Kwa Nini Izungumziwe
“Chuma hunoa chuma; ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.”—Mithali 27:17, Biblia.
MABAPA hayanolewi kwa kugonganishwa. Kunoa ni utaratibu mwanana. Vivyo hivyo, kunazo njia nzuri na mbaya za kunoa akili kupitia mazungumzo, hasa yanapohusu masuala yanayohitaji utumie busara kama vile dini.
Kwanza kabisa, ni lazima tuheshimu hadhi ya mtu tunayezungumza naye na tuonyeshe heshima hiyo kwa maneno na kwa mwenendo wetu. “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi,” Biblia yasema. (Wakolosai 4:6) Usemi unaotolewa kwa upendezi na uliokolezwa haulazimishi kwa namna yake ya sauti, hata wakati ambapo msemaji amesadiki kwamba yeye yuko sahihi na mwenzake amekosea.
Jinsi tunavyosikiliza hudhihirisha upendezi wetu pia. Ikiwa twakatisha mazungumzo au hatusikilizi kwa makini kwa sababu tunatayarisha bishano linalofuata, haiwezekani kuwa tunasikiliza kwa upendezi. Kuna uwezekano mkubwa kwamba yule anayesema atatambua hali yetu iliyo wazi ya kutopendezwa na maoni yake na labda atakatisha mazungumzo. Tena, tusimlazimishe au kumwogopesha kamwe mtu ili abadili maoni yake. Hii ni kwa sababu ‘Mungu ndiye huikuza mbegu ya ile kweli’ katika moyo wa msikilizaji mwenye kuitikia kwa njia nzuri.—1 Wakorintho 3:6.
Mtume Paulo ni kielelezo kizuri kwetu, kwa kuwa alitumia “kutoa sababu” na “ushawishi” katika huduma yake. (Matendo 17:17; 28:23, 24) Paulo aliizungumzia dini pamoja na watu popote alipowapata, kama vile mahali pa soko na katika nyumba zao. (Matendo 17:2, 3; 20:20) Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuiga mfano huo kwa kwenda popote ambapo huenda pana watu na kusababu nao kwa kutumia Maandiko.
Epuka Kutoelewana
Taifa la Israeli lilikuwa tu limetulia katika Bara Lililoahidiwa punde tu kulipotokea hali fulani ya kutoelewana iliyohusu madhabahu, ambayo ilikaribia kusababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe. Watu walioishi mashariki ya Mto Yordani walijenga madhabahu, ingawa yale makabila mengine yalifikiri kimakosa kwamba ilikuwa madhabahu ya ibada isiyo ya kweli. Kwa hiyo, wakapanga kuchukua hatua ya kijeshi wapate kuwaadhibu ndugu zao. Lakini wakatumia busara. Wale waliopanga kuchukua hatua ya uchokozi walituma ujumbe kwanza ili kuulizia kusudi la madhabahu hiyo. Waliambiwa kwamba hiyo ilikuwa tu nguzo ya ukumbusho—“ushahidi”—kuyakumbusha makabila yote juu ya umoja wao mbele za Yehova Mungu, na hilo likatokeza kitulizo kwao. Mazungumzo yalizuia vita—na uhai wa wengi ukaokolewa!—Yoshua 22:9-34.
Vivyo hivyo leo, hali za kutoelewana mara nyingi hutokeza uadui na hata chuki isiyo na sababu. Kwa mfano, watu fulani wamewaona Mashahidi wa Yehova kuwa ni washupavu wa kidini kwa sababu ya ripoti zinazohusu msimamo wao wa kukataa kutiwa damu mishipani. Lakini wale ambao wamechukua hatua ya kibinafsi ya kuulizia kutoka kwa Mashahidi kuhusu suala hilo mara nyingi wamefurahia kujua kwamba kunao msingi wa Kibiblia wa kuunga mkono msimamo wao na kwamba kuna matibabu ya badala yaliyo salama, na yenye matokeo mazuri. (Mambo ya Walawi 17:13, 14; Matendo 15:28, 29) Kwa kweli, mwandishi mmoja wa safu za gazeti alisema hivi, kuhusu matatizo ya kutiwa damu mishipani: “Mungu asifiwe kwa sababu Mashahidi wa Yehova wanaongoza katika utafiti wa vibadala vya kutumia damu katika tiba.”
Hali kadhalika, baadhi ya watu wamekataa kuongea na Mashahidi kwa sababu wameambiwa kwamba Mashahidi wa Yehova hawamwamini Yesu Kristo. Jambo hilo si la kweli hata kidogo! Kwa kweli, Mashahidi hukazia daraka la Yesu katika wokovu wetu, wakieleza kwamba yeye ni Mwana wa Mungu, ambaye Mungu alimtuma duniani ili kufidi wanadamu kutoka kwenye dhambi na kifo. Watu wanaposema na Mashahidi kuhusu suala hilo, kutoelewana kunaondolewa.—Mathayo 16:16; 20:28; Yohana 3:16; 14:28; 1 Yohana 4:15.
Kweli—Inapendwa na Wengi au Haipendwi na Wengi?
Labda jambo linalowashangaza wengi ni kwamba inapohusu dini, mara nyingi njia inayopendwa na wengi kwa kawaida ndiyo njia yenye kosa. Yesu Kristo mwenyewe alifundisha hivi: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.”—Mathayo 7:13, 14.
Ni watu wanane tu waliosema kweli ya kiroho katika siku ya Noa—Noa, mke wake, wana wake watatu, na wake za wanaye. Yaonekana ujumbe wao wa kutoa onyo na kazi ya kujenga safina viliwafanya wawe vitu vya kudhihakiwa, na hata kutendwa vibaya. Na bado Noa na familia yake hawakuogopeshwa; waliendelea kuhubiri na kujenga. (Mwanzo 6:13, 14; 7:21-24; 2 Petro 2:5) Vivyo hivyo, ni watu watatu tu waliotii maagizo ya Mungu na hivyo wakaokoka kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora.—Mwanzo 19:12-29; Luka 17:28-30.
Vipi wakati wetu? Mwenye nyumba mmoja aliwaambia Mashahidi wa Yehova hivi: “Ikiwa Kristo angerudi katika mwili wenye nyama leo, yaelekea watu wangemwua tena.” Mtu huyu alionelea kwamba mafundisho na viwango vya juu vya adili vya Yesu havingependwa na wengi leo kama vile havikupendwa na wengi miaka 2000 iliyopita. Je, unakubaliana na hilo?
Ikiwa wajibu ndiyo, uko sahihi, kwa kuwa Yesu aliwaonya wanafunzi wake hivi: “Mtakuwa vitu vya kuchukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu”—utabiri ambao umethibitika kuwa kweli. (Mathayo 24:9) Viongozi wa Kiyahudi mjini Roma walimwambia mtume Paulo hivi kuhusu Ukristo: “Kwa habari ya farakano hili . . . kila mahali huwa lasemwa vibaya.” (Matendo 28:22) Hata hivyo, wafuasi wa Kristo hawakuacha kuwaeleza wengine imani zao kwa sababu Ukristo haukupendwa na wengi. Wala hilo halikuwazuia watu wenye mioyo minyofu wasiongee na Wakristo.—Matendo 13:43-49.
Leo ujumbe wa Yesu una umuhimu kuliko wakati mwingine wowote. Kwa nini? Kwa sababu hali za ulimwengu zaonyesha kwamba sasa tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu na kwamba mwisho wa siku hizi utakuwa kuondolewa kwa utendaji wa makosa kutoka kwenye dunia. Yesu aliulinganisha wakati wetu na siku za Noa. (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:37-39) Sasa, huu sio wakati wa kuzishikilia imani zetu bila kuzichunguza, kwa kuwa ni wale tu wanaomjua Mungu na ‘wanaomwabudu kwa roho na kweli’ watakaopewa uhai wa milele.—Yohana 4:24; 2 Wathesalonike 1:6-9.
Jinsi ya Kupata Njia ya Kweli
Francis Bacon, ambaye alikuwa mwanafalsafa Mwingereza, mwandishi wa insha, mwana-sheria, na mtawala mwenye busara wa karne ya 17, aliwashauri wenye kutafuta kweli “wafikirie kwa makini na kutafakari.” Naye rais wa zamani wa Marekani, Thomas Jefferson, alisema hivi: “Kusababu na kuulizia waziwazi ndivyo vyombo pekee vyenye matokeo vinavyoshinda kosa. . . . [Vyombo] hivyo ndivyo maadui wa kosa.” Kwa hiyo ikiwa sisi tunatafuta kweli kwa moyo mweupe, “tutafikiria kwa makini na kutafakari” na tufuatilie “kusababu na kuulizia waziwazi.”
Akifafanua umuhimu wa mfikio huo, mwanasayansi Mwingereza Sir Hermann Bondi alisema: “Kwa kuwa ni imani moja tu inayoweza kuwa ya kweli, tokeo ni kwamba kuna uwezekano mkubwa sana wa binadamu kuwa na imani yenye uthabiti na unyofu katika kitu kisicho cha kweli kwa mambo yahusuyo dini iliyofunuliwa. Mtu angetarajia kwamba uhakika huu ulio wazi ungewafanya watu wawe wanyenyekevu kwa kiasi fulani, wawe na fikira ya kwamba hata ingawa huenda mtu akawa na imani yenye nguvu, yawezekana amekosea.”
Basi, mtu aweza kutambuaje ikiwa kwa kweli yupo kwenye ‘barabara inayoongoza kwenye uhai’? Yesu alifundisha kwamba ni lazima Mungu aabudiwe ‘kwa kweli.’ Hivyo, kufikiri kuzuri kunamfanya mtu aamue kwamba ikiwa mafundisho mawili yanapingana, yote mawili hayawezi kuwa kweli. Kwa mfano, ama wanadamu wana nafsi isiyokufa ama hawana. Ama Mungu ataingilia kati shughuli za binadamu ama hataingilia. Ama Mungu ni Utatu ama si Utatu. Watu wanaotafuta kweli wanataka majibu yenye uhakika kuhusu maswali haya muhimu. Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Mungu ametupa majibu katika Neno lake, Biblia.a
Kwa kuwa “Andiko lote limepuliziwa na Mungu,” njia kuu ya kuyapima mafundisho mbalimbali ni kwa kuyalinganisha na Biblia. (2 Timotheo 3:16) Ukifanya hivyo, ‘utajithibitishia mwenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’ (Waroma 12:2) Je, unaweza ‘kujithibitishia mwenyewe’ kwamba Biblia ndiyo msingi wa imani yako? Ni jambo la muhimu ufanye hivyo kwa sababu Mungu hataki uongozwe vibaya pamoja na “dunia nzima inayokaliwa.”—Ufunuo 12:9.
Je, Walimu Wanahitajiwa?
Yesu hakuwapa wanafunzi wake hati-kunjo chache na kuwaambia: “Majibu ya maswali yenu yamo humo. Nendeni nyumbani mkajitafutie wenyewe.” Badala yake, aliwafunza neno la Mungu kwa saburi na kwa fadhili. Halafu, wale waliokubali mafundisho yake waliwafunza wengine zaidi kwa kufuata mbinu zake. Fikiria mfano wa mwanafunzi Filipo. Alizungumza na ofisa mmoja Mwethiopia mwenye moyo mnyofu, ambaye hapo mapema alikuwa ameyafahamu Maandiko kupitia uhusiano wake na Wayahudi. Lakini mwanamume huyo alihitaji msaada. Hivyo Filipo—mwakilishi wa kutaniko la Kikristo—alielekezwa ili amsaidie. Ikiwa ofisa huyu angekataa kuizungumzia dini, hangejifunza juu ya daraka la Yesu katika kusudi la Mungu. Huyu Mwethiopia aliweka kielelezo kizuri kama nini kwa wote wanaotafuta kweli!—Matendo 8:26-39.
Je, wewe uko tayari kuzizungumzia imani zako na kuuliza maswali kama huyu Mwethiopia alivyofanya? Kwa hakika unaweza kupata faida nyingi ukifanya hivyo. Mashahidi wa Yehova hufurahia kuizungumzia Biblia pamoja na watu wanaotaka kikweli kujua yale ambayo Biblia inasema. Mashahidi hawatoi maoni yao wenyewe. Bali, wao hujitahidi kuwaonyesha watu yale ambayo Biblia yenyewe husema.
Huyo ofisa Mwethiopia alijifunza mambo fulani yenye kutokeza kuhusu Yesu Kristo, kama vile ambavyo angetumiwa na Mungu kuhusiana na wokovu wetu. Leo, utimizo wa kusudi la Mungu unakaribia sana kukamilika. Mambo ya ajabu, yenye kutia hofu yako karibu kutukia papa hapa duniani. Makala inayofuata itaonyesha kwamba kila mtu duniani ataathiriwa. Bila shaka, mtazamo na mwendo tunaofuata vitaamua jinsi tutakavyoathiriwa.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate uthibitisho kwamba Biblia ni Neno la Mungu, tafadhali ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ofisa Mwethiopia alikubali mazungumzo ya Biblia