Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Mwisho wa Umaskini Asanteni sana kwa ajili ya mfululizo wa makala katika Amkeni! la Juni 8, 1998, wenye kichwa “Mwisho wa Umaskini Wakaribia.” Kwa kweli mfululizo huo ulieleza mambo kwa njia yenye kueleweka nao ukafanya nitambue mtazamo wangu wa kulalamika. Sina kazi, sina fedha kwa ajili ya matumizi ya ziada. Nilijiona kuwa maskini. Kumbe sivyo! Makala hiyo yaonyesha kwamba kuna wengine walio katika hali mbaya zaidi kunishinda. Napaswa kuwa mwenye shukrani kwa vitu ambavyo tayari ninavyo—chakula, mavazi, afya njema na, muhimu zaidi, Yehova. Natazamia sana kuona mwisho wa umaskini. Nimeazimia kufuliza kuutafuta Ufalme wa Yehova na kuacha kulalamika.
C. W., New Zealand
Useja wa Kidini Kwa miaka kadhaa nimekuwa msomaji wa magazeti yenu. Lazima nitete dhidi ya ripoti yenu yenye kupendelea upande mmoja juu ya mafundisho ya Kanisa Katoliki katika makala “Maoni ya Biblia: Je, Useja wa Kidini Ni Takwa kwa Wahudumu Wakristo?” (Juni 8, 1998) Hakuna “useja wa kulazimishwa” katika Kanisa Katoliki! Kunao tu useja uliochaguliwa kwa hiari ambao ni wa lazima kwa ajili ya kazi fulani. Mtu yeyote anayedai kuwa alilazimishwa awe mseja anasema uwongo.
R. G., Ujerumani
Twaamini kwamba kuna tofauti kubwa kati ya maneno useja wa kulazimishwa na wazo la kwamba watu wanalazimishwa kuwa waseja. Kwa mfano, ikiwa shirika fulani linaanzisha kanuni za mavazi na linawaajiri wale tu wanaokubali kufuata kanuni hizo huku likiwafuta kazi wale wanaovunja mfumo huo wa sheria, basi yaweza ikasemwa kwamba shirika hilo lina kanuni za mavazi za “kulazimishwa.” Katika maana hiyo, ni jambo la kutopendelea kusema kwamba kunao “useja wa kulazimishwa” katika ukasisi wa Kanisa Katoliki. Hata hivyo, makala yetu inaonyesha hasa kukosekana kwa msingi wa Kimaandiko unaofanya useja uwe takwa kwa wahudumu Wakristo. (1 Timotheo 3:2) Badala ya kuwachambua wale wanaochagua useja kuwa njia ya maisha, makala hiyo ilisema kuwa huu “umethibitika kuwa njia ya maisha yenye kuthawabisha na kuridhisha kiroho kwa wengine.”—Mhariri.
Uchaguzi Wangu Kati ya Baba Wawili Nilipokuwa na umri wa miaka 14 nilijifunza kweli ya Neno la Mungu kutoka kwa rafiki yangu shuleni. Wazazi wangu, hasa baba yangu, alinipinga nisijifunze. Jambo zuri ni kwamba hakutekeleza vitisho vyake vya kunifukuza nyumbani. Nilistahimili na nilibatizwa miaka mitano iliyopita. Kama yule ndugu anayesimuliwa katika makala hiyo (Juni 8, 1998), ni tumaini langu kwamba siku moja wazazi wangu watashiriki tumaini nililo nalo la kuishi katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu.
W. S. L., Brazili
Niliposoma makala hiyo nilitokwa na machozi. Baba yangu amekuwa akipinga sana itikadi zangu. Hata ingawa tunakuwa na maongezi mazuri nyakati nyingine, mimi huhofu sana hasira yake ya ghafula wakati wowote ule mazungumzo yatajapo Biblia au Mashahidi wa Yehova. Amenishambulia kimwili mara kadhaa. Lakini makala hiyo ilinitia moyo sana nisimame imara, hata nijapokabili mkazo wa namna hiyo.
I. H., Ujerumani
Makala hiyo ilinigusa moyo sana. Kwa kuwa nililelewa katika familia iliyogawanyika kidini, naweza kuelewa magumu ya kihisia-moyo ya huyo mwanamume kijana ambaye alilazimika kufanya uchaguzi mzito wa namna hiyo.
A.M., Italia
Uyabisi wa Misuli Asanteni sana kwa makala “Kuelewa na Kuvumilia Uyabisi wa Misuli.” (Juni 8, 1998) Nimekuwa nikiugua ugonjwa wa uyabisi wa misuli kwa miaka sita. Makala hiyo ni sahihi na inataja mambo mengi. Na pia, yale maandiko yaliyotajwa kwenye sanduku yalinitia moyo sana.
N. M., Marekani
Makala hiyo ilitokeza upendezi mkubwa sana. Twatumaini kuchapisha maelezo zaidi katika toleo moja la wakati ujao.—Mhariri.