndoa? La hasha, mtu aliyefunga ndoa anayechezea mwingine kimapenzi aonyesha kwamba hastahi utakatifu wa mpango wa ndoa uliowekwa na Mungu. Kisha pia Waefeso 5:33 linaamuru mume Mkristo ‘ampende mke wake kama yeye mwenyewe’ na mke “kuwa na staha yenye kina kirefu kwa mume wake.” Je, kuchezeana kimapenzi ambako huzusha wivu kwaonyesha kwamba unampenda na kumstahi mwenzi wako?

Jambo zito hata zaidi ni kwamba kuchezeana kimapenzi kunaweza kusababisha uzinzi, dhambi ambayo Yehova hushutumu kabisa na kuiita hiana. (Kutoka 20:14; Mambo ya Walawi 20:10; Malaki 2:14, 15; Marko 10:17-19) Kwa kweli, Yehova aona uzinzi kuwa mbaya sana hivi kwamba anaruhusu waliokosewa kwa njia hiyo wapate talaka. (Mathayo 5:32) Basi, je, twaweza kuwazia kwamba Yehova angeruhusu jambo hatari kama kuchezeana kimapenzi? Mungu hawezi kuruhusu jambo hilo kama vile mzazi mwenye upendo asivyoweza kuruhusu mtoto wake mdogo acheze na kisu kikali kitumiwacho jikoni.

Kuhusu uzinzi Biblia inaonya hivi: “Je, mtu aweza kutia moto kifuani pake, na nguo zake zisiteketezwe? Je! mtu aweza kukanyaga makaa ya moto, na nyayo zake zisiungue? Ndivyo alivyo aingiaye kwa mke wa jirani yake; kila mtu amgusaye huyo atakuwa na hatia.” (Mithali 6:27-29, UV, chapa ya 1989) Lakini, hata kama uzinzi haufanywi, mtu aliyefunga ndoa ambaye anachezea mwingine kimapenzi anajihatarisha zaidi—kuhusika “kihisia-moyo.”

Mahusiano ya Kihisia-Moyo

Watu fulani wameanzisha mahusiano nje ya ndoa zao ambamo hisia za kihisia-moyo huibuka, ingawa hakuna mambo ya kingono yanayofanywa. Lakini Yesu alionya hivi: “Kila mtu ambaye hufuliza kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Kwa nini Yesu alipinga mapenzi ambayo yanabaki tu moyoni mwa mtu?

Jambo moja ni kwamba “kutoka moyoni huja . . . uzinzi.” (Mathayo 15:19) Lakini, uhusiano kama huo ni wenye kudhuru hata kama haujaendelea kufikia hatua ambapo wamo katika hatari ya kufanya uzinzi. Kwa njia gani? Kitabu kimoja chaeleza hivi juu ya suala hili: “Utendaji wowote au uhusiano wowote ambao unachukua muda mwingi sana na nishati nyingi sana kutoka maisha yako na mwenzi wako ni ukosefu wa uaminifu wa aina fulani.” Ndiyo, uhusiano wa kihisia-moyo huchukua wakati, uangalifu, na upendo wa mwenzi mmoja. Kwa kufikiria amri ya Yesu ya kwamba tuwatendee wengine kama tunavyotaka kutendewa, ni vizuri mtu aliyefunga ndoa kujiuliza, ‘Ningehisije ikiwa mwenzi wangu angefanya hivi na mtu mwingine?’—Mithali 5:15-23; Mathayo 7:12.

Ikiwa mtu amehusika kihisia-moyo kwa njia hiyo, yeye apaswa kufanya nini? Mtu aliyefunga ndoa mwenye uhusiano usiofaa wa kihisia-moyo ni kama dereva anayesinzia akiendesha gari. Anahitaji kuamka na kuchukua hatua ya mara moja kabla ya ndoa yake na uhusiano wake na Mungu kuharibika. Yesu alitoa kielezi cha uhitaji wa kuchukua hatua ya mara moja aliposema kwamba hata kitu chenye thamani kama jicho lapaswa kung’olewa au mkono ukatwe ikiwa utaharibu uhusiano mzuri kati ya mtu na Mungu.—Mathayo 5:29, 30.

Basi, lingekuwa jambo la hekima kupunguza wakati na mara ambazo mnaonana na yule mtu mwingine. Epuka kabisa kubaki na huyo mtu mkiwa peke yenu, na kama ni kazini, punguza mazungumzo yenu. Huenda hata ikahitajika kukatiza kabisa mawasiliano yote na mtu huyo. Kisha, udhibiti kabisa macho yako, mawazo yako, hisia zako, na tabia zako. (Mwanzo 39:7-12; Zaburi 19:14; Mithali 4:23; 1 Wathesalonike 4:4-6) Yobu, aliyekuwa amefunga ndoa, aliweka kielelezo chema aliposema hivi: “Nilifanya agano na macho yangu; basi nawezaje kumwangalia msichana?”—Ayubu 31:1.

Kwa wazi, ni hatari na si jambo la kimaandiko kwa mtu aliyefunga ndoa kuchezea mwingine kimapenzi. Lakini, Biblia ina maoni gani juu ya waseja wenye kuchezeana kimapenzi? Je, kuonwe kuwa jambo la kawaida, lisilodhuru, au hata la lazima ili kuanzisha mahusiano na watu wa jinsia tofauti? Je, kuna madhara yoyote yawezayo kutokea?

Vipi Kuhusu Watu Ambao Hawajafunga Ndoa?

Hakuna ubaya kwa waseja wawili kuonyeshana mahaba, maadamu wanafikiria ndoa na kwamba waepuke mwenendo mchafu. (Wagalatia 5:19-21) Upendezi kama huo waweza kutukia mapema katika wakati wa uchumba ambapo ndoa haijafikiriwa sana. Si lazima upendezi huo wa kimapenzi uwe mbaya maadamu kuna makusudi mazuri. Mwenendo kama huo hasa si kuchezeana vibaya kimapenzi.

Ingawa hivyo, namna gani kama waseja wanaonyeshana ishara za kuchezeana kimapenzi kwa ajili ya raha tu? Huenda ikaonekana kuwa haidhuru kwa kuwa hawajafunga ndoa. Lakini, fikiria uwezekano wa kuumia kihisia-moyo. Tabia ya mwenye kucheza kimapenzi ikichukuliwa kwa uzito kuliko alivyokusudia, hiyo yaweza kutokeza maumivu makali na kuugua kwa moyo. Maneno ya Mithali 13:12 ni kweli kama nini: “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima”! Hata kama watu wawili wanadai kwamba wameelewana kwamba hakuna mmoja wao apendezwaye na mwenzake sana—je, kweli yeyote kati yao aweza kuwa na hakika juu ya afikiriayo au ahisivyo yule mwingine? Biblia inajibu: “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua?”—Yeremia 17:9; linganisha Wafilipi 2:4.

Fikiria pia hatari ya kufanya uasherati, kukiwa na hatari ya kuambukizwa maradhi au kutungwa mimba haramu. Uasherati umekataliwa katika Maandiko, na wale ambao wanaufanya kimakusudi hupoteza upendeleo wa Mungu. Mtume Paulo aliwatahadharisha Wakristo kwa hekima kwamba ili waweze kukinza kishawishi, wao walipaswa ‘kufisha viungo vyao vya mwili kwa habari ya uasherati’ na waepuke “hamu ya ngono,” ambayo husababisha uasherati. (Wakolosai 3:5; 1 Wathesalonike 4:3-5) Kwenye Waefeso 5:3, yeye atushauri kwamba uasherati “hata usitajwe” yaani kwa njia ya kuamsha tamaa mbaya. Kuchezeana kimapenzi hakupatani na shauri hilo. Mungu hata hukataza mazungumzo yasiyofaa kuhusu ngono.

Kanuni za Biblia zafunua kwamba kuchezea wengine kimapenzi kwaweza kuwaumiza na kuonyesha hatumstahi Yehova, aliye Mwanzilishi wa ndoa. Maoni ya Biblia juu ya kuchezeana kimapenzi kusikofaa kwa hakika ni yenye upendo na yenye kufaa, kwa kuwa yanalinda watu wasipatwe na madhara. Basi, wampendao Mungu wataepuka kuchezeana kimapenzi na kuwatendea watu wa jinsia tofauti kwa usafi wa kiadili na staha.—1 Timotheo 2:9, 10; 5:1, 2.

[Maelezo ya Chini]

a Kuchezeana kimapenzi kusifikiriwe isivyofaa kuwa urafiki, bila kusudi lolote la kimapenzi.

b Ona makala “Mungu Huchukia Talaka ya Aina Gani?” katika toleo la Amkeni! la Februari 8, 1994.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]

© The Curtis Publishing Company

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki