Tumaini Linalotolewa na Dini ya Kweli
KWA asili sisi hupenda kusema juu ya mambo yanayotuhangaisha au yanayosisimua hisia zetu. Hii ni sababu moja inayowafanya Mashahidi wa Yehova wafurahie kushiriki na wengine ujumbe mzuri ajabu wa Biblia. Ujumbe huo, unaokazia Ufalme wa Mungu, unatoa majibu kwa mambo yanayowahangaisha watu kikweli leo, kama vile wakati ujao, usalama, afya, na furaha.—Luka 4:43.
Lakini kwanza, Ufalme wa Mungu ni nini?
Tumaini Lenye Kusisimua
Ufalme wa Mungu ni serikali ya Mungu, na Mwana wake, “Mfalme wa amani,” ndiye mtawala. Biblia yasema hivi kumhusu: “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake . . . Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe.”—Isaya 9:6, 7.
Unabii mwingine wa Biblia, ukitabiri mambo ambayo yangetokea baadaye kabisa, naam, wakati wa historia yetu wenyewe na watawala wake, ulisema hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, . . . bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Huu Ufalme wa Mungu, unaotawaliwa na Kristo, Mfalme wa Amani, utatimiza ile sala ambayo Yesu aliwafunza wafuasi wake kusali, yaani: “Baba yetu uliye katika mbingu . . . , acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:9, 10) Itakuwaje kwetu na kwa dunia Ufalme wa Mungu utakapokuja? Fikiria ahadi zilizotolewa na Yehova Mungu mwenyewe, kama zilivyorekodiwa katika Biblia. Baadhi ya ahadi hizo zimeonyeshwa katika kurasa hizi.
Ujumbe Kutoka kwa Mungu
Ahadi nzuri ajabu zinazopatikana katika Neno la Mungu hazipasi kufichwa, na jambo hili laturudisha kwenye lile suala la kuizungumzia dini. Yesu alitabiri kwamba kabla ya mwisho wa mfumo wa mambo uliopo, wafuasi wake wangechukua hatua ya kwanza ya kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 1:8.
Ujumbe huu unaohusu Ufalme wa Mungu ndio ujumbe ambao Mashahidi wa Yehova wanatangaza ulimwenguni kote. Gazeti jenzi, Mnara wa Mlinzi, sasa linachapishwa katika lugha 130, na juu ya jalada la kila moja ya nakala zaidi ya milioni 22 za kila toleo zinazochapishwa kuna maneno “Unaotangaza Ufalme wa Yehova.”
Ikiwa wewe ni mtu mwenye hekima, unahitaji kufanya maamuzi yanayotegemea ujuzi kuhusu uhai wako. (Mithali 18:13) Basi, twakutolea mwaliko wa kujifunza mengi yanayohusu Ufalme wa Mungu wenye utukufu na yale ambayo unaweza kumaanisha kwako. Ili uyafahamu hayo, usikatae kuizungumzia Biblia. Hakuna mazungumzo yoyote yanayoweza kuelimisha, kupendeza, na kuwa yenye umuhimu kuliko yale ya Biblia.—Yohana 17:3.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Ahadi za Dunia Paradiso
Amani kamili itaenea duniani. “Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma.”—Zaburi 72:7, 8.
Hata wafu watarudishwa kwenye uhai. “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.
Watafurahia afya kamili milele. “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.”—Ufunuo 21:3, 4.
Watu watajenga na kuishi katika nyumba zao wenyewe. “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu na kula matunda yake.”—Isaya 65:21.
Chakula kitakuwa kingi. “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.” —Zaburi 72:16.