Afya Bora kwa Wote Je, Ni Mradi Unaoweza Kutimizwa?
JE, WATAMANI kuona familia yako ikiwa na afya bora? Bila shaka. Wengi wetu hushikwa na magonjwa madogo mara kwa mara, lakini mamilioni ya watu husumbuliwa na magonjwa yenye kuumiza muda wote wa maisha yao.
Hata hivyo, jitihada kubwa zinafanywa ili kupunguza magonjwa. Fikiria jitihada za Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO), ambalo ni shirika la Umoja wa Mataifa. Kwenye mkutano mmoja uliopangwa na shirika la WHO mwaka wa 1978, wajumbe kutoka nchi 134 na mashirika 67 ya UM walikubaliana kwamba afya si hali tu ya kutokuwa mgonjwa. Walisema kwamba afya ni “hali ya kuwa kamili kimwili, kiakili na kijamii.” Kisha wajumbe hao wakachukua hatua madhubuti ya kutangaza afya kuwa “haki ya msingi ya binadamu”! Kwa hiyo shirika la WHO likaweka mradi wa kufikia “kiwango kinachokubalika cha afya kwa watu wote ulimwenguni.”
Mradi huo unapendeza na unafaa. Lakini je, kweli utatimizwa? Bila shaka kazi ya kitiba inapendwa na kutumainiwa sana kuliko kazi nyinginezo zote za wanadamu. Gazeti la The European, la Uingereza linasema kwamba watu katika nchi za Magharibi wamekuwa wakisikia kuhusu jitihada za kutafuta “dawa ya kimuujiza: dawa moja inayoweza kutibu ugonjwa kabisa.” Yaani, tunatarajia fani ya matibabu ivumbue dawa zitakazotibu kila ugonjwa kwa urahisi na mara moja. Je, kweli wataalamu wa tiba wanaweza kutimiza taraja hilo lisilo la kawaida?