Maoni ya Biblia
Mtu Anawezaje Kuwa Raia Mwema?
BAADA ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, watu wengi huko Ulaya na Japani waliojiona kuwa raia wema na wenye kutii sheria walishtakiwa kwa kupatikana na hatia ya uhalifu wa wakati wa vita. Miongoni mwao mlikuwa maofisa wa ngazi ya juu jeshini, wanasayansi, na wataalamu wengine. Katika jitihada ya kutetea matendo yao, baadhi ya wahalifu hawa walisema kwamba walikuwa tu wakitii amri, kama raia yeyote mwema anavyotarajiwa kufanya. Hata hivyo, huo uraia mwema waliotaja uliwaongoza kutenda uhalifu mbaya sana dhidi ya wanadamu.
Kwa upande mwingine, kuna wale ambao hukosa kustahi mamlaka ya Serikali. Wengine hupinga waziwazi mamlaka ya kiserikali, huku wengine wakiwa tayari kuvunja sheria maadamu hakuna hatari ya kushikwa. Bila shaka, wengi huona uhitaji wa kutii mamlaka, kwa kuwa bila mamlaka kungekuwa na ghasia na machafuko. Hata hivyo, swali ni, Mtu anapaswa kutekeleza wajibu wa kiraia na kutii sheria kwa kadiri gani? Fikiria kanuni chache za msingi zilizosaidia Wakristo wa karne ya kwanza wawe na maoni yaliyosawazika juu ya madaraka yao kuelekea Serikali.
Ujitiisho wa Wakristo kwa Mamlaka
Wakristo wa karne ya kwanza walijitiisha kwa hiari kwa sheria na kanuni za wale waliokuwa “mamlaka zilizo kubwa”—yaani, serikali zilizokuwa zikitawala. (Waroma 13:1) Wakristo waliitikadi kwamba ilifaa ‘kuwa katika ujitiisho na kuwa watiifu kwa serikali na mamlaka zikiwa watawala.’ (Tito 3:1) Ijapokuwa walimtambua Kristo kuwa Mfalme wao wa kimbingu, wao pia walikuwa raia wenye kutii sheria za watawala wao wa kibinadamu na hawakuwa tisho kwa usalama wa Serikali. Kwa kweli, walitiwa moyo ‘wamheshimu mfalme’ nyakati zote. (1 Petro 2:17) Hata mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo: “Kwa hiyo nahimiza kwa bidii, kwanza kabisa, kwamba dua, sala, maombezi, matoleo ya shukrani, yafanywe kuhusu watu wa namna zote, kuhusu wafalme na wote wale walio katika cheo cha juu; ili tupate kuendelea kuishi maisha yaliyo shwari na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili na uchukuaji-mambo kwa uzito.”—1 Timotheo 2:1, 2.
Wakristo wa karne ya kwanza walilipa kwa kudhamiria kodi zozote zile walizodaiwa, hata ingawa nyakati nyingine kufanya hivyo kulikuwa mzigo mzito. Walitii agizo lililopuliziwa lililotolewa na mtume Paulo juu ya jambo hili: “Walipeni wote haki zao, kwa yeye atakaye kodi, kodi.” (Waroma 13:7) Kulingana na maoni ya wanafunzi wa Yesu, serikali ya Roma na maafisa wake walitawala kwa ruhusa ya Mungu na kwa njia fulani walitumikia wakiwa “watumishi wa Mungu wa watu wote,” kwa sababu walidumisha kiasi fulani cha amani na uthabiti katika jamii.—Waroma 13:6.
“Tayari kwa Ajili ya Kila Kazi Njema”
Wakristo wa karne ya kwanza walitiwa moyo wakubali utumishi wa kiraia ulioamriwa na Serikali. Yesu Kristo mwenyewe aliwashauri wanafunzi wake wawe tayari nyakati nyingine kufanya zaidi ya kiasi kinachodaiwa na mamlaka za kiserikali. “Ikiwa mtu fulani aliye chini ya mamlaka akushurutisha ufanye utumishi kwa kilometa moja,” akasema, “nenda pamoja naye kilometa mbili.” (Mathayo 5:41) Kwa kufuata shauri hili, Wakristo walionyesha kwamba hawakutaka kujifaidi kwa kuishi katika jamii iliyostaarabika bila kufanya jambo lolote lenye faida. Sikuzote walikuwa “tayari kwa ajili ya kila kazi njema.”—Tito 3:1; 1 Petro 2:13-16.
Waliwapenda kihalisi jirani zao nao walitafuta njia za kuwasaidia. (Mathayo 22:39) Kwa sababu ya upendo huu na kufuata kwao viwango vya juu vya adili, Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa vielelezo bora katika jumuiya. Jirani zao walikuwa na sababu nyingi za kufurahia kuwa na jirani Mkristo. (Waroma 13:8-10) Wakristo walidhihirisha upendo wao katika njia nyingi zaidi ya kujiepusha tu na ubaya. Walitiwa moyo wawe wenye urafiki na wapendezwe na watu wengine, wafanye “lililo jema [si kuelekea waamini wenzao tu, bali] kuelekea wote,” kama Yesu Kristo alivyofanya.—Wagalatia 6:10.
“Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu”
Hata hivyo, utii wao kwa mamlaka za kilimwengu ulikuwa na mipaka. Hawangefanya jambo lolote ambalo lingechafua dhamiri zao au kuharibu uhusiano wao na Mungu. Kwa mfano, mamlaka za kidini katika Yerusalemu zilipowaamuru mitume waache kuhubiri juu ya Yesu, walikataa kutii. “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu,” wao wakatangaza. (Matendo 5:27-29) Wakristo walikataa kwa uthabiti kuhusika katika ibada ya maliki iliyo ya sanamu. (1 Wakorintho 10:14; 1 Yohana 5:21; Ufunuo 19:10) Matokeo yalikuwa nini? “Walishutumiwa,” asema mwanahistoria J. M. Roberts, “si kwa sababu ya kuwa Wakristo, bali kwa sababu ya kukataa kutii jambo lililoamriwa na sheria.”—Shorter History of the World.
Kwa nini katika hali hii ‘walikataa kutii jambo lililoamriwa na sheria’? Walitambua kwamba “mamlaka zilizo kubwa” zilitawala kwa ruhusa ya Mungu na hivyo zilitumika zikiwa “mhudumu wa Mungu” katika kudumisha sheria na utaratibu. (Waroma 13:1, 4) Lakini Wakristo bado waliiona sheria ya Mungu kuwa kubwa zaidi. Walikumbuka kwamba Yesu Kristo alikuwa amewawekea kanuni hii yenye usawaziko wale ambao wangekuwa wafuasi wake: “Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” (Mathayo 22:21) Wajibu wao kwa Mungu ungekuwa muhimu kuliko madai ya Kaisari.
Idhibati ya kwamba huo ulikuwa mwendo unaofaa inaonyeshwa na matokeo wakati wale waliodai kuwa Wakristo waliposhindwa kufuata kanuni hizi bora. Kwa mfano, viongozi waasi-imani wa Jumuiya ya Wakristo wakawa “watu walio tayari [kutumiwa] na serikali za kiraia, hasa katika kujenga na kutunza vikosi vya kijeshi,” asema mwanahistoria wa kijeshi John Keegan. Wafuasi wao waliishia kuunga mkono pande zilizopigana katika vita vilivyosababisha umwagikaji wa damu ya mamilioni ya watu wasio na hatia. Keegan asema: “Sheria ya Mungu ilipuuzwa kabisa wakati hasira ya wanadamu ilipochochewa.”
Hata hivyo, Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa kielelezo bora katika kudumisha usawaziko unaofaa. Walikuwa raia wema. Walitekeleza wajibu wao wa kiraia na madaraka yao vyema. Lakini wao walishikamana sana na kanuni zilizo wazi za Biblia na walifuata dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia katika mambo yote maishani.—Isaya 2:4; Mathayo 26:52; Waroma 13:5; 1 Petro 3:16.
[Picha katika ukurasa wa 26]
“Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari”