Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 8/22 kur. 16-19
  • Msiba wa Barafu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Msiba wa Barafu
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Ukanda wa Vita Ulio Maridadi”
  • Kunusurika Maafa
  • Walisaidiana
  • Ni Masomo Gani Waliyojifunza?
  • Hadithi za Biblia Zasimuliwa kwa Barafu na Theluji
    Amkeni!—2005
  • Kuvua Samaki Kwenye Barafu
    Amkeni!—2004
  • Kitu Kisichoweza Kuharibiwa na Dhoruba
    Amkeni!—2003
  • Baada ya Dhoruba—Kutoa Misaada Huko Ufaransa
    Amkeni!—2000
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 8/22 kur. 16-19

Msiba wa Barafu

“MSIBA wa asili ulio mbaya zaidi katika historia ya taifa.” Ndivyo gazeti The Toronto Star lilivyoiita dhoruba ya barafu ya mwezi huu wa Januari iliyoharibu kabisa mikoa ya Kanada ya Ontario, Quebec, na New Brunswick. Huko Marekani, Rais Bill Clinton aliyatangaza maeneo ya Maine na New Hampshire vilevile sehemu za Vermont na sehemu ya kaskazini ya jimbo la New York, kuwa maeneo ya msiba.

Inasemekana kwamba vifo vipatavyo 35 vilisababishwa na dhoruba, ambayo ilitia ndani siku tano za mvua ya barafu. Kwa kawaida mvua kama hiyo huchukua muda wa saa chache tu, lakini katika pindi hii tabaka ya hewa yenye joto ilibaki juu ya hewa baridi. Kwa hiyo mvua ilipoanguka, iliganda mara moja. Kukatokea tabaka za barafu zenye unene wa sentimeta nane. Kwa sababu ya uzito wa barafu, miti mingi, nyaya za umeme, na minara ya kupitishia umeme ilianguka, mara nyingi kwa matokeo yenye kuogofya.

Katika Quebec, mamia ya minara ya kupitishia umeme iliyotengenezwa kwa chuma ilianguka kana kwamba ilikuwa imetengenezwa kwa mabati. Msafiri mmoja mwenye wasiwasi alisimulia hivi: “Niliona mbele yangu [mnara] ukijikunja kana kwamba ulikuwa wa plastiki. Ulijikunja mara mbili, kisha ukawa kama mpira, na kuvunjika. Nyaya za umeme zilienea barabarani kote. Mnara wa kwanza ulipoanguka, minara mitatu iliyokuwa nyuma ya huo ilianguka.”

Rundo la barafu liliangusha nyaya za umeme zenye urefu uzidio kilometa 120,000, zinazotosha kuzunguka dunia mara tatu! Katika Kanada, kati ya watu milioni tatu hadi nne hawakuwa na umeme na moto, wengine kwa majuma matatu na zaidi.

Katika Maine, ambapo Gavana Angus King alitangaza hali ya dharura, zaidi ya watu 200,000 hawakuwa na umeme. “Huu ndio msiba mkubwa zaidi wa aina hii ambao umewahi kuathiri jimbo hili,” akasema huyo gavana. Gavana wa New York George Pataki alitangaza hivi: “Kuna majiji mazima yasiyokuwa na umeme kabisa.”

Kandokando ya ufuo wa kusini wa Mto St. Lawrence, vigingi vya umeme karibu 30,000 viliharibiwa wakati wa dhoruba. Baada ya muda wa saa 17 za mvua ya barafu, Jim Kelly, anayeishi karibu na mto huo katika kaskazini mwa New York, aliandika hivi: “Hatuwezi kuona kitu chochote tukiwa dirishani tena. Si ukungu au mvuke tu bali barafu kamili. Makelele yanasikika kutoka kila upande wa nyumba.”

Kelly aeleza hivi: “Kwa mbali waweza kusikia sauti kama mlio wa bunduki. Bang! Kimya. Bang! Kimya. Bang, bang!” Baadaye, alipata habari kwamba makelele yalikuwa yakitokana na miti iliyokuwa ikianguka na kuvunjika kwa vigingi vya simu.

Kwa kinyume, mandhari ilitokeza sura ya kupendeza, licha ya uharibifu uliotokea. Kulikuwa na hofu kwamba huenda Ontario ilipoteza miti ya maple milioni 20, ikiathiri uuzaji wa shira inayotokana na mti huu. Mkulima mmoja aliomboleza hivi: “Miti ilifanana na vijiti vilivyochongoka vinavyoelekea angani.”

“Ukanda wa Vita Ulio Maridadi”

Hicho kilikuwa ndicho kichwa cha habari cha gazeti Toronto Star kikieleza juu ya Montreal, jiji la pili kwa ukubwa katika Kanada. Mkazi mmoja alisema hivi kwa mshangao: “Barabara hapa zaonekana kana kwamba zimelipuliwa kwa mabomu!” Kadirio la mapema la uharibifu katika eneo la Montreal pekee lilikuwa zaidi ya dola milioni 500.

Mkazi katika Belleville, Ontario, alisema: “Inaonekana kana kwamba vita vya nyuklia vimeisha. Vumbi nyeupe imetanda juu ya kila kitu, inatisha.” Aliiita “umaridadi wa kutisha.”

Juma lililofuatia dhoruba, wakati ambapo mamia ya maelfu ya watu walikuwa hawana umeme bado na baridi ilikuwa kali sana, polisi walianza kuhamisha watu waende kwenye makao. “Je, tuwaombe au tuwaamuru?” akauliza ofisa mmoja.

“Wanapaswa kutoka,” akajibu msimamizi. “Lakini uwe mwenye busara kuhusu jambo hili.” Akaongezea: “Ungefikiri tulikuwa katika wakati wa vita.”

Kunusurika Maafa

Kwa sababu ya ukosefu wa umeme katika sehemu nyingi za Montreal, taa za kuongoza magari ziliacha kufanya kazi na huduma za reli za chini ya ardhi zilisimamishwa. Kufikia siku ya mwisho ya dhoruba, vituo vinne vya umeme kati ya vitano vinavyohudumia jiji ama vilizima au viliharibika. Matokeo yangekuwa nini?

“Alasiri tulijipata tukiwa bila umeme hata kidogo katika Montreal—bila maji,” akaeleza Waziri Mkuu wa Quebec Lucien Bouchard. “Kulibakia muda wa saa mbili tu za kupata maji kwa sababu vituo viwili vya kuchuja maji vilikuwa vimezima.” Kwa kuwa watu walitumia mishumaa na kulikuwa na uwezekano wa kukosa maji kabisa, uwezekano wa maafa uliongezeka hata zaidi.

Maafa mengine yalizuiwa karibu majuma mawili baadaye wakati ambapo kikundi cha watu 1,889 kilipokusanyika mnamo Januari 24 kwa ajili ya kusanyiko la mzunguko kwenye Jumba la Kusanyiko la Montreal la Mashahidi wa Yehova. Usiku kucha, zaidi ya sentimeta 20 za theluji zilikuwa zimefunika Montreal, na wakati wa programu ya asubuhi ya kusanyiko, madhara yalionekana kwenye kuta na dari. Programu ya alasiri ilifutwa, na waliohudhuria wakaombwa waende nyumbani, wabadili mavazi yao, na kurudi kwenye Jumba la Kusanyiko ili kufanya kazi.

Katika muda wa saa moja wajitoleaji 300 wakiwa na sepetu, sululu, na vyombo vingine walianza kuondoa theluji kwenye paa kubwa lenye meta za mraba 7,100. Theluji iliyokuwa juu ilipoondolewa, iligunduliwa kwamba katika sehemu fulani barafu ilikuwa na unene unaozidi sentimeta 60! Misumeno ya umeme ilitumiwa kukata barafu katika vipande vya mraba, kisha vikakokotwa mpaka kwenye ukingo wa paa na kuangushwa. Tani zipatazo 1,600 za theluji na barafu ziliondolewa! Baadaye uchunguzi ulifunua kwamba kama matokeo, dari ilijirudisha mahali pake na nyufa katika kuta zikajiziba. Programu ikaanza tena Jumapili asubuhi kwa usalama.

Walisaidiana

Kweli, watu fulani katika eneo hilo walijaribu kujinufaisha kutokana na taabu ya wengine wakati wa mvua na baridi, lakini kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, wengi walionyesha “fadhili ya kibinadamu isiyo ya kawaida.” (Matendo 28:2) Gazeti Daily Sentinel la Rome, New York, lilisema hivi kuhusu Mashahidi wa Yehova walioenda kuwasaidia watu: “Watu hao walikutana kwenye Jumba la Ufalme katika Watertown ili kujipanga na kutoka hapo walipewa migawo ya kwenda kwenye nyumba za washiriki wao mbalimbali. Lakini waliwasaidia majirani zao kotekote mtaani pia.”

Makala hiyo ilisema kwamba jitihada hizi za kutoa msaada ziliratibiwa watu kutoka “ng’ambo ya eneo la Adams, Potsdam, Malone, Ogdensburg, Plattsburgh, Massena, Gouverneur, na Ellenburg.” Wajitoleaji fulani waliandaa moto kwa nyumba kadhaa kwa saa chache kwa kuunganisha jenereta ili kuwasha tanuri. Kwa kusikitisha, kiwango cha halijoto kilipungua na kufikia chini ya sufuri katika maeneo mengi baada ya dhoruba.

Katika pindi moja polisi waliwaona Mashahidi wakizuru nyumba fulani na wakawachukulia kimakosa kuwa wezi. Mashahidi walipoeleza walichokuwa wakifanya, mmoja wa polisi alisema kwamba baada ya dhoruba, baba yake ambaye anaishi Montreal, alisaidiwa na Mashahidi wa Yehova, hata ingawa baba yake si Shahidi. Mwana huyo alithamini msaada uliotolewa.

Iliyoathiriwa hasa na dhoruba ilikuwa miji fulani 100 kusini ya Montreal katika eneo linaloitwa “eneo la giza.” Siku kumi baada ya dhoruba, miji hii bado haikuwa na umeme. Kwa kweli, watu wengi hawakuwa na umeme kwa zaidi ya mwezi mmoja! Mipango ilifanywa na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova karibu na Toronto ili ziara za pekee zifanywe kusaidia wanaoishi katika eneo hili. Ugavi kutia ndani mafuta ya taa, betri, na tochi ulisafirishwa kwa lori mpaka kwenye eneo lililochaguliwa kuwa kituo cha ugawanyaji, na kutoka hapo misaada ikagawanywa kwa waliokuwa na uhitaji.

Pia mipango ilifanywa kwa wazee Wakristo kuamua mahitaji ya wale walioishi katika maeneo haya. Kikundi kimoja cha wazee kilizuru makutaniko 11 kwa juma moja, na kuongoza mikutano mingi yenye kutia moyo. Baada ya mikutano hiyo, ambapo kitia-moyo cha kiroho kilitolewa, hakuna mtu aliyetaka kurudi nyumbani. Watu walikaa na kukaa, wakiongea na kuhadithiana, wakifurahia ushirika. Kwa kweli, hudhurio la kawaida la mikutano lilifikia kilele cha juu kabisa katika majuma ya baada ya dhoruba.

Wengi waliokuwa na chanzo fulani cha moto, kama vile jiko la kuni au jenereta ya kuandaa umeme, waliwakaribisha nyumbani mwao wale ambao hawakuwa na vifaa hivi. Mashahidi fulani walikuwa na watu wengi kama 20 hivi wakikaa pamoja nao. Pia wengi waliokuwa nje ya eneo lililopoteza umeme waliandaa malazi. Kwa kielelezo, Mashahidi katika Sept-Îles, jiji lililo kilometa zipatazo 800 kutoka “eneo la giza,” walijitolea kuandaa malazi kwa familia 85.

Mashahidi katika maeneo ya mbali ya mashambani, kama vile Rimouski, walikata na kusafirisha kuni. Wengine walitumia muda fulani kuandika maandiko kwenye magogo waliyotuma. Shahidi mmoja alishiriki zawadi yake ya kuni na jirani yake asiye Shahidi, ambaye alipata gogo lililoandikwa Zaburi 55:16 juu yake: “Na BWANA ataniokoa.” Akiwa amelibeba gogo hilo mikononi, jirani huyo alitazama juu na kusema: “Asante, Yehova.”

Ni Masomo Gani Waliyojifunza?

Wengi walishtuliwa na kutotegemeka kwa nguvu za umeme na jinsi walivyozitegemea. “Nakuhakikishia, tutakapojenga nyumba mpya,” akasema mtu mmoja, “kutakuwako jiko la kuni, kutakuwako jenereta . . , na kutakuwako jiko linalotumia gesi.”

Karibu majuma sita baada ya dhoruba, mtazamaji mmoja alisema hivi: “Kulikuwako barafu nyingi, giza jingi, muda mwingi wa kufikiri, ambapo inakuwa rahisi kufanya bila televisheni.” Kisha akasema: “Tumeshangazwa na jinsi tunavyoweza kudhuriwa na hali mbaya za hewa.”

Wanafunzi wa Biblia hutafakari juu ya ahadi ya Muumba ya kurudisha dunia kuwa paradiso ya tufeni pote baada ya kuondoa mfumo huu wa mambo, kama vile alivyoondoa ulimwengu kama huo wakati mmoja hapo awali. (Mathayo 24:37-39; 2 Petro 2:5) Akitaja juu ya silaha awezazo kutumia, Mungu auliza hivi: “Je, umeziingia ghala za theluji, au umeziona ghala za mvua ya mawe [kutia ndani mvua ya barafu], nilizoziweka akiba kwa wakati wa misiba, kwa siku ya mapigano na vita?”—Ayubu 38:22, 23.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Minara ya kupitishia umeme ilivunjika kama mabati

[Picha katika ukurasa wa 18]

Msiba ambao ungeweza kutokea ulizuiwa wakati wajitoleaji walipoondoa theluji na barafu kutoka kwenye paa la Jumba la Kusanyiko

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuni kwa wahasiriwa wa dhoruba

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki