Bima Ambayo Kila Mtu Anahitaji
UWE waishi mahali ambapo bima ni kawaida au mahali ambapo haipatikani, kuna bima moja ambayo kila mtu anaweza na anapaswa kuwa nayo. Kwa kuwa “bima” yaweza kurejezea “mpango wa kupata ulinzi au usalama,” unaweza kupataje bima ya aina hiyo?
Unaweza kuipata kwa kuchukua hatua madhubuti za kupunguza hatari unazokabili. Biblia yasema kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” huathiri kila mtu. (Mhubiri 9:11, NW) Lakini, ukiepuka kujihatarisha isivyo lazima, uwezekano wa kujeruhiwa au kupata hasara hupungua.
Fikiria Wakati Ujao
Kuwa na hekima inayotumika ni ulinzi. Unapokuwa na ufanisi fulani wa kiuchumi, unaweza kuweka akiba fulani kwa ajili ya wakati wa hari—wakati wa uhitaji. Katika nyakati za kale mwanamume mcha-Mungu aitwaye Yosefu alijipatia sifa ya kuwa “mtu wa akili na hekima” kwa kuweka akiba ya nafaka kwa ajili ya nchi yote ya Misri kulipokuwa na shibe. Nchi ilipokumbwa na njaa hatimaye, hatua ya Yosefu iliandalia chakula si Wamisri tu bali pia jamaa yake mwenyewe.—Mwanzo 41:33-36.
Tunaweza kujilinda pia kwa kuwa wenye kiasi katika matumizi. Tunaweza kuweka akiba ya fedha na kupunguza mkazo kwa kutokimbilia daima vifaa vipya, mitindo, au vitumbuizo—zoea ambalo halituletei usalama halisi. Kwa kweli, kama ilivyotajwa awali, kuna uwezekano mkubwa wa kuibiwa au kupata hasara unapomiliki vitu vingi vya kimwili.—Luka 12:15.
Jali Usalama Wako
Tunaweza kupunguza sana hatari maishani kwa kujali tu usalama. Ni aksidenti ngapi mbaya sana zingeweza kuepukwa endapo kila mtu angeendesha gari kwa uangalifu na kwa mwendo salama? Fikiria pia, uhai ambao ungeokolewa ikiwa kila mtu angeepuka kuendesha gari akiwa mchovu au baada ya kunywa kileo. Pia kuna hatari nyingine za uendeshaji-gari tunazoweza kudhibiti.
Kwa mfano, sheria za nchi nyingi zimepiga marufuku kutumia simu ya mkononi unapoendesha gari. Uchunguzi mmoja ulifikia mkataa wa kwamba kutumia simu hiyo huzidisha mara nne hatari ya aksidenti kutukia. Hatari hiyo ni sawa na hatari ya kupata aksidenti unapoendesha gari huku kipimo cha kileo katika damu yako kikiwa cha asilimia 0.1, sheria za sehemu mbalimbali huwaona watu wenye kipimo hicho kuwa walevi mno kuendesha gari.
Kujifunga mkanda wa usalama kwa ukawaida hupunguza pia hatari ya madereva na abiria kufa. Lakini usidhani kamwe kwamba kuwa na vifaa vya usalama kama vile mikanda ya usalama na mifuko ya kinga au kuwa na bima hukuruhusu kujihatarisha. Utafiti waonyesha kwamba maoni hayo husababisha aksidenti zaidi.
Kujali usalama ni bima nzuri nyumbani na kazini pia. Je, makazi na mahali pako pa kazi ni nadhifu bila hatari yoyote? Kagua kila mahali. Je, kuna kitu chochote njiani kinachoweza kuwakwaa watu? Je, vifaa vyenye makali au vilivyo moto—meko, vipasha-joto, pasi—vimewekwa mahali ambapo vinaweza kuwakata au kuwaunguza watu? Je, kuna rundo la karatasi au vifaa vingine vinavyoweza kushika moto? Uwe mwangalifu sana kuhusu hatari kwa watoto. Kwa mfano, je, vileo na bidhaa nyingine za kusafishia zenye sumu zimewekwa mahali pasipofikiwa na watoto wadogo?
Tunza Afya Yako
Kwa kutunza afya yako ifaavyo, unaweza kupunguza hatari ya magonjwa. Kuhusu hilo, kuwa na ujuzi kwaweza kuwa kama bima. Jihadhari na hatari kwa afya yako, na uchukue hatua mara moja matatizo ya afya yanapozuka. Jambo la muhimu zaidi, jifunze jinsi ya kutunza afya yako na ya familia yako. Kumbuka msemo wa jadi: “Kukinga ni bora kuliko kutibu.”
Kwa muda mrefu gazeti la Amkeni! limeandaa habari ambayo huwatia watu moyo kuishi kulingana na kanuni za Biblia na hivyo kuepuka mazoea na mitindo ya maisha inayodhuru afya. Mathalani, miongoni mwa habari nyingi zinazozungumziwa katika Amkeni! zimekazia umuhimu wa usafi, mlo unaofaa, kupata usingizi wa kutosha, na kufanya mazoezi kwa ukawaida na vilevile uhitaji wa kudhibiti mkazo na hekaheka za maisha.
Bima Muhimu Sana
Katika ulimwengu huu usio mkamilifu, bima yaweza kuwa mpango unaofaa sana, lakini hakuna bima iwayo yote inayoweza kutulinda kikamili au kulipia kikamili hasara zetu. Lakini, wawe na bima au la, kuna watu walio na uhakika wa kwamba hawataachwa peke yao. Kwa nini? Kwa sababu misiba inapozuka, wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo—wale wanaomtumikia Baba yake, Yehova Mungu—hujitahidi sana kusaidiana.—Zaburi 83:18; Yakobo 2:15-17; 1 Yohana 3:16-18.
Isitoshe, Yehova mwenyewe anaahidi kutowaacha kamwe watumishi wake waaminifu. Mtunga-zaburi wa Biblia aliandika hivi: ‘Baba yangu na mama yangu wakiniacha, BWANA atanikaribisha kwake.’ (Zaburi 27:10) Akiwa Chanzo cha uhai, Yehova anaweza kuwafufua wafu, na Biblia yasema kwamba amempa Mwanawe, Yesu Kristo, uwezo wa kufufua wafu. (Zaburi 36:9; Yohana 6:40, 44) Lakini, Neno la Mungu laonyesha kwamba si wote watakaofufuliwa. (Yohana 17:12) Hivyo basi, twaweza kufanyaje ili tukumbukwe na Mungu wakati wa ufufuo?
Kwa wazi, Yesu alizungumzia bima yenye kutegemeka zaidi katika Mahubiri yake maarufu ya Mlimani. Alisema: “Komeni kujiwekea akiba ya hazina duniani, ambako nondo na kutu hula kabisa, na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala ya hivyo, jiwekeeni akiba ya hazina mbinguni, ambako wala nondo wala kutu haili kabisa, na ambako wezi hawavunji na kuiba. Kwa maana ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.”—Mathayo 6:19-21.
Mara nyingi watu hufikiria kujiwekea akiba ya fedha wakitumaini kwamba itawawezesha kuishi raha mustarehe wanapozeeka. Hata hivyo, Yesu alitaja bima iliyo salama zaidi. Thamani yake haina kifani, haitashindwa kamwe! Alieleza hivi: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’—Yohana 17:3.
Kwa kutwaa ujuzi sahihi juu ya Mungu na Mwanawe na kutumia yale tunayojifunza maishani mwetu, tutajijengea jina zuri na Mungu. (Waebrania 6:10) Mtume Petro na mtume Yohana, wakitegemeza itikadi zao kwa mafundisho ya Bwana wao, Yesu Kristo, walikazia kwamba mfumo uliopo wa utawala wa wanadamu utakoma. Lakini, Yohana akaeleza: “Yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17; Mathayo 24:3, 14; 2 Petro 3:7, 13.
Tunaweza kuwa na hakika kwamba ikiwa tutamtumikia Mungu kisha tufe, atatufufua au ikiwa tutakuwa hai anapoleta mwisho wa mfumo huu wa mambo, atatuhifadhi tukiwa hai hadi kwenye ulimwengu wake mpya wa uadilifu. Kwa kweli, Mungu anaahidi ‘kufuta kabisa kila chozi kutoka katika macho [yetu]’ na kufanya “vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:4, 5) Kumtumikia Mungu na kutumaini kabisa ahadi zake kwa kweli ni bima bora kupita zote. Kila mtu anaweza kuipata.
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Kujali usalama na kutunza afya ni kama bima
[Picha katika ukurasa wa 10]
Kujifunza kumhusu Mungu na kufanya mapenzi yake ndiyo bima bora zaidi ya wakati ujao