Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 9/22 kur. 10-12
  • Naweza Kuvumiliaje Ukosefu wa Haki?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kuvumiliaje Ukosefu wa Haki?
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuondolea Mbali Uchungu na Hasira
  • Mwisho wa Ukosefu wa Haki
  • Kupata Msaada na Utegemezo
  • Yehova Ni Mpenda-haki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Jinsi ya Kukabiliana na Ukosefu wa Haki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Je! Kweli Kuna Wakati Ambapo Mungu Ataondoa Ukosefu wa Haki?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Unaweza Kukabiliana na Ukosefu wa Haki!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 9/22 kur. 10-12

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kuvumiliaje Ukosefu wa Haki?

“Wale wenye pesa tu ndio hustahiwa, lakini sisi ambao hata hatuna chakula chochote au mahali popote pa kulala hutendwa kama wanyama. Ninachotarajia wakati ujao ni kufa tu bila yeyote kutambua.”—Arnulfo, mvulana mwenye umri wa miaka 15, asiye na makao.

KUNA ukosefu mwingi wa haki duniani. Ripoti moja kutoka Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa (UNICEF) ilisema: “Katika mwongo uliopita, zaidi ya watoto milioni 2 wameuawa katika vita, zaidi ya milioni 4 wakanusurika baada ya kukatwa viungo vya mwili, na zaidi ya milioni 1 wakawa mayatima au wakatengwa na familia zao kwa sababu ya vita.” Njaa na umaskini, ambao pia husumbua watu wengi sana ulimwenguni, mara nyingi huambatana na utajiri na utele. Katika nchi zinazositawi, vijana wengi kama Arnulfo hunyimwa fursa ya kupata elimu.

Ukosefu wa haki unaumiza hasa ukisababishwa na wale wanaopaswa kukupenda na kukulinda. Mfikirie msichana mwenye umri wa miaka 17 aitwaye Susana. Yeye na ndugu zake wawili wadogo waliachwa na mama yao. “Miaka imepita,” Susana asema kwa uchungu, “na mamangu hajawahi kuniomba niishi naye, hata ingawa yeye anaishi katika mji uleule ninamoishi. Hajawahi hata kuniambia, ‘Nakupenda,’ na jambo hilo limeniudhi sana sikuzote, na lingali linaniudhi.” Huenda ikawa vigumu kwako kudhibiti hasira yako ukitendwa vibaya hivyo. Mwanamke mmoja aliyesumbuliwa kingono akiwa mtoto asema: “Jambo hilo hata limenifanya nimwone Mungu isivyofaa.”

Ni jambo la kawaida kuumia na kukasirika unapotendwa vibaya. Biblia husema: “Jeuri humpumbaza mwenye hekima.” (Mhubiri 7:7) Kuvumilia ukosefu wa haki kila siku kwaweza pia kukufanya uhisi umeshuka moyo. (Linganisha Zaburi 43:2.) Hivyo, huenda ukatamani sana ukosefu wa haki ukome. Msichana mmoja kutoka Amerika ya Kati akumbuka: “Nilijiunga na harakati ya wanafunzi nikiwa na umri wa miaka 13. Nilikuwa na mradi wa kusaidia kubadili mambo, ili watoto wasiwe na njaa. . . . Baadaye nikashiriki katika mapambano ya kutumia silaha.” Hata hivyo, badala ya kupata haki, alitendwa vibaya sana na wanajeshi wenzake.

Hali hizo hutukumbusha kwamba watu wengi hawana uwezo wa kuboresha hali yao. Hivyo basi, wahasiriwa wa ukosefu wa haki waweza kuuvumiliaje?a Je, waweza kushughulikaje na uchungu na hasira ambayo huenda ukawa nayo?

Kuondolea Mbali Uchungu na Hasira

Mara kwa mara, huenda ukahitaji kujikumbusha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. Biblia ilitabiri kwamba watu leo wangekuwa “wenye kutukana, . . .wasio na upendo, wasiosamehe, wachongezi, wasiojidhibiti, wakatili, wasiopenda mema, wasaliti.” (2 Timotheo 3:1-4, New International Version) Wengi “[wame]ishiwa na hisia zote za adili.” (Waefeso 4:19) Hivyo, ukosefu wa haki ni jambo lisiloepukika maishani. Hivyo, ‘ujapokuwa unaona maskini akionewa, na hukumu na haki kuondolewa kwa jeuri katika jimbo, usilistaajabie jambo hilo.’—Mhubiri 5:8.

Kwa sababu nzuri, Biblia yaonya dhidi ya kuacha uchungu ukudhibiti kabisa. Kwa mfano, hiyo yasema: “Acheni uchungu wote wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi . . . viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.” (Waefeso 4:31) Kwa nini? Kwa sababu hatimaye, kuendelea kuwa na hasira yenye uchungu hukudhuru na kukuangamiza. (Linganisha Mithali 14:30; Waefeso 4:26, 27.) Inakuwa hivyo hasa ukijikuta “unakasirika juu ya BWANA.” (Mithali 19:3, Zaire Swahili Bible) Kumkasirikia Mungu hudhuru uhusiano wako na Mtu yule awezaye kukusaidia zaidi. Biblia husema kwamba “macho ya BWANA [“Yehova,” NW] hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.”—2 Mambo ya Nyakati 16:9.

Biblia pia husema hivi kuhusu Yehova: “Njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Ukosefu wa haki ulisababishwa na uasi wa Adamu na Hawa. (Mhubiri 7:29) Mwanadamu—wala si Mungu—ndiye aliye na “mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Mhubiri 8:9, Chapa ya 1989) Kumbuka pia kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu,” Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Shetani, wala si Yehova, ndiye husababisha ukosefu wa haki ulimwenguni.

Mwisho wa Ukosefu wa Haki

Kwa uzuri, ukosefu wa haki hautaendelea milele. Kukumbuka hayo kwaweza kukusaidia uvumilie. Fikiria lililompata mtu aitwaye Asafu, aliyeishi nyakati za Biblia. Hata ingawa aliishi kati ya watu waliodai kumtumikia Yehova, ukosefu wa haki ulimzunguka kila upande. Badala ya kuadhibiwa kwa kutenda wengine vibaya, wakatili walionekana kuishi maisha yasiyo na usumbufu na yenye ufanisi! Asafu akiri: “Naliwaonea wivu . . . nilipoiona hali ya amani ya wasio haki.” Kwa muda, Asafu aliyumbayumba kwa kufikiria sana mambo hayo.—Zaburi 73:1-12.

Baada ya muda, Asafu akaelewa mambo kwa njia yenye kutokeza. Akasema hivi kuhusu waovu: “Hakika Wewe [Mungu] huwaweka penye utelezi, huwaangusha mpaka palipoharibika.” (Zaburi 73:16-19) Naam, Asafu alikuja kuelewa kwamba hatimaye, watu kwa kweli huadhibiwa kwa uovu wao. Mara nyingi, wao hupatwa na matokeo ya makosa yao nao hutiwa gerezani, wakafilisika, wakapoteza kazi ya kuajiriwa, au kuondolewa katika nyadhifa za mamlaka. Karibuni sana, waovu ‘wataanguka palipoharibika’ Mungu atakapotekeleza hukumu dhidi ya mfumo huu mwovu wa mambo.—Zaburi 10:15, 17, 18; 37:9-11.

Kujua kwamba karibuni Mungu atarekebisha mambo kwaweza kukusaidia kudhibiti hasira yako na kuvunjika moyo. “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote,” Biblia yashauri. “Andaeni mambo bora mbele ya macho ya watu wote. Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi hasira ya kisasi; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa, asema Yehova.’”—Waroma 12:17-19; linganisha 1 Petro 2:23.

Kupata Msaada na Utegemezo

Hata hivyo, huenda ukawa na maumivu makali ya kihisia-moyo, kama vile kumbukumbu zenye kuumiza. Kwa mujibu wa ripoti ya UNICEF, “watoto wanaoona jeuri daima, karibu sikuzote hupatwa na badiliko kubwa katika itikadi na mitazamo yao, kutia ndani ukosefu mkubwa wa tumaini katika wengine. Inakuwa hivyo hasa kwa watoto ambao wameshambuliwa au kutendwa vibaya na watu ambao hapo awali walionwa kuwa majirani au marafiki.”

Matatizo hayo hayawezi kutatuliwa kwa urahisi. Lakini ikiwa hisia zisizofaa au kumbukumbu zenye kuumiza zatawala mawazo yako, yaelekea wahitaji msaada. (Linganisha Zaburi 119:133.) Kwanza, unaweza kusoma habari inayohusu matatizo ambayo yamekupata. Kwa mfano, gazeti la Amkeni! limechapisha makala kadhaa ambazo hutoa mashauri yenye kutumika kwa waliobakwa, wakapokonywa, na kutendwa vibaya wakiwa watoto. Yaweza kusaidia sana kumweleza, msikilizaji mkomavu na mwenye hisia-mwenzi, mahangaiko na hisia zako. (Mithali 12:25) Labda unaweza kuzungumza na wazazi wako.

Lakini namna gani ikiwa utegemezo wa wazazi hauwezi kupatikana? Basi, tafuta utegemezo kutoka kwa kutaniko la Kikristo. Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, wazee wa kutaniko ni kimbilio kwa wale wanaoteseka. (Isaya 32:1, 2) Wanaweza kukupa mashauri yenye kutumika mbali na kukusikiliza. Pia, usisahau kwamba Wakristo wengine wakomavu wanaweza kuwa “akina ndugu na akina dada na akina mama” kwako. (Marko 10:29, 30) Je, wamkumbuka Susana aliyeachwa na mamaye? Yeye na nduguze walipata utegemezo kutoka katika kutaniko la Kikristo. Mhudumu mmoja Mkristo alipendezwa sana na familia ya Susana hivi kwamba, Susana humwita baba yake mwasilishaji. Utegemezo huo, asema Susana, “umetusaidia kukomaa na kusimama imara katika kweli.”

Wataalamu husema kwamba kudumisha kawaida ya kila siku ya utendaji wenye maana kwaweza pia kusaidia. Vivyo hivyo, kwenda shuleni na kufanya kazi zako za nyumbani kwaweza kukusaidia sana usiwe na mawazo yasiyofaa. Hata hivyo, utanufaika hasa kwa kufuata kawaida ya utendaji mbalimbali wa kiroho—kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kuhubiri habari njema.—Linganisha Wafilipi 3:16.

Ukosefu wa haki hautatoweka duniani hadi Ufalme wa Mungu uje na kutekeleza mapenzi ya Mungu duniani pote. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Wakati huu, fanya yote uwezayo kuvumilia. Jitegemeze kwa ahadi kwamba Yesu Kristo, akiwa Mtawala wa Ufalme wa Mungu, “atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.”—Zaburi 72:12, 13.

[Maelezo ya Chini]

a Ingawa makala hii yakazia ukosefu wa haki ambao huenda ukawapata vijana katika nchi maskini, kanuni zinazozungumziwa hapa zaweza kutumika kuhusiana na aina yoyote ya ukosefu wa haki ambayo huenda ikapata mtu.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

“Jambo hilo hata limenifanya nimwone Mungu isivyofaa”

[Picha katika ukurasa wa 12]

Utegemezo wa Wakristo wenzako waweza kukusaidia uvumilie ukosefu wa haki

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki