Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g 4/11 kur. 4-5
  • Kukabiliana na Hisia Mpendwa Anapokufa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukabiliana na Hisia Mpendwa Anapokufa
  • Amkeni!—2011
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Sikupata Nafasi ya Kuomboleza”
  • “Nilijihisi Nikiwa Mpweke Bila Mama”
  • Msaada kwa Wale Wanaoomboleza
    Amkeni!—2011
  • Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
  • Ninaweza kukabilianaje na huzuni ya kufiwa?
    Vijana Huuliza
  • Je! Ni Kawaida Kuhisi Hivi?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2011
g 4/11 kur. 4-5

Kukabiliana na Hisia Mpendwa Anapokufa

“Nilishtuka na kuwa hoi nilipopata habari za kifo cha baba yangu. Nililemewa na hisia za hatia kwa kuwa sikuwa karibu alipokufa. Hakuna kitu kinachoweza kulinganishwa na uchungu mwingi sana ambao mtu huhisi anapofiwa na mpendwa wake. Ninamkosa sana baba yangu!”—Sara.

WATU wengi huona kuwa ni vigumu kuzungumza kuhusu kifo, wawe ni wa dini au utamaduni gani. Lugha fulani hutumia maneno ya badala kuzungumzia kifo. Katika Kiswahili, badala ya kusema mtu “amekufa,” watu watasema “ametuacha,” “ameaga,” au “hayupo nasi tena.”

Lakini, hata watu watumie maneno gani, hakuna neno linaloweza kupunguza huzuni kali ambayo watu waliofiwa na mpendwa wao huhisi. Watu fulani hulemewa sana na huzuni hivi kwamba hawakubali kuwa mpendwa wao amekufa.

Ikiwa umefiwa na mpendwa wako, huenda wewe pia ukashindwa kukabiliana na hisia zako. Huenda ukaonyesha kwamba umekubali ukweli wa mambo, lakini huenda moyoni ukawa unahisi vingine. Bila shaka, watu wote hawaombolezi kwa njia ileile, kwa hiyo, ikiwa huonyeshi huzuni yako waziwazi, hilo halimaanishi kwamba huna huzuni.a Tatizo linaweza kutokea unapojilazimisha kuonyesha hisia fulani kwa sababu ya watu wengine—labda watu wa familia wanaoomboleza ambao wanatarajia ufanye hivyo.

“Sikupata Nafasi ya Kuomboleza”

Fikiria kisa cha Nathaniel, mwanamume ambaye alifiwa na mama yake alipokuwa na umri wa miaka 24. Anasema: “Kwanza nilichanganyikiwa. Nilihisi kwamba ninapaswa kumfariji baba yangu na marafiki wengi wa mama ambao walikuwa na huzuni. Sikupata nafasi ya kuomboleza.”

Baada ya zaidi ya mwaka mmoja, Nathaniel aligundua kwamba bado hakuwa amekabiliana na hisia za kifo cha mama yake. Anasema: “Bado Baba hunipigia simu mara kwa mara kunieleza hisia zake, na ni vizuri kwamba anafanya hivyo. Anahitaji kuzungumza kuhusu hisia zake, nami ninafurahi kumsaidia. Lakini mimi ninapohitaji faraja, ninahisi kwamba sina yeyote wa kunifariji.”

Wale wanaowatunza wagonjwa—kutia ndani madaktari na wengine ambao mara nyingi huona watu wakifa—huenda wakahisi kwamba wanapaswa kufungia hisia zao. Fikiria mfano wa Heloisa, ambaye amekuwa daktari kwa zaidi ya miaka 20. Alifanya kazi katika jamii ambayo ina desturi ya kushirikiana kwa ukaribu, naye alikuwa na uhusiano wa karibu na wagonjwa wake. Anasema: “Niliketi pamoja na wengi wao walipokuwa wakifa, na baadhi yao walikuwa marafiki wangu wapendwa.”

Heloisa alitambua kwamba kulia ni njia ya kawaida ya kupata kitulizo. “Lakini ilikuwa vigumu kwangu kulia,” anasema. “Nilihangaikia sana kuwategemeza wengine hivi kwamba nilihisi ninapaswa kufungia hisia zangu. Niliamini kwamba wengine walitazamia nifanye hivyo.”

“Nilijihisi Nikiwa Mpweke Bila Mama”

Huenda upweke ndilo tatizo kubwa zaidi ambalo huwapata wale ambao wamefiwa na mpendwa wao. Kwa mfano, Ashley alikuwa na umri wa miaka 19 mama yake alipokufa kutokana na kansa. Anasema: “Baadaye nilijihisi nikiwa nimechanganyikiwa kabisa na mpweke sana. Mama alikuwa ndiye rafiki yangu wa karibu zaidi. Tulikuwa pamoja mara nyingi!”

Inaeleweka kwamba Ashley aliona ugumu wa kurudi nyumbani kila siku na kutambua kwamba mama yake hayupo. Anasema: “Nilijihisi nikiwa mpweke bila mama. Mara nyingi nilienda chumbani na kulia huku nikitazama picha zake na kufikiria kuhusu mambo ambayo tulikuwa tukifanya pamoja.”

Ikiwa umefiwa na mtu wa familia au rafiki mpendwa, usijihisi kwamba ni wewe tu unayelemewa na hisia za huzuni. Kama tutakavyoona, wengine pia wamekabiliana na hali hiyo kwa njia inayofaa.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa kuwa kila mtu huomboleza kwa njia tofauti, haingefaa kuwahukumu wale ambao hawaonyeshi hisia zao waziwazi wanapofiwa na mpendwa.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Nilijihisi nikiwa nimechanganyikiwa kabisa na mpweke sana. Mama alikuwa ndiye rafiki yangu wa karibu zaidi”—Ashley

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki