Magereza Yamo Taabani
“Kujenga magereza zaidi ili kukabiliana na uhalifu ni kama kuchimba makaburi zaidi ili kukabiliana na ugonjwa hatari.”—ROBERT GANGI, MREKEBISHAJI STADI WA WAFUNGWA.
WATU huona neno “gereza” kuwa neno lenye kuudhi na hivyo hutumia maneno yasiyoonyesha waziwazi hali mbaya iliyopo. Watu hupenda kutumia neno “kifungoni” au “kituo cha kuwarekebishia wafungwa,” ambamo “elimu ya kiufundi” na “huduma za kijamii” huandaliwa. Watu hupenda pia kutumia neno “mfungwa” badala ya neno “mahabusu” lenye kumshushia mtu heshima. Lakini unapochunguza hali ilivyo, utaona kwamba magereza yanapatwa na matatizo makubwa sana leo, kama vile gharama inayoongezeka ya kuwatunza wahalifu gerezani. Isitoshe, jitihada za kuwarekebisha wafungwa huambulia patupu.
Watu fulani hutilia shaka umuhimu wa magereza. Wanasema kwamba ingawa kuna wahalifu zaidi ya milioni nane katika magereza ulimwenguni pote, uhalifu haujapungua katika nchi nyingi. Na ingawa watu wengi sana wamefungwa gerezani kwa sababu ya ulanguzi wa dawa za kulevya, biashara hiyo imepamba moto mitaani.
Hata hivyo, watu wengi huona kuwafunga wahalifu gerezani kuwa adhabu inayofaa. Wao huhisi kwamba mfungwa anapotiwa gerezani anapokea adhabu anayostahili. Mwandishi mmoja wa habari aita juhudi za kuwatia wahalifu gerezani kuwa “msisimko wa kujaza watu gerezani.”
Wale wanaovunja sheria hutiwa gerezani kwa sababu nne kuu: (1) kuadhibu wahalifu hao, (2) kulinda jamii, (3) kuzuia uhalifu unaoweza kutokea wakati ujao, na (4) kuwarekebisha wahalifu, na kuwasaidia wawe raia wanaotii sheria na raia wema baada ya kuachiliwa. Acheni tuone ikiwa magereza yanatimiza malengo hayo.