‘Twaishi Si kwa Ajili Yetu Wenyewe Tena’
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JACK JOHANSSON
Askari-jeshi Mwafrika, wa Malawi, aliniamuru nisimame kwenye ukingo wa mto katika nuru ya taa za mbele za Land Rover. Askari huyo alipoinua bunduki yake kwenye mabega, Lloyd Likhwide alikimbilia ukingo huo wa mto na kujisukuma mbele zangu. Alisihi akisema: “Nipige risasi! Badala yake, nipige risasi! Si mgeni huyu ambaye hajafanya kosa lolote!” Kwa nini Mwafrika alikuwa tayari kudhabihu uhai wake kwa ajili yangu mimi Mzungu? Acheni nieleze jinsi nilivyokuja kuwa mishonari katika Afrika miaka 40 hivi iliyopita.
MNAMO 1942, nilipokuwa na umri wa miaka tisa tu, mama yangu alikufa, akimwacha Baba na watoto watano. Nilikuwa kitinda mimba. Miezi minne baadaye, Baba, aliyekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova wa kwanza katika Finland, akafa maji. Dada yetu mkubwa zaidi, Maja alitulea, na tuliweza kulima shamba letu. Pia Maja aliongoza katika mambo ya kiroho, na baada ya mwaka mmoja kufuatia kifo cha Baba yetu, yeye pamoja na ndugu yangu mmoja walifananisha wakfu wao kwa Yehova Mungu kwa kubatizwa ndani ya maji. Mwaka mmoja baadaye nilibatizwa, nikiwa na umri wa miaka 11.
Uamuzi wa Maana
Baada ya kumaliza masomo katika chuo cha kiufundi katika mwaka wa 1951, nilianza kufanya kazi katika kampuni ya Ford Motor Company katika Finland. Miezi sita baadaye nilishtuliwa na mhudumu asafiriye wa Mashahidi wa Yehova mwenye hekima. Alinialika nitoe hotuba kwenye kusanyiko juu ya baraka za upainia, au huduma ya wakati wote. Nilihisi aibu, kwa kuwa nilikuwa nikifanya kazi ya kimwili ya wakati wote na nikahisi kwamba singepata kamwe kuongea kwa usadikisho. Nilisali kwa Yehova kuhusu jambo hili. Nilitambua kwamba Wakristo wanapaswa “kuishi si kwa ajili yao wenyewe tena, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao,” na kwa hiyo niliamua kubadilisha mambo niliyoyatanguliza maishani ili nitumikie nikiwa painia.—2 Wakorintho 5:15.
Mkubwa wangu aliahidi kuongeza mshahara wangu maradufu ikiwa ningeendelea kufanya kazi katika kampuni hiyo. Kisha, wakati alipoona nimeamua, alisema: “Umefanya uamuzi unaofaa. Nimetumia maisha yangu yote katika ofisi hii, na kwa kweli nimesaidia watu kadiri gani?” Kwa hiyo katika Mei 1952, nikawa painia. Majuma machache baadaye, ningeweza kutoa hotuba yangu kuhusu huduma ya upainia nikiwa na uhakika kamili.
Nilipotumika nikiwa painia kwa miezi michache, nilifungwa gerezani kwa miezi sita kwa sababu ya kutokuwamo kwangu kwa Kikristo. Kifungo hiki kilifuatwa na kuzuiwa kwa miezi minane pamoja na vijana Mashahidi katika kisiwa cha Hästö-Busö, katika Ghuba ya Finland. Tulikiita kisiwa hiki Gileadi Ndogo kwa sababu ya programu tuliyopanga miongoni mwetu wenyewe ya kujifunza Biblia kwa bidii. Hata hivyo, mradi wangu ulikuwa kuhudhuria Gileadi halisi, Shule ya Gileadi ya Watchtower, iliyokuwa karibu na South Lansing, New York.
Nilipokuwa ningali nimezuiliwa katika kisiwa hiki, nilipokea barua kutoka ofisi ya tawi ya Watch Tower Society, ikinialika nitumikie nikiwa mhudumu anayesafiri wa Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuachiliwa huru nilipaswa kuzuru makutaniko katika sehemu ya Finland inayozungumza lugha ya Kisweden. Wakati huo, nilikuwa na umri wa miaka 20 tu na nilihisi kuwa sistahili, lakini nilimtumaini Yehova. (Wafilipi 4:13) Mashahidi katika makutaniko niliyotumikia walikuwa wazuri sana bila kunidharau kamwe eti kwa sababu nilikuwa “mtoto” tu.—Yeremia 1:7.
Mwaka uliofuata nilipokuwa nikizuru kutaniko, nilikutana na Linda, ambaye alikuwa likizoni Finland kutoka Marekani. Baada ya kurudi Marekani alifanya maendeleo ya kiroho haraka. Upesi akabatizwa. Tulifunga ndoa katika Juni 1957. Baadaye, tulialikwa kwenye darasa la 32 la Shule ya Gileadi, mnamo Septemba mwaka wa 1958. Baada ya kuhitimu mnamo Februari iliyofuata, tulipewa mgawo kwenda Nyasaland, ambayo sasa ni Malawi, katika kusini-mashariki ya Afrika.
Huduma Yetu Katika Afrika
Tulipenda kuwa katika huduma ya peupe pamoja na ndugu zetu Waafrika, ambao wakati huo walikuwa zaidi ya 14,000 katika Nyasaland. Nyakati fulani, tulisafiri kwa Land Rover, tukibeba vitu vyote tulivyohitaji. Tulikaa katika vijiji ambavyo hakuna mzungu yeyote aliyepata kuvifikia, na sikuzote tulipokewa vyema. Tulipowasili, kijiji chote kingekuja kutuona. Baada ya salamu ya kirafiki, wangeketi chini wakiwa kimya kabisa, wakituchunguza. Walichunguza kila kitu!
Mara nyingi, wanakijiji walijenga kibanda hasa kwa ajili yetu, ambacho nyakati fulani kilitengenezwa kwa udongo na nyakati nyingine kwa nyasi kilichotoshea kitanda tu. Fisi wangekimbia-kimbia karibu na kibanda hicho usiku, wakitoa milio yenye kuogofya kando tu ya vichwa vyetu. Lakini Mashahidi katika Nyasaland walikuwa karibu kukabili kani hatari zaidi kuliko wanyama wa mwitu.
Utukuzo wa Taifa Wapata Kuwa Suala
Vyama vya kupigania uhuru vilikuwa vimechacha Afrika kote. Kila mtu alitarajiwa kujiunga na chama kimoja cha kisiasa kilichokuwako huko Nyasaland. Kwa ghafula, kutokuwamo kwetu kukawa suala kuu la kitaifa. Wakati huo nilisimamia kazi yetu ya ofisi wakati mwangalizi wa ofisi ya tawi, Malcolm Vigo, hakuwapo. Niliomba kukutana na Dakt. Hastings Kamuzu Banda, aliyekuwa waziri mkuu wa Nyasaland wakati huo. Mimi pamoja na wazee wawili Wakristo tulimweleza msimamo wetu wa kutokuwamo, na mkutano huo ukaisha kwa njia ya amani. Licha ya hilo, karibu mwezi mmoja baadaye, mnamo Februari 1964, Elaton Mwachande akawa mtu wa kwanza kuuawa katika mnyanyaso huo—alichomwa mkuki na umati wenye hasira. Mashahidi wengine katika kijiji chao walilazimika kutoroka.
Tulimpelekea Dakt. Banda telegramu, tukimsihi atumie mamlaka yake kukomesha ujeuri huo. Upesi nikapokea simu kutoka kwenye ofisi ya waziri mkuu, akiniita huko. Nikiwa nimeandamana na mishonari mwingine aitwaye Harold Guy, na Shahidi mwenyeji, Alexander Mafambana, nilienda kumwona Dakt. Banda. Mawaziri wawili wa serikali walikuwako pia.
Mara tu tulipoketi, Dakt. Banda, bila kusema neno, alianza kupeperusha ile telegramu huku na huku juu ya kichwa chake. Hatimaye, kimya kiliisha aliposema: “Bw. Johansson, unamaanisha nini kwa kupeleka telegramu kama hii?” Mara nyingine tena tulimweleza msimamo wetu wa kutokuwamo katika mambo ya kisiasa, kisha nikaongezea: “Sasa, kwa kufikiria mauaji ya Elaton Mwachande, wewe ndiwe mtu pekee unayeweza kutusaidia.” Dakt. Banda aliridhishwa na jambo hili, akatulia kwa kadiri fulani.
Hata hivyo, mmoja wa mawaziri wa serikali aliyekuwako alidai kwamba Mashahidi wa Yehova katika kijiji fulani cha mbali hawakushirikiana na wenye mamlaka wa mahali hapo. Kisha waziri wa pili akataja kijiji kingine cha mbali, akidai kwamba Mashahidi wa huko walikuwa wamemsema vibaya Dakt. Banda. Na bado hawakuweza kutoa majina ya yeyote aliyejiendesha kwa njia hiyo. Tulieleza kwamba sikuzote Mashahidi wa Yehova hufundishwa kustahi mamlaka za kiserikali. Kwa kusikitisha, jitihada zetu za kusahihisha maoni mabaya ya Dakt. Banda na mawaziri wake hazikufua dafu.
Maisha Yetu Yalikuwa Hatarini
Mnamo 1964, Nyasaland ilipata uhuru na baadaye ikawa Jamhuri ya Malawi. Kazi yetu ya kuhubiri iliendelea kukiwa na hali ya kawaida ya kiasi fulani lakini chini ya mkazo uliokuwa ukiongezeka. Wakati huo Mashahidi katika eneo la kusini ya nchi walipiga simu, wakisema kwamba maasi ya kisiasa yalikuwa yamezuka huko. Tuliona uhitaji wa kumtuma mtu huko ili akachanganue hali ya Mashahidi huko na kuwategemeza kiroho. Katika pindi zilizotangulia nilikuwa nimefanya ziara msituni, na Linda alikubali kwa ujasiri. Hata hivyo, wakati huu, aliniomba niandamane na Shahidi mchanga mwenyeji anayeitwa Lloyd Likhwide. Hatimaye nilikubali, nikijifikiria, ‘Ikiwa hili litamfanya asiwe na wasiwasi sana, nitalifanya.’
Tuliambiwa kwamba tulihitaji kuvuka mto fulani kwa feri kabla ya kafiu ya saa 12:00 jioni. Tulijaribu tulivyoweza kuingia katika feri hiyo kwa wakati huo, lakini tulicheleweshwa na barabara mbaya. Baadaye tulitambua kwamba amri ilikuwa imetolewa ya kumpiga risasi mtu yeyote atakayepatikana kwenye upande tuliokuwa wa mto baada ya saa 12:00. Tulipokuwa tukiteremka kuelekea kwenye mto, tuliona kwamba tayari feri ilikuwa imevuka ng’ambo ile nyingine ya mto. Ndugu Likhwide aliiita ije kutubeba. Ilikuja, lakini askari-jeshi aliyekuwa ndani yake alipaaza sauti akisema: “Lazima nimpige risasi yule mzungu!”
Mara ya kwanza nilifikiri ananitisha bure tu, lakini feri ilipokaribia, huyo askari-jeshi aliniamuru nisimame mbele ya taa za gari. Wakati huo ndipo rafiki yangu Mwafrika alipojitupa katikati yetu, na kumsihi askari-jeshi ampige risasi badala yangu. Yaonekana kwamba askari-jeshi aliguswa moyo na utayari wa rafiki yangu wa kufa kwa ajili yangu, na hivyo akaweka bunduki yake chini. Nilifikiria maneno ya Yesu: “Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” (Yohana 15:13) Niliterema kama nini kwamba nilitii shauri la Linda la kuenda pamoja na huyo ndugu mpendwa!
Siku iliyofuata barabara ya kurudi Blantyre ilikuwa imefungwa na vijana waliodai kuona kadi ya uanachama ya Ndugu Likhwide. Kulikuwa na jambo moja la kufanya—kupita katikati ya umati huo, kwa haraka! Niliweka gia na gari likasonga mbele kwa ghafula na hivyo kuwashtua vya kutosha kuturuhusu tuondoke. Iwapo kikundi hicho kingalimshika Ndugu Likhwide, labda kingalimwua. Tuliporudi kwenye ofisi ya tawi, tulikuwa tumeshtuka sana lakini tukiwa wenye shukrani kwa Yehova kwa ulinzi Wake.
Watiwa Gerezani kwa Ajili ya Imani Yao
Mnamo Oktoba 1967 kazi yetu ilipigwa marufuku rasmi katika Malawi. Wakati huo kulikuwa na Mashahidi wapatao 18,000 katika nchi hiyo. Majuma mawili baadaye, tulipata habari kwamba Mashahidi 3,000 walikuwa wametiwa gerezani katika jiji kuu la Lilongwe. Tuliamua kwenda huko usiku huo, mwendo wa kilometa 300, angalau kuwatia moyo. Tulipakia vichapo vya Watchtower kwenye Land Rover, na kwa msaada wa Yehova, tulivuka vizuizi vingi vya barabarani bila kukaguliwa. Kandokando ya barabara, katika kutaniko moja hadi jingine, tuliacha katoni za chakula cha kiroho cha wakati ufaao.
Asubuhi tulielekea gerezani. Tuliona jambo lenye kushtua kama nini! Kulikuwa kumenyesha usiku kucha, na ndugu na dada zetu Wakristo walikuwa wamezuiliwa nje katika uwanja uliozingirwa. Walikuwa wamelowa chepechepe, na wengine wao walikuwa wakijaribu kukausha blanketi zao kwenye ua. Tulifaulu kuongea na wachache kati yao kupitia kwenye ua.
Kesi yao ya mahakamani ilifanywa alasiri, na idadi kadhaa iliyodai kuwa Mashahidi walijitokeza kwenye kizimba. Tulijaribu kuwasiliana nao kwa macho, lakini nyuso zao hazikuonyesha hisia yoyote. Tuligutuka kama nini wakati wote waliokuwa kwenye kizimba walikana hadharani imani yao! Hata hivyo, nilipata habari kwamba Mashahidi wenyeji hawakujua hata mmoja wa wale waliokana kuwa Mashahidi wa Yehova. Yaelekea ilikuwa ni jitihada ya kuwavunja moyo Mashahidi wa kweli.
Katika wakati huohuo, amri ilitolewa kwamba tuhamishwe. Ofisi yetu ya tawi katika Blantyre ilikuwa imetwaliwa, na wamishonari walipewa muda wa saa 24 waondoke nchini. Tuliporudi nyumbani, jinsi ilivyoshangaza kupata ofisa wa polisi akitufungulia lango! Alasiri iliyofuata ofisa wa polisi alikuja, na kwa masikitiko, alitukamata na kutupeleka kwenye uwanja wa ndege.
Tuliondoka Malawi mnamo Novemba 8, 1967, tukijua kwamba ndugu zetu Wakristo huko watapatwa na majaribu motomoto. Tuliwahurumia kwelikweli. Makumi walipoteza uhai wao; mamia wakateswa kikatili; na maelfu wakapoteza kazi, nyumba, na mali zao. Hata hivyo, karibu wote walishika uaminifu-maadili.
Kuelekea Migawo Mipya
Licha ya magumu hatukutaka kamwe kuacha kazi ya mishonari. Badala ya hivyo, tulikubali mgawo mpya—kwenda Kenya, nchi yenye mandhari na watu tofauti-tofauti. Linda alivutiwa sana na Wamaasai. Wakati huo, hakukuwako Mmaasai yeyote aliyekuwa Shahidi wa Yehova. Lakini, ndipo Linda alipokutana na Dorcas, mwanamke Mmaasai, akaanza kujifunza Biblia pamoja naye.
Dorcas alijua kwamba ili ampendeze Mungu, alipaswa kuhalalisha ndoa yake. Baba ya watoto wake wawili alikataa, hivyo Dorcas alijaribu kuwaruzuku watoto wake akiwa peke yake. Mwanamume huyu alighadhabikia Mashahidi, lakini hakufurahi kutenganishwa na familia yake. Hatimaye, kwa kusihiwa na Dorcas, yeye pia akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alirekebisha maisha yake, akawa Shahidi, na kumwoa Dorcas. Dorcas akawa painia, na mume wake na mwana wao mkubwa zaidi sasa wanatumika wakiwa wazee wa kutaniko.
Kwa ghafula, katika mwaka wa 1973, kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Kenya ilipigwa marufuku, tukahitaji kuondoka. Marufuku hiyo iliondolewa baada ya miezi michache. Lakini kufikia wakati huo tulikuwa tumepokea mgawo wetu wa tatu—kwenda Kongo (Brazzaville). Tuliwasili huko mnamo Aprili 1974. Karibu miaka mitatu baadaye, sisi wamishonari tulishtakiwa kwamba tulikuwa wapelelezi, na kazi yetu ikapigwa marufuku. Mbali na hilo, mapigano yalizuka katika Brazzaville baada ya kuuawa kwa rais wa nchi hiyo. Wamishonari wote walipewa migawo katika nchi tofauti-tofauti, lakini sisi tuliombwa tubaki kwa muda mrefu iwezekanavyo. Kwa majuma kadhaa tulilala bila kujua kama tutaokoka usiku huo. Lakini tulilala vizuri tukiitibari utunzaji wa Yehova. Miezi hiyo michache, tukiwa katika ofisi ya tawi peke yetu, labda ndicho kipindi tulichopata kuwa nacho katika huduma yetu ya umishonari ambapo imani yetu ilijaribiwa zaidi na kuimarishwa.
Mnamo Aprili 1977 tulihitaji kuondoka Brazzaville. Kisha tulishangaa kwelikweli—tulipewa mgawo wa kwenda Iran ili kufungua ofisi mpya ya tawi. Jambo gumu la kwanza lilikuwa ni kujifunza Kifarsi, ambacho ni lugha ya Waajemi. Kujifunza lugha mpya kulitufanya tutoe maelezo sahili zaidi kwenye mikutano ya kutaniko, kama yale yanayotolewa na watoto wadogo! Katika mwaka wa 1978 mapinduzi yakaanza Iran. Tulibaki wakati wote mapigano yalipokuwa yamepamba moto kwelikweli, lakini mnamo Julai 1980, wamishonari wote wakahamishwa.
Mgawo wetu wa tano uliturudisha tena mpaka sehemu ya kati ya Afrika, hadi Zaire, sasa ni Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo. Tulitumikia katika Zaire kwa miaka 15, kwa kipindi fulani tukiwa chini ya marufuku pia. Tulipowasili huko, kulikuwa na Mashahidi wapatao 22,000 waliokuwa watendaji katika nchi hiyo—sasa ni zaidi ya 100,000!
Kurudi Nyumbani Tena!
Mnamo Agosti 12, 1993, marufuku dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika Malawi iliondolewa. Miaka miwili baadaye mimi na Linda tulipewa mgawo wa kurudi mahali tulipoanzia—Malawi, nchi maridadi ya kirafiki inayojulikana kwa uchangamfu wake katika Afrika. Tangu Januari 1996, tumekuwa na shangwe ya kufanya kazi miongoni mwa Wamalawi wenye furaha na amani. Tunathamini kutumikia tena pamoja na ndugu zetu waaminifu wa Malawi, wengi wao wakiwa wamevumilia mnyanyaso kwa miongo mitatu. Ndugu zetu Waafrika wamekuwa chanzo cha kitia-moyo, na tunawapenda. Kwa kweli wameishi kwa kupatana na maneno ya Paulo: “Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.” (Matendo 14:22) Sasa Mashahidi wapatao 41,000 katika Malawi wana uhuru wa kuhubiri peupe na kufanya mikusanyiko mikubwa.
Tumefurahia sana migawo yetu yote. Mimi na Linda tumejifunza kwamba jambo lolote, hata liwe lenye kujaribu namna gani, laweza kutufinyanga tuwe watu bora, mradi tunadumisha “shangwe ya Yehova.” (Nehemia 8:10, NW) Nimepatwa na magumu katika kujirekebisha wakati tulipohitaji kuacha migawo. Lakini uwezo wa Linda wa kubadilikana—na hasa imani yake yenye nguvu katika Yehova—imenisaidia, ikinifanya nithamini baraka ya kuwa na ‘mke mwema.’—Mithali 18:22.
Jinsi ambavyo tumekuwa na maisha yenye furaha na yenye kusisimua! Tumemshukuru Yehova kwa ulinzi wake tena na tena. (Waroma 8:31) Zaidi ya miongo minne imepita tangu nilipotoa ile hotuba juu ya baraka za huduma ya wakati wote. Tunafurahi kwamba ‘tumemjaribu Yehova na kuonja wema wake.’ (Zaburi 34:8; Malaki 3:10) Tumesadikishwa kwamba ‘kuishi si kwa ajili yetu wenyewe’ ndiyo njia bora ya maisha inayowezekana.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 24]
Nchi tulimotumikia
Iran
Jamhuri ya Kongo
Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo
Kenya
Malawi
[Picha katika ukurasa wa 21]
Tukielekea Malawi, kupitia njia ya Cape Town, Afrika Kusini
[Picha katika ukurasa wa 23]
Tulipokamatwa na kuhamishwa kutoka Malawi
[Picha katika ukurasa wa 25]
Dorcas, Mmaasai, pamoja na mumewe