Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 4/22 kur. 9-12
  • Kuchagua Talaka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuchagua Talaka
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ikiwa Kuna Watoto
  • Mambo ya Kifedha na ya Kisheria
  • Uhusiano Uliobadilika
  • Kujaribu Kurudia Hali ya Kawaida
  • Usikate Tumaini
  • Talaka Huwa na Majeruhi
    Amkeni!—1991
  • Mambo Manne Unayopaswa Kujua Kuhusu Talaka
    Amkeni!—2010
  • Mungu Huchukia Talaka ya Aina Gani?
    Amkeni!—1994
  • Talaka Matokeo Yayo Mabaya
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 4/22 kur. 9-12

Kuchagua Talaka

“Mwenzi wako wa ndoa akifa, watu wanaelewa hali yako hata ikiwa hukuwa mwenzi wa ndoa aliye bora. Lakini mume wako akikuacha—wengine, hufikiri hukuwa mke mwema. Tafadhali, tafadhali, NISAIDIENI!”—Msomaji wa Amkeni! katika Afrika Kusini.

KUKOSA uaminifu na talaka ni mambo yanayoweza kufadhaisha sana. Hata ingawa wengi wamepata sababu za kupatana na wenzi wao na kuhifadhi ndoa yao, wengine wana sababu halali za kufanya uchaguzi unaokubalika na Mungu wa kumtaliki mwenzi mzinzi. (Mathayo 5:32; 19:9) Kwa kielelezo, usalama, hali ya kiroho, na hali nzuri ya ujumla ya mke mwaminifu pamoja na watoto wake yaweza kuwa hatarini. Huenda pia akawa na wasiwasi kuhusu kuambukizwa maradhi yanayopitishwa kingono. Au labda amemsamehe mwenzi wake kwa kufanya uzinzi, lakini hakuna msingi wa kutumaini kwamba kuaminiana halisi kwaweza kupatikana tena na kwamba anaweza kuendelea kuishi pamoja naye akiwa mume wake.

“Huu ulikuwa uamuzi mgumu zaidi mai­shani mwangu,” akakiri mke mmoja aliyefadhaika. Ni uamuzi mgumu kwelikweli—si kwa sababu tu kusalitiwa husababisha maumivu makali bali pia talaka huleta matokeo ya muda mrefu yatakayoathiri maisha yake yote. Kwa hiyo, kama mke apaswa kumtaliki au kutomtaliki mwenzi wake asiye mwaminifu huo ni uamuzi wa kibinafsi. Haki ya mwenzi huyo inayoungwa mkono na Biblia kuhusu uamuzi huo yapaswa kuheshimiwa na wengine.

Ingawa hivyo, kwa kusikitisha watu wengi hufanya haraka kutaliki wenzi wao kabla ya kuhesabu gharama vizuri. (Linganisha Luka 14:28.) Ni mambo gani yanayotiwa ndani katika kuchagua talaka?

Ikiwa Kuna Watoto

“Mara nyingi mahitaji ya watoto husahauliwa au hupuuzwa na wazazi ambao hujizamisha katika matatizo yao,” chasema kitabu Couples in Crisis. Hivyo, unapofikiria kumtaliki mwenzi wako, kumbuka hali ya kiroho na hali njema ya watoto wako. Watafiti wengi wanasema kwamba kadiri talaka iwavyo ya amani, ndivyo yaelekea watoto hawatateseka sana. Hata chini ya hali ngumu, upole utamsaidia mtu ‘asipigane, bali awe mwanana kuelekea wote, akijizuia mwenyewe chini ya uovu.’—2 Timotheo 2:24, 25.a

Mtu akichagua kutaliki, yapasa ikumbukwe kwamba ni mume na mke—si watoto—wanaotalikiana. Bado watoto wanahitaji Mama na Baba. Bila shaka, kwaweza kukawa na hali zinazopita kiasi, kama vile mtoto anapokuwa katika hatari ya kutendwa vibaya. Lakini tofauti za kidini au za kibinafsi hazipasi kutumiwa kuzuia watoto wasipate manufaa ya kuwa na wazazi wawili.

Kwa kuongezea, jambo linalohitaji kufikiriwa ni hisia-moyo za watoto zinazoweza kuathirika kwa urahisi na uhitaji wa kupewa uhakikishio, upendo, na shauku ya kutosha. “Upendo huu unapoendelezwa,” chasema kitabu kimoja, “utawaandalia msingi wa kukabiliana na hali hiyo mpya.” Pia, kuhangaikia mahitaji yao ya kiroho ya kila siku kwaweza kuwasaidia wadumishe hali imara.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Mathayo 4:4.

Mambo ya Kifedha na ya Kisheria

Bila kuepukika talaka humnyang’anya kila mwenzi kiasi fulani cha mapato na mali, hali-njema ya kiasi fulani, na labda makao yaliyotunzwa vizuri. Kwa kuwa huenda mtu akahitaji kushughulikia matumizi yaliyoongezeka kwa mapato yaliyopungua, ni jambo la hekima kupanga bajeti iliyo halisi kulingana na mambo ya kutangulizwa kifedha. Msukumo wa kutaka kulipia hasara na maumivu ya kihisia-moyo kwa kutumia fedha nyingi zaidi au kuwa na deni wapaswa kuepukwa.

Ikiwa uamuzi unafikiwa wa kutalikiana, ni lazima pia mtu pamoja na mwenzi wake waamue namna watakavyoshughulika na akaunti za pamoja za benki. Kwa kielelezo, ili kuzuia matumizi mabaya ya fedha katika akaunti za pamoja za benki, huenda likawa jambo la hekima kumwomba meneja wa benki aombe sahihi za wenzi wote wawili wanapotaka kutoa fedha hadi kila mmoja atakapokuwa na akaunti yake mwenyewe.

Pia ni jambo la busara kuweka rekodi nzuri za mapato na matumizi, unapojitayarishia majadiliano ya fedha utakazokuwa unapewa kwa matumizi. Katika nchi nyingi pia, ni takwa la kisheria kwamba watu wawaeleze wasimamizi wa kodi kuhusu badiliko la hali yao.

Kwa kuongezea, watu wengi zaidi hunufaika kwa kutafuta mashauri kutoka kwa mtaalamu wa mambo ya kisheria—mtu ambaye ana uzoefu hususa katika masuala ya talaka. Nchi fulani huruhusu wapatanishi wawasaidie wenzi washirikiane kufikia makubaliano ya pamoja na ya amani, ambayo baadaye huthibitishwa rasmi na mahakama ya kisheria. Hasa katika visa vinavyohusisha watoto, wazazi wengi hupendelea kutafuta huduma za mtaalamu asiye na upendeleo. Badala ya kujipatia faida kubwa za kimwili, wazazi hunuia kupunguza kuhitilafiana na kuumizana. Vitu fulani vya kimwili kwa kweli havistahili kumfanya mtu ateseke kihisia-moyo na kutumia fedha nyingi.

Uhusiano Uliobadilika

“Hatupaswi kudharau mfadhaiko na ukosefu wa uhakika ambao watu wengi huhisi kuhusu marafiki wao waliotalikiana,” asema mtafiti mmoja. Hata ikiwa mwenzi mwaminifu anachukua hatua kulingana na haki zake za kisheria, kiadili, na Kimaandiko, huenda kukawa na wengine watakaomwona kuwa kisababishi cha kuvunjika kwa ndoa. Huenda wakaonyesha hivyo kwa kumsalimu kwa ubaridi hadi kufikia hatua ya kumwepuka waziwazi. Lililo baya hata zaidi, ni kwamba waandamani wa karibu wa zamani waweza kumwonyesha uhasama wa waziwazi.

Kwa kweli wengi hawatambui mtu huhitaji utegemezo kiasi gani anapotaliki; huenda wakafikiri kwamba barua fupi au kadi inatosha. Hata hivyo, kwa kawaida kuna marafiki ambao “huonyesha hisia-mwenzi zinazofaa,” chasema kitabu Divorce and Separation, “na watakutembelea kuona ikiwa unataka mtu wa kuandamana naye mahali popote, unataka ufanyiwe jambo fulani au ikiwa unataka kuzungumza tu.” Kwa kweli, wakati huo maishani, mtu huhitaji, kama Biblia isemavyo, “rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.”—Mithali 18:24.

Kujaribu Kurudia Hali ya Kawaida

Miaka 16 baada ya kutalikiana, mama mmoja akiri hivi: “Bado kuna nyakati ambazo ninahisi upweke kwelikweli—hata ninapokuwa na watu wengine.” Yeye hukabilianaje na hali hiyo? “Nimebuni utaratibu wa kufanya mambo mengi,” akumbuka, “kwa kuwa na shughuli nyingi kazini, kumtunza mwana wangu, na kutunza nyumba yangu. Pia nilianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, na kushiriki itikadi zangu pamoja na majirani, na kuwafanyia wengine mambo. Kufanya hivyo kulisaidia sana.”

Tarehe na nyakati fulani za mwaka zaweza kuamsha kumbukumbu na hisia-moyo zenye kuhuzunisha: siku ambayo kukosa uaminifu kulifunuliwa, wakati alipotoka nyumbani, ta­rehe ya kesi ya mahakamani. Matukio yenye furaha ambayo wenzi walishiriki—kama vile kwenda likizo na ukumbusho wa kila mwaka wa arusi—yaweza kuwa mambo yaliyo magumu kushughulika nayo kihisia-moyo. “Mimi hushughulika na siku hizo kwa kupanga nitumie wakati pamoja na familia yangu au na marafiki wa karibu wanaofahamu hali yangu,” asema Pat. “Sisi hufanya mambo yatakayofuta mawazo ya zamani na kuwa na kumbukumbu mpya. Lakini mimi hupata msaada mkubwa zaidi kupitia uhusiano wangu na Yehova—nikijua kwamba yeye huelewa ninavyohisi.”

Usikate Tumaini

Wenzi wasio na hatia ambao hutumia kanuni za Biblia na kuamua kufuatia haki waliyopewa na Mungu ya kumtaliki mwenzi mzinzi hawapaswi kuhisi hatia au kuhofu kwamba Yehova amewatupa. Mwendo wa udanganyifu wa mwenzi mzinzi—ambao umesababisha “kulia na kuugua”—ndio humchukiza Mungu. (Malaki 2:13-16) Hata Yehova, Mungu mwenye “huruma nyororo,” anajua jinsi ambavyo mtu huhisi anapokataliwa na mpendwa wake. (Luka 1:78; Yeremia 3:1; 31:31, 32) Basi, uwe na hakika kwamba, “BWANA hupenda haki, wala hawaachi watauwa wake.”—Zaburi 37:28.

Bila shaka, ingekuwa afadhali ikiwa hapo mwanzoni kukosa uaminifu katika ndoa na matokeo yake mabaya yangeepukwa. Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia,b ambacho ni mwongozo unaotumika wa familia, kinasaidia watu wengi ulimwenguni pote kujenga ndoa zenye furaha na kuepuka kukosa uaminifu katika ndoa. Kina sura zinazohusu kujenga ndoa yenye furaha, kuwazoeza watoto, na kukabiliana na matatizo ya ndoa. Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu au wachapishaji wa gazeti hili watafurahi kuandaa habari zaidi.

[Maelezo ya Chini]

a Habari zaidi yaweza kupatikana katika mfululizo wa makala “Malezi ya Mtoto—Ni Maoni Gani Yaliyosawazika?” katika toleo la Amkeni! la Desemba 8, 1997, na kwenye makala “Kusaidia Watoto wa Talaka,” ya Aprili 22, 1991, Kiingereza.

b Kimechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

WATOTO HAWASTAHILI KUWA NA WAZAZI WALIOTALIKIANA

Mwaka wa 1988 Diana aliyekufa, Binti-Mfalme wa Wales, alisema kwamba katika Uingereza peke yake, kila siku watoto 420 hushuhudia wazazi wao wakitalikiana. Thuluthi moja ya watoto hao wana umri unaopungua miaka mitano. Kwa kuhuzunisha, asilimia 40 hivi ya watoto hao hupoteana kabisa na mmoja wa wazazi wao baada ya talaka.

Kinyume cha vile watu wengi hufikiri, “ni watoto wachache sana wa wazazi waliotalikiana hukubali mvunjiko huo,” asema mwandishi anayeheshimiwa wa masuala ya afya na ya kitiba. “Watoto wengi wangependelea kuona wazazi wao wakiishi pamoja hata ikiwa hali ya familia ni ngumu.” Hata ikiwa wenzi walibishana sana wakati kukosa uaminifu kulipogunduliwa, hawakupaswa kufikia kwa haraka mkataa wa kwamba kuvunja ndoa kungeleta hali bora kwa watoto. Kufanya mabadiliko katika mtazamo na tabia yao kwaweza kuwafanya waendelee kuishi pamoja kwa hali-njema ya familia nzima.

“Waume wanaofanya ngono za ovyo-ovyo,” asema mwandishi Pamela Winfield, “wanapaswa kufikiri juu ya maumivu watakayosababishia watoto wao nyumba yao itakapovunjika kufuatia upumbavu wao.”

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

JE, MUNGU HUCHUKIA TALAKA ZOTE?

“Jambo lililonitia wasiwasi zaidi,” akiri Pat, “lilikuwa wazo la kwamba ‘BWANA huchukia kuachana.’ Sikuzote akilini mwangu nilikuwa nikijiuliza, ‘Je, ninafanya jambo linalompendeza Yehova?’”

Acheni tutazame muktadha wa Malaki 2:16 ili kujibu swali hilo. Katika siku za Malaki yawezekana wanaume wengi Waisraeli walikuwa wakiwataliki wake zao, ili kuoa wanawake wapagani, wachanga zaidi. Mungu alishutumu mwenendo huu wenye udanganyifu na hila. (Malaki 2: 13-16) Kwa sababu hiyo, jambo analochukia Mungu ni mtu kumtupilia mbali mwenzi wake kwa sababu isiyo na msingi ili kuchukua mwenzi mwingine. Mtu anayefanya uzinzi kwa njia ya udanganyifu na kisha ama anamtaliki mwenzi wake ama anamsonga mwenzi wake amtaliki anakuwa amefanya dhambi yenye hila na yenye kuchukiza.

Hata hivyo, mistari hii haishutumu talaka zote. Hili laweza kuthibitishwa na maneno ya Yesu: “Yeyote yule atalikiye mke wake, ila kwa sababu ya uasherati, na kuoa mwingine afanya uzinzi.” (Mathayo 19:9) Hapa Yesu alikiri kwamba uasherati ni msingi unaokubalika wa kutaliki Kimaandiko—kwa kweli, ndio msingi pekee unaokubalika ili kufunga ndoa tena. Mwenzi asiye na hatia aweza kuamua kumsamehe mwenzi aliyekosea. Hata hivyo, mtu anayeamua kutumia taarifa ya Yesu kama msingi wa kumtaliki mwenzi mzinzi hafanyi jambo linalomchukiza Yehova. Mungu huchukia mwenendo wa mwenzi wa ndoa wa kukosa uaminifu na wenye udanganyifu.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wenzi wasio na hatia pamoja na watoto wao hunufaika na utegemezo wenye upendo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki